Reader Settings

“Uimara ni  kuyashinda  yale ambayo hujayatarajia , uendelevu  ni kuishi , lengo la kuwa imara ni kufanikiwa”-Jamais Cascio

 

SEHEMU YA 12.

Amosi alitaka  kazi  mpya ambayo amepatiwa kuifanyia kazi kwenda sawia bila ya  kuwa na dosari, na ili hilo kufanikiwa  hakutaka kuwa na  watu ambao wanaweza kuhatarisha usalama wake.

Siku ya jana alichokipata  akiwa nyumbani kwake  hakikuwa kitu cha kawaida kabisa , watu waliokuja kumvamia na kumpa sulubu ya kipigo hawakuwa na huruma  hata kidogo , kama sio kuomba  sana kutojeruhiwa zaidi pengine siku hio asingeweza kuamka kabisa  na  kufika ofisini.

Mara baada ya kutoka katika ofisi yake  baada ya kupokea bahasha katika akili yake kitu pekee kilichomjia ni kwenda kumalizana na Eliza  mwanamke ambae  ndio aliekuwa chanzo cha kupigika kwake na kumfanya kuonekana na  nundu asubuhi hio.

Ijapokuwa kazi ya kumsumbua  Eliza haikuwa matakwa yake bali ya bosi wake , lakini  hakutaka hata kushauriana nae.

Alienda kusimamisha  gari yake katika  jengo  la  makao makuu ya kampuni ya Dosam na kisha kuelekea eneo la mapokezi na  kueleza shida yake, lakini kwa kile ambacho kimetokea kwenye  mitandao ilimfanya watu wa usalama wa eneo la mapokezi kutomruhusu moja kwa moja  na  aliitwa mkuu wa kitengo cha ulinzi.

Yonesi mwanamke mrembo na mkakamavu ndio aliekuwa  kiongozi wa kitengo cha ulinzi wa kampuni ya Dosam  lakini vilevile alikuwa mlinzi binafsi kwa  bosi wa kampuni hio ya Dosam , yaani  Regina Wilson.

“Mzee Amosi  unafanya nini  hapa  baada ya kumdhalilisha  mfanyakazi  wa Dosam?”Aliuliza

Yones kikauzu mara baada ya kumfikia Mzee Amosi , kwa jinsi aivyotaja jina lake ni kama alikuwa akifahamiana nae.

“Mdogo wangu  Yonesi bora umekuja wewe , nadhani tutaelewana   kulingana  na historia yetu”Aliongea  Amosi na kumfanya  Yonesi kumwangalia  Amosi kwa  macho yasiokuwa na hisia za aina yoyote , huku wakati mmoja akijiuliza  nani kamshikisha adabu  mpaka kuwa na manundu hayo usoni.

“Kitendo cha kufika hapa na kinachoendelea mitandaoni  ni kuibua taharuki , umemdhalilisha  Eliza na watu wakarekodi  na kutuma mtandaoni , unadhani  Eliza anajisikiaje , Mzee wewe ni mtu mzima na Eliza ni kama  mwanao  kwanini kwenda mbali  vile?”Aliongea Yonesi huku akionyesha hasira.

Amosi na yeye alionekana kushangaa , hakuwa na habari ya  tukio la   jana kufahamika kwa watu wengi  na kwa kauli ya Yonesi alijua lazima  kuna mtu alirekodi, aliishia kutoa tusi la ndani akiwalaani Chongolo na wenzake kwa kutokuwa makini.

“Sio kama unavyofikiria Yonesi, ila unachoongea  ni sahihi  jana nilivuka mpaka na ndio maana nipo hapa , kumuomba  Eliza msamaha  kwa tukio la jana”

“Kwa kauli yako sidhani hata huo msamaha  ni wa dhati , unaongea kwa namna ya amri ukitarajia kusamehwa mara moja ,  sitaki kumsemea Eliza juu ya  kilichomtokea  na kama atakuwa tayari kuonana na wewe  nitaruhusu  vinginevyo utaondoka”Aliongea kibabe na kumfanya Mzee Amosi kutabasamu.

“Nilidhani  kufanya kazi  chini ya watu wazito kutakubadilisha Yonesi , lakini naona  upo vilevile ,  msichana  wa shoka ambae  huna utani hata kidogo , ukiendelea hivyo utakosa mume  maisha yako yote, jilegeze kidogo mimba iingie”

“Ni kheri mimi  ambae sijabadilika  kuliko  wewe ambae umegeuka  kuwa mbwa usie na mmiliki , yoyote mwenye pesa unawinda kwa ajili yake, kwa tabia  yako utazeeka ukiwa huna familia”Amosi hakuwa na familia , aliishi peke yake na alikuwa tayari ni mtu mzima na kauli ya  Yonesi ilimgusa.

