Reader Settings

SEHEMU YA 02.

MWAKA  2002-SUMBAWANGA.

Ni mwezi wa  kwanza wa mwaka 2002 katika kijiji cha Kizwite  mkoani Rukwa Wilayani Sumbawanga  alifika  mwanamke mmoja  ambaye  alijipatia umaarufu sana kwa watu wote wa kijiji hicho na vijiji vya pembeni , umaarufu wa mwanamke huyo ulitokana na  kuwa na watoto wengi ambao  walikuwa wamepishana  kwa miaka michache sana  kwa namna ambavyo walikuwa wakilingana  kwa muonekano wa nje, lakini kubwa zaidi  ni  namna walivyokuwa na rangi zinazotofautiana  ikidhihirisha  baba zao kuwa tofauti tena wa  makabila tofauti  duniani.

Yaani kwa maneno marahisi kati ya watoto hao kuna waliokuwa na mchanganyiko wa Kiarabu , Kizungu , Kichina , kijapani na  Kiafrika.

Kwa maelezo ya awali ya wanakijiji  wanasema  mwanamke huyo tokea afike hapo haikuwahi kujulikana alitokea wapi na  kuhusu watoto aliokuwa nao aliwapata pata vipi  au baba yake alikuwa ni nani haikujulikana  , kitu pekee ambacho wanakijiji  wa Kizwite walijua kuhusu mwanamke huyo ni jina lake lake tu   ambalo lilifahamika kama Chakwe.

Wanakijiji wanaelezea kwa kusema kwamba  Chakwe alionekana kama mwanamke ambaye  alikuwa hana akili nzuri sana  na walikuwa na makisio  hata watoto aliokuwa nao walitokana na kubakwa , hayo yalikuwa ni makisio tu ya wanakijiji hao  lakini ukweli wote alikuwa nao Chakwe mwenyewe  lakini kutokana na hali yake ilivyokuwa  haikuweza kufahamika moja kwa moja  maisha ya nyuma ya Chakwe yalikuwa kuwaje mpaka akawa katika hali kama hio na alipelekea  stori nyingi kumuhusu zikitungwa ndani ya  kijiji hicho.

Chakwe mara baada ya kufika katika kijiji cha Kizwite hakujali kushangawa na watu  bali alifuatishana na watoto wake huku na huko kujipatia  chakula ,alikuwa na mbinu  za kipekee sana katika kujipatia chakula,  mbinu yake ya  kwanza ilikuwa ni kuamua  kwenda kukaa na watoto wake nje ya nyumba ambayo ameichagua  kwa siku  na  mwenye nyumba asipowapa chakula basi Chakwe na watoto wake hawawezi kuondoka.

Mbinu ya Chakwe kukaa  nje ya nyumba  ya watu   ilikuwa ikimsaidia sana , kwani watu wengi   kutokana  na ile hali ya kumnyanyapaa  yeye na watoto wake  ilibidi tu kuwapa chakula ili kuwaondosha  katika eneo lao.

Mbinu  yake nyingine ilikuwa ni ya kuiba , lakini mbinu hio haikumsaidia sana kukidhi mahitaji ya watoto wake wote kumi  ambao alikuwa nao  hivyo mbinu ambayo ilikuwa ikifanya kazi ni ile ya kupewa chakula.

Chakwe hakuwa na nyumba   ya kuishi hivyo hakuweza kupika  na mara nyingi sehemu ambayo waliishi ni  sehemu ambayo alijenga yeye mwenyewe kama hema  chini ya mti na kuishi na watoto wake.

Aliweza kujenga nyumba hio  kwa  kutumia   turubai ambalo  aliiba kwa mwanakijiji mmoja ambaye alikuwa akilitumia kufunikia matofali yake  na hata mwanakijiji huyo alipokuja kugundua Chakwe ndio alieiba hakuwa na la kufanya  zaidi ya kusamehe..

Baada ya wanakijiji kuona Chakwe alikuwa akiteseka na watoto wake ndipo wanakijiji hao wakiongozwa na mwenyekiti wao  waliamua kumpatia  Chakwe nyumba ambayo ilisemekana  alikuwa akiishi mwanaume ambaye hakuwa na familia , lakini mwanaume huyo alifariki  kwa kuwekewa sumu.

