Reader Settings

SEHEMU YA 19.

Kitendo cha Linda kumwelezea namna utaratibu wa CEO unavyokuwa  kila akifika kazini , hatimae  lift iliweza kufnguka katika floor ya saba  na ndio sehemu ambapo idara ya  uwekezaji inapatikana na meneja wa idara hio alikuwa tayari  ameshaandaa nyaraka nje ya lift  na kumpatia Regina.

“Mkurugenzi  malighafi mpya ambazo zinatengenezwa  na Taita Chemical, zinaenda kubadilisha  kabisa teknolojia ya utengenezaji wa raba  na kuzima teknolojia ya  zamani katika maeneo mengi , hii itapelekea kupunguza gharama za  udhalishaji  wa bidhaa zote zinazotumia  raba kwa zaidi ya asilimia arobaini na tano, tulikubaliana  katika kikao  kuongeza hisa zetu ndani ya kampuni ya Taita kwa asilimia 4.3%”Meneja wa idara ya uwekezaji alisoma ripoti  kwa haraka.

Regina alipitia nyaraka ambayo alikuwa amekabidhiwa haraka haraka  na baada ya pale aliitupia kwenye lift  na ukauzu ukamvaa.

“Uza  hisa zote tunazomiliki ndanni ya kampuni ya Taita”Aliongea na kauli ile ilimfanya  meneja kushangaa , kana kwamba amesikia vibaya.

“Mkurugenzi kwanini  kuuza katika wakati  muhimu kama huu?”

“Bidhaa zao zinaenda kupoteza  thamani muda si mrefu na kudorora  sokoni hivyo hisa zao kushuka”Aliongea na kauli ile ilimchanganya meneja.

“Umeshindwa kuona  mabadiliko ya   wafanyakazi ndani ya kampuni ya Taita , unadhani ni kwanini  idara ya usafirishaji  imeongeza  wafanyakazi  katika maghala yao?”

“Kwasababu  uwezo wao wa kudhalisha umefika  mwisho , hivyo  presha ya  bidhaa kuwa kubwa kuliko uwezo wao.., kwanini sikulifikiria hili”Aliongea yule Meneja huku akijiona mzembe .

Meneja yule kabla hata hajaanza kutaka kumsifia  Regina kwa  uwezo wake wa kuona  mbali  Linda alikuwa ashabonyeza kitufe tayari na lift ilijifunga.

Ilienda kufunguka tena katika floor  nyingine na Regina hakutoa kwenye lift lakini mbele yake kulikuwa na  mwanamama wa makamo  na alimkabidhi Linda nyaraka ambazo alimpatia Regina.

“Mkurugenzi!, Farida Group hawapo tayari  kuhamisha  umiliki wa ardhi kwetu, wanasema wanataka ongezeko la milioni mia mbili ,  tuchukue hatua gani?”

Regina palepale alichukua  karamu ya rangi nyekundu na aliandika maandishi makubwa  kwa lugha ya kingereza

“Waambie tutawaongezea mpaka milioni mia tano’

Mwanamama yule mara baada ya kuona maandishi yale alishangaa  na aliona pengine  Boss wake amekosea.

“Mkurugenzi wanataka   ongezeko la thamani la milioni mia mbili tu”

“Fanya kama nilivyokuambia , kisha subiri  mpaka wafanye maamuzi na kuja kwangu kwa  ajili ya  kusaini”

Mwanamama yule  aliishia kutoa mdomo tu  lakini aliishia kutingisha kichwa asijue  bosi wake anachopanga ni nini.

Lift ilijifunga  tena  na Hamza ambae alikuwa amesimama nyuma ya Regina  alikuwa kwenye dumbuwazi na  alishikwa na shauku ya kutaka kujua  kauli ile ilimaanisha nini.

“Mkurugenzi au nimesikia vibaya , kama  wanahitaji ongezeko la thamani ya milioni mia mbili  kwanini  uwaongezee  mpaka milioni mia tano , inamaana unatoa milioni miatatu ya bure?”

