Reader Settings

SEHEMU YA 34.

Hamza aligonga mlango kwa muda mrefu kidogo , lakini hakusikia majibu hivyo aliamua kushika kitasa na kuufungua  kisha akaingia ndani.

Mara baada ya kuingia  katika chumba hicho cha kujisomea aliweza kugundua Regina alikuwa amelalia meza akiwa usingizini  ,  huku mbele yake kukiwa na furushi la nyaraka ambazo ilionekana

alikuwa akizifanyia kazi, Hamza aliishia kujiuliza inamaana huyu mwanamke tokea mchana alikuwa akifanya kazi licha ya kwamba ni jumapili.

Hamza licha ya kwamba alikuwa mpenzi feki , lakini  kumuona namna alivyokuwa akijitesa kwa kufanya sana kazi alijisikia vibaya.

Alijikuta akisogea upande mwingine na kumwangalia Regina ,  na kwa jinsi alivyokuwa amelala alikuwa  ni kama  mdoli  kwa jinsi alivyokuwa mzuri , ule ukauzu  wote ulikuwa umepotea  akiwa usingizini na kumfanya kuzidi kuvutia.

“Sura yako ingekuwa  muda wote kama hivi , ingekuwa vizuri lakini  tabia yako ya ukauzu  inaficha  mengi ya kuvutia”Alijiongelesha Hamza.

Chumba kilikuwa na ubaridi wa AC  mkali mno  lakini bado alikuwa  amelala  na kutoa sauti  kabisa , Hamza  hakutaka kumuamsha hivyo aliweka alivyoshika mkononi na aliona shuka  kwenye sofa na  kumfunika lakini kitendo cha kumaliza tu  Regina alishituka.

Aliishia kuegamia kiti chake  huku akitoa miayo  na mara baada ya kufikicha macho yake  ndio sasa anagundua kuna mtu pembeni yake 

Hamza upande wake alikuwa amekodoa macho tu , alikuwa akiushangaa uzuri wa mrembo Regina hata wakati wa kuamka.

“Unafanya nini hapa , nani kakuruhusu kuingia?”Aliongea kibabe.

“Sijafanya makusudi kuingia  bila  ya ruhusa , ulikuwa umelala , Shangazi kanipatia hizi doghnut  na chai nikupe , anasema hujala chakula cha usiku” “Mh Doghnut! “Regina alijikuta akigeuza macho yake  na aliweza kuona Doghnut nane kwenye sahani  na alishindwa  kujizuia zaidi ya kumeza mate.

Kitendo hicho kilimfanya Hamza kuona itakuwa kweli Regina  anapenda sana  hizo Doghnut.

Regina muda ule  alijihisi kuna kitu kilikuwa kimemfunika mabega yake hivyo alipeleka mkono nyuma kukitoa na aligundua ni shuka.

“Wewe ndio ulinifunika?”

‘Ndio ,  chumba umekifanya kimekuwa na ubaridi mkali ndio maana nimekufunuka , haina haja ya kunishukuru kwa upendo wangu”

“Nani kasema nitakushukuru , ulitakiwa kuniamsha baada ya kunniona nimelala sio unanifunika”

“Nilikuwa nikijali kuhusu  afya yako , ningejuaje kama ulitaka kuendelea na kazi”

“Huna haja ya kunijali, hatuna uhusiano wowote , nadhani itakuwa vizuri ukiweka akili  yako kwenye  kumjali mpenzi wako , unaweza kuondoka sasa”Aliongea kikauzu.

Hamza aliishia kupumua kwa masikitiko , alikuwa akionyesha  vitendo vya kumjali kama bosi wake , lakini  anakasirika , alijiuliza kwanini kuna utofauti mkubwa kati ya  Eliza na  huyu mrembo.

Ijapokuwa Regina alikuwa amemzidi kila kitu Eliza kwanzia  muonekano , akili , mali  mengineyo lakini Eliza alikuwa rahisi sana kuishi nae.

“Kheri nikale zangu tembele  kila siku na Eliza  kuliko kula vinono na Regina, mtu gani ana tabia kama za Mzimu uliolazimishwa ndoa bila mahari”Aliwaza Hamza. “Una mwemweseka nini?”

“Hamna , naenda na mimi kula hivyo vitairi”

“Utajua mwenyewe , toka nje”

“Nani kakuambia nataka kuendelea kukaa hapa?”Hamza alitamani kuongea kwa sauti  lakini aliishia kumezea ndani kwa ndani na kutoka  kwa hasira.

Hamza wakati anataka kuelekea kwenye chumba chake Shangazi alimwita tena. “Hamza njoo tena”

“Shangazi kuna nini tena?”

“Nimesahau kuweka sukari kwenye ile chai , hebu nisaidie  ukamuwekee”Aliongea Shangazi na kumpatia Hamza mkononi.