Nyumba ambayo Chakwe alipewa na wanakijiji hao ilikuwa mbali kidogo  na makazi ya  wanakijiji , yaani ilikuwa imejitenga kidogo lakini haikuwa mbali sana ,  ni nyumba ambayo ilikuwa karibu  sana na barabara ikizungukwa na miti,baada ya Chakwe kupewa nyumba hio angalau sasa  aliweza kupata sehemu ya kuwasitiri watoto wake.

Maisha ya  Chakwe na watoto wake ambao hawakufahamika majina yaliendelea ndani ya kijiji cha Kizwite kwa miezi  mitano kamili  na baada ya hapo ndipo  Chakwe na watoto wake walipokumbwa na janga la Asili  ambalo lilimuua yeye mwenyewe na  takribani watoto wake wote  kasoro mmoja tu.

Ilikuwa ni mwezi wa  masika yaani mwezi wa tano kwenda wa sita  ndani ya kijiji hicho  sasa usiku mmoja Chakwe akiwa amejisitiri  na watoto wake  ilipiga Radi ambayo haikuwa ya kawaida  katika nyumba ambayo alikuwa akiishi  Chakwe.

Kama ujuavyo Radi inavyotokea hupiga mara moja   au mara mbili  na kisha   hupotea  na  kuacha madhara basi hicho ndio kilichotokea.

Sasa  mara  baada ya Radi  ile kupiga  , yaani zikiwa zimepita kama dakika mbili kilionekana kivuli kikifika katika maeneo ya  nyumba ya Chakwe.

Alikuwa ni mtu  lakini mtu  huyo hakuonekana sura kutokana na mavazi yake ambayo alivaa  yalikuwa ni mavazi  flani kama ya kininja lakini hayakuwa ya kininja yalikuwa ni   mithili ya  mavazi ambayo kwa kingereza hufahamika kama Cloak, mavazi flani hivi kama majoho  ya rangi nyeusi ambayo  huunganishwa na kofia kama vile ni  Sweta lakini Kofia flani hivi ambayo mtu akijifunika huwezi kuona sura yake.

Sasa kivuli cha mtu huyo kilionekana hivyo  na  kwa namna mtu huyo alivyoweza kutokezea katika eneo hilo haikujulikana  ametokea upande  upi lakini aliweza tu kuonekana akiwa amesimama  pembeni ya nyumba ya Chakwe ambayo ilikuwa imeharibiwa na  Radi.

Yule mtu mara baada ya  kusimama kwa dakika kadhaa katika eneo hilo , akiwa anamulikwa na mwezi  uliokuwa ukitoa mwanga hafifu  alipiga hatua  kusogea mbele na sasa hata kile  alichovaa miguuni mwake kiliweza kuonekana , alikuwa amevalia  aina flani ya  buti  ndefu  za rangi nyeusi  mithili ya zile za mvua lakini hizo zilikuwa ni za kubana miguu  kiasi  na kisigino kirefu.

Nyumba ile haikuwa imeharibika  yote , upande mmoja ulikuwa umebomoka na mwingine ulikuwa umesimama  na yule mtu aliingia upande  ule uliosimama na ndani ya dakika chache tu  baada ya kupotelea kwenye  uharibifu ule wa nyumba aliweza tena kuonekana  kutokana na mbalamwezi,

Katika mikono yake alionekana akiwa amebeba kitu  na kwa  maelezo ya shuhuda ambaye aliweza kuona kila kitu anasema kwamba  mtu huyo alionekana  kama amebeba mtoto, kwa mara ya kwanza hakuweza kujua kama ni mtoto lakini  baada ya  wanakijiji kuweza kufika katika  nyumba hio ili kuangalia kama kuna aliebakia hai ndipo walipobaini  Chakwe mwenyewe  amekufa  na maiti yake ilionekana  pamoja na ya watoto tisa.

Shuhuda alieshuhudia kila kitu alikuwa ni mwanakijiji  wa hapo hapo  na anaendelea kusema kwamba baada ya yule mtu kutoka akiwa ameshikilia  mtu  palepale hakuweza kumuona tena , anasema ni kama vile  alipotea mara baada ya yeye kupepesa macho.

