Reader Settings

SEHEMU YA 30.

Fellini alifikiria kwa muda na kisha alimwangalia Regina kwa  uso kidogo uliokuwa  hauna ridhiko.

“Miss Regina , naomba nikuambie tu  kwamba  hatuwezi kufanya kazi pamoja  zaidi  kwasababu  hatuna maelewano ya kisera kati ya kampuni zetu”

“Inakuwaje  Mr Fellini , tulijiandaa kukutana na wewe  kwa muda mrefu na tumeshaandaa mipango ya  kibiashara ya muda mrefu  ya ushirikiano wetu, hujaona hata  vipengele vya mkataba  lakini kwasababu ya kutofautiana mtazamo  unatukataa , hii sio haki”Aliongea Linda.

“Wewe  ni msaidizi tu , hujapewa ruhusa ya kuongea”Aliongea Salma.

“Haina haja ya kubembeleza zaidi Linda , alichoongea Mr Fellini ni sahihi kabisa , mimi sina maarifa  mengi likija  swala la fasheni” “Mkurugenzi wewe  sio  mbunifu wa mavazi  na hujasomea  fasheni , haina haja ya kuwa mnyonge , ulichoongea wewe ni katika jicho la kibiashara”

Upande wa  Fellini alionekana kwenye kutafakari kwa dakika kadhaa na kisha aliwaangaia wote wawili yaani  Salma na Regina.

“Mnaonaje tukifanya hivi , wote wawili mmevaa na mmependeza sana , je kuna sababu yoyote ya kuchagua  staili ya mavazi mliovaa leo?,  watu wenye pesa hatuvai kupendeza tu , kuna mengi zaidi ya kuelezea kuhusu aina ya  maisha yetu kupitia nguo , nataka kusikia kutoka kwenu”Aliongea , Fellini hakutaka kuonekana mkatili ndio maana alitaka kumpa Regina nafasi ya mwisho.

“Bila shaka nitaelezea”Aliongea Salma na kisha alisimama  akiwa na tabasamu na kuonyesha vazi lake.

“Mr Fellini  nadhani utakuwa umejua hili ni  vazi  kutoka Louis Vuitton lililovuma  kwenye  maonyesho ya wiki ya  mitindo jijini Paris?”Aliuliza na  Fellini alitingisha kichwa akikubali.

“Hili  vazi linaweza kuonekana la kawaida lakini linadhihirisha  ujasiri wa mbunifu, mpangilio wa eneo  la kiuno  unamfanya mwanamke yoyote  ambae  amevaa  kumpa heshima yake  kwa kuonyesha ni kiasi gani ni mrembo,  dizaini iliotumika  ni ya kibalkani  na udarizi  wa eneo la mkanda wa kiunoni  pamoja na vazi  lote juu hadi chini  linaashiria tabia ,  sifa yangu kubwa ni ucheshi ndio maana nimechagua vazi hili leo hii”Aliongea na kisha akakaaa 

“Vipi kuhusu Miss Regina , wewe unasemaje?”

“Vazi langu ni mtindo toleo la mwisho kutoka Zara”Aliongea na Fellini alitingisha kichwa.

“Najua  kabisa ndio ni kutoka Zara , mimi ndio nilihusika na ubunifu wake, tulilipatia jina la Norse  Goddes style , limekupendeza mno ulivyovaa ni kama tulikutengenezea wewe peke yako”

“Kweli… kwahio staili yake ndio inaitwa Norse , sikuwa hata nikijua , kwa macho yangu mimi ni gauni kama gauni tu, nimenunua  kwa zaidi ya Euro  elfu ishirini na tatu , lakini  sokoni kuna staii hii  hii  bilaBrand ya  Zara na wanauza kati ya milioni moja mpaka tano, kwangu mimi niliona ni vazi linalonipendeza na nikalipenda mno ndio maana  nimelivaa lakini sababu nyingine niliamini kuvaa  mavazi ya kampuni ya  Zara itatuweka karibu zaidi kibiashara”

Mara baada ya kumaliza  Fellin  alishangaa   hata kwa  Linda alikuwa  amekakamaa mwili wakati wa maelezo ya Regina.

Upande  wa Hamza na sikio lake kama  antenna za kisimbuzi  cha Zuku  aliweza kusikia kila kitu na alionekana kumkubali  Regina , aliona ni kama kuna kitu ameelewa katika maelezo yake.

“Mr Fellini nadhani sasa umeona , Regina  kila anachoongea ni katika  msingi wa kibiashara , huyu  ni  mashine ya kutengenezea hela na hajali chochote zaidi ya  faida ,  hawezi kujua thamani  halisi ya vazi nje ya  gharama yake”

Fellini upande  wake alionesha kukatishwa tamaa kabisa na Regina  na  kulikuwa na ishara ya kukereka katika macho yake.