Hamza alitamani kutoa chozi , alijiuliza kwanini huyu  shangazi alikuwa akimuonea hivyo , lakini baada ya kukumbuka ni mpenzi  akiwa hapo nyumbani aliishia kukubali kinyonge.

Awamu hio  alikuwa na hasira hivyo  baada ya  kufikia mlango hakujisumbua hata kugonga na alisukuma mlango na kuingia.

Lakini  picha alioiona pengine  asingeisahau kwenye maisha yake kuonyeshwa na mwanamke kama Regina.

Regina alikuwa ameshikilia   Doghnut mbili mikono yote  huku zikiwa zimeng’atwa zote , mdomo ulikuwa umetuna  kiasi kwamba alikuwa akitafuna kwa shida, kilichomshangaza zaidi alikuwa akitingisha kichwa  kwa furaha zote kiasi kwamba kiti kilikuwa kikinesa nesa.

Hamza alijiambia huyu Regina aliemfurusha ndani kwake  ni wa tofauti sana , kama mbingu na ardhi , hakuwa  na ule kauzu tena bali muda huo ni kama mtoto anaeshindana na chakula.

Hama alijiuliza au  Regina  ana tatizo la akili  la kuwa na nafsi mbili kwa wakati mmoja .

Ughh!!

Regina alijikuta akitoa macho mara baada ya kugundua kuna mtu ameingia  na aligeuza uso wake na kugundua ni  Hamza , aliishia kupepesa macho kama ana kifafa  huku akianza kuwa mwekundu.

Tukio lile lilimfanya Hamza  kujiambia   atakuwa ameona kitu ambacho  hakustahili kuona 

Alijifanyisha Mzembe na kisha alipeleka sukari mpaka kwenye meza.

“Samahani bosi kwa kukusumbua wakati unakula , shangazi kaniambia nikuletee hii sukari kwa ajili ya kuweka kwenye maziwa”

Baada ya kumaliza  aliondoka haraka hraka ndani ya  chumba hicho  akiwa katika hali ya utulivu na  kufunga chumba.

Baada ya Hamza kutoka  Regina kivivu alijikuta akiweka kila alichoshikilia kwenye mikono yake na kulalia mikono yake  kuzika kichwa  , uso ulipata moto  na alitamani kuingia chini ya meza  kwa aibu alizokuwa akisikia.

Upande  wa Hamza picha ya Regina  kutuna mashavu huku akisindilia vile vitairi ilikuwa ikijiurudia rudia  na alijikuta akikaa kwenye ngazi na kutoa  kicheko  cha ajabu kama kichaa.

Kutokana na tukio hilo hasira yake zidi ya Regina iliisha mara moja , aliona tukio hilo linachekesha zaidi kuliko  la kule  kazini.

Hamza  mara baada ya  kurudi chumbani kwake na kumaliza kuoga , aliweza kuona lile boksi alilopewa na  Frida jana yake  na shauku ilimvaa hapo  hapo na kutaka kujua  ni mshumaa gani  ambao alikuwa akizungumzia.

Hamza  alichukua kile kiboksi na kurudi nacho kwenye kitanda  haraka sana na kufungua ndani  na mara baada ya kuona kilichokuwa ndani yake aliishia kuguna tu , haukuwa mshumaa kama mshumaa , bali kifaa cha kieletroniksi kilichokuwa na muonekano kama wa mshumaa , pengine ndio maana kiliitwa mshumaa, kwa chini kulikuwa na kitako kama cha Bunsen Burner za gesi , kilikuwa cha rangi ya zambarau huku eneo la katikati kukiwa na kifaa  kama kioo , juu kabisa kulikuwa na kioo pia kama  vile ni hadubini.

Hamza aliangalia kwenye boksi na aliweza kuona pia  waya wenye adapter, ilionekana ni kama chaji ya kifaa hiko, hakukuwa  na kingine  cha ajabu zaidi kutoka katika huo mshumaa wa nuru zaidi ya Manual, kikaratasi flani hivi cha maelekezo.

Hamza aliweka pembeni na kuanza kusoma kile kikaratasi  taratibu na  aliweza kuelewa  maana kiliandikwa kwa lugha ya kingereza.

Hakuwa na  cha ajabu sana zaidi ya  maelekeo ya kufunga mlango na madirisha wakati wa kulala na kuchomeka kifaa hicho kati ya saa tano na saa sita za usiku kwenye umeme.

Hamza hakuwa akimwamini Frida bado hivyo hakutaka kukurupuka na kufauta maelekezo aliompatia.

Hivyo alirudisha kama vilivyo na  kujitupa kitandani  na hakuchuua muda alishapotelea usingizini.