“Wote tuna malengo  yanayofanana  Yonesi , njia tu ndio tofauti, juu ya yote kuwa na familia na kutokuwa na familia sio sheria  ni aina ya maisha ambayo mtu anachagua  hivyo sioni tatizo, ushauri wangu  ni wewe kubadilika kidogo au kutafuta mwanaume , jilegeze hata  akupe mimba tu”Aliongea  Amosi  kwa kejeli.

Maneno yale yalimfanya hata yule  mwanadada wa mapokezi kumfanya  kukosa amani , maneno hayo yalionekana kuwa na ukweli , tabia ya ukakamavu  ya  Yonesi  ilimfanya kuogopwa na wanaume wengi licha ya kwamba alikuwa mrembo.

Yonesi licha ya kauli ya  Amosi kupiga kwenye mshono  hakutaka  kuruhusu  hasira zake zimtawale na   hakutaka kujibishana nae maana hata hivyo Amosi alikuwa mtu mzima kwake , hivyo alimpa ishara  mtu wa dawati la mapokezi kuwasiliana na  Eliza.

Yule mwanadada wa mapokezi mara baada ya kuongea kwa dakika kadhaa alirudisha jibu, Eliza hakuwa tayari kuonana na  Amosi.

“Hey , mwambie sipo hapa kwa ubaya  nataka kuomba  msamaha”Aliongea .

“Samahani baba , nimemwambia  hivyo?”Aliongea yule  mwanadada kwa kipole lakini kwa chuki kidogo.

“Nadhani ushasikia jibu  wewe baba, hapa ni eneo la kazi na sio sehemu ya kuomba msamaha  hivyo unapaswa uondoke , aliekuadabisha jana na kukufanya  uje kuomba  msamaha  amefanya  vizuri , pengine akili  ya ki utu uzima imekurudia”Aliongea Yonesi kwa chuki.

“Yonesi, ijapokuwa nishatoka  jeshi la polisi  muda mrefu  haimaanishi  cheo changu cha usenior kimekoma , unapaswa kuniheshimu  pia”

“Heshima haiombwi , kama kweli unataka nikutambue  kama mkubwa wangu basi ishi kama mkubwa wangu , acha kuwa mfano  mbaya  kwa jamii, hata kama umeamua kuwa mbwa  wa  wakubwa , jiwekee sheria zako za ki uwindaji”

“Asante kwa ushauri wako  binti”Aliongea Amosi huku akikunja sura  na palepale aligeuka  na kuanza safari ya kutoka katika jengo hilo , alijua hakuwa na haja ya kulazimisha , isitoshe  alikuja kuomba msamaha kwa ajili ya kujiepusha na marudio ya tukio la jana.

Amosi mara baada ya kutoka nje  aliangalia upande wa kulia , ilikuwa ni kama alihakiksiha sura yake ikionekana katika moja ya gari iliokuwa imepaki   mita kadhaa kutoka alipo na  alitingisha kichwa na kisha  akaingia ndani ya gari yake.

“Damn! Hisia zangu ziliniambia vizuri , yule kijana  hakuwa wa kawaida , lakini inafikirisha  kuwa na ukaribu na  Eliza wa ghafla tu , hatujawahi kumuona wakiwa pamoja , jana ni siku ya kwanza, lakini imekuwaje  akawahusisha Chatu  kuja kunipa onyo?”Aliwaza Amosi  kabla ya kuwasha gari, mtu aliekuwa akimzungumzia ni  Hamza ambae aliwavurugia jana  katika mpango wa kumlazimisha Eliza kulipa deni kupitia mwili wake.

Amosi alisifika kwa ubishi na ukiburi , kitendo cha kufika  kwenye kampuni   na kuomba msamaha ni dhahiri   maji yalikuwa yamemfika shingoni , sio kwamba watu waliomshambulia jana hakuwa akiwajua , alikuwa akiwajua fika ndio maana  hakuaka  kuleta ubishi wa aina yoyote  na kutii maagizo yao , Chatu ni kundi la wahalifu ambalo  siku zote alihakikisha  hatengenezi nalo uhasama, lakini  jana ikawa siku yake ya kwanza kujiingiza  katika uhasama na  ili kuondoa uhasama huo alilazimika kuja kuomba  msamaha mbele  ya Eliza.

Uwepo wa kundi  la kihalifu  la Chatu  katika nchi yenye ulinzi  mkali wa kipolisi katiika kupambana na uhalifu  kama Tanzania ilikuwa ni swala la  kushangaza(mystery).

Baadhi  ya watu wanasema kundi la chatu  ni   jina  jipya  la kundi la kihalifu ambalo lilikuwa likisumbua sana  taifa kwa muda wa miaka mingi , kundi ambalo  lilifahamika kwa jina la Panya  Road.

Wengine wanasema kundi la Chatu  linaendelea kushamiri ndani ya Tanzania kwasababu ya baraka  zote kutoka serikalini.

