Reader Settings

SEHEMU YA 42.

“Mchomeni mchawi huyo , Aderon kutoka Cathedral anakwenda kuchoma mchawi”

“Burn that damn witch to ashes”

Woga  na mshituko uliweza kumshika  kwa kusikia  lugha ya kingereza  ambayo  waongeaji wake lafudhi zao  zilimchanganya.

Swali  lilimvaa pale na kujiuliza yupo wapi , ni ulimwengu gani ambao  mchungaji anashiriki  kumchoma mchawi  moto.

Hamza aliweza kuhisi kabisa  kuna kitu hakipo sawa  na kuna jambo kubwa ambalo  anakwenda kushuhudia , lakini mawazo yake yalikata mara baada ya  kishindo  kusikika  kutoka katika mlango  wa kuingilia katika chumba ambacho yupo.

Dakika ileile aliweza kuona mlango  ukifunguliwa  na akaingia  kijana mzungu  kabisa wa miaka kama kumi na tatu hivi.

“Luther !!” Yule  kijana mdogo mwenye nywele zake za rangi ya kahawia aliita , alikuwa amevalia nguo za kitani   ambazo zimemfika magotini na alikwenda kusimama kandokado  ya  kitanda alichokuwa amelala Hamza   huku akimwangalia  kwa macho  ya  mshangao.

“You’re awake , thanks God”

Hamza alijikuta akimwangalia yule  mvulana wa kizungu  namna mavazi yake yalivyo na aliishia kutingisha kichwa  bila ya kujielewa.

“Luther , Mchawi , Cathedral , kuchoma  mchawi”Mawazo hayo yalianza kupita katika kichwa cha Hamza na kujiuliza yupo  wapi na amefikaje , ilikuwa ni kama vile anaangalia filamu zilizoigizwa kwa kuiga  mazingira  kati ya Karne ya  tano mpaka kumi  na tano maarufu kama Middle ages ndani ya bara la Ulaya , kipindi ambacho  kulikuwa na matukio makubwa ya  kuwinda wachawi na kuwaua.

Rangi ya  kijana aliekuwa mbele yake na mavazi yake , ilikuwa ni ushahidi tosha wa kile ambacho anakiwazia 

Yule kijana mdogo   mzungu ambae alikuwa na  uchafu mweusi kwenye  paji  la uso wake alionyesha kuwa na furaha kubwa.

“Mama hakuniamini na  kuendelea kulia usiku  wa manane kila mtu akiwa amelala  huku akitaja jina lako kana kwamba ushakufa na kuzikwa tayari,  baba hakujua cha kufanya  na aliamua  kumtuma  Simoni kwenda kwa Lord  Venn, akiomba  kaka kurudi nyumbani , sasa hivi amekuwa Knight(mwanajeshi), mbele ya kaka yule daktari asingekataa kukutibia , lakini ona sasa  juhudi hazikuwa za bure hatimae  umeamka , nilijua tu huwezi kufa”Yule kijana aliongea  kwa sauti huku akionyesha ni kwa kiasi gani ana furaha na baada ya sentensi hio alimshika Hamza mkono.

“Hebu twende  nje kwanza, wanaenda kumchoma yule mchawi aliesababisha uende jela  na kuhojiwa usiku kucha  na walinzi wa kanisa”

Hamza  hakujua kinachoendelea , kijana aliekuwa mbele yake hakuwa akimfahamu  na wala hakujua  eneo alipo , alihitaji muda wa kufikiria amefikaje hapo   na sio kwenda nje.

“Huyo mchawi anahusiana vipi na mimi?”Swali liliingia katika akili ya Hamza na alijikuta akibadili mawazo palepale  na alimshikilia mkono yule mzungu  na akajikokota kutoka nje.

Hamza mara baada ya kutoka alijikuta akiangalia  mazingira na watu  wake  na alijikuta akipagawa , watu wote walikuwa wamevaa mavasi staili inayofanana , nguo za kitani  za mikono  mirefu , ukiachana na  hali ya joto lakini  mazingira yalikuwa tofauti kabisa.