*****

Ilikuwa ni siku ya jumatatu  na mara baada ya  Hamza kushituka  aliona kwanza siku hio aende kazini  na siku inayoafuata aelekee chuo  kwa ajili ya kwenda kuchukua barua   na kujua utaratibu wa kimasomo utaendelea vipi.

Baada ya kujiweka sawa kimwili walivaa mavazi yake kama kawaida na kisha alishuka chini.

Regina alikuwa tayari ashajiandaa na alikuwa mezani akipata kifungua kinywa  na muonekano wake ulikuwa  uleule wa siku zote, ilikuwa ni kama  jana hakuna kilichotokea.

Upande wa Hamza aliona Regina alikuwa akiigiza kuwa kauzu  tu  mbele yake  hivyo aliona inafurahisha sana.

Baada ya  wote kumaliza kifungua kinywa  Hamza alishika usukani na safari ya kuelekea kazini ilianza, wakati huo  Hamza alikumbuka swala la kampuni ya Zena ilio chini ya  James kununua  kampuni ya Omega  na shauku ilimvaa.

“Regina hivi..”

“Kaa kimya, sitaki kuongea chochote na wewe”Aliongea  na kumfanya Hamza kushangaa  na aliwaza au alidhani anauliza swala la jana.

“Sio kama nataka..”

“Nimekwambia kaa kimya , kama huwezi funga  mdomo wako shuka kwenye gari”Aliongea akiwa siriasi  na Hamza aliishia kuufyata.

Hamza palepale alipata wazo  na  alitumia mkono mmoja kuendesha gari na  mkono mwingine alitoa simu yake na kuandika maneno kadhaa kwenye  simu na kumuonyesha  Regina kuona.

“Nilitaka kuuliza kama kuna tatizo kubwa  na kampuni ya Zena juu ununuzi wa Omega?”

Regina  mara baada ya kuona  aliona alikuwa amemdhania vibaya juu ya kile alichotaka kuongea , ukweli hakutaka utani wowote kutoka kwa Hamza juu ya tukio la jana  ndio maana alizidisha ukauzu.

“Huna haja ya kuwa na wasiwasi , nina mpango wangu”Alijibu  

“Nauliza , hata hivyo  haina maana mimi kuwaza , ninachotaka kusema usijipe presha  sana , jaribu kutafuta kitu kitakachokufanya angalau  utulie, kama vile jana  ulivyokuwa ukisindilia…”

“Nyamaza”Alifoka Regina ,  kwa jinsi alivyobadirika ni dhahiri angekuwa na nyundo ingetua katika kisogo cha Hamza. “Hey , usipaniki hivyo nimeacha”

*****

Baada ya kufika  kwenye kampuni  Hamza kama kawaida aliingia katika ofisi yake  na kuanza kuvuna  Bitcoin mpaka inatimia mchana muda wa chakula ndio alitoka.

Baada ya kwenda mgahawani  na kuonekana mbele ya wafanyakazi  watu  walionekana kumwangalia.

Warembo wengi walionekana kumwangalia kwa macho ya kumkubali  kitu kilichomfanya kujiuliza kwanini wanamwangalia sana.

“Hamza kumbe  haikuwa utani  unajua  mapigano  hata kumzidi  Yonesi , hatimae tumejua siri kwanini umefanywa kuwa msaidizi wa  bosi kumbe upande mwingine ni bodigadi”Aliongea Asha wa idara ya mauzo  na sasa Hamza alijua kwanini walikuwa wakimwangalia.

Wiki iliopita  kitendo cha kumdhibiti Master Konki mara baada ya  Yonesi kupigika , swala hilo lilionekana kusambaa katika kampuni kwa  wafanyakazi wote.

“Hamza hebu tuambie , tulisikia sijui  ulitumia mbinu ya kucha za tai , hivyo vidole unaweka vipi  tuonyeshe”Aliongea Mirium rafiki yake Asha.

Hamza aliwaza na kujiambia mbinu hio ya Kucha za tai  ina historia kubwa sana  tokea enzi  za kale , sasa anawezaje kuwaelezea kirahisi, lakini mara baada ya kuona wamejawa sana na shauku , aliamua kuwaelezea ki uwongo uwongo kama  mtoto anaejifanysiha kujua  mapigano, kitendo kile kiliwafanya  Mirium na Asha kuvuta midomo na kumuacha.

Lakini hata hivyo  Hamza  kutokana na kuangaliwa na wafanyakazi  wengi kwa macho yaliojaa sifa , kichwa kilimvimba  na mara baada ya kuchukua chakula chake alibadili  mwendo kabisa na kuanza kudunda  huku akisogelea meza aliokaa Yonesi akiwa peke yake.

“Habari Kapteni , naona leo sioni Suasage kwenye sahani yako?”