Haikuwa mara ya kwanza kwa watu  kufa   kwa kupigwa na radi lakini tukio la Chakwe lilizua gumzo , moja ya sababu ambayo ilipelekea kuzua gumzo ni  maelezo ya  mzee Kabwela  ambaye alishuhudia kila kitu , ukweli ni kwamba kwa stori yake hio alioelezea kuna ambao waliamini na kuna ambao hawakuamini ,walioamini   waliamini kutokana na  kutokuonekana kwa mwili wa  kumi wa mtoto wa Chakwe  mwenye asili ya kizungu na wale ambao hawakuamini ni kwasababu ya  stori ya Kabwela ambayo ilikuwa ni ya kufikirika.

“Mimi siwezi kuamini kabisa  , Mzee Kabwela ametupiga kamba labda alikuwa amelewa kama kawaida yake”

“Lakini  hata kama hamumuamini kutokana na tabia yake , je  vipi kuhusu kupotea kwa maiti nyingine?”

“Swali zuri Kizito,  huenda mtoto  hakulala na mama yake au  alipona na kukimbia”

“Mimi naamini  maneno yake , mambo mengi ya  ajabu yalitokea ambayo yalikosa maelezo  mpaka leo  hii  , naendelea kuamini kutokana na kwamba niliweza kuulizia katika kijiwe cha  pombe ambacho Mzee Kabwela hupendelea  kwenda na niliambiwa siku hio hakuweza kufika , hivyo moja kwa moja inaniaminisha kwamba siku hio hakulewa”

Yalikuwa ni malumbano ya  vijana  ambao walikuwa wakicheza Draft ndani ya kijiji  hicho ambao walikuwa wakizungumzia tukio  lililotokea  juzi yake mara baada ya kukamilisha kumzika Chakwe na watoto wake.

Vifo vya watu kumi  na moja wa kijiji hiko vilizua  gumzo sio kwa wanakijiji tu lakini  hadi kwa taifa mara baada ya kutangazwa katika  vyombo  vya habari, huku  maelezo ya  Shuhuda Mzee Kabwela yakiamsha  msisimko wa hali ya juu.

Ukweli ni kwamba kila   watu waliokuwa wakiongelea tukio hilo na hata baadhi ya waandishi wa  habari waliweza kufika katika kijiji hicho na kujaribu kuwahoji wananchi  na  habari walizoambiwa zilikuwa zikichanganya kidogo lakini kutokana na kutumia usomi  wao  kuna wengine ambao waliondoka kwa kuona  maelezo ya wanakijiji hao  hayakuwa na mantiki na kuna wengine waliweza kuamini kutokana na sifa kuu ya  vijiji vingi vya Sumbawanga kwa kusifika na uchawi,

Hata wanakijiji wengine walienda mbali na kusema   kwamba  huenda hata radi hio ilikuwa ni ile ya kutengenezwa na walozi wakubwa wa kijiji hicho lakini  hata hicyo hakukuwa na ushahidi wa moja kwa moja, hivyo jalada la  tukio hilo likafungwa  rasmi na  tukio likasahaulika.

******

Hamza ambaye alikuwa kwenye gari alikuwa akikumbuka  kwa uchache sana maisha ya utoto wake , yaani   yeye na  mama yake na ndugu zake , alikuwa akikumbuka  kabisa  alikuwa na wadogo zake wengi na walikuwa na maisha magumu sana  , maisha ya kutanga tanga huku na huko wakimfuata mama yake, Hamza anakumbuka kabisa  katika akili zake  japo kwa uchache katika watoto wa mama yake yeye ndio aliekuwa mkubwa  , ambaye kwa kiasi  flani alikuwa akijitambua kutokana na kuwa wa kwanza , kumbukumbu zake nyingine ambazo alikuwa akikumbuka  ni namna ambavyo aliweza   kushuhudia  namna  wadogo zake walivyopoteza  maisha mara baada ya  kumulikwa na mwanga wa  ajabu.

