Reader Settings

Wakati  Regina anaamka alijikuta akiwa kwenye gari  akiwa ameegamia kwenye siti.

Alijikuta akivuta kumbukumbu ya kile kilichotokea  na alikaa kitako kwa haraka na ndipo aliweza kuona gari ipo kwenye mwendo  na Hamza ndio dereva.

“Regina umeamka , vipi unahisi

kizunguzungu?”Aliuliza Hamza  akiwa amegeuka na kumwangalia na tabasamu.

Regina alijikagua na kukagua mazingiara na kuthibitisha alikuwa salama.

“Wewe ndio umeniokoa?”Aliuliza

“Unaweza kusema hivyo , lakini haina haja ya kunishukuru , isitoshe  hili limekutokea kwa sababu   yangu “Aliongea Hamza  

Regina aliishia kubakia kimya , alikuwa na hisia zisizoelezeka katika  moyo wake  na kujiambia inamaana huyu mwanaume ni kweli  ameamua kuhatarisha maisha yake kweli na kuja kumsaidia.

“Umewezaje kuniokoa  kwa wale watu?”Aliuliza maana  alikuwa  hana fahamu wakati Hamza akikinukisha.

“Nilifika pale na kisha nikawashushia kipigo , walivyoona hawaniwezi wakakimbia”Aliongea  Hamza.

“Acha kunidanganya , mimi sio mtoto , wale watu walikuwa na visu na  bunduki , halafu wewe ambae ulikuwa mikono mitupu ndio umewaweza mpaka wakakimbia?”Aliongea huku akionyesha kukasirika maana  Hamza anamchezea akili yake  kwa kumwambia uongo.

“Regina  wewe hujui tu ,  lile lilikuwa kundi la watu wazembe , walikuwa wakikukuogopesha tu uwaone  sio wa kawaida . halafu  ile bunduki ulioona  ni feki , ni kama zile wanazochezea watoto”

“Kama unachosema ni kweli , basi niambie kitabu cha Anka ndio  nini , walisema sijui cha mti wa uzima?”Aliuliza huku akimwangalia  Hamza kwa macho makali.

Hamza alijikuta akiingiwa  na ubaridi mara baada ya kuulizwa swali  lakini alirudi katika hali ya tabasamu kuficha wasiwasi wake.

“Anka ndio nini?”Aliuliza lakini kauli ile ilimfanya  Regina  asage meno yake kwa hasira.

“Wewe ni nani haswa , unajulikana kama mwanafunzi wa chuo   na  fundi,au wewe sio mwanafunzi kweli kama ulivyosema , kuna kitu unajaribu kuficha sio?”Aliuliza.

Hamza alijua hakuna uwezekano wa kumdanganya mwanamke huyo ambae vipimo vya IQ yake ni 180, hata kama anaweza asiwe vizuri kwenye maswala ya kimaisha lakini  katika kitu  muhimu kama hicho ambacho kilihusisha uhai wake ingekuwa ngumu kuepuka bila ya kujibu  swali  lake.

Lakini Hamza alijua kama  Regina atajua vitu vingi kuhusu yeye basi moja kwa moja angekuwa katika hatari.

Alitaka kujali usalama wake  sana  kuliko kitu chochote ili isije ikatokea ajali huko mbele ya safari.

Hamza alienda kusimamisha gari  ndani ya mgahawa wa Golden fork  Mbezi beach.

“Hebu  tutoke tukale kwanza , baada ya kumaliza kula  nakuahidi nitakujibu maswali yako yote , sawa?”Aliongea  Hamza.

Ni muda huo huo ndio  Regina alijua kumbe walikuwa mbali sana na nyumbani , nje kulikuwa na giza hivyo hakuweza kuangalia hata walikuwa wapi.

“Kwanini tule hapa?”Aliuliza  

“Saa tatu  usiku sasa hivi , huoni kwamba mpaka  tufike na kuanza kutafuta  chakula itatuchosha sana, chukulia  hii  kama nafasi ya mimi kuomba msamaha kwa kilichokutokea, au  unataka kula chakula kilichopikwa na shangazi?”