Ki ufupi ni kwamba  uwepo wa kundi  la Chatu  ndani ya   Tanzania  ni moja  wapo  ya  habari za kusisimua mno na habari zilizidi kusisimua mara  baada ya moja ya mgombea wa uraisi  kupitia chama cha wanaopinga kusema kwamba  hatua ya kwanza akiingia madarakani ni kutokomeza kundi  hilo  la kihalifu ambalo linafadhiliwa na serikali.

Mgombea huyo wa uchaguzi  anaenda mbali kwa kuliunganisha kundi hilo  na vijana watekaji na  wezi waliokuwa wakijiita Panya Road.

Ki ufupi ni kwamba  katika  kipindi hiki ambacho  ni cha uchagunzi nchini Tanzania  kila mgombea alitafuta namna ya  kujipatia pointi za kujinadi mbele ya  wananchi.

“Bosi tuendelee kumfuatilia?”Aliuliza  kijana  aliekuwa  ameshikilia usukani  , huku pembeni  yake  kukiwa na kijana mwingine ambae alikuwa amevaa hat pamoja na miwanin ya jua.

“Kazi yetu  ilikuwa ni kuhakikisha  kama  amefika na kuomba msamaha , lakini  ngoja niongee na bosi Lau  kama ana maagizo mengine”Aliongea yule bwana  na palepale alipangusa simu yake , alikuwa amevalia glovusi nyeusi.

“Mkuu Lau , Jasusi mstaafu ameonekana akiingia ndani ya jengo la makao makuu ya kampuni  ya Dosama , amekaa kwa dakika  therathini  na kutoka , inaonekana onyo limefanya kazi ,  kuna maagizo mengine tunapaswa kufuata?”

“Kazi nzuri Bwalia  , mnaweza kurudi chimbo”

“Sawa  mkuu”Aliongea Bwalia  na palepale simu ilikatwa na akampa ishara dereva wa forester hio kuondoa gari maeneo hayo kuelekea Chimbo.

Upande  wa Kijichi , mrembo Dina aliekuwa amvalia suti ya rangi nyeupe alikuwa amekaa kwenye sofa  akiwa amekunja nne akipata mvinyo wake taratibu huku akifurahia  kiyoyozi   kinachomwepushia   na adha ya  joto la jiji la  Dar.

Macho yake yote yalikuwa katika  runinga akiangalia  kampeni za  mgombea kiti cha  uraisi kupitia chama cha wanaopinga.

“Hatuwezi kukubali  kabisa nchi hii kuendeshwa kihuni , tunapaswa kukemea  hili kwa nguvu zote , njia sahihi  ya sauti zetu kusikika  ni kupitia kura zetu

, sisi ndio waamuzi wa  mwisho wa namna tunavyotaka nchi hii iendeshwe ,  haiwezekani  Wapenda madaraka  wafadhili  kundi la Panya Road na sisi tuone ni sawa , haiwezekani kabisa  wahalifu waliotuulia ndugu zetu  waishi chini ya mwamvuli ya viongozi wa chama cha wapenda madaraka  tofauti  na kuwaadhibu  kwa  makosa yao , hii ni dharau  kwa sisi  wananchi ,  na dharau hizi zimefika  mwisho , iwe ni Chatu , Cobra au  panya Road lao ni moja , hao ni wahalifu ambao wanapaswa kuwajibishwa mbele ya sheria  na  hakuna namna ya hili kuwezekana bila  ya nyie wenye nchi  kutukabidhi dhamana hii , nipatieni kura  muone ni kwa namna gani nitawajibisha kundi lote  la wahalifu hapa nchini , haitakuwa kwa machatu tu , kunguni wote wanyonya haki zetu watawajibishwa, huu ni wakati wa maamuzi makubwa… na Mimi Msemakweli nitumieni kama siraha…”

“Bosi..!!!”

Sauti ya Lau ndio iliomgutusha  mrembo Dina ambae alionekana  kusikiliza kampeni ya mgombea wa chama cha Wakosa madaraka , licha ya kwamba alionekana kusikiliza kwa umakini lakini moyoni mwake ni kama alikuwa akidharau kile ambacho Msemakweli alikuwa akizungumza.

“Msemakweli , unaweza ukawa wewe raisi lakini huwezi kuiondoa Chatu  katika mfumo , hujasoma faili letu bado ndio maaa, ni haki yako kuongea chochote kujipatia kura”Hayo ndio yalikuwa mawazo ya Dina.

“Boss kazi  ulionipatia imekamilika , hizi ndio  taarifa za mwanamke ambae Bro Hamza anamlinda”Aliongea Lawrence na kukabidhi kishikwambi kwa mrembo Dina.

Picha mbalimbali za mrembo  Eliza zilionekana katika  skrini ya kishikwambi hicho  na zilimfanya Eliza kukunja  sura  kiasi sana  na kurudi katika hali yake ya kawaida.

Kwa namna moja alionyesha kukasirika  na  kushukuru kwa wakati mmoja

“Kuna taarifa nyigine  tofauti na hizi picha?”

