Reader Settings

SEHEMU YA 38.

Saa  moja kamili  za asubuhi  ndio  muda ambao  Hamza alirudi  Egret , baada ya  kuingia sebuleni aliweza kumkuta  Regina ambae alikuwa ashajiandaa kuelekea kazini na  sasa alikuwa akipata kifungua kinywa.

“Hamza  umerudi , mbona jana hukupiga hata simu kututoa wasiwasi , Regina alikuwa na wasiwasi”Aliongea  Shangazi ambae alikuwa akitokea  jikoni.

Kauli ile ilimshangaza Hamza  kwani alisahau kabisa jana kupiga simu , sio kwamba alifanya makusudi bali  ni kwamba  amezoea kuishi  mwenyewe  kwa muda mrefu hivyo mazoea yalimfanya  kusahau kupiga.

“Shangazi unaongea nini , mimi sikuwa hata na wasiwasi , nilichelewa tu kumaliza kazi zangu”Aliongea Regina ambae  ni kama ameanza kuwa mwekundu, alijihisi  kukosewa   kutokana na kauli ya Shangazi.

Upande  wa Hamza alijua  kabisa Shangazi aliongea hivyo makusudi  kabisa  lakini hata hivyo aliamua kuichukua kauli yake kama ilivyo.

“Regina   siku nyingine nitakuwa napiga simu  ili nisikutie wasiwasi”Aliongea Hamza na  kumfanya  Regina ambae hakutaka hata kuangaliana na Hamza usoni  kuinua macho yake akitaka kumfokea lakini alisita mara baada ya kugundua Hamza alikuwa amebadili mavazi  mapya kabisa tena yanaonekana kuwa ya bei ghali , kulikuwa pia na  harufu ya marashi ya  kike ambayo  alikuwa akiyanusa.

Nguo ambazo  jana Hamza alivaa zilikuwa  ni zile ambazo zlipewa na Regina  na hata marashi ambayo Hamza anatumia   amempatia yeye , sasa mara baada ya kugundua  amebadilisha mavazi  na  pia kunukia   marashi ya kike, alijikuta akivuta picha juu  ya kile amabcho kilikuwa kikiendelea usiku kucha  na kumfanya kurudi asubuhi ,  muonekano wake ulizidi kuwa   na ukauzu usiokuwa wa kawaida na hakuongea  neno zaidi ya kuendelea na kifungua kinywa chake kimya kimya.

Hamza mara baada ya kuona ukauzu huo   hakutaka kumchokoza zaidi  ya kupata kifungua kinywa maana hata yeye hakupata  chochote.

Jana baada ya  kuondoka  katika eneo la tukio ,  muda ulikuwa umeenda na  alitaka kurudi  nyumbani moja kwa moja lakini  Dina alimzuia  na kumwambia akalale nyumbani kwake.

Hamza alitaka  kugoma  lakini Dina alimuwahi kwa kumwambia   atalala katika chumba cha wageni  ndio Hamza alikubali, sasa kutokana  na mavazi yake   aliondoka nayo kuchafuka  ilibidi  Dina kumwandalia  nguo zingine.

Dina hakuwa na hasira tena na Hamza kwani   kama sio yeye  hakujua ni kwa namna gani tukio la  jana lingeisha.vipi.

Mara baada ya chai Hamza hakuwa hata na haja ya kwenda chumbani  na  aliongozana na Regina kwenye gari kuelekea kazini.

Mara baada ya wote kuingia ndani ya gari pamoja na  kumfunga mkanda  Regina alimwangalia  Hamza kwa macho  makavu.

“Hizo nguo zako  umepewa na mpenzi wako?”Aliuliza Regina.

“Ah!.. ndio”

Hamza aligwaya kidogo , ukweli   alitaka kusema  ni rafiki yake wa kike mwingine  kabisa  lakini aliona asiende mbali , isitoshe  aliona namna ambavyo Regina  alivyokauzu.

“Vipi kuhusu nguo nilizokupatia?”

“Zimepata misukosuko  nikabadili”Alijibu Hamza akiwa na tabasamu.

“Misukosuko gani  iliokufanya kukesha usiku mzima”

Hamza alifikiria na kujiuliza au amwambie kilichotokea lakini hata hivyo aliona bado haina maana.

“Misukosuko  ya  hapa  na pale , halafu Regina kuna kitu nataka pia nikwambie..”

“Sitaki kusikia  uongo wako , isitoshe sijali unachofanya na mpenzi wako maana hakinihusu”

“Hujali lakini unauliza..”Hamza aliongea kwa chini chini.