Regina mara baada ya  kumsikia  Hamza akimtaja Shangazi   ndio  wasiwasi ulimwingia.

“Vipi shangazi anajua kilichonitokea?”

“Usiwe na wasiwasi , nilimpigia simu na kumwambia tupo date”

“Mimi!? , Date na wewe?”Aliuliza huku  akimwangalia  kwa ukali usoni lakini hata hivyo aliridhika  kuona  Hamza alikuwa makini kutompa presha shangazi yake.

Alikuwa na njaa  pia hivyo   aliamua kutoka bila ya kuleta ubishi.

Mgahawa ulikuwa bize,  jiji la  Dar ilikuwa ni tofauti na maeneo mengine , saa tatu  ndio watu walikuwa wakitafuta chakula cha usiku ,  mgahawa huo ulipendwa pia na  wapenzi wanaowatoa out wenza wao, hivyo meza zilikuwa zimejaa watu wawili wawili.

Waliweza kupata meza ya wazi upande wa kulia  karibu na mlango wa kuingilia , watu waliokuwa ndani ya eneo hilo  walikwa wakiwapiga macho mno..

Ukweli ni kwamba walikuwa wakiendana sana , kwa urembo wa  Regina na muonekano wa  Hamza hakukuwa na tofauti kubwa kati yao  na hakuna ambae anaweza kubisha kama wawili hao sio wapenzi.

Lakini  macho ya wanaume  yalikuwa yakimwangalia sana  Regina ambae alikuw ana urembo usiokuwa wa kawaida , ijapokuwa  nywele zake hazikuwa zimemkaa vizuri lakini alikuwa akivutia mno.

Pia kwa Regina alionekana kuzoea kuagalia hivyo haikumpa  shida , lakini pia  alipenda mgahawa huo.

Hamza aliagiza chakula   kwa wote lakini  aliomba maji  ya kunywa yaletwe kwanza.

“Umesema utanielezea kilichotokea na wewe ni nani , niambie sasa”Aliongea Regina , hakuweza kuificha  shauku yake.

“Usiwe na haraka ,  hebu  tunywe kwanza maji tupoze koo maana siku imekuwa ndefu sana kwetu”Aliongea   huku akimpatia  glasi  yenye maji.

Regina alikuwa na kiu pia hivyo alipokea  na kunywa glasi ya kwanza  akaongeza na ya pili na akawa ametosheka , aliishia kuangalia upande wa nje kana kwamba kuna kitu anafikiria.

“Shangazi alisema wewe ni Yatima, kabla ya kuzamia  nje ya nchi  ulikulia katika kituo gani cha kulelea watoto?”Aliuliza.

“Sikulelewa katika kituo chochote,niliishi mtaani”Aliongea  Hamza, ndio njia jibu  rahisi ambalo  aliona linaweza kumridhisha  Regina  kwa muda huo.

“Ndio maana unaonekana mjanja janja, naamini  haikuwa rahisi kuendesha maisha  mtaani  ukiwa katika umri mdogo”.

“Ni ngumu kwa mtoto  yoyote  asie na wazazi  , iwe ni mtaani  au  katika kituo cha kulelea Yatima , ni swala la unafuu  tu , kulikuwa na watoto wa mtaani ambao wametoroka vituo vya kulelea Yatima pia”Aliongea Hamza.

“Nimekulia  kituo cha kulelea  Yatima pia , mazingira yanaweza kuwa mazuri na kupata mahitaji yote lakini  kisaikolojia kuna kitu unakosa hasa ukifikia ule umri wa kujitambua , nadhani  ndio maana  baadhi ya  watoto wanatoroka , lakini  ni kheri kituoni kuliko mtaani , ni asilimia ndogo sana  ya watoto wanaokulia mtaani kuwa na  maisha ya kawaida”

“Nakubaliana na wewe ,  Vituo  vya kulelea Yatima ni  njia nzuri kimalezi   kwa Yatima kuliko mtaani ambako watoto hujenga tabia  za  ajabu , lakini  vipi  kama wale wamiliki wa vituo wakiwa na ajenda nyingine juu ya watoto hao?”