“Ndio bosi ,  huyu msichana ni Katibu muhtasi na msaidizi  binafsi wa bosi wa kampuni ya Dosam  , anaitwa Eliza Msuya”

“Imekuwaje mpaka akajiingiza katika mgogoro na Amosi?”

“Alikopa  kiasi cha pesa  kutoka kwa Amosi  kwa ajili ya matibabu ya mama yake ambae alikuwa na shida ya moyo, aliweza kulipa kiasi chote  pamoja na  nusu ya riba , lakini  nusu iliobaki hakushindwa kuilipa  ndani ya muda hivyo deni lake kuongezeka  ndio maana  Amosi alikuwa akimlazimisha  kulipa riba iliobaki”Aliongea Lawrence na kumfanya mrembo Dina kufikiria  kwa dakika kadhaa.

“Vipi kuhusu  yeye na Hamza walivyokutana?”

“Bosi sijajua   walivokutana , lakini kwa  maelezo ya taarifa vijana waliyokusanya Bro  jana alienda Lotus apartment kwa ajili  ya  kazi yake ya ufundi na hapo ndipo  alipotokea kumsaidia Eliza kutoka katika mikono ya Amosi , kulingana na mashuhuda wa tukio wanasema  ni  mara yao ya kwanza kumuona   akiwa na Eliza , kwa mtazamo wangu kuna uwezekano  Bro aliamua kumsaidia  tu”Aliongea  na kumfanya Dina kutafakari.

“Madam  sidhani  kuna haja ya kuwa na wasiwasi , huyu  ni wa kawaida sana kwa Bro  kulingananisha na wewe”

“Unaongea ambacho sijataka kusikia  Lau, ila asante , unaweza kwenda sasa , hakikisha  vijana hawasababishi matatizo, wala kufanya vitu bila  maagizo yangu”

“Sawa bosi , najua  hiki ni kipindi muhimu kwetu, nitakuwa makini”Aliongea  na kisha alimuacha  Dina  akiwa peke  yake.

Dina alikuwa na wivu kwa kitendo cha  Hamza kuonyesha  kumsaidia  mwanamke  Eliza, katika hali kama hio aliona pengine  ni  bora kutokuwa na uwezo wa kujilinda  pengine Hamza angeongeza umakini wake juu yake.

Lakini licha  ya hivyo hakuwa na hofu , baada ya kumuona Eliza hali yake  ilitulia na kujiambia  nafasi bado anayo.

*****

Sehemu ambayo Hamza alikuwa akiishi haikuwa na uwezo wa kufika gari , mara baada ya kufika  barabarani ilibidi  asimamishe na yeye pamoja na Yonesi walianza kutembea kuingia katika uchochoro.

Yonesi licha ya kazi yake ya ulinzi kuonekana  sio ya hadhi kubwa lakini ukweli ni kwamba alikuwa ni mwanumke ambae  familia yake haikuwa  vibaya ki uchumi, hivyo  mazingira ya maeneo kama hayo ambayo  Hamza alikuwa akiishi hajawahi fika kabisa licha ya kuishi mjini  Dar Es salaam.

Sio kwamba hakuwahi kuingia ktika uchochoro kabisa , lakini mazingira ya anapo ishi Hamza  yalikuwa mabaya mno ,  kulikuwa na harufu kali ya maji machafu mtaroni.

Hamza aliweza kuona mabadliko ya Yonesi lakini  hakutaka kutia neno ,isitoshe alijua mazingira hayo yalikuwa ya kimasikini mno  na kwa mwanamke wa aina yake lazima  akose utulivu.

Kitu kumoja pekee ambacho kilimfanya Hamza kutokumzingaria Yonesi ni namna watu wa eneo hilo walivyokuwa wakimwangalia ,  mwanzoni alijua  pengine ni kwasababu ya kuja  na Yonesi mwanamke mrembo na mkakamavu lakini  baadae aligundua  hio sio sababu.

Baada ya kutembea  kwa  umbali wa  kilomita moja hatimae aliweza kufika katika sehemu ambayo amepanga.

“Huku mbali hivi , mizigo yako tunabeba vipi?”Aliuliza Yonesi ambae alionekana kabisa kukosa utulivu , macho ya watu yalivyokuwa yakimwangalia ni kama alielewa ni kipi ambacho walikuwa wakifikiria ,  ilionekana  ni kama mwanamke  wa kishua ambae ameletwa geto uswahilini, mambo ambayo yanaonekana sana kwenye simulizi au filamu huku kwenye uhalisia yakiwa ni nadra.

“Sina mizigo mingi  ya kubeba , nachukua begi langu tu   , vingine nitamwachia  mwenye nyumba”Aliongea  Hamza huku akiongeza umakini  wa mazingira.

Eneo ambalo alikuwa akiishi halikuwa na watu wengi sana , ni kwasababu lilikuwa ndani  ndani na  baadhi ya watu wanaoishi huko wapo katika kazi zao za kujitafutia kipato , walikuwa watu wachache sana ambao walikuwa wakionekana kupita pita.