Karibia watu wote alioona walikuwa ni wazungu  na nywele zao ni  za rangi ya  kahawia , walikuwa wamevaa viatu ambavyo havikuwa na visigino , wanawake  walikuwa wamevaa  magauni ambayo yalikuwa na mifuko mirefu mno.

“Hizi ni  zama za kale  ndani ya Ulaya?”Alijiuliza  Hamza na sasa wakati huo ndio alianza kujichunguza mwili wake , alijishangaa baada ya kujiona  anafanana  kila kitu  na watu wale , kilichompagawisha  hakuwa na muonekano wake wa Hamza aliokuwa nao , bali alikuwa ni mzungu  kamili  ambae hajachanganya rangi ,  huku akiwa na mavazi kama ya wale wengine tu.

Nyumba zilizokuwepo zilikuwa ni zile  ambazo zlikuwa akiziona ni za hali ya chini , mara nyingi  ungeziona katika bara la  Afrika , vilikuwa ni vijumba vingi vilivyojipanga.

Baada ya kutokezea nje kabisa hatimae aliweza kuona jengo kubwa ambalo lilikuwa mbele yake , ambalo  paa lake lilikuwa limeenda hewani na kuchongoka kama mkuki  huku katika ncha yake kukiwa na  Msalaba wa rangi nyeupe , vidirisha vya   kanisa hivyo vilikuwa vyembamba mno.

Watu wengi walikuwa wamejikusanya mbele ya uwanja wa kanisa hilo , Hamza alikuwa hajui kinachoendelea  na alikuwa  akionekana mshamba  mshamba na alichofanya  ni kumfuata yule kijana mdogo wa kizungu , Hamza  alimuiga yule kijana  kwa kusukuma watu pembeni na kujipenyeza  ili kupita mbele kabisa katika kundi la watu hao  na  vitendo vyao viliwafanya watu kukasirika na kuwaangalia kwa macho makali.

Hatimae Hamza aliweza kuona  mbele kabisa  ya eneo hilo , walikuwa wamefika mbele ya kundi lile  la watu.

Katikati ya  sehemu ambayo ilikuwa ni kama steji ya kanisa  alionekana mwanamke  mrembo  wa kizungu ambae amevalia nguo mfano wa  kaniki  nyeusi , alikuwa amefungwa kwenye  msalaba  kwanzia mikono yake  na watu walikuwa wakimtupia mawe  na vipande vya kunni   huku wakiongea kwa nguvu  kutaka mwanamke huyo kuchomwa moto.

“Go to hell!! Damned witch”(Nenda kuzimu wewe mchawi  mpumbavu)

“You wanted everyone  in Aderon  to die(Ulitaka  kila mtu ndani ya Aderon kufa).

“Jamani Tracy , amekufa  mwezi mmoja uliopita , lazima  umemua wewe  shetani”

Mwanamke yule ambae  alikuwa  katika joho la rangi  nyeusi  alikuwa akipokea kila  lawama pamoja na kurushiwa kila  kilichowezekana kurushwa , lakini jambo la ajabu , yule mwanamke alikuwa amemkazia macho Hamza  pekee , ilikuwa ni kama alikuwa akimtambua  na hali ile ilimfanya  Hamza kuwa na wasiwasi , ngozi yake haikuwa tofauti  na wale wazungu , lakini kwanini mwanamke yule alikuwa akimwangalia  kwa kumkazia macho , tena kila alipokuwa akipokgea pigo  na kugeuzwa uso wake pembeni aligeuza na kumwangalia Hamza kwa macho yaliojaa ujumbe.

Watu  hawakujiuliza alikuwa akiangalia wapi , ni Hamza pekee ambae alikuwa akipata hisia  mwanamke yule alikuwa akimwangalia yeye.

Pembeni ya mwanamke huyo alikuwa amesimama  mwanaume  wa makamo , alikuwa amevalia joho la  rangi  nyeupe ambalo lilikuwa limedariziwa  na michoro ya aina yake , kichwani alikuwa amevalia kofia aina ya bereti , huku mkononi akiwa ameshikilia  msalaba , alionekana kuwa kimya muda wote , akiwa na hali ya kumakinika  na heshima , kulikuwa na wanawake na wanaume ambao walikuwa nyuma yake  wote pia walikuwa wamevalia majoho ya rangi nyeupe , walikuwa na sura  angavu  na zenye kudhihilisha hadhi yao .

