Reader Settings

SEHEMU YA 43.

Hamza aliwahi kutoka kazini  kuliko kawaida ili kuwahi miadi  na  Prisila , mrembo huyo alikuwa ameshamtaarifu ni wapi amkute  hivyo alisogea  mpaka Mlimani City  na ndani ya  dakika tano tu kupita  Prisila alitokea , siku hio alikuwa akitumia gari  nyingine  kabisa  aina ya   Bentley.

“Inaonekana ni kama nilivyotarajia , unajali muda “Aliongea Prisila huku akimwangalia Hamza  na kuonyesha ishara ya kuridhika.

“Umependeza mno  Prisila , unaonekana kama wale warembo  ma’model’ maarufu?”.Aliongea  Hamza na kumfanya  Prisila kutabasamu. “Halafu  hili  gauni nimelinunua muda mrefu sana , lakini  sijawahi kupata ujasiri  wa kulivaa”Aliongea  akiwa na tabasamu.

“Kwanini umepata huo ujasiri leo , kwangu mimi uzuri wako naona hautokani na mavazi”Aliongea.

“Nimepata ujasiri  wa kuvaa  hivi  kwasababu   nipo na wewe  mbele ya Classmate wangu wa  kitambo ”Aliongea  na kumfanya Hamza kushangaa.

“Unamaanisha nini?”

“Namaanisha  leo unakwenda kuigiza kuwa boyfriend wangu  mbele  ya wanadarasa  zangu  wangu wa Highschool , tuna Reunion leo  na nimewaambia nina boyfriend”Aliongea Prisila akiwa siriasi , hakuwa hata na aibu   kuongea hayo maneno na ndio kitu kilichomshangaza zaidi Hamza.

“Mwanamke mrembo kama wewe unakosaje mpenzi au ndio  unapanga kuniingiza kwenye matatizo?”Aliuliza Hamza ,  aliona haya maswala ya kufanywa boyfriend feki na kila mtu yanaanza kumchosha , swala la  kujiingiza kwa Regina lishaanza kumuumiza kichwa kuhusu usalama wake,lakini tena  Prisila anamwingiza.

“Ndio ujue sina  ,ndio maana  upo  hapa , kama ningekuwa nae ningehangaika vyote hivi , kabla sijaondoa gari fanya maamuzi  hapa hapa, je upo tayari kuigiza  kuwa bofriend wangu kwa leo tu?”Aliuliza na kumfanya Hamza kuanza kukuna kichwa.

“Sikia Prisila  mimi kazi yangu sio  kuigiza kuwa  boyfriend feki , nina mpenzi tayari,  kwa urembo wako sidhani kama unaweza kukosa mtu  ambae anaweza kufanya unachotaka , nipo tayari kulipa fadhila ila  sio kwa njia hii”Aliongea Hamza na palepale alifungua mlango wa gari  kutoka.

“Huyo mpenzi wako anajua unaigiza kuwa mpenzi wa Regina?”Aliuliza  na kumfanya  Hamza  kusita  kwanza na kumgeukia.

“Kwahio kwasababu bosi wako ameniajiri kuwa mpenzi feki  na wewe unataka kufanya hivyo, haiwezekani  kwa kila mtu , nilichokifanya kwa bosi wako ni shauku ilionifikisha hapa , lakini sio kurudia tena kwa mtu mwingine, kuhusu mpenzi wangu kujua ama kutokujua hili ni  swala  ambalo lipo juu yangu, nadhani unajua siwezi kuendelea kuwa na bosi wako  kwa muda mrefu”Aliongea Hamza.

Prisila alijikuta aking’ata meno ,  aliamini  ingekuwa  rahisi kwa mwanamke mrembo kama yeye kukubaliwa  na Hamza hata kimaigizo tu, lakini mawazo yake   yalikuwa tofauti kabisa , Hamza anamkatalia tena akiwa siriasi kabisa.