“Afande Chumba changu ni kile  pale , shika   ufunguo huu hapa nakuja”Aliongea Hamza  huku akinyooshea mlango  wa chumba chake cha uwani.

“Unanipa ufunguo wa nini ,  katoe nguo  zako tuondoke”Aliongea  huku akionyesha kukasirika.

“Tutapoteza muda sasa , wewe tangulia ndani , mimi naenda kumuaga  mama mwenye nyumba”Aliongea Hamza na hakusubiri  jibu alimkabidhi mkononi Yonesi ule ufunguo na kisha alikimbia kuelekea upande mwingine  huku akiwa na tabasamu usoni.

Yonesi aliishia kuangalia ile ufunguo   na kisha akageuza macho yake kwa Hamza ambae alikuwa akitokomea upande wa pili  na aliishia kutingisha kichwa, alijishauri kutokwenda kufungua kile chumba lakini kwa namna flani alionekana  hakutaka kuendelea kusimama hapo hata kwa sekunde  kutokana na  kukosa utulivu.

“Kuna watu wanaishi kwenye mazingira magumu sana”Alijiongelesha kisha alipiga hatua kusogelea chumba cha Hamza.

Wakati huo  kuna watu  kutoka nyumba za majirani ambao walikuwa wakimwangalia  Yonesi kwa  macho  ya kumshangaa.

Yonesi alijua alikuwa akiangaliwa  kwasababu alikuwa mgeni , lakini haikuwa hivyo  na alifahamu hivyo mara baada ya kusogelea mlango wa chumba cha Hamza , mlango wa chumba hicho ulionekana ulikuwa wazi na umerudishiwa tu kidogo.

Kilichomfanya  kujua mlango ulikuwa wazi ni ile kunesa nesa kwake , ikiwa  ni kama vile ulikuwa ukipeperushwa na upepo na kwasababu alikuwa na ufunguo wa Hamza mkononi na aina ya kitasa cha mlango alijua lazima kuna watu waliokuwa  ndani na hio ni kutokana na watu walivyokuwa wakimwangalia kwa wasiwasi, ni kama walikuwa wakitaka kumwambia asiingie.

Yonesi aliongeza umakini , akili yake ilikuwa ikifanya kazi kwa  spidi kubwa mno na kwa haraka haraka alishainusa hatari.

“Mshenzi  sana , alijua kuna hatari nini ndio  maana akaniachia huu msala?”Aliwaza  Yonesi na  kitendo cha kuushika mlango tu  kuusukuma ulifunguliwa kwa ndani  na alichomoka mtu kama mshale   akitanguliza mguu wa kulia kumlenga Yonesi , lakini ilikuwa ni kama   kitendo kile Yonesi alikuwa amekitegemea kwani alisogea  pembeni kidogo na mara baada ya  mtu yule kumfikia usawa wake alizungusha mguu wa kushoto  na kumgonga eneo la kigoti.

“Puuh!!”

Yule mtu  alidondoka chini kama furushi huku akigugumia maumivu, lakini  hakupoa kwani palepale alichomoka mtu mwingine akiwa  ameshikilia rungu na kutaka kumlenga nalo Yonesi, lakini muda ule Yonesi alionyesha kwanini  alikuwa mlinzi ambae aliaminiwa mpaka kumlinda mtu mzito kama Regina.

 Kijana yule kitendo cha kumsogelea na ile rungu  ni kama Yonesi aliitega na kuifanya ipite kwapani na kisha alimvuta yule mtu  kwake na  ilikuwa pigo moja la karate lililopiga shingoni na kuwafanya  watu wote wawili kuwa chini, mmoja akiwa hajitambui mwingine akiwa  anaungulia maumivu.

Yonesi alimtaka yule  ambae alikuwa akiugulia maumivu ili kumhoji, watu wote wawili walionekana kuwa vijana   katika sare za jeshi la polisi , lakini kwa uzoefu wake alijua hao  sio polisi hata kidogo.

“Nyie  ni nani , nani kawatuma?”Aliongea Yonesi kibabe  mara  baada ya kumsimamisha yule ambae alikuwa akijitahidi kusimama baada ya kutenguliwa  mguu.

“Sisi  ni….  Sisi  niii..”Kabla hata hajamaliza kuongea alikuwa tayari ashapoteza fahamu, jambo ambalo lilimshangaza Yonesi , hakuwa amempiga kiasi cha kupoteza fahamu.

Muda uleule  Hamza aliweza kurudi na mara baada ya kukutana na Yonesi kumaliza kazi yake alitoa tabasamu  huku akitafuna karanga.

“Upewe  maua yako mwanajeshi”Aliongea Hamza mara baada ya kumfikia Yonesi.

“Wewe mwanaume muoga sana , ulishajua kuna hatari ndio maana ukaniachia  ufunguo”Aliongea Yonesi huku akimwangalia Hamza kwa macho makali.