Kulikuwa na walinzi  pia  ambao  walikuwa wameshikilia mikuki kama wale wanajeshi wa Crusaders , wapigania dini ya kikristo.

Mwanaume yule wa makamo aliangalia saa yake  ya  mfukoni  na kisha alipiga hatua kusogea mbele  na kisha akainua bango ndogo ya mviringo  na  ghafla tu wale watu wote waliokuwa wakipiga makelele walinyamaza.

Hamza bado alikuwa amekutanisha macho ya  yule mwanamke  muda wote, huku mapigo yake ya moyo yakienda mbio.

Kitendo kile cha utii  wa ghafla  mbele ya yule  mwanaume alieonekana kama mchungaji  ilimfanya Hamza kushangaa   lakini pia  kuona  namna watu hao walivyokuwa watiifu,  na palepale swali lilimwingia na kujiuliza huyo mwanaume ana mamlaka gani kiasi cha kutuliza watu wote hao kwa kunyanyua  tu lile  bango iliokuwa kwenye mkono wake.

Yule mwanaume mara baada ya watu kutulia alianza kuongea kwa sauti ya kupenya katika  kila ngoma za masikio ya kila mmoja

“Ewe Mkosefu uliejaa dhambi , umedanganywa  na shetani, tamaa ikakuvaa na kuufanya mwili wako na

nafsi  yako kujaa ufisadi , ni nuru pekee itakayokusafisha , ni hukumu yako lakini vilevile  ni rehema za mwenyezi  Mungu”

“Burn her , Burn her !!”Watu walianza kupiga mayowe huku wakiinua mikono yao juu wakitaka yule mwanamke kuchomwa moto.

Sauti hizo za watu kukemewa mwanamke huyo kuchomwa moto  na namna ambavyo  yule mwanamke  alievyokuwa akimwangalia   kwa kumkazia macho ilimfanya Hamza kujawa na hofu na kuona pengine  yule mwanamke anaweza kumjumuisha  kama mshirika wake na wakachomwa wote.

“Kabla ya  kivuli  cha nuru hakijawa juu yako , ungama dhambi zako ,  toba ya kweli  inaweza kuokoa roho yako , ndipo roho yako  itapaa mbinguni anapoishi Mungu”Aliongea yule Askofu.

Yule mwanamke ghafla tu alianza kucheka kwa sauti kubwa , sauti yake  ilikuwa na nguvu  kiasi kwamba ilikuwa ikitisha   na alianza kuongea kwa nguvu.

“Ninachotafuta na kuamini ni  nguvu  halisi ya uchawi , si  nguvu ya kimungu , nichome tu , Nitazishuhudia  mbingu za Mungu wako  zikiharibika  na kanisa lako likiungua kwa miale ya moto”Aliongea  na  kuonyesha tabasamu huku akimwangalia Hamza.

“Kichaa huyo”

“Ana wazimu”

“Amechanganyikiwa”

“Amemlaani  Askofu , wachawi wote na wauwawe  wakifuatiwa na majini”

“Achomwe mpaka awe majivu”

Yule askofu   alionekana kuwa kimya , lakini  makelele ya watu yalizidi  kusikika zaidi na zaidi , chuki katika sauti za watu hao ndio ambacho Hamza aliweza kusikia.

“Kwanini nipo hapa , nafanya nini?”

Hamza alitamani  kwenda kumuokoa yule mwanamke ,  ni kama kuangaliwa na yule  mwanamke  alikuwa akiomba msaada , lakini  kundi hilo la watu wengi aliona kabisa ni kitendo ambacho hawezi , swala lingine  hakujua kama alikuwa na uwezo huo,  maana mwili wake  ulikuwa umebadilika.

Swali palepale liliingia katika akili ya Hamza na kujiuliza , wanakwenda kumchoma vipi ilihali hakukuwa na kuni  zaidi ya  mwanamke yule kufungwa juu ya msalaba.