Regina hakujibu swali lile kwani Lift  ilikuwa ishafunguka tayari  na kwa mara nyingine kulikuwa tayari na mtu aliekuwa akisubiri na alikabidhi nyaraka ambazo zilisainiwa na Regina.

Floor kwa floor mwanamke huyo alipita  na kila floor alikuwa akifanya maamuzi  na kuweka sahihi baadhi ya  mambo  kwa umakini mkubwa  na mengi ya maamuzi yalikuwa kinyume na  meneja wa  idara husika lakini licha  ya hivyo hakuna ambae alipinga maamuzi yake , ilikuwa ni kama vile  walijua   maamuzi yake yapo  sahihi zaidi kuliko ya kwao waliokubaliana.

Kilichomshangaza zaidi Hamza  ni  namna 

walivyofika katika floor ya juu zaidi baada ya kukutana na mama mtu mzima alieonekana kuwa  na uzoefu wa muda mrefu lakini  alitii kauli ya Regina  bila ya kuuliza kabisa.

Baada ya kumaliza floor zote za jengo hilo , hatimae  walifika floor ya juu kabisa ambapo ndio ofisi  ya mrembo huyo hupatikana , ilikuwa ni ofisi kubwa mno  yenye vioo vikubwa ambavyo havipitishi risasi 

Kupitia madirisha hayo ya vioo alikuwa na uwezo wa kuona  hadi maeneo ambayo yapo nje ya jiji  la Dar es salaam.

Hakukuwa na mapambo mengi ukiachana na  vyungu vya maua  na shelf kadhaa za mafaili , yaani  ilikuwa ofisi kubwa  lakini vitu vichache na rangi yake iliendana na wajihi wa  Regina kabisa.

Regina alikaa katika kiti chake cha kibosi huku kulia akiwepo Hamza na kushoto  akiwepo  Linda ambae alimkabidhi Regina  nyaraka nyingine kuzipitia.

Regina alitumia muda mrefu kidogo kupitia zile nyaraka na Hamza alionyesha kuchoka hivyo alijikalia zake kwenye sofa huku akicheza game la pooltable kwenye simu yake lakini muda uleule Regina aliinua macho yake na kumwangalia.

“Linda mpatie nyaraka za Farida  Group”Aliongea Regina na Linda alifungua faili kupitia kishikwambi na kumpatia Hamza ambae alianza kusoma mara moja 

“Hii inahusu nini?”

“Si uliuliza  swali kwanini nimeongeza  pesa zaidi licha ya  ongezeko la thamani waliloomba katika kipande cha ardhi nilichotaka kununua?”Aliuliza Regina  na Hamza alitingisha kichwa.

“Sasa nakupa nusu  saa unitafutie sababu kwanini  nimefanya maamuzi  hayo  kupitia hizo taarifa za kiuchunguzi  za kampuni ya Farida  Group , ukifanikiwa  utapatiwa ofisi ya kwako peke yako”

“Ofisi ya kwangu , unamaanisha  itakuwa na tarakishi kabisa?”Hamza alikuwa  na mpango wake , alijua  ofisi kubwa kama hizo zina mtandao  wa internet wenye spidi hivyo atatumia muda huo kutengeneza pesa online.

“Ndio, kila kitendea kazi”Aliongea  na Hamza aliona vizuri na  kwa haraka sana alianza kusoma taarifa  hio.

Regina hakumjali tena , alichokifanya ni kwa ajili ya kumzuia  Hamza  kuwa  bize kwa muda , akijua fika hawezi kupata sababu ndani ya muda  wa dakika ishirini ,hata Linda mwenyewe alijua  kabisa  Hamza hawezi kutoboa  na  kujua sababu , lakini baada ya dakika tano  Hamza  alipumua kwa nguvu huku akijinyoosha.

“Nini tatizo?”Aliuliza Regina.