Upande wa Hamza mara baada ya kuona mwanamke huyo   anawaza ndio aliona ni muda wa kuondoka na alishuka kwenye gari na kuanza kupiga hatua akitaka kuvuka barabara kurudi  kwenye kampuni maana hakufika hapo na gari.

Prisila alijikuta akifumba macho  kwa dakika kadhaa  na kisha alifungua mlango haraka na  kutoka. “Hamza wait!!!”

Aliita akimaanisha  Hamza amsubiri  na Hamza  ambae tayari alikuwa ashaanza kupiga hatua kuvuka barabara alisimama akimsubiria.

Ijapokuwa alimkatalia mrembo huyo lakini mara baada ya kushuka kwenye gari muonekano wake ulizidi kumfanya kuonekana mrembo , Prisila alikuwa mwanamke mzuri sana   pengine  alikuwa akishika nafasi ya pili baada ya  Regina.

Hata watu waliokuwa karibu na eneo hilo walimkodolea macho  na kwa jinsi ambavyo  alimwita Hamza ni kama ilidhidhirisha kuna kitu kinachoendelea baina yao.

Prisila alikaza  mwendo na kumsogelea  Hamza , awamu hio  alikuwa mpole kuliko mwanzo.

“Hakuna namna unaweza kunibadilisha mawazo”Aliongea Hamza.

“Unakumbuka asubuhi ulichosema kwenye simu , upo tayari kufanya hicho kitu baadae , hii  ni ahadi umeweka, kosa lako ni kutokuuliza , kwanini

unanikatalia sasa hivi ilihali sina mbadala?”Aliongea.

“Na wewe kosa lako  ni kuamini naweza  kukubali  kila utakachoniambia na nifanye, hata  kama ni kujishusha thamani  na kukubali ombi  lako”Aliongea Hamza  akiwa na uso  usiokuwa  na hisia zozote. Lakini kauli yake ilimfanya  Prisila kushangaa na kujikuta akisugua meno, ilikuwa ni dhahiri  alitaka kusema yaani mwanamke mrembo kama yeye  kuigiza nae  kuwa mpenzi ni kujishusha thamani.

“Basi  naomba unisindikize , sina chaguo lingine, nitakutambulisha kama  rafiki yangu wa kawaida tu”Aliongea  katika hali ya kujishusha , lakini kilichomshangaza ni baada ya  kuona  Hamza anacheka.

“Unacheka nini .. umekubali au?”Aliuliza .

“Ukweli  ni kwamba nilikuwa nishakubali  tokea asubuhi , katika kitabu changu  cha kumbukumbu  sijawahi kushindwa  kulipa deni   hata liwe kubwa vipi?”Aliongea na  palepale alimpa mkono  Prisila ambae alikuwa akimshangaa,  alipokea kiwasiwasi na wakaanza kupiga hatua kuelekea  kwenye gari na  awamu hio Hamza hakumwingiza upande wa

dereva bali alimzungusha kwenye siti ya abiria na  mara baada ya kumfungulia mlango  aliingia ndani.

“Kama ulikuwa umenikubalia kwanini ulikuwa ukinizungusha , ulikuwa unanijaribu?”

“Huwezi kusema nilikuwa nikikujaribu , unaonekana  kuwa mtoto  unaepndwa na kupewa kila kitu,  lakini kumbuka  huwezi kupata kila kitu unachohitaji”

“Nani  kakuambia napewa kila kitu , ni kweli napendwa  na wazazi wangu lakini  wakati wao wa kunipa  kila ninachohitaji  ushaisha  na sasa natafuta ninachotaka ,  nilitaka wewe kuigiza kuwa boyfriend wangu kwa leo kwasababu  unanilipa na baada  ya hapo kila mtu anajua  mambo yake , ningeweza kupata mwanaume yoyote ndio  lakini hakuna ninaemdai hivyo  watakuwa  wananidai , unadhani  mimi mtoto wa kike nitakuwa nalipa kwa

njia ipi , watataka  mahusiano na mimi na mengineyo, labda hujui tabia yangu , napenda kudai  kuliko kudaiwa ndio maana najitahidi  kufanya kila namna  niwe nadai watu na sio kudaiwa”Aliongea na kumfanya Hamza kutoa tabasamu.

