Reader Settings

Iliwachukua  muda mchache sana  kwa Amiri na Hamza kufika  mwisho wa safari yao , katika maikazi ambayo  anaishi mpenzi wake   Amiri  afahamikae kwa jina la Mellisa.

Ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Hamza kufika  ndani ya hili eneo   na lilikuwa likivutia mno kama sifa zake zilivyokuwa zikivuma  kwa watu wengi  ndani ya jiji la Dar es salaam.

Ni moja wapo ya Apartment ambazo zinamilikiwa  na kampuni ya kimataifa ya  Dosam Global.

Kwa  machache ambayo alikuwa akijua Hamza kuhusu kampuni yaDosam ni kwamba ilikuwa ni kampuni  namba moja Afrika ambayo  inajihusisha na maswala ya mahoteli na Real estate  ambayo  makao makuu yake ni  hapa nchini.

Dosam ni kampuni namba mbili kwa ukubwa ukiachana na kampuni ya Vexto group ambayo imeweza kuwa na biashara karibia kila kona ya Dunia, ndio kampuni ya Kitanzania ambayo imeorodheshwa katika Nasdaq.

“Bro hii sehemu ni nzuri sijapata ona”Aliongea Hamza mara baada ya  kuruhusiwa kuingia  na watu wa usalama wa eneo hilo.

“Ni sehemu ya hadhi ya juu hii broo, asilimia kubwa wanao ishi hapa ni aidha michepuko ya vigogo wakubwa serikalini  au familia zinazojiweza kiuchumi”Aliongea Amiri huku akiweka tabasamu la kirafiki.

Hamza aliishia kutingisha kichwa huku akizungusha kichwa  kulia na  kushoto akijaribu kushangaa mazingira.

Ndani ya jiji la Dar es saalam kuna apartment  nyingi tu ambazo zina mazingira ya juu lakini ukizungumzia Apartment hii ya Dosam’s Homes sio  tu ukubwa wa  jengo  hilo bali ni  uzuri wa jengo lenyewe , usanifu wake ulikuwa ni ule wa  ulioendelea  na pengine ndio jengo la makazi lenye mvuto mkubwa ndani ya Afrika nzima.

Hamza alijiambiaAmiri alikuwa na haki ya kuwa na wivu na  mpenzi wake kama kweli amempangishia hili eneo.

“Bro hapa   kwa mwezi   malipo yake yakoje?”

“Kwa mwezi hapa ni  doller elfu tano”Aliongea Amiri    bila wasiwasi lakini bei yake ilimfanya  Hamza kushindwa kupumua vizuri maana kwa haraka haraka pesa hio kama ikibadilishwa kwenda hela za kitanzania ni zaidi ya milioni  kumi na mbili.

Pesa hio  kwake ingeweza kumtosha  kutatua changamoto zake zote  hata  kuanzisha biashara  ambayo itaweza kumsaidia kwenye maisha  yake ya hapo jijini Dar es salaam.

Dakika ambayo  wanasubiria mlango wa  lift kuweza kufunguka waliweza kukutana na harufu nzuri ya marashi na Hamza mara baada ya kuangalia mbele aliweza kukutanisha macho yake na mwanamke mmoja mwenye urembo wa ajabu mno  ni aina flani ya wanawake ambao ni ngumu sana kuwaona mtaani , aliishia kujisemea Mungu anajua kuumba  maana  ni kama macho yake yanamdanganya na mwanamke huyo alikuwa akimuona ndotoni.

“Broo !!!, Oya Hamza!!”

“Eeh..!!”Hamza alijikuta akishikwa na mshangao  na  aliishia kujifikicha macho  na kisha akatumbukia kwenye Lift huku yule mwanamke mrembo   wa rangi ya chocolate akitoa tabasamu la dhihaka na kumpita Hamza kama kituko.

Alionekana ni wale wanawake ambao  washazoea  kushangawa na wanaume kutokana na urembo wao.