Yule askofu alianza kuomba kwa  nguvu  na kadri alivyokuwa akiendelea  ni kama sauti yake ilikuwa ikibadilika kutoka katika hali ya kubembeleza na kuwa ya kikauzu.

“Wewe mchawi , binadamu mkosefu mbele za Mungu sehemu yako ni Kuzimu,  na nakupeleka huko kwa  nguvu ya Nuru”Aliongea vile na ghafla tu ule msalaba  aliokuwa ameshikilia ulitoa  mwanga mkali kama vile ni  wa radi , ulikuwa mkali kiasi kwamba Hamza alishindwa kuuangalia.

Ilikuwa ni kama vile  Askofu yule alikuwa ameshikiria jua dogo katika mkono wake , mwanga ule ulikuwa msafi na  wa kutisha wenye msisimko wa ajabu  , watu wote katika lile kundi  pamoja na yule kijana  ambae alimwita Hamza kwa jina la Luther  waliinamisha vichwa vyao chini kwa heshima.

Yule mchawi alianza kuongea kwa nguvu  kana kwamba anaimba ushairi kwa lugha ya kingereza.

“In the blazes  I will see your shrewd paradise demolished”(Katika miale ya  moto nitashuhudia  patadiso yako iliojaa hila ikiharibika)

“In the blazes  I will see your fabulous house  of God Crumbling”(Katika miale ya moto   nitashuhudia nyumba  kubwa ya Mungu wako ikidondoka) 

“In the Blazes , I will see your indiduals  evelastingly worsened”(Katika miale ya moto nitashuhudia watu wako wakiteseka  milele)

Alizidi kuongea maneno mengi kwa kurudia rudia sehemu ya mwanzo na kumalizia tofauti mwishoni , huku ule mwanga ukizidi kumuunguza.

“Hapana hapa  sio duniani , huu ni ulimwengu mwingine , mimi sio Hamza , mimi ni Luthe…”

Ilikuwa ni  kama vile  kuna mtu aliemsukuma  na kudondoka chini , Hamza alijikuta  akishituka  huku akihema kwa  nguvu , jasho jingi lilikuwa likimtoka usoni.

Alijikuta akikimbilia taa na kuiwasha  haraka haraka  na kuangaza huku na huko , alijikagua mikono yake na kujiona  ni yeye  Hamza  mzungu wa kuchnganya rangi  au Shombeshombe.

Katika maisha yake hakuwahi kukumbwa na hali ya namna hio , alijikuta akihema  kwa nguvu kwa namna ya ahueni.

“Afadhali  ilikuwa ndoto”Aliongea Hamza  huku akikaa  kitandani na aligundua  alikuwa ameloanisha  shuka kwa jasho, lakini  muda huo kadri akili yake ilivyokuwa ikikubaliana  kwamba alichokuwa akiota ni ndoto  hali  nyingine ilimuanza , haikuwa hali ilikuwa ni harufu  ambayo ilianza kugusana na pua zake.

“Haya marashi  yanatokea wapi?”Hamza alijikuta akishangaa , chumba kizima kilikuwa kimebadilika harufu, haikuwa  marashi kama marashi ni harufu ambayo haikuwa ikielezeka  yenye kuvutia na kukera kwa wakati mmoja, ilikuwa ikipenyeza kwenye pua zake kama vile ni udi.

Hamza alijikuta akiangaza kulia na kushoto kutafuta  marashi yalipokuwa yakitokea  na mara baada ya kuangalia  kwenye bedside ya  kitanda chake alijikuta akishangaa.

“Huu mshumaa  nani ameuchomeka kwenye umeme?”

Ndio swali ambalo  lilimvaa Hamza palepale, huku asiamini kilichokuwa mbele  yake , alikuwa akikumbuka kabisa  mara ya mwisho mshumaa huo ulikuwa kwenye boksi lake na alihifadhi katika  kabati  sehemu ambayo aliona ni salama , lakini cha kushangaza  ulikuwa  kwenye Bedside tena ukiwa umechomekwa kwenye  umeme.

Hamza  sasa  ni kama anapata  mwanga wa kile ambacho kilikuwa kikiendelea , pengine harufu hio  pamoja na ndoto ya ajabu  aliokuwa  ameota imetokana na mshumaa huo kuwa katika umeme.