“Kwahio mpango wako ni kunitengenezea deni  tokea mwanzo na sio kunisaidia?”

“Nadhani ushaanza kunielewa sasa , lakini katika  watu niliowadai wewe ndio nimekupa namna ya kunilipa kirahisi lakini unaleta ujeuri”Aliongea huku akivuta mdomo.

“Hehe… ingekuwa miezi kadhaa iliopia  nisingekuzungusha hata kidogo”

“Unamaanisha nini?”

“Ninachomaanisha  sikuwa na  mpenzi  hata wa maigizo , sasa hivi nazungukwa na warembo  ni kawaida  kwangu kuringa kidogo”Aliongea na kumfanya Prisila kutabasamu.

“Endesha kuelekea  Kunduchi Prima  hotel”Aliongea  na Hamza alikata kulia kwake na kuichukua barabara  ya Bagamoyo Road kutoka Sam Nujoma.

Dakika chache mbele  walikuwa washafika katika hoteli ya  Kunduchi , ilikuwa hoteli ya kisasa na  ukweli  ni kwamba  Hamza hajawahi kufika katika hoteli hio licha ya kwamba sio mara yake ya kwanza kuwa katika hoteli  kubwa.

Prisila  alikuwa akiungana na wanafunzi wenzake  aliosoma nao High school, alikuwa amesoma shule za  hela nyingi hivyo  ilikuwa  ni sawa kukutana katika eneo la hadhi ya juu kama hilo.

Mara baada ya kuingia   katika hoteli hio ya rangi nyeupe , Hamza aliweza kuona bango ambalo  lina maandishi makubwa  yaliokuwa yakitambulisha hoteli hio, lakini kuna kitu ambacho kilimshangaza sana Hamza , ilikuwa ni picha  chini ya maandishi ambayo ilitumika kama Logo ya hoteli hio.

“Mbona unashangaa , unaangalia nini?”Aliuliza Prisila kwa shauku.

“Hamna  tu”Aliongea na kisha  alisogeza gari mpaka  eneo la maegesho na wakatoka, ile wanaanza kuzipiga hatua waliweza kuona  wenza wengine ambao mwanamke alikuwa amening’inia katika mkono wa mwanaume  wakiingia, walionekana kuwa romantic.

Mwanaume alikuwa amevalia shati  la mikono  mirefu  chapa ya Fendi  na saa  ambayo haikuonekana kwa ukaribu ni ya kampuni gani  lakini ilionekana ya thamani.

Mwanamke upande wake alikuwa amevalia  gauni la Chanel  la mkato wa chini , alikuwa amebeba begi  kwenye mikono yake chapa ya Hermes, licha ya kutokuwa mrembo sana lakini alikuwa  akivutia  na kuonyesha  ni wale wanawake wa hadhi ya juu.

“Lidya!!”Aliita  Prisila , alionekana kumtambua  huyo mrembo.

Mwanamke yule mara baada ya kugeuka kwenye macho yake kulionekana aina flani ya wivu lakini alibadilisha na tabasamu  bandia.

“Wow! , Kama kawaida yako  Prisila , unazidi kuwa mrembo siku hadi siku”

Aliongea  lakini upande wa yule mwanaume  mara baada ya kumuona Prisila macho yake yalichanua   na ilionekana  ilikuwa ngumu kuacha kumkagua  Prisila juu hadi chini.

“Lidya na huyu ni rafiki yako uliesoma nae?”Aliuliza yule  mwanaume huku akiendelea kumchunguza  Prisila.