“Hahaha…. Bro  naona mtoto kakuchanganya mpaka  ukawa unaota?”Aliongea Amiri huku akishindwa kujizuia kucheka.

“Bro  huyo manzi sio  wa kawaida, nilidhani naangaliana na jini”

“Hahaha..huyo ni demu wa kawaida mbona ,  halafu mwanangu usihadaike na huo uzuri ni wa  kutengeneza”

“Unamaanisha nini wa kutengeneza?”

“Namaanisha  sio wa kuzaliwa nao , huyo manzi  uliepishana nao  nimemjua vizuri sana kupitia Mellisa, kwa  habari za chini nasikia anafanya kazi  Binamu Island”Aliongea  Amiri kwa sauti  ya  chini kama vile  jambo analoongea ni  la  usiri na usiriasi.

“Binamu Island !!?”Aliongea Hamza kwa mshangao kidogo na palepale macho yake  yaliongezeka ukubwa.

Hamza  alikuwa na taarifa chache sana kuhusu Kisiwa cha Binamu(Binamu Island) ,  taarifa chache alizokuwa nazo kuhusu kisiwa hicho ni kwamba kwanza kabisa ni cha kutengeneza  ambacho  kinapatikana bahari ya Hindi karibu kabisa na jiji la  Dar es salaam.

Kwa  fununu ambazo aliweza kusikia ni kwamba  kisiwa hicho  muda unafanya kazi tofauti na nje ya dunia(Timeless island),  ni uzushi ambao kwenye maisha yake  hajawahi kukubaliana nao hata mara  mara moja.

Siku ambayo aliweza kusikia habari hizo kwanza alicheka na kujiambia waru wanadanganyika  kirahisi  sana ili tu kuweza kwenda kutembelea katika eneo hilo.

Ukiachana na fununu ambazo  anasikia Hamza ukweli ni kwamba Kisiwa hicho kipo   kabisa na  kimejibebea jina kwa zaidi ya miongo kumi  dunia nzima  na kimekuwa chanzo cha kuendelea kwa  mataifa ya Afrika mashariki  kutokana na kutembelewa sana ,kimekuwa kivutio kikubwa sana kwa watalii.

Kwa maelezo machache ni kwamba   sio watu wote ambao walikuwa na uwezo wa kufika katika kisiwa hicho kwani  ni gharama kubwa sana.

“Nimesikia hivyo bro lakini bado siamini , mimi mwenyewe  pamoja na kuwa na hela sijawahi kufika katika hiki kisiwa   , lakini kwa upande mwingine naweza kumuamini Mellisa kwani maisha ya Tresha  ambayo anayaishi hapa jijini sio ya kawaida”

“Tresha ndio nani?”Aliuliza Hamza muda huo mlango wa Lift ukifunguka na kuwaruhusu kutoka.

“Ni huyo mrembo uliekutana nae kule chini , anafahamika kwa jina la Tresha Noah ni maarufu sana mtandaoni”Aliongea na kumfanya Hamza kutingisha kichwa vhake kumwelewa.

Asilimia kubwa ya   wakazi wa  hili jengo   kwa muda huo wanakuwa kazini na  hata wale wachache wanaobaki majumbani ilikuwa ni ngumu sana kuonana nao nyakati za muda huo  nadhani  ndio maana  Amiri akachagua kazi yake kufanyika  katika wakati huo.

Baada ya kutembea umbali mfupi walisimama kwenye Apartment namba 103  na Amiri alitumia ‘pasword’ kufungua mlango huo  na kisha  wote wakaingia.

Hawakuwa wamesahau  vifaa vya kazi  kwani Amiri alikuwa amebeba begi kubwa wakati huo huku na  Hamza mwenyewe akiwa na  begi dogo.

Hamza mara baada ya kuingia ndani  aliishia kutingicha kichwa na kujiambia kuna watu wanaishi pazuri , ijapokuwa  watanzania wengi walikuwa wakidharau  kuishi   katika  nyumba za kupanga aina ya Apartment  lakini ufahari uliokuwemo humo ndani ulimpa msukumo  na yeye siku moja kuweza  kuishi katika mazingira kama hayo.