“Unamaanisha  ajenda  gani  kwa mfano?”Aliuliza Regina  lakini muda huo  waliletewa chakula chao na kumfanya Regina kukikagua.

“Sipendi vitunguu vya hivi  mimi?”Aliongea  Regina mara baada ya kuangalia namna samaki alivyopikwa kwa kuungwa na Scallion(Vitunguu vya kijani).

“Hio ndio  Recipe  sasa  inafanya samaki  walioungwa na Scallion kuwa watamu, inakuwaje hupendi  vitunguu vya kijani  wakati ni vizuri zaidi kuliko vitunguu  aina ya Bombay, kama vipi  niongee na watu wa jikoni wakubadilishie”

“Acha tu , hata Shangazi anavipenda kweli .. halafu mbona unaongea  kwa kukunja sura  hivyo kama unanifokea”

“Nimekufokea saa ngapi  wakati nilikuwa nikikuelezea faida  yake , au ndio umechukia  kukuchagulia chakula chenye viungo  usivyopenda”

‘Sijamaanisha hivyo , ila tu sipendi  harufu ya hivi vitunguu”

“Mh, inaonekana  Shangazi anafanya  juhudi kubwa  kukuridhisha na chakula anachopika”Aliongea Hamza huku akichezesha vidole.

“Haikuhusu , nitakula  hizi chipsi tu ,  hao samaki kula wote mwenyewe”Aliongea  kibishi  na kumfanya Hamza aishie kutabasamu kutokana na ujeuri wa Regina.

“Angalau leo kwa mara ya kwanza na ya mwisho tunakula nje pamoja japo hatujakuwa pamoja kwa  muda mrefu”

“Unataka kusema nini?”Aliongea Regina huku akimwangalia Hamza maana  ni kama amekuwa siriasi  ghafla tu.

“Namaanisha baada ya  kutoka hapa  kila mtu ataelekea uelekeo wake”Aliongea  Hamza  na kumfanya  Regina aliekuwa  akichoma chipsi na uma kusita na kumwangalia  Hamza usoni na ukimya ulimvaa ghafla.

“Umesema unakuja hapa ili kuniambia kilichotokea na wewe ni nani  lakini mwishowe naona  unataka tuachane”.

“Hatuachani kwasababu  uhusiano wetu ni feki , tunachokwenda kufanya ni kusitisha tu  mkataba wa kazi na  kila mtu  kuendelea na maisha yake kama ilivyokuwa”Aliongea.

******

Upande mwingine katika makao makuu ya   kitengo

cha usalama wa taifa kinachodili na nguvu sizizoonekana  kifahamikacho kwa jina la MALIBU kulikuwa na kikao kilichohusisha watu watatu , mmoja akiwa ni Kanali Msuya ambae ni  mkuu msaidii wa kitengo hicho, Kapteni Kwavava  na  Afande Mdudu.

Wote macho  yao yalikuwa kwenye skrini  wakiangalia wanajeshi ambao walikuwa eneo  la tukio.

“Afande wote wamepoteza maisha , hakuna hata mmoja ambae yupo  hai, vifo vyao ni vya kikatili  mno”sauti  kupitia simu ya upepo ilisikika , simu ambayo ilikuwa imeshikwa na Afande Mdudu

Afande Msuya na Afande  Kwavava  waliangalia kwa mshangao  na macho  yao  yalijaa  maswali.

“Inawezekana vipi , au taarifa  tulizopokea zilikuwa hazina ukweli wowote?”Aliuliza  Afande Msuya. “Sidhani kama hazikuwa na  ukweli , intellijensia ile ilikuwa ni sahihi  kabisa  Afande”

“Kwahio inamaanisha aliehusika na vifo vyao  anaweza kuwa na uwezo wa juu kuliko wao?”Aliuliza  na Afande Kwavava aliishia kutingisha kichwa.