“Miss Regina  nimependa ulivyomuwazi”

“Asante sana Mr  Fellini , natumaini siku zijazo  utajifunza pia kutoka kwangu  na kuwa muwazi, maana umekuja nchini ukiwa  tayari  na mpango wa kufanya kazi na kampuni ya Salah na sio sisi , hivyo sidhani kulikuwa hata na haja ya kukutana”

“Hapana, umenielewa vibaya , sijafanya maamuzi kabla”Aliongea Fellini akijitetea.

“Kutoka mwanzo mpaka mwisho ulikuwa ukiongelea maswala ya utamaduni wa kampuni  na sera  ila hukuniuliza hata  swala  la  soko  lilivyo  na mtaji kiasi gani tulipanga kuwekeza kwenye ushirikiano wetu , unajua  kabisa nimesomea maswala ya uchumi , masoko na usimamizi  , lakini  mmeanza na kuongea  nadharia zenu za fasheni na  mambo mengine ambayo yapo nje ya taaluma yangu , unanilinganisha na Salma ambae  amesoma chuo kikubwa dunniani cha mitindo  na kazi yake ni  ubunifu wa mavazi , ulichofanya ni kama kutengeneza mazingira ya kampuni  ya  Salah kushinda  na si vinginevyo”

Mr Fellini mara baada ya kusikia kauli  hio  alijikuta kwa namna flani akiona aibu  lakini alivuta moshi  wa sigara kidogo kujituliza.

“Kama  ndio unavyoamini basi  sidhani kuna haja ya kuendelea na haya mzungumzo , kwa bahati mbaya hatuwezi kushirikiana na kampuni yako”

“Nashukuru hujachagua kampuni yetu kwani nisingependa kuishi katika ulimwengu  wa kufikirika na mshirika mnafiki”

“Unasemaje , mimi ni mnafiki?”Aliongea  mzungu yule huku  uso wake ukijikunja .

Alikuwa maarufu kwa zaidi ya miaka  ishirini  sasa  na kila mtu alikuwa akimheshimu  lakini leo hii anatukanwa  na msichana mdogo  kutoka  taifa masikini kama Tanzania.

Upande wa Regina hakujali tena kuhusu  hasira za Fellini alimpa ishara Linda na kisha walisimama kuondoka.

“Regina simama  hapo hapo”Alifoka Salma.

“Unaonyesha tabia gani mbele ya  mtu  mwenye heshima zake kama Fellin , unadhani ni mtu unaeweza kumtusi  hivi hivi  tu , omba msamaha kabla hujaondoka 

“Miss Regina nakuhakikishia utalipa kwa  dharau ulizonionyeshea, usisahau  mikataba ulioingia na baadhi ya kampuni za mavazi tunamiliki hisa zetu pia”

Regina alisimama na kisha aligeuka , macho yake ya kirembo yalikuwa na ukauzu usiokuwa wa kawaida. “Kwahio mnajaribu kuniogopesha  na kunitishia?”

“Kwahio vipi , ulimwengu wa mitindo  sio mtu   wa hadhi ya chini kama wewe unaweza kuingia unavyotaka”Aliongea Salma.

“Vyovyote vile , mwisho wa  siku sio mimi nitakae anguka bali ni mtu mwingine”

Mara baada ya kumaliza kauli hio  sauti ya mtu akipiga makofi ilisikika , alikuwa ni Hamza.

“Vizuri sana ,  hakika bosi  wetu   una ujasiri wa hali ya juu,Awesome”Aliongea Hamza huku akicheka akisogea karibu.

Regina na Linda waliishia kushangaa , ni kama sasa wanakumbuka  Hamza alikuwa  hapo , akiwa kimya tu  akisikiliza.

“Wewe ni nani?”Aliuliza Salma huku akikunja mdomo.

“Kwa  majina yangu  naitwa Hamza  Mzee , Msaidizi namba mbili  wa bosi  Regina , kuwa sahihi zaidi unaweza niita dereva wake”

“Haha.. Dereva, Hamza!!”Salma alicheka  kwa nguvu  kwa kejeli.

“Regina vigezo vyako  ni vya chini mno , yaani umemuajiri mshamba  kutoka porini huko kuwa dereva wako?, nadhani  maamuzi ya Mr Felllini ni sahihi kabisa , kufanya  kazi na mtu asiezingatia hadhi ya wafanyakazi wake  ni kujidhalilisha tu  na kushusha thamani ya Brand ya kampuni”Aliongea na kisha alimwangalia  Fellini kama anamsapoti katika dhihaka zake.