“Acha kumsumbua Mkurugenzi na sauti zako za ajabu”Aliongea Linda kwa kuonya 

“Sio kama namsumbua ,  nishaona sababu tayari”

“Mh , nakupa nafasi nyingine   tafuta kwa umakini”Aliongea  Regina , hata Linda mwenyewe alijua  haiwezekani kwa muda mchache hivyo , ukweli ni kwamba alijua  Hamza hata hakumaliza kabisa kusoma taarifa yote maana  ilikuwa na kurasa za kutosha.

“Farida ni kampuni ambayo  ineonekana imara kwa nje lakini kwa ndani wapo katika hatari ya  mlolongo wao  wa  kimapato . kama hii ardhi hawatoiuza  mapema  ili kupata pesa , kuna uwezekano wakafirisika”Aliongea Hamza  na kauli ile ilimfanya Regina kumkazia Hamza macho 

Katika akili yake alikuwa akishangaa na kujiambia yaani ndani ya dakika tano tu alikuwa ashaona  taarifa iliojificha ya namna hio  katika nyaraka hio , spidi yake ya kusoma  aliona  ni ya kutisha  mno.

Linda hata yeye alikuwa kwenye mshangao , hakuamini kama Hamza aliweza kumaliza kusoma  tayari hio nyaraka  ndani ya dakika chache.

“Murugenzi  niseme  tu mbinu yako  ni  kuntu sana , kama ungeongeza milioni mia mbili  kama walivyohitaji wangekuuzia haraka , lakini  kitendo cha  kuongeza milioni  mia tano zaidi  watapatwa na mashaka  na kujiuliza kwanini unataka kununua  ardhi yote kwa gharama kubwa kiasi hicho , watajiuliza au kuna kitu ambacho hawakuzingatia kuhusu hio ardhi ambacho kinaweza kukupa  faida kubwa , kwa mbinu hio watasita kwanza kuuza ili wajue sababu ya wewe kutaka kununua kwa  gharama kubwa , lakini wakati huo hakuna kampuni ambayo itakuwa tayari kununua ardhi kwa bei kichaa kama hio  , hivyo  wasiwasi wao  utawafanya kupitisha siku muhimu ya kuuza  na siku  watakayo ona wakuuzie  kwa  ongezeko la milioni mia tano  , unachofanya ni kuwakataa  tu kiana   na hawatakuwa na jinsi tena , mwishowe watakuuzia  kwa thamani ya  mwanzo  kabisa, hawatokuwa  hata   na ubavu wa kuomba kuongezewa milionni mia mbili nyingine kwasababu hawana muda wa kutafuta mnunuzi mwingine”

Baada ya  Hamza kumaliza kuongea  Regina  macho yake yalionyesha ishara ya kuridhika na jibu lake , aliona hakuwa amekosea tokea mwanzo , ijapokuwa Hamza anaonekana kama  mwanaume muhuni muhuni mwenye tamaa na mbahili  lakini akili yake ilikuwa ikifanya kazi vizuri , anao uwezo wa kujifunza na kuelewa kitu kwa haraka na kwa tabia hio  ana uwezo wa kufanya  jambo kubwa baadae. Hayo ndio yalikuwa mawazo ya Regina kwenda kwa Hamza.

Linda  ambae alikuwa pembeni ya Regina  alijikuta akishagnaa pia , aliona alikuwa amemchukulia poa huyo msaidizi mpya wa bosi wake  lakini aliona  yeye ndio alikuwa na makosa , inakuwaje bosi  wake mwenye akili kubwa  kutafuta mtu ambae  hana uwezo , hivyo hakumpa sifa  Hamza  kwa kuwa na akili  bali  sifa alizielekeza kwa bosi wake  kwa kuwa na  jicho  la ziada katika kujua  uwezo wa   mtu.

“Murugenzi, kama hii mbinu  ikifanikiwa , nakuambia  watu wa kampuni ya Farida watakuchukia kufa , watapata athari kubwa za mzunguko wa pesa ndani ya kampuni yao”Aliongea Hamza.