Hamza hakukumbuka kwa usahihi sana kuhusu maisha yake ya utoto lakini baadhi ya kumbukumbu ambazo zilikuwa ngumu   aliweza kuzikumbuka, hakuwa akijua alikuwa na miaka mingapi katika kumbuukumbu zake za utoto akiwa na mama yake.

Baada ua  janga la asili kumkumba  Hamza na kusalimika maisha yake  yaligeuka  na kuwa msururu wa matukio ya kusisimua sana , huku mtu anaefahamika kwa jina la Mzee akichukua nafasi kubwa katika  msururu wa matukio hayo.

******

Hamza hakuwa akishukia kituo cha karibu na chuoni kwake,  ni utaratibu aliokuwa amejijengea , alipenda kuchangamsha mwili wake kwa kutembea umbali mrefu kidogo

Sasa mara baada ya kushuka wakati akiwa anatembea  kando ya barabara akipishana na watu wengi  ambao walikuwa katika harakati za maisha  palepale alijikuta akiitwa kwa nyuma na sauti ambayo alikuwa akiitambua .

Nyuma ya Hamza alionekana  kijana wa rika lake aliekuwa amevalia suruali ya kitambaa nyeusi , shati  la rangi   ya mikono mirefu  jeupe  na  moka ya rangi ya  kahawia , alikuwa amependeza kwa namna ambavyo alikuwa amechomekea  ukijumlisha na mwonekano wake kwa ujumla , alikuwa  na kila sababu ya kuitwa mwanaume mtanashati au  Handsome , kama utamfananisha na Hamza basi  moja kwa moja  kijana huyo angeshinda upande wa nanmna mavazi yake yalivyo lakini katika upande wa sura ilioumbwa vyema   Hamza alikuwa akichukua nafasi kubwa.

Hamza  alikuwa  na mchanganyiko wa rangi na  kwa kumuangalia tu kwa haraka haraka lazima ungejua   ni mchanganyiki wa mzungu na mwafirka, kinachomfanya Hamza kutoonekana wa kuvutia ni namna ambavyo anajiweka , alikuwa akivaa kawaida sana  pengine kuliko mwanafunzi yoyote wa chuo cha FEMU na hilo lilimfanya  kuonekana wa kawaida sana macho ya  watu wengi.

“Muuza vyungu  mwenyewe   nakuona kama kawaida yako”Aliongea Hamza huku akiuonyesha tabasamu kwa rafiki yake afahamikae kwa jina la Alex..

“Kwa  namna ambavyo unataongea , ni kama kazi ninayofanya  ni ya hali ya chini ,  lakiini ukawaida unaoniona  nao leo ndio unatokana na kazi yangu”Aliongea na kumfanya Hamza kutoa tabasamu la  uchungu na kuendelea kutembea.

“Imekuwaje leo  hii ukatembea kwa miguu, nilitegemea  muda kama huu  upo njiani ukiwa umempa mtoto  wa kike lift”

“Hahaha.. sio kila siku nampa mwanamke lift  siku nyingine ni washikaji kama nyie ,  gari imezingua  kuwaka asubuhi  ya leo, nimekuja kwa lift  kutoka kwa jirani yangu na aliniacha kule  upande wa chini ndio maana  nikaamua kutembea tu”Aliongea Alex  na kumfanya Hamza kutingisha kichwa.

Baada ya kukaribia getini Alex aliungana na watu wengine waliokuwa wakimfahamu na kuingia huku wakiongea kwa kucheka  lakini  kwa  upande wa Hamza alionekana kuwa na mawazo yake kichwani kwani hakujichanganya katika stori za watu hao ambazo mara nyingi zilihusisha wanawake.

Hamza alikuwa na   muda mrefu kidogo  tokea aanze kusoma ndani ya chuo hicho lakini mpaka kipindi hicho hakuwa amezoeana na watu wengi , pengine ni kutokana na   hulka yake  ya ukimya.

Licha ya Hamza kufahamiana na Alex  ukaribu wao huwezi kusema ni  ule wa kirafiki, ukweli ni kwamba Alex alikuwa ni mcheshi mno kiasi cha kuongea na kila moja na kucheka nae , alikuwa amezoeana karibia na darasa zima.