Lakini upande wa Fellini alikuwa akimwangalia Hamza kwa  macho kodo kana kwamba alikuwa ameona  mzimu, alikuwa ameshikwa na bumbuwazi ashindwe kusema neno.

Hata kwa Regina waliona muonekano wa  Fellini , alionekana kama ni mtu mwenye wasiwasi.

“Nini tatizo Mr Fellini , huyu mshamba  kakuogopesha?”Aliongea Salma.

“No ,, impossible”Aliongea  Fellini akisema haiwezekani  huku akimsogelea  Hamza karibu.

Mara baada ya kumfikia  alishindwa kujizuia na kunyoosha mkono wake na  kushika kolla ya   nguo alizovaa Hamza.

Cha kushangaza ni kwamba mikono yake  ilikuwa ikimtetemeka  kana kwamba ameshika kitu cha thamani sana.

“Mr Fellini umepatwa na shida gani?”Aliuliza Salma asijue kwanini huyo mzungu   alionekana kama vile amepandwa na wazimu.

Regina  upande wake pia alikuwa kwenye hali ya kushangaa na alijiuliza au  Fellini alikuwa amevutiwa na  uchakavu wa tisheti ya  Hamza 

“Wewe Mzungu vipi , acha kunigusa bwana mimi sio bwabwa”Aliongea  Hamza na kumzuia   Fellini kwa kumshika mkono.

“Umesema unaitwa Mr Hamza si ndio ,  naomba nikuulize swali , umezipata wapi hizi nguo ulizovaa?” “Kuna mzee ambae ni rafiki yangu alinnipatia  kama zawadi , ni miaka mingi kidogo imepita”Alijibu Hamza.

“Mzee  rafiki yako , unaweza kunitajia jina lake?”Aliuliza na kumfanya Hamza kukunja kichwa.

“Mimi napenda kumuita Mzee Roboti , ila jina lake  lote ni   Alec sijui nini”

“Ni Alec Von Blumer sio”

“Ewaaa.. hilo ndio jina lake  yule mzee , amenipa nguo nyingi sana kama zawadi, ni mkarimu sana haha..”

Mara baada ya kusikia hivyo  Fellini alijikuta akijikokota kurudi nyuma  kwa mshangao na alijitahidi  kujiegamiza kwenye sofa asidondoke

“Mr Fellini what wrong?” Aliuliza msaidizi wake  huku  Salma na Regina  wakiwa wameshangazwa pia na tukio hilo.

Fellini kwa haraka haraka alichukua glasi ya maji na kuigida yote  na kuiweka chini akijitahidi kujituliza.

“Master George  Alec Von Bliimer ndio mwalimu wangu , kwa maneno mengine ndio   mbobezi …”Mara baada ya kuongea hivyo  Regina , Linda na Salma walishikwa na mshangao wa kutokuamini.

“Mr Fellini si umehitimu kutoka chuo cha sanaa cha London , kwanini unasema  una mwalimu wako?”Aliuliza lakini  Felini  alimdharau  Salma kwa ujinga.

“The real art of clothing is not  in any   Academy , but in Seville street , Miss Salma  haven’t you heard  about it ?”Aliuliza  Fellini.

“Najua ndio , Sevile ni mtaa  uliopo ndani ya  London Mayfair , sehemu wanapopatikana  mafundi nguo  maarufu , hususani   mafundi wa nguo za kiume, ukisikia  neno ‘Customized clothes’  asili yake ni  katika mtaa huo, wafalme  na viongozi wakubwa duniani  walipendelea sana wazo la kushonewa nguo  zinazoendana na  wao  katika mtaa  wa Sevile , maduka mengi ndani ya  Sevile yana historia ya karne kadhaa”Aliongea Salma.

Ilikuwa ni kweli kabisa, kama ilivyokwa mtu wa kawaida kupendelea kwenda kwa cherehani kushona suti inayoendana na vipimo vya mwili wake basi ipo hivyo  hata kwa matajiri na  viongozi wa  daraja la juu ikiwemo wafalme wa mataifa makubwa.

Sasa mtaa wa Seville ndani ya London Mayfair ndio  kunapatikana mafundi cherehani ambao hushona nguo hizo za watu wazito wazito.

Regina  hata  yeye ashawahi kusikia kuhusu Seville  lakini  hakujua hadhi ya mtaa huo  ilivyo.