“Ukiwa mfanyabiashara , soko unalichukulia kama uwanja wa vita , kwasababu wao wenyewe  ndio wameonyesha tamaa na kwenda kinyume na bei ya mwanzo , sidhani  wanahaki ya kunilaumu kwa kutokuwa na huruma, pili kama  wana akili ni kheri   wakanifuata na kuniuzia ikiwa  mapema , wakichelewa watakuwa wanajiingiza wenyewe katika mtego wangu kwa tamaa zao”

“Bosi , una akili sana , mtu wa kawaida  hawezi kufikiria  kwa namna yako”Hamza alimsifia.

“Hata wewe upo vizuri , sio mbaya umeweza kujua sababu ndani ya dakika  tano tu”

Hamza mara baada ya kusifiwa kwa mara ya kwanza aliachia cheko  lakini ambalo lilikuwa la kistaarabu kidogo 

“Hamna , unajua nini bosi , mimi ni wa kawaida sana, akili yangu ipo ndani ya  wastani  wa kila mtu”

“Don’t be too  arrogant , our CEO  is a member of Pars Society , don’t think that just  because you’re a little smart, you’re  that great”Aliongea Linda kwa kujiamini kwa kingereza akimaanisha kwamba  aache  majigambo  kwani  bosi wake  ni mwanachama wa Pars , hivyo  kwa viakili vyake vidogo asijione mkubwa  na kuanza kupandisha mabega.

Upande wa Hamza alishangaa mara baada ya kusikia  Regina  ni mwanachama wa Pars.

“Kwahio  Boss wetu  ni moja ya wanachama wa  jamii za watu wenye IQ kubwa?”

“Unaonekana kujua  mengi kama umeelewa sentensi

yangu , ndio  bosi wetu  ana IQ 180 hivyo  huhesabika kama Genius , kama sio hivyo unadhani kwanini kila  mtu ndani ya kampni anaamini maamuzi yake na kuyafauta?”

The Standard wisdom societies  ni  umoja   ambao wanachama wake  wana IQ kubwa, inasemekana ili kujiunga katika umoja huo  mtu anapaswa  kufikia angalau vipimo vya IQ  kuanzia 175 na kuendelea , sio   umoja ambao unaweza kujiunga kwa pesa  na hadhi.

Kwa  kadri ambavyo  alikuwa akielewa watu ambao huhesabika kama Genius  ambao IQ zao ni kuanzia 180 wana uwezo wa juu sana katika maswala ya kitafiti , ubunifu  na biashara , lakini wakati huo huo  wakiwa vibaya sana katika baadhi ya  sehemu  kiasi kwamba wanaonekana kama watu dhaifu.

Kwa lugha nyepesi ni kwamba  majiniasi wanaweza kuwa juu ki  uwezo  aidha iwe katika maswala ya kitafiti au  biashara lakini likija sehemu nyingine  wanafanya vibaya sana , na hili linaweza kukushangaza, ki ufupi ni kwamba wanaonekana sio wa kawaida na maamuzi yao yanaweza kuwa ajabu mno.

Hamza aliweza kuliona hilo , hasa ukizingatia na tabia ya  Regina mbele ya familia yake, alikuwa  na mahusiano mabaya sana na  baba yake.

“Huruhusiwi kuongea kuhusu jamii hio  tena siku nyingine”Aliongea Regina na kumfanya Linda kufubaa kwa kuona alifanya kosa, lakini aliitikia kwa adabu. 

Hio ndio moja ya sifa nyingine ya Regina ,  wafanyakazi wa kampuni hio walikuwa wakijua taarifa hio nyeti juu ya kuwa mmoja ya mwanachama wa  jamii ya watu wenye busara  na  hawakuwa wakizungumzia hilo hadharani.