“Me najuaje , nimekuaga  naenda kuongea na  mama mwenye nyumba na ndio nimerudi”Aliongea na kumfanya  Yonesi kukunja sura na kisha alimwachia yule kijana aliepoteza fahamu kwa kumuweka chini na kuanza kuangalia baadhi ya watu wachache waliokuwa waishangaa.

“Una wafahamu?”

“Siwafahamu , nadhani ndio hatari aliokuwa  akizungumia Regina , mtu kama mimi masikini sinaga maadui”Aliongea Hamza.

Kauli yake ilikuwa sahihi,watu hao waliokuja kuvamia walionekana kutokuwa na mafunzo yoyote  ya kivamizi ni kama vibaka tu ambao wameagizwa  kuja kumshambulia , lakini hata hivyo  aliona hakuna uwezekano  wa  James mchumba wa  Regina kutuma watu hao , maana ndio kwanza amefahamiana nae leo.

“Kwahio tunawafanyaje ,  tupigie polisi waje wawachukue?”

“Haina haja ya polisi , ni  kujiingiza matatizoni tu  na maswali mengi”

“Sema unaogopa polisi , huna lolote”

“Hey , kwanini niogope polisi wakati sina kosa , sitaki kupoteza muda mwingi hapa”Aliongea  Hamza  na kisha aliingia ndani kwake na kuanza kutafuta kitu cha kubeba na vingine vya kuacha.

Upande wa Yonesi aliishia kuzungusha macho katika chumba cha  Hamza na kutokana na namna maisha yake yalivyokuwa ya kimasikini aliishia kumuonea huruma.

“Hatimae  naona   kitu cha thamani”Aliongea Yonesi mara baada ya Hamza  kuchoropoa  kiboksi kidogo ambacho mara baada ya kukifungua I kulionekana kitu kama mkufu wa dhahabu uliofungwa na medali  ya Dhahabu , pamoja   na mchoro usioelezeka.

“Upo sahihi , hiki ndio  kitu cha thamani nilichokuwa nacho”Aliongea Hamza na kisha alirudisha medali ile kwenye  kiboksi na kutumbukiza kwenye  begi.

“Unatabasamu nini sasa ,  malizia tuondoke”

“Sawa sawa  Kapteni”

Mara baada ya kufungasha kila kitu chake  na kuacha alivyotaka kuacha hatimae  walitoka na Hamza aliwamwagia wale wavamizi na maji  ili wazinduke na kisha wakaondoka zao huku wakiacha watu nyuma wakiongea kila neno  na kumshangaa Yonesi.

Egret  ni mtaa uliokuwa ukipatikana kilomita kumi kutoka  feri kigamboni ,  ndani ya mtaa  huo ni majumba makubwa ya kifahari tu ndio yalikuwa yamejengwa , ulikuwa ni mtaa tulivu ambao  wanaoishia hapo ni wale wenye ukwasi mkubwa wa pesa.

Kilichopendezesha zaidi mtaa huo ni   mazingira yake ya kijani kibichi na upepo  mwingi kutoka baharini.

Sasa Regina  alikuwa akiishi ndani ya mtaa huuu  katika   nyumba au kasri namba saba , na  kuishi katika  namba  hio  ilikuwa ikioneisha ni kwa namna gani utajiri wake ulikuwa mkubwa.

Mara baada   ya gari kuruhusiwa kuingia  ndani  ya geti  Yonesi aliendesha  na kwenda kupaki  katika nyumba anaoyoishi  Regina , nyumba  yao haikuwa imezungukwa na geti , ndani ya eneo lote la Egret  kilichoteganisha nyumba na nyumba ni uzio  na sio ukuta  na hiii imefanya eneo hilo liwe la kupendeza mno , ilikuwa ni kama vile  ni Ulaya.

Mara baada ya kusimamihsa gari  mwanamke  mama hivi  mwenye umri wa miaka kama  arobaini kwenda hamsini hivi alitoka,  licha ya kuvaa kikawaida sana lakini  afya yake ilikuwa nzuri.

“Kapteni Yonesi , karibu ndani hata upate  maji tu”Aliongea yule mama mara baada ya Yonesi kusalimia.

“Aunt Mari , kwa leo sitokunywa maji , napaswa kurudi haraka kazini”Aliongea  Yonesi huku akitabasamu.

“Kama kawaida yako,mtu mwenye haraka zako”Aliongea huku akiweka tabasamu lakini alionekana kumwelewa Yonesi na muda uleule ndio sasa alimgeukia Hamza.

“Nadhani wewe ndio Mr Hamza kama  sikosei , Regina amenitaarifu  ujio wako kwamba utaishi na sisi kwanzia leo, karibu sana  nyumbani”Aliongea yule mama  lakini Hamza muda wote alionekana kumshngaa na   aliishia kujiambia huyu mama sio wa kawaida  kuna  msisimko ambao alikuwa akiupata  ila hakujua unahusiana  na nini.