“Ndio  jina lake anaitwa  Prisila ila   alikuwa

akifahamika zaidi kwa jina la Pria , Prisila huyu ni mchumba wangu anaitwa Bahati” 

“Mchumba!, aisee hongera zako , naona unaenda kuolewa”Aliongea  Prisila  akionekana kuwa  na furaha juu ya Lidya.

“Bahati  wangu usimuone hivi , ni mtoto wa Mzee Mtei  mmiliki wa  makampuni ya Mtei Enterprise , ijapokuwa huwezi kumuweka katika kundi  la vijana

matajiri kama Saidi , lakini  ni  bilionea kibongobongo, nadhani kuwa kwetu pamoja imepangwa”Aliongea  Lidya  akitoa taarifa ambao hazikuhitajika kabisa na baada ya kusema hayo aliinua  uso wake na kumwangalia kijana mtanashati anaejiita Hamza Mzee.

“Na huyu  kaka ni..?”Aliuliza  na  kumfanya  Prisila  kusita kumtambulisha  Hamza, sio kama hakutaka kumtambulisha bali  hakujua amtambulishe vipi.

“Niite Hamza ni zaidi ya rafiki kwa  huyu mrembo”Aliongea Hamza akiwa na tabasamu.

“Hamza!!, nakumbuka  mara ya mwisho wakati tunakutana Prisila  ulisema mpenzi wako amesharudi kutoka  nje ya nchi  na kwasababu alikuwa bize  hakuweza kuhudhuria , Mr Hamza unaweza kutuambia  kwanini ukamuacha mrembo kama huyu kuja   peke yake , wengi tulidhani huna mapenzi ya kweli kwa Prisila”Aliongea.

“Nadhani  wakati  mnakutana ndio kipindi ambacho  joto  la Dar lilikuwa kali sana , hivyo kazi za kutengeneza AC zinakuwa nyingi”Aliongea Hamza.

“Wewe ni fundi wa kutengen4eza AC?”Aliuliza akiwa mshangao na Hamza alitingisha kichwa kukubali.

“Hii ni mara yangu ya kwanza kusikia  mtu alietoka nje ya nchi  kuwa fundi  wa  kutengeneza AC , Are you for real?, unanifanya nitamani kucheka”Aliongea huku akichanganya kiswahili na  kingereza.

“Sorry , Prisila   nadhani unaijua tabia yangu ya kuropoka, hehe..”Aliongea  lakini  wanasema ndege wanaofanana huruka pamoja , hata kwa

Bahati Mtei alikuwa na tabasamu lililojaa kejeli.

“Lidya  hutakiwi kucheka , unajua fika AC zikiharibika kuna hitajika fundi, hivi ni vitu ambavyo hatuwezi kufanya  sisi wenyewe”Aliongea. “Ndio mpenzi ,  una akili sana”Aliongea  

Prisila alionekana kutopenda  jambo lile na alikuwa akitaka kusema kitu lakini  Hamza alimzuia kwa kumtingishia kichwa akimwashiria asibishane  nao.

Hakuona haja ya kubishana nao , ili mradi ashajua tabia zao hilo lilikuwa likitosha hivyo   kucheza ngoma yao ni kujishusha.

“Sioni sawa  kuchekana  kwasababu ya  vipato vyetu ,  hakuna aliezaliwa  nacho  , wote tunatafuta”Aliongea Prisila.

“Prisila sioni tatizo  kwa wao kucheka na kudharau wa chini  yao ,   sio wa kwanza , ni jamii ndio ilivyo, unaweza usiongee waziwazi lakini ubaguzi wa kipato  umeshamiri  kila kona, hata hili  kusanyiko  nadhani   halijalengwa kukutana  na kukuumbushiana habari za shule bali ni  kuvimbiana nani ana kipi  zaidi ya mwingine”Aliongea Hamza.

“Unanifanya nisitamani kuingia kabisa”Aliongea

Prisila.