Umaarufu wa Alex ndani ya chuo hicho hutokana na biashara yake ya uuzaji wa vyungu  vya aina mbalimbali , Alex alikuwa akihusika katika uuzaji wa vyungu  vya kupikia , vyungu vya kuwekewa maua  ambavyo vina urembo wa aina yake na  bidhaa nyingine za aina hio  na hili ndio ambalo lilimpatia umarufu kwani biashara yake ilikuwa sio ya kawaida  na imekaa vibaya lakini ukweli ni kwamba ndio biashara ambayo ilimfanya Alex kuonekana mtu mwenye pesa  na  alikuwa akimiliki kabisa  gari aina ya  IST gari ambayo ilimpatia umaarufu na kufanya ashobokewe na  wanawake wengi chuoni.

“Alex mambo?”Sauti nyororo  iliweza kusikika  nyuma ya  vijana wa kiume wa chuo  hicho cha FEMU akiwemo  Hamza ambaye muda wote alionekana kuwa kimya  akiwa sio mwenye kusikiliza stori za  wenzake.

“Anitha..!!!”

Alex aliitikia kwa kubabaika  kiasi  huku  kundi la wenzake  likikaa kimya kumwangalia  mrembo Anitha.

Alikuwa ni mwanadada mrembo  mno , huenda ndio ambaye alikuwa akishika namba moja  kwa uzuri  ndani ya chuo chote cha FEMU  ni mwanadada huyo huyo ambaye alimfanya Hamza kuwa maarufu ndani  ya  chuo cha FEMU.

“Niambie  mamii ,, uko poa?”Aliongea Alex kwa mbwembwe huku akianza kulamba midomo yake  na kusugua sugua mikono  kiswaga  na kumfanya Anita kutabasamu  kiasi cha kupelekea mashavu  yake  kutengeneza vishimo.

“Niko poa”Alijibu Anitha huku akiangalia kundi la watu hao na ilishangaza kwamba licha ya   wanaume waliokuwa wametangulizan na Alex kuwa  wanadarasa lakini hakujihangaisha kusalimiana nao , lakini hata hivyo ni jambo la kueleweka.

Hakuna ambaye hakuwa akijua  tabia ya maringo aliokuwa nayo Anitha  ndani ya chuo hicho  na  ni kupitia maringo hayo ndio yaliomfanya  Hamza kudhalilika na kujipatia umaarufu wa aina yake baada ya kukataliwa waziwazi.

Anitha alionekana kuwa na maongezi na Alex  hivyo wale wengine kila mmoja alijiongeza na kupiga hatua za kuelekea  darasani , isitoshe   ni muda mfupi uliobaki  mpaka kipindi kuanza.

*******

Shauku ni msingi  wa kitabia  ambao ni muhimu  kwa binadamu kuwa nao  ili kumuwezesha kujifunza  na  kukua.

Tukiwa na shauku  inatupelekea kupata motisha ya kujifunza vitu  vipya  jambo ambalo linaweza kutupelekea kupata gunduzi za vitu  vingine vipya ambavyo hatujawahi kuvifikiria.

Shauku ya muda mfupi inaweza kukupeleka kupata shauku ya muda mrefu  na mwisho wa siku kujibu maswali  uliokuwa ukijiuliza kwa muda mrefu, kwa mfano unaweza ukawa na  shauku  ya  kumjua mtu  kwasababu  mtandaoni kaandika jambo  ambalo ni fikirishi  mwisho wa siku shauku yako inakupa motisha ya kutaka kuonana na huyo mtu  na anakuelezea kwanini aliandika vile    na katika maneno yake unajikuta unapata kitu kipya ambacho  hujawahi kufikiria na shauku nyingine kuanza.

Ni muhimu kuwa na shauku inayoendana na vipaumbele vyetu ili tuweze  kukua na kujifunza zaidi na zaidi na mwisho wa siku kuyafikia  mafanikio.

Kumbuka  kila kitu kilianza kama shauku  na shauku ikaibua mawazo na hatimae ikaipelekea dunia  kuwa kama inavyoonekana leo.

“Paaa.. Paaah”Wanafunzi walijikuta wakipiga makofi ya  nguvu.