“Umesemaje?”Aliongea Regina huku akimkodolea  Hamza na macho makubwa.

“Sijasema kitu , hakuna nilichosema”Aliongea Hamza  huku akitingisha kichwa lakini  Regina hasira zilikuwa zimempanda kiasi kwamba hata kuhema alikuwa akishindwa.

“Hamza  naomba unisikilize kwa umakini , ijapokuwa  nimekuruhusu kuishi nyumbani kwangu , kula chakula changu   na kutumia kila kitu changu lakini  uvumilivu wangu una mwisho, kwasababu unao uwezo wa kuvaa nguo  zinazogharimu  kiasi kikubwa cha hela , nenda dukani nunua nguo zako , nunua gari lako  na jaza mafuta kwa hela zako  na kisha mtoe  out mpenzi wako katika gari yako , kwanzia leo na kuendelea nisije kuona  unaondoka na gari yangu  isipokuwa tu  kwa ruhusa yangu  wakati wa kazi,umenielewa?”

Hamza hakuelewa kwanini  Regina kapaniki asubuhi yote hio , isitoshe ni nguo tu  kutoka mara moja na gari yake.

“Nimekuelewa bosi , Vipi nikitumia baiskeli yangu?”

“Utajua mwenyewe , sitaki kukuona unatumia gari yangu kwenda  kuzurula zurula na wanawake zako”

“Halafu kingine  hakikisha  James na baba yake hawajui  mambo yako , ukitaka  mkataba wetu kuingia dosari basi wewe fanya unavyojisikia  tu”

Hamza aliishia kutingisha kichwa kwa haraka haraka  ili mradi asiendelee kufokewa.

*****

Upande     mwingine         ndani    ya                      nyumba    ya

Mheshimiwa raisi ya mapumziko katika upande wa vyumba vya kuchukulia mazoezi(GYM), alionekana  mwanaume  wa makadirio ya miaka kama   sitini kwenda sabini   hivi akichukua mzoezi kwa kukimbia katika  Treadmil.

Hakuwa peke yake , kulikuwa na mwanamke mrembo pia mwenye shepu matata sana ambae  alikuwa akifanya  pia mazoezi, mwanamke huyo mrembo alionekana kijana sana makadirio ya miaka ishirini na nane hivi kwenda therathini.

Kwa jinsi Mzee huyu  alivyokuwa  akikimbia kwa spidi   na muonekano wake wa kimwili ilionyesha ni kwa namna gani alikuwa akiijali afya yake.

Mzee licha ya kuwa makini na mzoezi  hakuacha kukaza macho yake kwenye kioo kikubwa akiangalia shepu  la mwanamke mrembo aliekuwa akichukua mazoezi pia.

Baada  ya kama nusu saa ya  Mzee   yule kukimbia alijikuta akizma mashine  na kukaa chini  huku akihema  kwa nguvu na kumfanya  na yule mrembo  kuzima mashine na kisha kujifuta jasho na kitaulo. “Sam   endelea bwana , dakika ishirini kila siku?” “Tresha mpenzi , unataka nishindane na  wewe  ambae damu yako inachemka”

“Hufanyi mazoezi kushindana , bali unafanya kwa ajili ya kujenga  afya yako , kadri ambavyo unapiga hatua moja mbele katika  kufanya mazoezi ndio  unaongeza  dakika hamsini  za kuendelea kuishi”.

“Kama ni kuongeza dakika  haina haja  kufanya mazoezi ,  ninachopaswa ni kulipa hela na  kuingia ndani ya  Lazarus Lounge  kwa dakika hamsini tu”Aliongea  na kumfanya Mrembo Tresha kutoa tabasamu.

“Halafu mpenzi tukizungumzia kuhusu Lazarus Lounge, natamani  na mimi siku moja kuingia”Aliongea  Tresha  huku akilegeza jicho mbele ya Mzee Sam.

“BINAMU wamekuwa na sheria kali  sana juu ya nani anaingia ndani ya Lazarus Lounge , Tresha wewe ni  mfanyakazi wa Binamu nadhani unajua  ninachomaanisha , ila siku  wakiondoa  vigezo  vyao nitahakikisha unakuwa   wa kwanza kuingia , kwangu pia imekuwa ngumu kupata nafasi mara kwa mara ndio maana nimekubali kuchukua mazoezi kuweka mwili sawa”Aliongea  na  mwanamke huyo mrembo alionekana kutokuwa na shida.

Alikuwa  ni Mrembo Tresha ndio , muda huo alikuwa mwanamke ambae  mbele ya mwanaume lazima ulegee, alikuwa akivutia haswa , kama ndio kuengeneza sura na umbo  basi alifanikiwa.