“Afande Kiduma  hakikisha mnapiga picha ya  tukio zima na majeraha yao  ili kufanyiwa uchunguzi wa kina”Aliongea Afande Mdudu.

“Sawa Afande”

“Hakikisha hili swala linabakia siri mpaka  tupate ufumbuzi wa  kila kitu kilichotokea”Aliongea Kanali Msuya na  Afande  Mdudu alipiga saluti na  kisha akakaa chini.

“Mnadhani  kuna kitu gani tunamisi?”Aliuliza  Afande Msuya.

“Kwanini  Afande?”

“Hawa wahalifu wameingia nchini kwa zaidi ya wiki mbili  zote , lakini kitengo chetu kimejua  taarrifa ya uwepo wao leo hii na ndio siku wamepoteza maisha  wote, mnadhani hakuna kilichokosekana katika mfumo wetu wa intellijensia?”

“Mkurugenzi , unachoongea ni sahihi  kuna kitu  tunamisi , lakini nadhani hii haimaanishi   kitengo chetu  uwezo wake ni mdogo , ni swala la kuzidiwa  kitaalamu tu na kama ilivyokuwa siku zote ndio namna tunavyochukulia  kama changamoto  ya kujioboresha zaidi”Aliongea Kwavava.

“Hiki ni kipindi  ambacho vitengo vyetu vya usalama lazima  viwe katika ubora  wake  hasa likija swala la kukusanya intellijensia , Uchaguzi mkuu unakaribia  , kosa kidogo   tu  usalama wa taifa unaweza kuwa  hatarini , Wahalifu hatari namna hii wanaingia nchini , lakini  tumeshindwa kuwadaka katika lada zetu za usalama , mtu wa nje anatupenyezea taarifa na  vikosi vyetu vinakuta wamepoteza maisha wote , Nani  mhusika wa tukio  hili la kutisha hata pa kuanzia hatuna”

“Kwa  uchunguzi wa awali wa  Afande Kiduma  anasema  Gonzo Fisheries ndio  wamiliki wa  Ghala, nimeongea na Mzee Sinzwe  hana taarifa ya kukodishwa kwa  ghala lake”

“Inamaanisha vijana wake ndio wamekodisha ghala hilo , kama ni hivyo basi lilikodishwa kwa muda mfupi tu”

“Ndio na kwasasa wote wapo  baharini wanavua  hivyo  imekuwa ngumu kupata taarifa ya kilichotokea”Aliongea  Afande  Mdudu.

“Afande  kwa   taarifa niliozokuwa nazo juu ya  hili kundi  ,  wanajiita Waray Bounty hunters , jina lao la utani ni Tumbili wenye mbawa za mwewe , ukiachana na sifa zao za kimafia na umahili wa kutafuta watu  lakini pia wanahusishwa  kutokea  Biringan”Aliongea Afande Mdudu.

“Unataka kumaanisha nini Mdudu?”

“Kama inavyosemwa ni kweli wanatokea Biringan basi  sio watu wa kawaida ,  sijui kama mnajua hili ila   Biringan  ni eneo ambalo halipo kwenye ramani ya dunia zaidi ya hadithi za  kiimani tu ,  pointi yangu kama watu wa  aina hii wamefika Tanzania  kwa ajili ya  kutafuta  kitu , basi  moja kwa moja  mpango wao umefeli na  kuna uwezekano watarudi wengine”

“Mdudu unapendekeza nini?”Aliongea Afande Kwavava.

“Lazima tujue kwanza ni kipi ambacho wamekijia hapa  Tanzania”

“Nadhanni tunarudi palepale tu , katika uchunguzi wetu tunachotaka kujua  ni nani ambae amehusika kuwaua  na ikitokea  tumemfahamu basi ni  dhahiri huyo ndio wanaemtaka hivyo  tutaweza kupata majibu”

“Kwavava  mkuu wako Dastani ana shida gani siku hizi , kwanini amekuwa bize  sana , mpaka kwenye vikao muhimu kama hivi anakosekana?”