Alikuwa ni Profesa Issai Stephano  a.k. a  Mr Bonus point, alikuwa amepewa jina hilo la utani  kutokana na  mwishoni mwa kipindi chake   lazima atoe ushauri nje ya somo lake  kwa wanafunzi wake ambao mwenyewe anaita Bonus  point na  siku hio alikuwa akielezea kuhusu Shauku.

Ijapokuwa  mara nyingi mwishoni   mwa kipindi chake aliongea kama utani lakini maneno yake  yalikuwa   na maana kubwa  kwa wale ambao walikuwa wakimchukulia siriasi.

Katika watu ambao walikuwa wakipenda  kipindi chake kiishe na kuweza kusikiliza Bonus Point ni  Hamza , alipenda sana kumsikiliza Profesa Stephano kwani maneno yake licha ya kuyaweka  kimatani zaidi lakini  alikuwa akifikisha ujumbe  wenye maana nzito ambayo kwa mtu  aliekuwa siriasi kwa kile anachoelezea basi  pengine  angepiga hatua kubwa katika ukuaji wa kifikra.

Hamza  wakati  wenzake wakitawanyika katika ukumbi kwa ajili ya kusubiria kipindi kingine , yeye alikuwa akifikiria neno Shauku , maneno ya Profesa  Stephano ni kama yamegusa kile kinachoendelea katika maisha yake.

“Ili kutimiza shauku yako ya muda mrefu  unapaswa kufanyia kazi shauku yako ya muda mfupi , pengine majibu utakayoyapata kwenye shauku yako  ya muda    mfupi ndio mlango wa kutimiza shauku yako ya muda mrefu”Maneno hayo yalijirudia rudia katika kichwa chake.

“Shauku yangu ya muda mfupi kwa sasa ni ipi?”Alijiuliza Hamza  lakini alishindwa kujibu swali lake mara baada ya kuja kushituliwa na moja wapo  ya rafiki yake wa karibu afahamikae kwa jina la Amiri  au Pacha mdogo.

“Mzee unawaza  nini  tena , ushasahau mpango wetu wa jana?”Aliuliza Amiri mara baada ya kumsogelea Hamza.

“Hamna  nilikuwa nayawazia maneno ya  Profesa , yanaonekana kuwa na uhalisia”

“Hahaha… Profesa watu wanamchukulia kama  mzee wa Komedi kwa aina yake ya ufundishaji lakini yule mzee ni mtu ambaye  ana uzoefu  wa mambo mengi, kuna  tetesi ambazo  nimesikia  pia jamaa  inasemekana ni jasusi mstaafu”Aliongea Amiri  na kumfanya Hamza kumwangalia kwa  mshangao.

“Unasema kweli?”

“Nimesema ni tetesi  tu mzee ,  kama swali lako ni kuthibitisha hizo tetesi basi  naweza kukujibu  ndio,  ni tetesi  ambazo zinazungumzwa na  watu wengi”Aliongea  na kumfanya  Hamza kutoa tabasamu la uchungu na aliona  ameuliza swali la kijinga.

“Oya  halafu mwana unaonekana kuwa na mawazo mengi  ujue , vipi tunaenda  au hatuendi?”Aliuliza Amiri mara baada ya kuona  utayari mdogo wa Hamza.

“Tunaenda  ili mradi tu malipo yawe ya uhakika”

“Haha.. hilo  ondoa shaka   ili mradi  tu ufanye kazi kama ulivyosema maana  bado hata siamini kama unaweza  tengeneza”

“Siwezi kusema  naweza halafu nikashindwa, ongoza njia tuondoke”Aliongea na  Amiri alitabasamu na kisha walianza kutoka  kwenye Hall 5 hiio  kupitia mlango wa nyuma na kutoka.

Dakika chache mbele   walitokea katika maegesho ya chuo  ya muda mfupi  na kusogelea gari aina ya Ford.

Ilikuwa ni gari ambayo  anatumia Amiri ambayo ni ya kwake kabisa , Amiri  hakuonekana mnyonge, ijapokuwa alikuwa akisoma chuo cha   kawaida kama hicho lakini maisha yake yalikuwa  ni yale ya juu   lakini licha ya hivyo   hakua akibagua watu wa kufanya nao urafiki.