“Ushafika , haina haja ya kujificha , ukiondoka watakuonna ni muoga  na utawapa sababu za kuendelea  kuongea, isitoshe kila aliekuja ni  kwa ajili ya kuonyesha anaendelea vizuri kimaisha , hivyo sidhani ni swala baya pia”Aliongea na kumfanya Prisila kumwangalia  usoni.

“Unaonekana  kuwa  mtu mzima na  mwenye kujiamini”Aliongea Prisila na kumfanya Hamza kutabasamu.

Kwasababu  Lidya  na mpenzi wake wameshatangulia kuingia na Hamza  na Prisila walianza kuzipiga  hatua kuingia ndani pia , lakini  Hamza alisimama ghafla mara baada ya kuhisi kuna mtu alikuwa akimwangalia na  macho yake alikuwa ameyakazia upande mwingine wa  maegesho ya  watu mashuhuri  na alikodolea macho  gari ya Roll Royce na kwasababu kioo cha upande wa kulia kilikuwa kimeshushwa aliweza kuona aliekuwa yupo ndani.

“Twende Hamza , mbona umesimama

tena?”Aliuliza Prisila  na kumshitua Hamza.

“Ulikuwa ukiangalia nini , ni mara ya pili nakuona unashangaa”

“Hamna  kitu, nadhani utanashati wangu unafanya watu kuniangalia sana, kuna mtu alikuwa akinikodolea macho”Aliongea huku akiwa na tabasamu  na kumfanya Prisila kutingisha kichwa chake  kwa masikitiko.

Walipokewa na mhudumu wa hoteli  ambaye aliwaongoza moja kwa moja  mpaka katika  chumba binafsi  ambacho kilikuwa na meza kubwa iliojaa wanaume na wanawake.

Watu wale mara baada ya  kumuona Bahati na Lidya akiingia walianza kuongea chini kwa chini wao kwa wao na baada ya kuonekana kwa Prisila  walizidisha.

“Prisila!!”

Mwanaume mrefu  wa mita kama moja na nusu hivi aliita , na alionekana kumwangalia  Prisila kwa sekunde kadhaa kabla ya kuhamishia macho yake kwa Hamza.

Prisila aliishia kutoa tabasamu na waliingia ndani na alichukua nafasi hio kumtambulisha  Hamza na walionekana kuridhika nae , pengine  ni kwasababu ya mavazi yake , lakini upande wa Lidya  hakuwa na kifua.

“Oteeni kazi anayofanya  mpenzi wa mrembo wa darasa”

“Kwa muonekano wake nadhani anahela za kutosha , sio watu wa kawaida wenye kudumu mavazi ya bei hio, muonekano wake unaongea kila kitu”

“Ahah , muonekano wapi , ni fundi wa  kurekebisha AC zilizoharibika”Aliongea Lidya.

“Nini!!?”

Watu wote waliokuwa ndani ya eneo hilo walionekana kushangaa, sio kwamba walikuwa wakishangaa kazi ya Hamza bali walikuwa wakishangaa  Prisila mwanamke ambae alikuwa mrembo wa darasa wakati  wakiwa shule kuwa na mpenzi ambae  ni fundi wa kawaida na  wengi  walianza kumwangalia Hamza  kwa kejeli.

Asilimia kubwa ya waliokuwa hapo ndani walikuwa wametokea katika zie familia za matajiri , ijapokuwa Prisila famiia yake ilikuwa na pesa  lakini hawakuwa matajiri , baba yake ambae ni profesa hakupata mshahara wa kuitwa tajiri, hivyo  ni kama yeye ndio ambae familia yake ipo kinyonge zaidi.

“Mbona mnashangaa , hamjawahi kusikia wala kuona  mafundi?”Aliongea Prisila huku akionyesha kukosa utulivu.