Hamza kama kawaida yake mara baada ya kuingia eneo la ndani alianza kukagua sebule hio na macho yake yalikuja kutua katika  picha mbao yenye  kuonyesha sura ya mwanamke mrembo ilioning’inizwa ukutani.

“Oya huyu ndio demu wako?”Aliuliza Hamza.

“Ndio huyo babu , unamuonaje?”

“Aisee ni kisu hata zaidi ya yule Tresha?”

“Hahaha,.. bro sipingani na wewe  , Mellisa ni mzuri kuliko unavymuona kwenye hio picha , ukimuona laivu ndio utajua yule Tresha ni wa kawaida  sana halafu Mellisa yeye uzuri wake ni wa asili sio wa kutengeneza”Aliongea Amiri kwa kujigamba.

“Ndio maana hujiamini?”

“Hehe ,, bro  hata ni wewe ungekosa amani, nina pesa na  namtimizia kila kitu lakini bado tu siamini kama ananipenda na hatonisaliti, isitoshe  pia aina ya kazi yake  inamkutanisha na vibopa zaidi yangu”

“Anafanya kazi  gani?”

“Ni meneja wa benki  ya Dosam Commercial Bank(DCB)  tawi la Ubungo”Aliongea na kumfanya Hamza kushangaa kidogo.

“Anaonekana amepiga hatua katika maendeleo binafsi, naweza kusema haumhudumii kwa kila kitu, maana  kwa ninavyojua wafanyakazi wa Dosam sio  kama wafanyakazi wa  mabenki mengine”

“Hicho ndio kinachonitia wasiwasi bro Mellisa hanitegemei kwa kila kitu  hana njaa na mengine namfanyia  kwasababu  ni mapenzi, ukumbuke  pesa  ya mwanamke katika mahusiano   pia haina thamani na wanajali sana wanachopewa  kuliko wanachonunua”

“Haha uko sahihi”Aliongea Hamza huku akimuonea wivu  Amiri  kuwa na mwanamke mrembo  mwenye mafanikio kama  Mellisa,alijiambia yeye kama mwanamke  wa kawaida kama Anitha amemshindwa ndio atafanikisha kwa  Mellisa.

Ijapokuwa maelezo ya Amiri yalimwambia Mellisa ni  mzuri zaidi kuliko anavyoonekena kwenye picha lakini kwa haraka haraka alimuona ni mzuri zaidi kuliko  Anitha mwanamke ambaye alijaribishia  bahati yake na akamdhalilisha mbele za watu  kwa  kejeli huku akimwambia  ananuka  umasikini.

Hamza  mara baada  ya kukumbuka  matusi ya Anitha  alijikuta akijichekea moyoni  na kuachana na mwazo hayo na kisha alianza kufanya  uchunguzi wa namna ya kufanya kazi yake.

“Bro unaonaje  hapa , nataka picha kwanzia chumbani  kwake mpaka hapa eneo la sebuleni , nataka kila kinachofanyika hapa  niweze kukiona kupitia simu  yangu”Aliongea  na kumfanya Hamza sasa kuona kuna kitu  hajakifikiri.

“Hizo ni Camera aina gani umenunua?”

“Ni IP Camera , vipi kuna tatizo?”

“Kama ni hizo hakuna tatizo, unachotaka kinawezekana”Aliongea huku akifungua mfuko  wa  vifaa na kuchunguza kamera hizo za kiuchunguzi  na palepale Hamza alianza kufanya vipimo vyake kwa  kutumia Angle ,ili kuweza kufunga Camera hizo kwa siri

Hamnza aliomba aonyeshwe na eneo la chumbani ili kuanza kazi yake  na  Amiri   hakupimgas na  waliingia wote chumbani na baada ya Hamza kuridhika alianza kazi  yake ya ufundi, alifanya kazi kwa spidi kubwa mno huku akimuagiza  Amiri kumpatia  kila   anachohitaji.