Pengine  kutokana na maisha yake ya juu angechagua marafiki wenye  pesa  kama yeye lakini ajabu alimchagua Hamza kama moja wapo ya marafiki zake ,

Kwa mara ya kwanza Hamza na  Amiri kujenga urafiki wao ni siku ambayo  Hamza alitokea kuweka wazi hisia zake  mbele ya mrembo Anitha, Hamza anakumbuka siku  kilichompelekea mpaka kuweka hisia zake wazi  ni  kutokana na kuamua kutumia  Bonus Point zilizotolewa mwisho wa kipindi na Profesa Singano.

Pointi ambazo zilimpa ujasiri Hamza  na kuomba kuongea na  Anitha pembeni na kumweleza hisia zake  kwamba anampenda na bla blah kibao lakini mwisho wa siku Hamza aliambulia kejeli  na  kusonywa tena mbele ya Kadamnasi ya  wanafunzi  wenzake , ilikuwa ni kama vile  Anitha alimfanyia makusudi kwani licha ya kwamba  alikuwa na uwezo wa kumjibu kistaarabu lakini mwisho wa siku akaamua kumjibu kwa sauti kubwa  ili mradi tu  kumdhalilisha huku akimwita  Hamza mtu masikini ambaye hana hadhi kabisa ya kutoka na yeye kimapenzi  na aende kutafuta wa hadhi yake.

Amiri ambaye alikuwa ni sehemu ya wanafunzi  hakuchulia swala la Hamza  kama la aibu bali alichukua katika upande wa Chanya  na kumuona Hamza kama mtu jasiri  hususani  pale alipoweza kumsikia Hamza na yeye kiropoka mara baada ya kukataliwa na kumwambia Anitha:

“Anitha unaweza usinipende leo , lakini  mimi ni mbishi kufa  na siku moja  wewe mwenyewe ndio utanifuata na kutaka  mahusiano na mimi , ndio itakuwa wakati wangu wa kukukataa”Aliongea Hamza bila ya aibu na kisha  akapangua watu  na kuondoka.

……..

“Oya mzee sasa  sikia  , inshu niliokuambia  jana  ni complex kidogo  lakini malipo yake ni ya kueleweka”

“Unamaanisha nini , si kufunga tu kwanini iwe Complex?”Aliuliza  Hamza kwa mshangao kidogo.

“Ni kama nilivyokuambia Kamera ambazo unapaswa kufunga ni za siri sana  na anaeishi hapaswi kujua”Aliongea   na kumfanya sasa Hamza kuelewa  anachotaka kumaanisha.

“Kwahio unamaanisha  unataka nikusaidie kufunga spy Camera?”

“Ndio  nilichokuwa nikimaanisha , najua tulikubaliana ni kufunga tu kamera lakini sijakuambia ni  wapi  na  kwa ajili   gani ,  ndio maana nikasema ni inshu Complex lakini  ambayo ina malipo makubwa kama utafanikisha”

Kwa jinsi ambavyo Amiri alikuwa akiongea ilimfanya Hamza kuona pengine  hamjui vizuri rafiki yake kwani ombi  lake lilionekana kuwa na utata lakini ambalo limekaa kijasusi zaidi.

“Amiri kama ndio ulikuwa mpango wako  najitoa  , nina shida kweli ya pesa lakini  vipi kuhusu usalama wangu , ninaweza kufanya kama unavyotaka lakini kama itagundulika ni mimi inaweza kuniletea matatizo”Aliongea Hamza.

Ukweli ni kwamba  siku ya jana mchana  Amiri alimuuliza Hamza kama alikuwa na ujuzi wowote wa kufunga CCTV Kamera  amsaidie na  Hamza alimjibu Amiri kwamba alikuwa na uwezo huo   jibu ambalo lilimfurahisha sana Amiri na kumwambia kwamba kuna kazi anataka kumpatia  na ina malipo mazuri kama tu atamsaidai katika jambo hilo.

Hamza alimwambia atamsaidia kwasababu ni rafiki yake lakini Amiri akagoma na kusema lazima amlipe  na Hamza mara baada ya kuona Amiri  analazimisha malipo hakutaka kukataa isitoshe alikuwa na shida ya pesa.