Dakika  chache wakati  Mzee Sam na mrembo wake wakijiandaa kuchukua mazoezi ya kunyoosha  viungo ili kumalizia  bwana mmoja  alievalia suti  aliingia ndani ya ukumbi huo  na kumsogelea Mzee Sam huku akiwa  na simu  mkononi , bwana huyo alionekana kuwa mlinzi.

“Mheshimiwa  kuna simu  hapa  kutoka kwa mstaafu”Aliongea  yule bwana .

“Mgweno   ukiona anapiga asubuhi asubuhi jua kuna  kitu hakipo sawa”Aliongea  na kisha  alipokea simu ile na kuweka sikioni mara moja. “Habari za asubuhi  Mzee Mgweno?”

“Mbilu umezisikia taarifa juu ya misheni ya  jana  ilivyoenda”Sauti upande wa pili iliuliza.

“Sijapata  taarifa , nasubiria ripoti kutoka kwa Afande  Chika”Aliongea Mheshimia Samweli Mbilu huku akikuna sura.

“Basi habari za asubuhi sio nzuri  kwako na kwangu , nilikuambia  mpango uliokuwa nao hauwezi kufanya kazi mbele ya yule mwanamke”Raisi Samweli Mbilu mara baada ya kusikia kauli hio  furaha ya uso ilimpotea

“Nini kilitokea , Chika ameshindwa kumdhibiti Dina licha ya  kuruhusu  watumie siraha?”

“Taariza zilizonifikia  jana kuna kijana  anafahamiika kwa jina  la Hamza aliefika eneo la tukio  na kwa msaada wake alifanikisha kushambulia vijana wote waliokuwa na  bunduki na  wamepoteza uhai , ndio namna mpango ulivyovurugika”

“Hamza ! kwanini nahisi  kama nishawahi kusikia hili jina  likitajwa kwenye ripoti?”

“Umelisikia ndio , ni msaidizi  ndani ya kampuni ya Dosam  na mpenzi wake  Regina  kwasasa”Mara baada ya Mheshimiwa Sam kusikia kauli hio sasa alikumbuka.

“Nimekumbuka sasa , hili jina nimelisikia kutoka kwa Brigedua  Simoni Doswe  katika ripoti ya  mauaji yaliotokea  Zinga,  inamaana ni huyu huyu ndio aliejitokeza kumsaidia na Dina?”

“Inaonekana kuwa hivyo , lakini swali langu ni kwanini   ausaidie mtandao wa Chatu?”

“Dina nilimdharau , ila inaonekana kajitafutia  msaidizi mzuri awamu hii , Mzee Mgweno 

nitahakikisha kila kitu kinaenda sawa, kuhusu huyu Hamza MALIBU wanafatilia taarifa zake kwa undani , nadhani ndani ya muda mfupi  tutamjua”

“Mbilu hili sio kipaumbele kwasasa , kwanini huulizi  kilichowatokea  Debora  na wenzake,Debora anajua siri nyingi  akiropoka kidogo tu mipangyo yangu na yako  itaharibika kabisa”Kauli hio ilimfanya  Mzee Mbilu kukuna kichwa.

“Mzee Mgweno  kuwa na amani , najua nini chakufanya juu ya hili?”.

“Hakikisha hakuna makosa  Samweli , kumbuka unaondoka Ikulu na una muda mchache wa kuweka mambo sawa  kabla ya Jongwe  hajachukua kijiti, nadhani unajua Jongwe sio chaguo  letu  ndani ya chama , lazima tuwe makini”Aliongea  na  Mheshimiwa Samweli Mbili alimhakikishia  kuwa  atafanya  kila linalowezekana kukamilisha mpango  wao.

Kitendo cha kukaa simu  Mheshimiwa   Mbilu alijikuta akivuta pumzi  nyingi na kumfanya Tresha kumwangalia kwa macho yaliojaa udadisi.

“Maulid Mpigie simu Brigedia Doswe  amuachie  Dastani  hata kama  hajahojiwa na afike ikulu  mchana  bila ya kukosa”

“Sawa Mheshimiwa”

Maulidi  alikuwa ni  msaisizi wa karibu  wa mheshimiwa Mbilu  na  mara baada ya kupokea maagizo hayo  aliondoka kwa ajili ya kuyatekeleza.