Amiri kwa upande wake  alijikuta akimshangaa tu Hamza na kujiuliza ujuzi huo Hamza katolea wapi , ijapokuwa  alikuwa akijua anaiweza kazi   hakutegemea kama anaweza kuwa mtaalamu hivyo kwani ilikuwa ni kama anaangalia filamu za kijasusi,  ndani ya dakika ishirini  tu kila kitu kipo tayari  na  Hamza alirudisha mazingira sawa kama yalivyokuwa na kumwambia  Amiri akague kama anaweza kugundua   na mara baada ya Amrii   kuangalia   matokeo yake yalizidi  matarajio aliokuwa ameyaweka kwa Hamza.

“Bro sijategemea kama kazi ingekuwa nyepesi kwako  kiasi hichi , unaonekana ni mtaalamu wa hali ya juu”Aliongea Amiri huku akitoa mwanya wake nje lakini kwa wakati mmoja akimwangalia Hamza kwa wasiwasi na kujiambia pengine bwana huyo anajifanyisha kuishi maisha ya chini   tu  na ni mtu mwenye historia  yake..

“Kaka sisi ambao maisha yetu  ni ya chini tunajitahidi kujifunza  aina mbalimbali za ujuzi ili tu tusiweze kupitwa na fursa , kwa wewe  ambaye maisha yako  yana msingi mzuri huwezi kunielewa”Aliongea Hamza na  kumfanya Amiri kutoa tabasamu kwani maneno yake hayakuwa  mbali na ukweli.

Yeye amezaliwa katika familia ambayo ilikuwa  na kipato cha juu , hivyo ni rahisi kusema utajiri ameukuta  na hata  anachokisomea ni kwa ajili tu ya kuendeleza mali, kwake shida yake  kubwa pengine ni maswala ya kimapenzi tu lakini likija swala la  pesa alikuwa vizuri.

Baada ya kukamilisha kazi Hamza alimwambia kazi nyingine wanaweza kuifanyia mbali na  eneo hilo  kumsaidia kuseti kila kitu kuweza kuonekana kwa vifaa vya mbali na Amiri hakuwa na shida.

“Kwahio kwanzia hapa  nitaweza kuona kila kitu?”

“Yeah zile ni aina ya Camera ambazo zinatuma teknolojia  ya live streaming na zinatuma vidio   kwako  kwa njia ya internet, ni rahisi  kuunganisha  kupitia   tarakishi kuliko hio simu yako ya Apple, unapaswa kuwa na  Android tuweze  ku install Apk maalumu ili kufanya configuration ya RTSP”Aliongea Hamza.

“Ninayo hapa hapa  simu ya Android”Aliongea na palepale alifungua mkebe wa gari na kutoa simu janja kampuni ya Sumsung tole jipya na kumpatia Hamza.

Hamza  alitumia dakika chache tu  aliweza kumuunganishia Amiri kila kitu  na kumpa aangalie  na bwana huyo mara baada ya kuona mitambo imekaa vizuri alijikuta  akishindwa kuzuia furaha yake.

“Mellisa japo  nakuamini lakini   kwa mapenzi yangu kwako  nimeona niende mbali hivi , utanisamehe lakini  naheshimu hisia zangu, naomba unithibitishie  ninachowaza sio cha kweli”AluwazaAmiri huku akiangaalia mazingira ya eneo la Sebuleni kwa Mellisa na ndani  chumbani wake.

“Hamza shukrani sana  kwa  msaada wako mzee , ukiachana na hisia zangu mbaya zidi ya Mellisa  lakini  kama  ni kweli nina shauku ya kutaka kumuona mwanaume  anaenisaliti nae”

“Nadhani unajitafutia maumivu ya moyo tu  ndugu yangu?”