Sasa  hata wakurugenzi wa bodi walielewa  kwanini  Mkurugenzi wa Zamani yaani babu yake Regina aliweka ngumu kumfanya msichana mdogo aliekulia katika kituo cha kulelea Yatima kuwa kichwa cha kampuni , kwa taarifa walizokuwa nazo alionyesha kuwa na akili isiokuwa ya kawaida tokea akiwa mdogo, kitu pekee  ambacho wakurugenzi wa bodi hawakuwa wakifahamu ni  ukichaa wa Regina, kutokana na Regina kuwa na akili nyingi ndio moja ya sababu ambayo  ilimpelekea kuwa na ugonjwa  wa  nafsi mbili.

“Mnaweza kuondoka sasa, Linda muonyeshe Hamza ofisi yake”Aliongea  Regina.

Hamza alikuwa na hamu ya kuona ofisi yake hivyo hakuwa na pingamizi na mkufuata Linda  kwa haraka.

“Linda ,vipi kama nisingeweza kujibu , ni ofisi gani ningepelekwa?”Aliuliza Hamza mara baada ya kufikishwa katika ofisi  ndani ya floor hio hio  ambayo ilikuwa haina vitu vingi  zaidi ya tarakishi  ya thamni ya kampuni ya Apple na printer

“Haijalishi ungejibu kwa kukosea au  kupatia , hii ofisi ndio niliandaa tokea juzi kwa maelekezo ya boss”

Hamza aliona kabisa Regina alikuwa akimchora tu , aliona kabisa Regia anatumia akili yake vibaya  kumchezea akili.

Hamza mara baada ya kuchunguza tarakishi hio  alitoa tabasamu , ilikuwa na sifa zote za kuitwa tarakishi yenye uwezo wa  juu  na kwa kuliona hilo alijua kabisa mpango wake wa kuvuna Bitcoin ungeenda vizuri  sana. Mara baada ya kujinyoosha kwa kuanza kazi yake ya kutengeneza pesa, Linda aliingia akiwa na rundo la nyaraka na kuzitua mezani.

“Boss amesema unajua kuongea kifaransa kwa ufasaha , anataka utafsiri  nyaraka zote kuwa katika lugha ya kingereza , ndio kazi yako utakayofanya  kwanzia leo mpaka Ijumaa, ukimaliza print na niletee ofisini kwangu mlango unaofuatia”Aliongea  katika sauti  ya kiheshima.

Hamza alipitia nyaraka hizo kwa haraka haraka na aligundua ni taarifa za moja ya kampuni ya kifaransa  na ilionekana  ni nyaraka ambazo hazikupatikana kirahisi ndio maana hawakutaka mtu wa nje ya kampuni kuzitafsiri kutokana na unyeti wake.

“Huyu mwanamke , inaonekana alikuwa  amepanga kunipa kazi tokea muda mrefu na sio kwasababu ya  kumdanganya Eliza”Aliwaza  Hamza mara baada ya kuona kazi ya kwanza ni  kutafsiri kifaransa. “Naona sasa nina kazi ya kufanya”

“Hakikisha unafanya kazi na huleti uzembe  , kampuni  yetu inajali  sana watu wachapakazi na sio watu wazembewazembe kazini”

“Sawa”

Alijibu Hamza  lakini mara baada ya  Linda kutoka Hamza alikimbilia mlango na kuufunga kwa ndani na  kisha  alirudi  kwenye tarakishi yake na  kuanza kazi  ya kutengeneza mzingira ya kuvuna sarafu.

“Kama nilivyotarajia  spidi ya hii internet ni kiboko”Alijiongelesha Hamza , lakini  alishituliwa  na  simu yake ilioanza kuita , aliitoa mfukoni  na mara baada ya kuangalia jina la anaepiga ni mama Iryn.

Hamza alishasahau kama alikuwa na mwanafunzi  na  ni kama simu hio ilimkumbusha alikuwa na miadi  ya kumfundisha Iryn wiki hio.