Upande wa mrembo Tresha  alionekana kuwa bize wakati wote  wa kuchukua mazoezi lakini ukweli  ni kwama sikio lake liliweza kusikia maongezi  yote  na mara baada ya kusikia   Mheshimiwa anatoa maagizo ya  Kanali Dastani kuachiwa huru  alijikuta akitoa  tabasamu la chini chini.

“Kazi yangu imemalizika kabla  hata sijamshawishi  Mbilu”Aliwaa Tresha kwenye akili yake.

Mheshimiwa Mbilu hakuwa hata na hamu ya kuendelea  na mazoezi tena  na aliambatana na  Tresha na kutoka katika ukumbi huo, alihitaji kurudi Ikulu kudili na  baadhi ya mambo haraka sana.

“Hili dili lazima lifanikiwe kwa namna yoyote ile kabla  ya uapisho  wa raisi mpya, Bilioni  tisini  kwa mwaka  ni pesa nyingi sana  ninazoweza kupata kama mstaafu..huyu Hamza lazima  adhibitiwe kabla  hajaniharibia  mambo yangu”Aliwaza Samweli Mbiu wakati akiingia katika gari  kuianza safari ya kuelekea ikulu.

********

Hamza mara baada ya  kufika kazini  alienda  moja kwa moja mpaka kwenye ofisi yake , alipanga kusubiri hadi saa nne kisha aelekee chuo  maana   ni zaidi ya wiki hajakanyaga na hakuwa na taarifa ya kinachoendelea hususani maswala ya barua za  kuanza field.

Ilipotimia saa tatu na nusu alitoka na kuelekea katika ofisi ya Regina , lengo lake ni kutaka kumwambia   anaelekea chuo.

Lakini  mara baada ya kuingia ofisini kwa Regina  aliweza kumkuta Regina akiongea na simu  na alionekana kuwa makini kweli.

“Bibi  hii ni fursa adimu sana kwako , unajua ni kwa kiasi gani tuliweza kutafuta mawasiliano  nae  lakini hatukufanikiwa , huyu Dokta ni bingwa  na anakuja  hapa Tanzania  , ni vizuri kama  utaonana nae”Aliongea  Regina huku akionekana kama vile  anabembeleza , alikuwa ameweka mkono mmoja kwenye paji la uso wake.

“Naomba  ulichukulie hili kama ombi   langu  kwako , najua  una huzuni  baada ya babu kufariki  lakini  afya yako ni muhimu kwa sasa ….”

Regina  alionekana kubembeleza kwa muda mrefu  kidogo lakini muonekano wake  ulitosha kuonyesha hakukuwa na mfanikio na aliishia kukata simu. “Mkurugenzi  nini tatizo  la bibi yako , anaumwa?”Aliuliza Hamza ambae hakuwa akizijua taarifa za Regina kuwa na bibi.

“Unauliza wakati umesikia kila kitu?”Aliongea Regina  kichuki chuki , ilionekana hakuwa katika mudi nzuri.

“Kwanini upo hapa?”Aliuliza.

“Naelekea chuo  , lolote linaweza kutokea huko hivyo  kama nitachelewa  unaweza kwenda moja kwa moja nyumbani”

“Hivi kumbe  hampo  likizo bado?”

“Ni kipindi cha field  hiki,  semista ya mwisho hii mambo ya kuweka sawa ni mengi”Aliongea Hamza na  Regina alitingisha kichwa kuonyesha  ishara ya kumwelewa.

Lakini muda  huo Linda aliingia  ndani ya ofisi hio akionekana kuwa na taarifa.

“Bosi , Dr Ronicas  ametua  nchini Tanzania  muda huu , nimefuatilia  ratiba yake inaonekana atakuwa hapa nchini kwa siku  mbili au tatu”Aliongea  na  taarifa hio ilimfanya  Regina kuonyesha furaha.

“Linda  haraka sana fanya appointment  tukiwa wa kwanza itakuwa rahisi kuonana nae”

Hamza mara baada ya kusikia jina la Dokta  Roinicas likitajwa macho yake yalichanua.

“Huyu Dokta Kichaa kumbe ni maarufu hivi mpaka 

hapa  Tanzania ,mpaka Regina anamfahamu”Aliwaza Hamza lakini aliona anafikiria ujinga , kwa matajiri ilikuwa  swala la kawaida kuwatambua madaktari bingwa    maarufu sana kutatua shida zao za kiafya.

“Lakini bosi Dokta Ronicas amekataa  miadi   na wagonjwa ,  msemaji wake amesema  Dr Ronica yupo Tanzania  kwa ajili ya kukutana na rafiki yake na  sio maswala  ya kutibu”Aliongea Linda na kufanya furaha ya  Regina kuzima mara moja.