“Haha.. usituelewe vibaya  Prisila , kwa  urembo wako na hadhi uliokuwa nayo wote tulitegemea mpenzi  wako kuwa wa hadhi  ya juu, nilitarajia  ungekuja na Chriss  mtoto wa tajiri  Gabusha labda ndio maana tulikuwa na hamu ya kumjua”Aliongea mwanaume ambae alikuwa akiitwa  Dismasi.

“Umejuaje nina mawasiliano na Chriss?”Aliuuliza 

Prisila.

“Karibia marafiki zote wa Chriss wanajua  nyie ni wapenzi , nimeshangaa kuona ukimtambulisha mtu mwigine”Aliongea na kumfanya Hamza kumwangalia Prisila.

“Hata kama , sina mahusiano na Chriss  ni mwanaume ambae ananifuatiia  ila hana kigezo cha kuwa mpenzi wangu”Aliongea.

“Prisila unamaanisha  nini hana kigezo,  ni kipi ambacho  huyu Hamza wako kamzidi , kama ni ushombeshombe  hata  Chriss anao na kubwa zaidi  ndio mtoto wa pekee wa Mzee Gabusha hivyo  mali zote  za baba yake ni za kwake”Aliongea Lidya huku akiona kabisa  Prisila anajaribu kujikweza mbele yao,  Lidya alijiambia kama Chriss yupo tayari kutoka  nae kimapenzi basi angeachana na Bahati saa hio hio bila  huruma yoyote.

“Hivyo ni vigezo vyako   usitake  kila mmoja avitumie katika kuchagua watu sahihi, unaongea kama vile  Hamza  hana  vigezo , unamjua vizuri au

kisa  umnemuona leo ndio unaanza kumhukumu?”Aliongea Prisila  alionekana kukasirika mno , angejua  hilo lingetoka asingekuja kabisa na Hamza.

Aliona amemleta mtu wa watu kwa ajili ya kupokea vichambo , lakini mara baada ya kugeuza macho yake pembeni kumwangalia Hamza ambae anasemwa , alionnekana kuwa bize na  chakula ambacho kimeandaliwa.

Hamza hakutaka kuwa na hasira , aliona kuwa na hasira ni kujishusha kuwa katika levo sawa na wao, kwake  hali hio ilikuwa ikimfurahisha sana kwani aliona  ni kama vichaa wamekutana na kuanza kulumbana.

“Jamani  haya mambo yametoka wapi , hii ni mara ya kwanza  kwa  Prisila kumtambulisha mpenzi wake  kwetu , tunachoongea hakina umuhimu kabisa , kazi yake inahusiana vipi , isitoshe   hata kazi yake ni muhimu pia, nani kati yenu anajua kutengeneza AC?”Aliongea Saidi kijana tajiri zaidi ambae ndio  kiongozi wa kuandaa mkusanyiko huo wa  wanafunzi wenzake kila mwaka.

Kundi hilo   la watu walicheka  na  kukubaliana nae , huku wengi wakijikomba kwake kwa kumpamba kama mtu mwenye busara.

Gharama zote za  kukutana zilikuwa juu ya  Saidi Mohamed na vyakula vya bei ghali viliandaliwa na kubadilishwa kila  dakika  na jambo hilo liliwafanya  watu wote kuendelea kuwa chawa  kwa kumsifia sifia na kujipendekeza.

“Nimesikia kutokana na  wateja wengi kuipenda hii hoteli , mmiliki ametengeneza mfumo wa kutoa kadi za uanachama kwa  baadhi ya watu wa hadhi ya juu tu, hivyo kukaa hapa  lazima  uwe mwanachama na si vinginevyo, nasikia bosi wa mahoteli yote ya Prima  ni mwanamke”

“Sio hivyo tu , nasikia pia  asilimia kubwa ya wanachama ni wale ambao wanafahamiana na mkurugenzi , Bro Side mpaka kutupatia nafasi ya kukutana katika hii hoteli lazima  uzito wako baada tu ya kurudi  Tanzania umeongezeka”Aliongea Lidya.