“Habari za  uzima mwanangu?”Sauti iliita , Mama Iryn alikuwa akipendelea kumuita Hamza   mwanae.

“Salama  kabisa mama , habari za nyumbani?”Hamza aliongea alikuwa  na upole  kabisa.

“Salama  kabisa , wiki hii mwanafunzi wako alikungojea hujatokea , kanikumbusha nikupigie simu”Hamza mara baada ya kusikia kauli ile  alishindwa kujua afanyaje , kama ingekuwa siku kadhaa nyuma asingekuwa  na shida ya kujibu lakini muda huo ni mwajiriwa wa milioni kadhaa hakuona haja ya kwenda kufundisha.

“Naomba unisamehe sana mama , ila nipo field  kwasasa , muda wa masomo unanibana sana , semister  yetu  hii ya mwisho mwisho”Hamza alijitetea , ndio  namna pekee alivyoona  ajibu. “Oh! , ndio nilichomwambia  Iryn lakini hanielewi , mimi naelewa upo mwaka wa mwisho na unahitaji muda mwingi kujiandaa”

“Ni kweli kabisa mama , nahitaji muda wa kujiandaa”Aliongea Hamza , ukweli ni kwamba hajawahi hata kufanya discussion  na wenzake , maisha yake ya chuo  yeye ni kama vile  anafanya utani , lakini likija test hajawahi kufeli.

“Basi  hakuna shida baba yangu , nikutakie masomo mema na kujiandaa kwema”

“Asante  mama  nikutakie na wewe afya njema na  masomo mema kwa Iryn”

Baada ya kuongea hivyo   mama Iryn aliaga na kukata simu na kumfanya Hamza  avute pumzi na kujiambia ni bora kukiepuka kikombe hicho,alijua  kwenda kwa Iryn kwa vyvoyte  vile ni kujiingiza kwenye majaribu ya  mwanafunzi  huyo wa Advance.

Hamza hakutaka kuwaza sana na alirudi kwenye kazi aliokuwa akitaka kuendelea  nayo.

Baada ya  kupoteza lisaa lizima kwenye  mtandao wa Blockchain  alirudi katika kazi ya kutafsiri , Hamza aliangalia nyaraka alizokuwa amepewa na aliona haikuwa kifaransa kigumu,  ni kile  cha kibiashara hivyo alikaa vizuri kwenye tarakishi na kuanza kuchapa  kwa spidi kubwa , alikuwa na spidi sio ya kawaida  na ndani ya masaa matatu  bila ya kupumzika alikuwa amemaliza kila kitu  na alipoangalia saa  ilikuwa ni saa saba kasoro mchana, hivyo alimalizia kuprint kabisa.

Baada ya kumaliza alisimama na kuanza kujivuta vuta lakini ni dakika hio hio sauti kutoka nje  pamoja na kugongwa kwa mlango ilisikika , alikuwa  ni Linda aliekuwa akimtaka kufungua.

“Kwanini umejifungia?”

“Ofisi ni yangu ni maamuzi yangu kufunga  na kufungua”Aliongea na kumfanya Linda  amwangalie kwa kejeli  huku akimpita na kusogelea tarakishi. “Ulichokuwa ukifanya umeficha wapi?”Aliuliza  

“Nliichokuwa nikifanya, unamaanisha  nini?”

“Ulikuwa ukicheza michezo yako ya Blockchain”

“Umejuaje nilikuwa nikifanya hivyo?”

“Unadhani  idara ya  IT inafanya kazi gani ,spidi ya Internet ilipungua kwa kiasi kikubwa na  kufanya uanze kufuatiliwa unachofanya”

Hamza mara baada ya kusikia hivyo alijikuta akianza kujikuna kichwa na kuona  ni ukatili kwa kampuni kufatilia  kile wanachokifanya wafanyakazi ndani ya ofisi zao.