“Kwanini  iwe hivyo , si daktari?”

“Bosi  hauna haja ya kuwa na huzuni , Dokta Ronica anafahamika  kwa  kuchagua  wagonjwa anaotaka kutibia , umaarufu wake duniani unampa  uwezo huo  ndio maana sio mtu wa kupokea  miadi ya kuonana na wagonjwa wa kila aina , kwa umaarufu wake  ndani ya dunia kila mgonjwa mwenye pesa   nyingi na watu maarufu watataka kutibiwa nae , nadhani  asipokuwa na vigezo atakuwa bize mno”

“Lakini  Bibi ugonjwa wake umekuwa changamoto  mno  kwa madaktari  wengi. Hata Dokta ambae alialikwa  kumtibia mara ya mwisho kutoka India amesema tumaini la mwisho ni  labda Dokta Ronica kumfanyia  tiba, kwa afya   ya bibi imeshauriwa asisafiri kwa ndege  umbali mrefu, bahati imekuwa upande wake Dokta Ronica  yupo hapa Tanzania, hii ni nafasi pekee   ya kuhakikisha anamuona  bibi”Aliongea Regina na kumfanya Linda kumuonea huruma bosi wake.

“Bosi   lakini  si   wamesema yupo  hapa nchini kwa ajili ya kuonana na  rafiki yake , kwanini tusitumie ushawishi wetu kumjua mtu  huyu mzito  ni nani , pengine anaweza kutusaidia kukutana nae”

“Upo sahihi  Linda , hebu  nenda kafanye uchunguzi  ni rafiki gani anazungumziwa , itakuwa  njia rahisi  zaidi”

Upande wa Hamza  alijifanyisha kuwa bize na simu yake lakini alikuwa akisikiliza maongezi yao.

“Regina  bibi yako anaumwa nini?”Aliuliza Hamza  akiwa na huzuni usoni.

“Kuumwa kwa bibi  yangu hakukuhusu , ondoka ofisini kwangu kwanza”Aliongea Regina kihasira , hakuwa na mudi kabisa ya kuongea  na Hamza.

“Hey , nimeuliza tu kwa nia nzuri , unajuaje pengine naweza kukusaidia”Aliongea Hamza.

“Anaumwa na saratani ya Kongosho na  anatumia betri ya moyo”Aliongea Regina kivivu na Hamza  aliweza kuona  ni kweli bibi yake ilionekana  alikuwa na tatizo kubwa ,saratani ya Kongosho haikuwa ya kawaida.

“Haya umejua sasa anachoumwa  , unaweza kumtibu?”Aliuliza  Regina.

“Mimi sijui  kutibu”Aliongea Hamza na jibu lake lilimfanya Regie mudi yake kuzidi kuwa mbaya.

“Ndio uondoke sasa , unauliza nini kama huna msaada , wewe ondoka zako sijui unaenda chuo  kweli au  kuonana na mpenzi wako  yote ni kheri ,  sipendi uendelee kunisumbua , sitaki kukuona unaweza kulala huko huko ukijisikia”Aliongea.

Kitendo cha Hamza kufokewa ilihali anajaribu kuonyesha kujali kilimfanya  kushikwa na hasira ,  alikuwa na uvumilivu  ndio lakini hasira  za Regina mbele yake zilimfanya  kuona itafikia  siku atakosa uvumilivu .

“Kama ni  hivyo naondoka , ila  usije kujutia  tu maneno yako”Aliongea Hamza huku akijitahidi kuzuia hasira yake isijionyeshe.

Upande wa Regina mara baada ya kusikia kauli hio  kiasi flani aliona ni kama ameenda mbali , lakini hata hivyo tabia yake isingemuwezesha kujishusha kabisa.

Alikuwa na hasira na Hamza  sana ,  kila akifikiria  namna ambavyo  Hamza ameondoka na kwenda kulala huko na mwanamke wake usiku kucha mpaka  kuacha mavazi aliompatia na kuja na mengine nyumbani  hasira  ndio zilizidi kumkaba.

“Usiwe na wasiwasi kabisa , Mimi Regina  siwezi kujutia  maneno yangu”Alijibu  Regina kwa jeuri.

Hamza mara baada ya kupokea jibu  hilo hakuina haja ya kuendelea  kuongea  na alitoka.

Kitendo cha Hamza kutoka tu palepale  simu  yake ilianza kuita  na mara baada ya kuangalia namba ilikuwa ngeni ila alipokea moja kwa moja.

“Hey ! Prince Rich , did you miss me…”

Previoua Next