“Amekuwa akiwafatilia wale Wabrazili kwa muda mrefu , nadhani ndio kinachomfanya kuwa bize”Aliongea  na  Afande Msuya alionekana kutoridhika.

“Dastani ndio mtu ambae   ana utashi mkubwa wa mambo kama haya , wasiliana  nae na umshirikishe  huu uchunguzi nahitaji majibu ya haraka”

“Sawa Afande”

“Kwavava   kaa na timu yako  ya intellijensia , nahitaji  ripoti  kamili kwanini idara  yetu inazidi kuwa butu  siku hadi siku  na kushindwa kunusa hatari  kwa haraka”

“Sawa Afande”

“Hakikisheni pia tunajua nani kapenyeza taarifa  ya uwepo wa hawa  wahalifu  nchini kwetu ,  tunaweza kupata  pa kuanzia”Aliongea na  kisha alisimama.

“Afande  kuna taarifa pia nahitaji kuripoti”

“Jnahusu nini?”

“Amosi ameshambuliwa na risasi , yupo  mahututi hospitali ya jeshi?”Aliongea  Mdudu na  ilimfanya  Afande  Msuya  kushangaa kidogo.

“Amosi si alikuwa chini  ya Kanali  Dastani , kwanini  unaripoti  wewe hii taarifa”

“Msemakweli  katika  kampeni zake  ameendelea kuituhumu   kushirikiana na Binamu , nadhani inafahamika  ndani ya kitengo  Amosi ameshawahi kufanya kazi  kama undercover Agent  kwa ajili ya  kuwachunguza Binamu”Afande Msuya alijikuta akirudi kwenye Sofa na kuketi huku akionekana kuwaza kidogo.

“Kuna  uwezekano Binamu ndio walimshambulia , lakini kwasasa hakuna uhakika kwani Amosi bado fahamu hazijamrudia, nina uhakika hili  ndio  sababu ya  Kanali  kutokuonekana katika vikao  vyote leo, ila kama kweli ni Binamu basi  watahakikisha  wanaona kifo chake”

“Mtafute Kanali popote alipo , kesho afike  katika ofisi yangu na ulinzi uimarishwe  katika wodi ya  Amosi ,  tutahitaji  maelezo kutoka kwake”Aliongea na maagizo yale alipewa Mdudu na alitoa saluti na kisha akatoka nje.

“Anachosema Msemakweli sio uongo , lakini hili swala  linachukua sura mpya , kumekuwa na mijadala mingi mtandaoni , inayozusha kile kinachoendelea mtandaoni ,  wengine wanadai  Night Shadows  wapo chini ya Binamu”Aliongea Afande Kwavava.

“Kwavava hivi  unaamini hawa Night Shadows wapo  kama watu wanavyozusha?”

“Kitengo chetu kimekuwa kikifanya uchunguzi kwa muda  mrefu , lakini hatujafanikiwa  kupata ushahidi wa  moja kwa moja wa kuamini, maoni  yangu ni aidha wapo  kweli kama watu wanavyosema au  kuna kundi la  watu wanajaribu kujaza watu hofu”

“Sio sisi tu ambao tunawafuatilia hawa Nightshadows, serikali zote kubwa wanafatilia hili lakini hakuna ushahidi unaotolewa, inanifanya mwisho wa siku kuamini ni uzushi pia”.

“Lakini Afande una uhakika gani kama serikali kubwa duniani hawana ushahidi  , vipi kama jambo  hili wanalifanya  kuwa siri kama ilivyotokea  kwa tukio lililopita?”

“Kwasasa   ni ngumu kwangu kuweka neno lolote kuhusu hili , isitoshe  tunatarajia serikali mpya hivi karibuni , nadhani tulipe muda kwanza, Kwavava nadhani unajua ninachomaanisha” “Ndio  Afande”.

Previoua Next