“Nimepewa maagizo nikakuripoti kwa  Mkurugenzi  na kulingana na sheria mshahara wako unakatwa asilimia ishirini”Mara baada ya kuongea kauli hio  Linda aligeuza kutaka kuondoka.

“Hebu subiri kwanza , kazi ulionipatia nishaimaliza , kwanini mnikate mshahara , sikuwa na chakufanya ndio maana  nikaingia kwenye  vitu vingine”

“Unaongea nini wewe , yaani umemaliza  kazi ya siku tatu  ndani ya masaa machache?”

“Ndio , kama huamini  angalia , sikupata muda tu wa kukukabidhi kazi”Aliongea Hamza huku akimpatia  Linda  katarasi ambazo ashamaliza kuziprint.

Linda alijikuta akishangaa mara baada ya kukagua karatasi hizo , zilikuwa zimeandikwa   kwa usanifu mzuri sana tena kwa  kingereza  rasmi  cha  kikazi kabisa, lakini hata hivyo hakutaka kumuamini , aliingia kwenye mtandao na kujaribu kukopi na kupaste  baadhi ya maneno ya kifaransa   katika programu ya kutafsiria  ili kuhakiki na kweli  ilikuwa sahihi kabisa  na aliishia kumwangalia Hamza kwa maswali mengi.

“Umewezaje kukamilisha kazi hii kwa muda mfupi tu?”Aliuliza  na Hamza alitingisha mabega.

“Halafu  kuna  baadhi ya maneno yalikosewa  kuandikwa , nimeyawekea alama  na kisha nikayabadilisha wakati wa kutafsiri unaweza hakiki pia”Aliongea Hamza  huku akimkabidhi Linda zile karatasi nyingine.

Linda aliishia kumwangalia  Hamza kwa sekunde kadhaa na kisha akageuka.

“Ni muda wa lunch  unaweza  kwenda kula , nitampatia  hizi nyaraka  mkurugenzi”

“Subiri kwanza ,vipi kuhusu mshahara wangu sasa?”

“Kwa leo nitaacha hili lipite , ukirudia tena kufanya mambo nje ya utaratibu wa kazi  kwa tarakishi za kampuni   sitolifumbia macho”Aliongea  na kisha  alifungua mlango kutoka nje.

“Vipi wewe huendi kula , Mkurugenzi yeye anakula wapi?”

“Nipo kwenye diet ,  kuhusu  mkurugenzi hali chakula mchana  , hivyo jali  mambo yako”Aliongea na hakutaka tena kuendelea kuongea na Hamza hivyo aliondoka.

Hamza licha ya kwamba  alikuwa feki mbele ya Regina lakini kusikia kwamba hakuwa akila chakula cha mchana  aliona mwanamke huyo anatia huruma na pengine  jambo hilo hata  Shangazi hakuwa akilijua la sivyo angekuwa mkali,  lakini kwasababu hakuwa na chakufanya aliamua kupotezea na kutoka ndani ya ofisi yake na kwenda chini kabisa mgahawani .

Kampuni kubwa kama hio  hakukuwa na haja ya kuongelea maswala ya  maisha mazuri ya wafanyakazi wakiwa kazini , mgahawa wa kampuni ulikuwa  mzuri mno  na kulikuwa na kila aina ya chakula kizuri

Kila mtu alikuwa bize na chakula , wafanyakazi walikuwa wengi na baadhi yao walikuwa makundi makundi , kwasababu Hamza alikuwa mgeni yeye alienda zake kuchukua chakula na kisha kutafuta pakukaa.

Kampuni hio  ni kama ilikuwa na upendeleo  na wanawake kwani  walikuwa wengi mno kuliko wanaume , Hamza licha ya kwamba alikuwa mgeni hakutaka kujitenga hivyo aliona sehemu sahihi ni mahali ambapo  kuna watu ili kujenga kidogo mazoea.