“Ni kweli unachosema , lakini nimewekeza hisia zangu  nyingi kwa yule mtoto nampenda kuliko hata neno lenyewe , najua ninachofanya ni hatari lakini najua nini nitafanya hata kama nnikigundua ananisaliti ,  ila nikwambie  tu Mellisa ni mwanamke ambaye siwezi kumuacha”

“Unaonekana kuwa jasiri ,  lakini usisahau  ni  vizuri   kupenda na kupendwa pia”

“Haha..hata wewe mwenyewe  ni mtu  jasiri usisahau  nilivutiwa na ujasiri wako ndio maana leo hii sisi ni marafiki , tuna tabia zinazofanana”

“Haha.. sidhani ule ulikuwa ujasiri , pengine wewe unaweza kuona ni ujasiri ila wengine wanaona ni ujinga  na wananichukulia kama mwanaume dhaifu”

“Haijalishi   wanafikiria nini ili mradi kama mwanaume  umeweka wazi hisia zako bila ya kujali mazingira , mengine yapo nje ya uwezo wako”Aliongea  na kumfanya Hamza  kutabasamu.

*******

Ni masaa kadhaa  baada ya Hamza kuachana na  Amiri moja kwa moja alichukua  daladala kuelekea mahali  anapoishi.

Amiri alitaka kumpeleka lakini Hamza alimgomea na kumwambia atapanda daladala na Amiri hakutaka kwenda mbali kwenye kumbembeleza hivyo  alikubali aondoke kinyonge.

Amiri  alishangazwa na rafiki yake Hamza  kwani alionekana kuwa na shida ya pesa lakini  alikataa  malipo  kiasi cha kumfanya kukosa   raha   lakini kwasababu yalikuwa ni makubaliano  hakutaka kulazimisha sana , aliona pengine Hamza amemsaidia  kutokana na mara  nyngi alikuwa akimsaidia.

Wakati Hamza akiwa  kwenye  daladala akiwa amepata siti yake kwa kuigombania, alitoa simu yake kwa ajili ya kuingia mtandaoni maana  yalikuwa yamepita masaa bila kuingia  huko kuona kinachoendelea.

Alikuwa akipenda sana mitandao ya kijamii na alikuwa ni radhi asile chakula ili mradi tu kuwa na bando  hiyo yote ni kutokana na kwamba hakuwa na  marafiki wengi na  mitandao hio lilikuwa sehemu ya kupunguzia mawazo.

“Huu uzi bado tu una trend?”Aliongea Hamza huku akijaribu kuufungua tena na alishangaa kulikuwa  na  maoni mengi mno, alijaribu kutafuta maoni ya mtoa  mada lakini hakuona chochote na kuishia kujawa na shauku zaidi  juu ya mtoa mada   aliona pengine anamaanisha alichokiandika.

“Kwanzia sasa hivi ngoja nifanyie kazi  maneno ya Profesa Stephano nione kama yana uhalisia”Aiongea Hamza akikumbuka somo la  Bonus point lililokuwa likizungumziwa na  Profesa kuhusu Shauku.

Hamza  alijikuta  akipotezea makelele ya watu waliokuwa kwenye  daladala kushabikia maswala ya uchaguzi  na  kwenda katika PM ya mtoa mada na  kutuma ujumbe.

“Kwa kuzingatia tangazo lako , nipo tayari  kwa ajili ya Ajira  mawasiliano yangu  ni 0656786***** naishi mkoani Dar es salaam”

Ni ujumbe mfupi ambao Hamza aliandika na alijikuta akijicheka mwenyewe , aliona ni kama anajiingiza  kwenye mtego wa mtoa mada  lakini aliona potelea pote , ngoja  ajaribu bahati yake.

Baada ya kutuma ujumbe huo  aliamua kuendelea na  kutafuta  mada  nyingine ambazo zilikuwa  zikimfurahisha na kupitia mada pamoja na maoni , lakini hata hivyo hakuna kizuri  alichoona zaidi ya habari za uchaguzi tu, pengine habari ya ajira  ya mahusiano ndio ambacyo ilikuwa ni habari mpya  iliopata umaarufu   na kutrend katika hizo siku kadhaa..