Sasa   walikubaliana kesho yake ambayo ndio siku hio  sasa , lakini ajabu ni kwamba Amiri anampatia Hamza maelezo tofauti  na  ya jana yake na kusema  Kamera ambazo anapaswa kufunga ni Spy Camera , yaani sio kamera za ulinzi bali kamera za  kiuchunguzi tena  katika nyumba ya mtu, jambo hilo linamfanya Hamza kuona ni swala la hatari kwani inaweza ikabainika yeye ndio muhusika na kujiingiza  matatizoni.

“Sikia  Hamza  najua ni kweli nimekuahidi malipo , lakini nimekuchagua kunisaidia hii kazi kwasababu wewe ni rafiki yangu , kuna  kitu muhimu sana  nataka kufatilia   ili niweze kupata   majibu ya  wasiwasi wangu na shauku ya muda mrefu”

“Shauku gani na majibu gani?”Aliuliza.

“Ni stori ndefu  rafiki yangu , lakini jua ni maswala ya kimapenzi ndio yananifanya niende mbali namna hii,  nataka Kamera hizi zifungwe katika  Apartment anayoishi demu wangu , kuna vitu  ambavyo  sivielewi kuhusu Mellisa  ndio maana”Aliongea huku akianza kutia huruma kidogo.

“Kama nitakuwa sawa basi naweza kusema   ni kwamba humuamini mpenzi wako , lakini  sidhani kama kufunga Kamera sehemu anayoishi inaweza kukupa majibu  ya kile unachokitaka ,  wenzako  sehemu ambayo wanatakiwa kuweka  umakini ni kwenye simu   na sio  mambo ya Kamera”

“Upo sahihi  , lakini hayo unayoyasema ni kwamba nishayafanya tayari na ni mwaka sasa  tokea nianze kumfatilia Mellisa kuhusu mawasiliano yake  lakini sijawahi kuona kitu  cha tofauti  lakini bado  hisia zangu zinaniambia Mellisa ananisaliti  tena  ananisaliti ndani ya  nyumba ambayo nimempangishia mimi , Bro hebu nisaidie katika hili ni swala la dakika chache tu  kulifanya na mimi lazima nikulipe” Aliongea  na kumfanya  Hamza kuanza kukuna kicha chake kwa namna flani alianza kumwelewa  Amiri   lakini bado kuna kitu hakipo sawa katika maelezo yake.

“Kama ni hivyo  hisia zako zinakuambia nini  na kwa nini ubahisi  anakusaliti  ndani ya nyumba  uliompangishia ,  kuna viashiria vyovyote  ambavyo umevipata?”

“Ni stori ndefu  ambayo ina mlolongo wa matukio   ambayo hata kama nitakuelezea hapa huwezi kunielewa  bro , ila  ninachojua ni kwamba  Mellisa ananisaliti  tena usaliti anaufanyia  ndani ya Apartment niliompangia mimi , sina uhakika wa hisia zangu na  hizo Kamera  zitanipa majibu  ya  kile ninachotafuta , Bro  nikipata ushahidi wa hisia zangu  nitakuambia kila kitu kwasasa naomba unisaidie”

Amiri alimbembeleza Hamza  kwa kila namna  ili tu aweze kumsaidia  na mwisho wa siku Hamza alikubali , isitoshe  Amiri alikuwa amemsaidia katika mambo mengi  sana  ambayo yalihitaji pesa.

“Okey nitakusaidia   katika hili lakini lazima tukubaliane jambo moja”

“Nipo  tayari kukubaliana na chochote unachotaka , Hamza ili mradi tu  unisaidie  katika hili”Aliongea  Amiri  na kumfanya Hamza kutoa tabasamu la uchungu.

“Sikia nitakusaidia lakini sihitaji malipo  ya aina yoyote ile”Aliongea na kumfanya  Amiri kushangaa kidogo lakini alijikuta akilipukwa na furaha isiokuwa ya kawaida  haikuwa furaha kwamba  hatolipa bali ni furaha kwamba  ataweza kufungiwa hizo Kamera maana Amiri hakuwa na shida  ndogo ndogo za pesa.

Previoua Next