Lakini kabla hata hajapata sehemu , aliitwa  na kumfanya ageuke na hapo  ndio aliweza kumuona  Asha  pamoja na msichana mwingine aliemfahamu  kwa jina la Mirium ,  walikuwa ni wasichana ambao aliwakuta pamoja  na Eliza wakiwa mwembeni Bar.

“Hello, nakuona Asha ulivyopendeza”Aliongea  Hamza.

“Kwahio umemuona  Asha  tu , mimi hujaniona?”Aliongea Mirium huku akijifanyisha mwanamke  mwenye wivu.

“Ndio”Alijibu Hamza akiwa siriasi  na kufanya warembo wale kumshangaa kidogo na kisha waliangua kicheko.

“Eliza hajarudi kutoka safarini bado , lakini alituambia umepata kazi hapa makao makuu kama msaidizi namba mbili wa bosi , Hamza usitusahau kwenye ufalme wako”Aliongea  Asha   kwa tabasamu.

“Ah! , msinitegemee sana , mwenyewe sijui ni kwa muda gani nitafanya kazi , pengine ninaweza kufukuzwa ndani ya miezi mitatu tu”

“Sio kirahisi hivyo , kama umemfanya bosi kukupa kazi muhimu kama hio basi ni wazi upo vizuri  

upstairs “

“Hebu  acheni soga  bwana , tutafuteni pakukaa kwanza muda unaenda”Aliingilia Mirium ambae alionekana kuchoka kusimama na kuachwa kwenye mazungumzo.

Baada ya kusogea upande wa kushoto  mwa mgahawa huo  Hamza aliweza kuona nafasi za wazi na kulikuwa na mwanamke mmoja  tu aliekuwa akila peke yake  na alimfahamu ,  alikuwa ni  Kapteni Yonesi  mkuu wa idara ya usalama wa kampuni.

“Twendeni pale”Aliongea Hamza, alitokea kumkubali  Yonesi , ijapokuwa alikuwa na tofauti sana na  wanawake wengi waliokuwa hapo ndani lakini   ukauzu wake ulimfanya kuvutia , isitoshe alikuwa mrembo

“Unamaanisha tutakae na Kapteni Yonesi, Akha hatuendi pale sie”Aliongea Asha.

“Kwanini sasa , yule si mtu kwanini kama mnamnyapaa?”

“Ana sheria  ngumu sana  ukikaa nae kwenye meza , hataki muongee ongee wakati wa kula, hasa umbea umbea , yaani ukikaa nae Mjeda yule hakuna amani na chakula  ni kama unakula sumu”Aliongea Mirium.

“Halafu ukimchokoza kidogo tu atakasirika , lazima akushikishe adabu , ni mkali mno   mbele ya wafanyakazi , na hakuna wa kumfanya lolote maana anaaminiwa sana na  Mkurugenzi”

“Hamza usije kujaribu bahati yako pale , kuna wenzako  waliowahi kufika hapa na wakajifanya wana swaga na kuanza kutupia  maneno pale , kilichowakuta ni udhalilishaji”Asha naMirium walikuwa wakipokezana kumjadili Yonesi na  washasahau walikuwa wameshikilia vyakula mkononi.

“Kama nyie  hamtaki kukaa pale ,  tafuteni eneo lingine mimi nitakaa”Aliongea Hamza na  hakusubiri hata majibu yao na alitembea  mpaka  katika meza  aliokaa  Kapteni Yonesi.

Wafanyakazi waliokuwa ndani ya mgahawa huo waliona kitendo kile na kwasababu walishamjua Hamza ni mgeni , walitaka kuona kile kitakachotokea.

Yonesi alikuwa zake bize na chakula na mara baada ya kuhisi mtu kuongezeka katika meza yake ndio aliinua uso wake na alishangaa kumuona ni Hamza.

“Ni wewe?”

“Niambie Kapteni   naona tunakutana tena”Aliongea Hamza   akiwa na tabasamu na kukaa mkao wa kula.

“Kakae kwenye meza nyingine”Aliongea  Yonesi , kibabe.

 

 

 

Previoua Next