“Hebu jali mambo yako , muone  kichwa kilivyokuvimba , kumfukuza  yule mzee ndio unaona umefanikisha kitu kikuubwa?, mpaka mwendo unabadilika”Aliongea Yonesi

“Hehe .. najua hata wewe mwenyewe unanikubali lakini unaona aibu kusema  waziwazi ,  hata usiongee mimi naelewa  unachojjisikia moyoni”

“Nani anakukubali , unadhani mimi ni chizi?, Wewe nisubiri nishaanza kufanya mazoezi makali , nakuhakikishia lazima nikupige mpaka uombe

msamaha , ni  kazi tu ziliniweka bize na nikaacha kuchukua mazoezi ndio maana”Hamza hakuongezea neno na aliishia kukaa kimya.

“Unadhani natania , nilibweteka kwa muda tu ndio maana”

“Najua  kapteni wewe ni mtaalamu  wa hali ya juu”Aliongea Hamza lakini Yonesi hakuridhika.

“Najua unanidanganya tu kunifariji , kwenye moyo wako unaniona mnyonge”

“Kapteni , unadhani ni kipi napaswa kukuambia ili  nipate amani ya kula chakula changu”

“Kama unataka kula chakula chako , nenda meza nyingine, kwani lazima ukae kwenye meza yangu” “Hapana lazima nikae meza  moja na wewe”Aliongea Hamza na   Yonesi hata yeye aliona kabisa Hamza alikuwa  kila siku na mpango  wa kukaa meza moja na yeye , ukweli ni kwamba kulikuwa na wanawake wengi ambao walikuwa wazuri  kuliko  yeye , hivyo aliuliza kwanini analazimisha wakae meza moja.

“Kwanini?”

“Huchoki kula  peke yako  kila siku , mimi nipo hapa kukupa kampani , anagalu sasa hivi  sio mpweke sana maana una rafiki”

Yonesi mara baada ya kusikia hivyo  alishangaa na kuguswa na jambo hilo  na mwili wake ulikakamaa.

Yonesi hakuwa mzaliwa wa  jijini  Dar , ki ufupi ni wa mkoani  na kutokana na baadhi ya mambo alijikuta akitofautiana na wazazi wake na ndio  maana  alikuja kuhamia Dar akiwa nje ya kazi , katika kipindi hicho cha upweke   ndipo alipokuja  kukutana na Regina  na akafanywa mkuu wa kitendo cha ulinzi wa kampuni  ya  Dosam  baada ya Regina kutumia ushawishi wake serikalini na  Yonesi kupewa ruhusa.

Lakini sasa kutokana na mazingira  aliokulia na  namna alivyosoma elimu yake kuanzia  akiwa mdogo mpaka ukubwani , ilimfanya kuwa ngumu sana kutengeneza marafiki , hata kwa walinzi wenzake wakike hakuweza kuendana nao zaidi ya maswala ya kikazi tu.

Alikuwa akiishi peke yake , kazi alikuwa akifanya peke yake , kula peke yake, kila kitu peke yake ,  kila siku  ilikuwa hivyo kwa  miaka mitatu yote.

Kula kwake ndani ya mgahawa  wa kampuni  ukiachana na wanaume ambao walikuwa na  ajenda zao mpaka kutaka kula nae  hakuna  mtu alishawahi kuja katika meza yake kwa ajili ya kuwa rafiki  tu , wala kujali kama alikuwa mpweke.

Katika macho ya wafanyakazi wenzake , Yonesi alionekana kama sio  mtu wa kawaida wa kufanya nae urafiki.

Yonesi alikuwa imara kwasababu alikuwa  ni mwanajeshi  hivyo  anao uwezo hawa wa kuishi jangwani , lakini haikumaanisha kwamba yeye sio mwanamke ambae  upweke haumuathiri.

Hivyo mara baada ya Hamza kusema ni mpweke  alijihisi huzuni  moyoni mwake , aliishia kugeuza macho yake pembeni ili asionekane machozi yalikuwa yakitaka kumtoka.

“Napenda kula peke yangu , sijawahi kusema mimi ni mpweke , na pili sihitaji muhuni kama wewe kuwa rafiki yangu , kaa mbali na mimi”

Upande wa Hamza hakumjali kabisa  na aliishia kucheka tu huku akiendelea kuwa bize na chakula chake.

Yonesi aliishia kutulia na kuendelea kula chakula chake taratibu huku mara kwa mara akimwangalia Hamza kwa jicho la pembeni.

Hamza mara baada ya kula  kama kawaida alichukua matunda na kupandisha nayo juu.

Baada ya kufika katika ofisi ya Regina  aliweza  kukuta baadhi ya sura anazozifahamu na nyingine asizozifahamu , walikuwa ni wafanyakazi wa juu wa kampuni na ilionekana kuna kikao  kilichokuwa kikiendelea na kitendo cha kuingia bila ya hodi ni kama iliwafanya wote wamkodolee macho.

Previoua Next