“Hivi ni kweli hii hoteli ipo chini ya Prima Real Estate , nilichosikia Boss Yulia  anatokea katika  familia kubwa tu hapa  nchini”Aliongea Dismasi.

“Haishangazi sana , ulimwengu wa kitajiri ni wa tofauti sana na watu wa kawaida”Aliongea bwana aliefahamika kwa jina la Jimmy.

“Nasikia  kampuni ya Prima licha ya kuwa na sifa za kuingia katika soko la hisa  ilishindikana kutokana  na asili ya  wanaoimiliki , lakini kama ingeingia katika orodha ya  soko la hisa  ingekuwa moja ya kampuni  yenye thamani kubwa  sana  kimtaji, ijapokuwa kuna usiri mkubwa juu ya familia anayotokea Yulia  lakini hata mimi naamini 

atakuwa  na koneksheni kubwa ndani ya serikali”Aliongea mwingine.

“Boss Side , umewezaje kupata  kadi ya uanachama ndani ya hii hoteli , utaratibu wao   wa kutoa uanachama huwa unakuwaje?”Aliuliza Lidya.

“Ilikuwa kama bahati  tu  nikakutana  na Mkurugenzi na ndio  alinialika kwa kunipatia kadi ya uanachama”Aliongea Saidi na muda uleule aliingiza mkono kwenye koti lake la suti na kuchomoa kadi na kumpatia Lidya.

“Aiyaa .. kadi inapendeza kweli ,  Bosi Side  hebu tuione na sisi”Waliongea huku wakigombania.

Lakini  upande wa Side alionekana kama vile hajaridhika mara baada ya kuona  Prisila hakuwa akijali  kabisa  jambo  lile.

“Jamani ilivyokuwa nzito , nadhani  imetengenezwa kweli na  madini ya dhahabu kama walivyosema”

“Ni Gold kweli , Lidya hebu acha kukaa nayo muda mrefu , nipe na mimi nione”Aliongea mwingine 

“Subirini kwanza , bila ya kapicha  hili halipiti hivi hivi”Aliongea huku akitoa simu yake ya I phone  na kuanza kupiga selfie.

Bahati mpenzi wake alionekan kutoifurahia  tabia  ya mpenzi wake kumpapatikia  Saidi, aliona  ni kama vile anapotezewa licha ya yeye pia kuwa tajiri.

Lidya hakuishia kupiga picha akiwa ameshikilia ile kadi, lakini vilevile alipiga  Selfie akiwa na  Bosi Side  na dakika ileile aliposti huku akiandika  Caption

“It feels so good  to have a meal with Director Said Mohamed of Vodocum Corporation”

Mara baada ya kuona  Lidya  alichokuwa akifanya wanawake waliokuwa hapo pia walitumia nafasi hio kupiga picha  na Saidi Mohamedi , Mkurugenzi mtendaji wa  kampuni kubwa ya mtandao  ya Vodocum.

“Prisila angalia  na wewe ,  ni  watu wachache sana wanabahatika kushika kadi kama hizi kwenye maisha yao yote”Aliongea mwanadada aliefahamika kwa jina la Phina.

“Nishaiona tayari , mnaweza kuendelea tu kuiangalia”Aliongea Prisila akiwakatalia.

Bahati  licha ya kuwa bosi wa kampuni ndogo  hakutaka kujishusha  lakini hata hivyo hakutaka kukaa kizembe kutotumia fursa hio na palepale alitoa  kadi yake  ya biashara.

“Mkurugenzi  mimi ni GM  kutokea kampuni ya Mtei Enterprise.tafadhari naomba upokee kadi

yangu ya biashara kwa ajili ya

mawasiliano”Aliongea  lakini  Bosi Side aliishia kuipokea na kuiweka  juu ya meza.

“Uniwie radhi ndugu , tupo hapa kwa ajili ya kukutana  na sio  kuongea maswala ya kazi , hivyo  hatuwezi kubadilishana  mawasiliano.”