“Wewe mkorofi, Aunt Mari anakuoangelesha unakaa kimya , usije kumletea ukorofi, ni shangazi yake Regina lakini ni kama mama kwake”Aliongea  Yonesi kwa kuamrisha.

“Sio hivyo , nilikuwa nikishangaa , sikutegemea  Aunr Mari  kuwa kijana hivi?”Aliongea  Hamza akijitetea.

“Haha.. Mr  Hamza nadhani utakuwa ni mtu unaependa utani , mimi na ujana vipi wakati  bado miaka miwili tu kutimiza miaka  sabini”Aliongea na kauli ile ilimfanya Hamza kuthibitisha hisia zae, miaka sabini  lakini anaonekana kuwa kijana.

“Aunt Mari, akikuletea ukorofi usisite kuniambia , nitafika mara moja kumshikisha adabu”AliongeaYonesi kibabe.

“Hapana , sidhani yupo hivyo , isitoshe   naamini  maamuzi ya Regina”

Kapteni Yonesi  alionyesha kuwa na wasiwasi na  Hamza  na aliongea maneno kadhaa na  mwanamama huyo na kisha aliondoka.

Sasa akabakia  Shangazi Mariposa  na Hamza peke yao , wote waliangaliana kwa dakika kadhaa na   Shangazi  Mariposa alivunja ukimya.

“Mr Hamza  ngoja nikuonyeshe mazingira ya nyumba”Aliongea  

“Shangazi  niite tu Hamza , ninaona vibaya ukiniita Mr”

“Nitakuita basi Hamza , Mr  ni jina la heshima kwasababu umeshakuwa boyfriend wa  Regina”Aliongea na Hamza alitingisha kichwa kukubali.

Mara baada ya kuingia ndani ya kasri hilo , Hamza alivutiwa sana  na usanifu wa ndani  na mapambo yake, ulikuwa usanifu mwepesi lakini  wa kisasa zaidi , nyumba ilikuwa na mwanga flani hivi  wa rangi ya  majivu  na bluu  na muonekano huo uliendana  sawa kabisa na tabia ya Regina.

Vifaa vya umeme  vyote vilikuwa  ni vile  va  bei ya juu na  vya teknolojia kubwa , hakukuwa hata na ishara ya vumbi kwenye sakafu , kulikuwa na  michoro ya thamani iliokuwa imening’inizwa ukutani. Ijapokuwa uzuri wake ulikuwa ukifurahisha macho  lakini  pia  kulikuwa na ile hali ya  flani ya kujisikia kinyumbani.

Sehemu  pekee ambayo ilikuwa na vitu vingi ni jikoni pekee , kulikuwa na chillers tatu na friji moja  na kumfanya  Hamza kuwaza  ni kiasi gani cha chakula huhifadhiwa  kwenye  hizo chillers maana ni kubwa  mno.

“Shangazi  hii ndio sehemu ambayo  wewe na Regina  mnaishi siku zote?”

“Ndio , Mzee Wilson  na mke wake hawaishi hapa , tokea  Regina aondoke nyumbani  aliishi na mimi hapa , hii sehemu  ipo kimya sana  miaka  yote tokea tuhamie”

“Aisee , nadhani inachosha sana kuishi kwenye mjumba wote huu watu wawili pekee”

“Labda  kwangu  lakini kwa Regina  anaona sawa , anapenda sana  ukimya , akirudi nyumbani  ni kula na kulala  au  afanye kazi katika chumba chake cha kujisomea , sio mtu wa kujichanganya changanya  na nimeshamzoea hivyo hivyo”Aliongea Shangazi  Mariposa.

“Tena  vipi wewe , familia yenu ni ya watu wa ngapi?, wazazi wako wanajua umehamia hapa?”

“Mama yangu alifariki , kuhusu baba sikumbuki sana , nimeishi peke yangu tokea mdogo”

“Ah!, Jamani , pole sana na samehe huu mdomo wangu wa kiropo ropo , sikupaswa kuuliza”

“Haha..Shangazi  usiwe na wasiwasi kabisa , nishazoea , hebu niangalie nipo  vyema licha ya kwamba nimeishi  mwenyewe maisha yangu yote, sina utofauti wowote”

Bi mkubwa huyo hakuongea zaidi  na  alimchukua Hamza na kwenda kumuonyesha chumba chake.

“Hamza utakuwa unalala kwenye hiki chumba kwanzia leo  na kuendelea , chumba kinachofuatia  ni  cha Regina cha kusomea na  mbele yake ni  chumbani kwake, nimekuweka karibu karibu na yeye ili angalau  mapenzi yenu yashamiri, hii ndio mara ya kwanza kwa Regina kuwa katika mahusiano hivyo  juhudi ya ziada inahitajika , nadhani  ni Mungu amewakutanisha   hivyo hakikisha  unatimiza wosia wa  babu yake”Aliongea Shangazi.