Usiku wakati Hamza akijiandaa  kulala  aliingia katika mtandao wa Watsapp na kutafuta jina la Anitha ambalo baada ya kulipata aliweza kuona  mrembo huyo yupo Online , Hamza alitoa tabasamu na kisha akatuma ujumbe mfupi  wa kumtakia mrembo Anitha usiku mwema huku akimsifia maneno ya hapa na pale  kuusifia uzuri wake.

Aliangalia ujumbe huo kusomwa huku akiwa kama mtu mwenye matarajio ya kujibiwa ilihali alijua kwa asilimia tisini na  nane  Anitha hawezi kujibu  ujumbe wake, mara baada ya kusubiria kwa dakika  kadhaa alishuhudia tu  ujumbe wake kusomwa na  kisha palepale DP ya mrembo huyo  ikipotea na kuweka kivuli cha sura  ya mtu  na kwa akili yake ya haraka haraka alishajua ashalambwa tofali.

“Hahaha… maringo ya huyu  mwanamke  inamfanya kutabirika”Aliongea  Hamza huku akitoa kicheko  cha  uchungu  na kujikuta akirusha  simu pembeni, alijilaza kwenye gorodo  lake la  wanafunzi  la nchi sita huku akiangalia darini kama kuna kitu anachokiwaza, aligeuza kichwa cheke upande wa kushoto  lakini palepale alijikuta akikunja uso mara baada ya kuhisi harufu nziro iliokuwa ikitoka kwapani.

“Hizi ndio sababu ndogo ndogo ambazo  zinampelekea Anitha kutonipenda , ngoja nikaoge kwanza”Aliongea Hamza na kisha alipiga teke dumu  moja kivivu kuona kama lina maji  na alitoa tabasamu  mara baada  ya  kuhisi lilikuwa na maji  japo kidogo.

Baada ya kuyamimina  yote kwenye ndoo , licha ya  kwamba haikujaa mpaka juu lakini hakujali, palepale alipunguza nguo na kisha akachukua taulo  lake lililochakaa na kutoka  nje kulitafuta bafu la  pamoja(public)  kuoga.

Ilikuwa usiku hivyo muda kama huo mara nyingi hakukuwa na bughuza  upande wa bafuni na  ilikuwa ratiba yake mara nyingi kuoga muda huo ili kuepuka kero za wapangaji wengine.

Hamza alitumia dakika chache  kuoga pamoja na kukata gogo(Haja kubwa) huko huko na kisha alirudi  na kujifuta maji na kisha  akavaa   bukta yake ya jezi  ya Simba na kujitupa kitandani  lakini  usingizi ulikuwa mbali   hivyo alichukua  simu yake  na kuzama tena JamiiForum.

“Hapa ngoja nitafute bandiko lolote la kizushi  refu  litanisaidia kupata usingizi”Aliongea huku akifungua  mtandao wa JamiiForuma  na  kwenda moja kwa moja mpaka  kwenye  jukwaa la Jamii Intelligence na kutafuta bandiko la kizushi.

‘Wajue Night Shadows , kikundi cha siri kinachotawala Dunia  nyuma ya pazia”

Hamza mara baada ya  kukutana na  uzi huo  alijikuta akivutiwa nao mara baada ya  kuona una maoni ya watu wengi pamoja na Views , aliufungua kuona kuna kipi  ambacho kimewavutia watu.

“Je unawajua  Night Shadows ndio wamiliki wa kisiwa  cha Binamu?”

Hamza mara baada ya kuona swali hilo ambalo mwandishi alionekana kuliweka makusudi  ilimfanya kuvutiwa kwani ni mchana tu  aliweza kukutana na mrembo  Tresha Noah katika Apartment za Dosam Homes , alijiambia hapo ni mahali pake.

Previoua Next