Hamza alikumbuka  wakati wa  Frida anampatia huo mshumaa alimwambia  auchomeke kwenye umeme kati ya saa tano  mpaka sita , Hamza  mara baada ya kukumbuka  jambo hilo alikimbilia simu yake ili kuangalia saa  na ile anawasha  tu  ile simu kilichoanza kuonekana katika macho yake ni ujumbe wa meseji, ambao ulifanya mapigo yake ya moo kwenda mbio.

“Mzee!!”

Ndio  neno la kwanza ambalo alianza kulitamka katika  mdomo wake  huku hofu ikimvaa.

Hamza  kwa haraka haraka alifungua ule ujumbe  na aliweza kuusoma kwa hofu kubwa , ulikuwa umeandikwa  kwa kingereza.

“The history  of your past life in  onother  world has already  begun to echo , if you fail to  inherit your history , it  will be  the end of your life  in this world,

Your greatest enemy  has already  awakened” “Historia ya maisha yako ya nyuma katika ulimwengu  mwingine imeanza kuita, kama utashindwa kurithi historia yako , itakuwa ni mwisho wa uhai wako katika huu ulimwengu , adui yako mkubwa amekwisha kuamka”

Hamza alijikuta akisoma  ujumbe ule kwa kurudia rudia , hakuwa akielewa sentensi nzima ya ujumbe huo ilikuwa ikimaanisha nini , hakuelewa  nini maana ya adui yake , kila kitu kilikuwa kipya  kwake na alitamani maelezo , alishangaa pia kuona mtu ambae ametuma ujumbe huo ni Mzee na jambo hilo lilimfanya  kupagawa zaidi.

Usingizi wote ulimpotea , alikuwa ni jasiri lakini likija swala la Mzee Hamza alikuwa dhaifu sana , sio kwamba alikuwa akimuogopa  lakini ni kwamba hakujua Mzee  ni adui yake au ni rafiki kwake na mbaya zaidi hakuwahi kumuona na ghafla tu anaota ndoto  ya ajabu .

Hamza alikaa akianza kuwaza  hisia zilimwambia pengine  ni huyo mzee ambae  ameweka mshumaa huo  kwenye umeme. Hisia mbaya zilimvaa , kifaa hicho kisingejichomeka chenyewe , lazima kuna mtu alikichomeka.

“Kwahio Mzee alikuwa hapa, inawezekana vipi?”

Hamza aliamka kutoka kitandani na alijaribu kufungua mlango  wa chumba chake    na ulionekana kuwa wazi ,  lakini hakushangaa maana ilikuwa tabia yake kuacha mlango wazi , alijikuta akikosa namna ya  kujitengenezea sababu ya kuamini mzee alikuwa hapo , sio madiirsha ya kutokea kwenye balkoni na sio mlango kila kitu aliacha wazi wakati wa kulala.

Hamza hakutaka kuwazia sana kuhusu  Mzee kufika hapo  au kutokufika, ukweli ni kwamba sio mara ya kwanza kutokewa na  tukio la namna hio , anakumbuka siku ambayo  alikaidi  maagizo ya Mzee na hali iliomkuta  ilimfanya kuitikia kila kitu ambacho alikuwa akiagizwa na mzee  licha ya mtu huyo kutokumuona kabisa wala kumtambua.

Usiku Mzima Hamza aliwaza  jambo ambalo lilimpata , alijikuta akiwaza ndoto  aliona  na  maana ya maneno katika ujumbe ule na alijikuta akiona pengine historia ambayo Mzee anamaanisha ni  kuhusiana na kile alichoota , isitoshe sio mara ya kwanza, hata Frida kabla ya kumpatia huo mshumaa alimuuliza kama ashaanza kuota ndoto.

Mpaka  kunakucha Hamza hakuweza kupata usingizi tena , baada ya saa kumi na moja kufika  ili kupotezea mawazo yaliokuwa yakimwandama alitoka mpaka  nje  na kuanza kuchukua mazoezi kwa kasi sana , siku hio  alianza kucheza  ule mdundiko kama  hana  akili nzuri.