“Nini , hii ni mara ya kwanza kwa Regina kuwa na mpenzi?”

Hamza alishangaa , ijapokuwa  yule mwanamke alikuwa kauzu  na ngumu sana kuwa na ukaribu nae  , lakini alikuwa mrembo mno  na  haijalishi  juu ya tabia zake lazima kuna wanaume ambao walikuwa wakitaka kutoka  nae kimapenzi , labda kama  tu  walikuwa  wamefeli kumshawishi mrembo huyo au kuna sababu  nyingine  inayomfanya Regina kutojihusisha  kimapenzi.

“Hakuna anaemini ila huo ndio ukweli , ijapokuwa mimi ni shangazi   yake lakini ni mlezi wake vilevile , nilimuona tokea akikuwa   mpaka kusoma kwake na kuhitimu , ni kweli vijana mbalimbali  wa tabia zote walikuwa wakimfuatilia lakini  hakuonekana kupenda  kabisa kujihusisha kimapenzi…hii ilimpa wasiwasi hata babu yake.

Mwanzoni nilijua  ataendelea tabia yake hii mpaka akipita kipindi cha kubeba ujauzito , lakini imekuwa bahati nzuri umetokea, Hamza hakikisha unajitahidi , ninasubiri kwa hamu siku ambayo mtaoana na kukuitana mke  na mume na mimi kukuita mkwe”

Hamza aliishia kujiuliza na kujiambia  kuoa tena  na kuitwa mke , mbona kwake ni kama haiwezekani.

Ukweli hakujua acheke au anune , aliona ni kama Shangazi  Mari alikuwa akienda mbali sana kimawazo  na kuona kwamba jambo hilo haliwezi kutokea , isitoshe  amesaini mkataba wa miezi mitatu  tu kwa maana hio ataishi hapo kwa miezi hio mitatu.

Lakini kwa namna ambavyo Shangazi huyo alivyokuwa akionekana , ilikuwa  ni kama Regina hakumweleza kila kitu kama mahusiano yao yalikuwa ya  mkataba.

Upande mwingine ilionekana Shangazi alikuwa akiishi  na Regina kwasababu ya babu yake Regina pekee.

Hamza  aliweka nguo zake katika chumba chake na kisha akashuka chini  na aliweza kumuona Shangazi Mari  akiwa amebadili mavazi  na ilionekana  ni kama alikuwa akijiandaa kutoka.

“Shangazi unaelekea wapi ?”

“Oh , kuna samaki tu  ndio  wamebaki kwenye mafriji  ,  hivyo naenda  angalau kununua mbonga za majini  na  vitu vingine , nataka kuandaa chakula cha kukukaribisha usiku ,  wewe  bakia tu hapa , unaweza kuangalia Tv  au kwenda nje kuogelea”Aliongea. “Lakini si unaendesha kwenda huko  sokoni”

“Na umri huu , najulia wapi kuendesha gari , natembea mpaka  nje huko  kisha nichukue daladala au bajaji”Aliongea huku akicheka.

“Twende wote , nadhani  kutakuwa na gari  nyingine hapa nyumbani , nitakupeleka”Aliongea  Hamza mara baada ya  kukumbuka  Regina alikuwa na gari aina ya Maserati.

“Hakuna shida , kama hujali kuongozana na  mzee kama mimi kwenda Supermarket”

“Hehe , kwanini nijali , nataka kuhakikisha safari haikuchosi ili  chakula  kiwe kitamu usiku”Aliongea Hamza  bila ya wasiwasi  na kumfanya  Shangazi  kutoa tabasamu , hata yeye alikuwa amechoka kupanda vibajaji.

“Tuingie kwenye lift kwenda Gereji ya magari”Aliongea  na kumfanya Hamza kushangaa ,  nakujiambia inamaana utajiri wa Regina ulimpa hadi nafasi ya kumiliki gereji ya magari.

Hamzamara baada ya  kuingia  katika lift ndipo alipojua hili jengo licha ya kuonekana kuwa na ghorofa tatu kwenda juu lakini  ni kama lina ghorofa tano kwani kulikuwa na floor mbili kwenda chini ambazo zote ni gereji,  yaani B1 na B2 , 

“Hamnza utapendelea kuendesha lipi hapa , chagua moja mwenyewe , Regina anaendesha magari ambayo yapo B1 pekee na B2 yote  hayaendeshi na analetaga fundi tu kuyashitua shitua”

Hamza aliingia katika  magesho ya B1 na  aliweza kuona magari  kumi  na yote alikuwa ya kifahari , gari pekee ambayo ilikuwa  ya bei rahisi ilikuwa ni  BMW Z4, halafu  inafuatia  Mercedenz Benz ML 400 , kisha BMW X6 na kuendelea  , ikiwemo Porsche 911 latest model  na pia  hata ile Maserati  ambayo Regina alitumia mara ya mwisho ilikuwepo..

Previoua Next