“Upo sahihi , tokea nilipokuwa mtoto ndoto yangu ilikuwa  ni  kuja kuwa mbunifu  wa watu wazito wazito duniani , hivyo niliweka bidii na   hatimae nikaja kufanikiwa kuingia  mtaa wa Seville kama  mwanafunzi wa ufundi cherehani na mbunifu , nilijifunza ufundi kwa mwalimu wangu George  na  hatimae nikawa fundi  wa daraja la  chini kigezo ambacho kilinifanya kushindwa kuendelea kuwa chini ya George ,   ni kwasababu  sikuwa na kipaji kikubwa cha ushonaji , hivyo mara baada ya kutopata  nafasi

zaidi  niliamua  kuachana na maswala ya ushonaji

nikaingia chuo “                           

“Nini, Mr Fellin  mbona unakipaji kikubwa  mno , unasemaje huna kipaji”Aliongea Salma.

“Salma unaweza ukwa umemaliza kwenye chuo kikubwa  na ukawa mbunifu wa kimataifa lakini huwezi kufikia hadhi ya mwalimu wangu George ,  wateja wake ni wafalme , malkia , Watoto wa wafalme na Princess  au watu matajiri duniani na wanasiasa wakubwa, hahitaji umaarufu wowote ndio maana wengi  hawamfahamu , unadhani ana haja gani ya kutengenezea nguo watu wa kawaida , ki ufupi muda huo hana  ndio maana hajawahi kujitangaza”

Maneno yale yalimsahgnaza Salma , Fellini alikuwa mtu mzito kwenye ubunifu lakini kulikuwa bado kuna watu wa hadhi ya juu kuliko yeye, liishangaza zaidi na zaidi.

Tatizo  hapo sasa sio swala la huyo anaeitwa mwalimu kushonea nguo watu wazito  , tatizo ni kwamba  Hamza alikuwa amevaa nguo ambazo zimetengenezwa na mtu huyo.

Regina na  Linda hawakutaka kukubali kirahisi , kwani dakika chache zilizopita walikuwa wakibeza mavazi ya Hamza.

Walijikuta wote wakiangalia mavazi  ya Hamza lakini bado yalionekana ya kawaida  mno , aina ya  mavazi ambayo unaweza ukayakuta katika soko la mtumba .

Regina alienda mbali na kukumbuka aligombana na Hamza kwa kutotaka kutupa mavazi yake , alishindwa kuzuia  hisia mbaya zilizoanza kumvaa na kujiambia kama kweli anachosema Fellini ni kweli basi mavazi hayo ya thamani si yatamfanya aonekane mjinga  na mshamba.

“Mr Fellini macho yako yatakuwa yanakudanganya , haya mavazi aliovaa unaweza kuyakuta kila mkoa ndani ya Tanzania yanauzwa”Aliongea Regina kuepusha kuabika.

“Msiniambie hakuna  ambae anaona  uzuri wa mavazi  aliovaa Mr Hamza pamoja na pensi yake?”Aliongea  huku akiwaangalia mmoja mmoja kana kwamba anaomba kuungwa mkono.

Lakini wote walitingisha  vichwa vyao kukataa , hakuna cha maana  kwenye hayo mavazi zaidi ya uchakavu tu”

“Nyie watu hamjui  kabisa , nadhani kwasababu sio mafundi,  katika ulimwengu wa kifundi   utaalamu wa juu zaidi ni  kutengeneza vazi ambalo unao uwezo wa kulirudisha  upya kwa mchakato mwepesi sana na ukauza sokoni kwa bei ileile”Aliongea   mzungu huyo lakini hakuna hata mmoja ambae alielewa anachomaanisha, hata  Salma aliesomea Person chuo  namba moja cha mitindo kutoka Marekani hakuelewa.

MWISHO WA SEASON ONE.

Unadhani Hamza ni  nani mpaka  kuvaa  nguo zilizotengenezwa na  George Alec Von Blumer  fundi nguo wa  wafalme , matajiri  na  watu wa hadhi ya juu.

Unadhani  Hamza  ana siri gani  tokea kuokolewa  kutoka kwenye janga la Radi mpaka kuwa  nchini Tanzania akiwa  mtu mzima.

Vipi kuhusu kitabu  kinachowindwa na  watu , vipi kuhusu lugha iliokuwa katika  kitabu hicho ambayo hakuna binadamu anaeijua , unadhani ni kweli Hamza anao uwezo wa kuijua lugha hio, Frida anamaanisha nini kusema Hamza  kuna kumbukumbu hazikumbuki.

Unadhani Binamu ni  Cousin  mtoto wa Mjomba au

Shagazi au  ni kitu kingine tofauti, vipi Sinagogi ni watu gani.

Wakuu ndio  tunaanza  yani , kuna siri  nzito sana katika hii simulizi , Kodi nyingi  zitatumika.

Previoua Next