Mbinu hio  ya mazoezi  kwa mtu mtaalamu  angeweza kuifahamu kwa jina lake maarufu la Mdundiko wa jini.

Kadri ambavyo  alikuwa akicheza ndio  alivyoweza kuifanya akili yake kutulia  na  mawazo kumpotea , mpaka inafika saa  moja  hatimae alihisi kurudi kwenye ari yake.

Upande wa Regina mara baada tu ya kuamka alimwambia  Hamza kuongea na Dokta   kwani siku hio  haendi kabisa kazini ili kushughulikia swala la bibi yake na Hamza hakubisha , alimpigia  Flora simu  na kumuomba  na  hakukataa kabisa , jambo ambalo lilimfanya Regina kuzidi kushangaa zaidi na kujiuliza mengi kuhusu  Hamza, lakini hakukuwa na namna ya kupata majibu kwani Hamza alikuwa akiishia kumdanganya.

Licha ya  Regina  kutokwenda kazini  Hamza alipaswa kwenda  lakini aliona uvivu kwani  kazini   hata Eliza pia  siku hio hakuwa na  ratiba ya kwenda kutokana na daktari  kwenda nyumbani kwao  kumtibia mama yake.

Hamza  ilibidi kutoka na gari nyingine  kabisa BMW X7 ya 2022 na hayo yalikuwa maelekezo ya Regina ambae alitaka kutumia ile Lexus.

Hamza  akiwa ndio  anakaribia kutoka  nje  tu ya geti kuelekea kazini  simu yake ilianza kuita mfululizo na alipoangalia anaepiga ilikuwa ni namba mpya na alipokea palepale huku akisimamisha gari  kwanza.

“Hello!!”

“Wewe baba ninaekudai habari za asubuhi”Sauti upande wa pili ilisikika , ilikuwa ni sauti  tamu  kweli na kumfanya  Hamza kuitambua mara moja , ijapokuwa aliisikia kama mara moja au mara mbili hivi lakini haikusahaulika.

“Prisila!!”

“Eh! wewe mwanaume hujasahau sauti  yangu?” “Nasahau vipi sauti ya mrembo  kama wewe , niambie  kuna shida ndio naelekea kazini?”

“Najua ndio ni muda wa kazi , lakini kwasababu nakudia naweza kupiga  muda wowote, au umesahau una deni langu?”Prisila aliongea na kumfanya Hamza kutoa tabasamu.

“Nakumbuka na nipo tayari ya kulipa  ila sio sasa hivi?”

“Hakuna haja ya kujikaza , mimi najua kudai kistaarabu, ili kulipa,  baadae  tukutane?”

“Tukutane!, unamaanisha nini tukutane?”

“Namaanisha tukutane , kuna kipi cha kushangaa  hapo?”

Hamza mara baada ya kusikia sauti hio ilivyokuwa siriasi  aliishia kujiuliza huyu mwaamke mbona  amekaa kibabe  sana ,  hata hajamuuliza kama ana ratiba gani  lakini anataka wakutane.

“Namaanisha  hatuna sababu ya kukutana  maana hatuna mahusiano , au usiniambie ndio unataka yaanze?”Aliongea na upande wa pili  ulitulia kidogo. “Kuna kitu nataka tufanye pamoja  baadae , sitaki kumuomba mtu msaada  wewe nakudai hivyo ni sawa  kukuambia tuonane muda huo , kama haupo tayari kulipa deni langu sitokulazimisha”Hamza hakujua alie au acheke ila  aliona tu akubali kwasabau alikuwa akidaiwa fadhila.

“Okey  nipo tayari kufanya hicho kitu pamoja hapo baadae , niambie tu muda na eneo”

“Nitakutumia ujumbe kwa meseji”Aliongea na simu palepale ilikatwa, Hamza aliona ilikuwa ikileta maana  Prisila alizisikia  habari  zake juu juu ,  wakati akiwa  kazini   alikuwa pia ni  mwanamke  siriasi sana ambae anajua anachokitaka.

“Kampuni ya  Dosam imejaa  wanawake vichaa tu kasoro  Eliza”Aliwaza Hamza na kuondosha gari  haraka. Kuelekea kazini.

Previoua Next