“Haina shida , umekuwa role model wangu katika  maswala ya kibiashara  sio rahisi kuongoza kampiuni kubwa   ya mabilioni ya fedha  kwa umri mdogo , baba pia  mara nyingi amekuwa akiniambia niige mfano kwako, ni juzi tu  kutokana na  mwelekeo wa  kampuni yako  tulikuwa tkipanga kuwekeza kwa kununua hisa Vodocum”

“Nadhani tule kwanza , tutaongea baadae kama tutapata nafasi hio”Aliongea  akimkatisha.

“Oh .. basi hakuna shida”Bahati alijikuta akinywea , alitamani kuwa na ukaribu na mtu mzito kama Side  katika orodha ya  mawasiliano yake,alitamani hata  kuwa  na namba yake tu ili  kwenda kujigamba kwa wenzake, lakini  Side alionekana kumkataa mbele ya watu.

“Side hebu fanya hivyo kwa ajili yangu bwana  na kumpokea  Bahati kwa mikono miwili , Mtei Enterprise  sio kampunni ndogo naamini baadae itakuja  kuwa  kubwa,    kwasasa  kampuni yao ina thamni ya bilioni kumi, sidhani kama inaweza kuitwa kampuni ndogo”Aliongea Lidya.

“Lidya naona  mchumba wako anatokea katika familia ya kitajiri , hongera sana ukiolewa na wewe moja kwa moja unakuwa tajiri”Aliongea Phina kwa wivu na kauli ile ilimfanya  Bahati kuona angalau sasa na yeye ameanza kuonekana.

“Ukiilinganisha kampuni yetu na Vodocum  sisi ni kama sisimizi tu”Aliongea  akijaribu kwa mara  ya pili kuwa chawa.

Ki ufupi kusanyiko hilo halikuwa  na ile  hali ya kuvutia kwani   kila mtu alikuwa akiongea kile alichokuwa nacho na walichokamilisha  huku wengine wakiwa chawa na walisahau hata kula.

Upande wa Hamza alikuwa bize  na Kambakochi ya bei ghali ambayo imeandaliwa  na  alimwangalia  Prisila na kuona mwanamke huyo alikuwa na wasiwasi mno.

“Prisila huna njaa , kula  hata kidogo?”Aliongea Hamza na kumfanya Prisila kutoa tabasamu  baada ya kuona  Hamza hakuathirika na  kilichoendelea na angalau alipata hamu ya kuanza kula japo kidogo.

“Prisila ombi langu la mara ya mwisho  juu ya kuja kufanya kazi katika kampuni yetu bado lipo hai , lakini sijasikia majibu yoyote kutoka kwako?”

“Boss Side unataka  Prisila kwenda kufanya kazi katika kampuni yenu , nasikia  licha ya Dosam kuwa  kampuni kubwa na kulipa vizuri lakini  kwa

Vodocum ni habari nyingine”

“Vodocum ni kampiuni Kongwe ina matawi  Afrika nzima , kuna rafiki yangu mjomba wake licha ya kuwa kitengo cha kawaida lakini ana maisha”

“Prisila  uwezo wake  ni mkubwa sana , makampuni  mengi yanamhitaji kwa ajili ya  kufanya nae kazi , si  jambo la ajabu  kuombwa na sisi aje afanye kazi Vodocum Tanzania   na  kutokana na thamani yake kuwa juu  nipo  tayari kwenda juu zaidi katika mshahara wake kuliko anaopata pale Dosam”

“Boss tupo wafanyakazi wenye uwezo zaidi ya  Prisila mbona , au kuna sababu za kutaka kumuajiri yeye tu ,unampenda nini tajiri?”Aliongea  mmoja wapo lakini  Side alimpotezea.

“Kwasasa niseme napenda kazi yangu  katika

kampuni ya Dosam ,Bosi Side uniwie radhi sipo tayari”

“Hakuna shida ,  una muda wa kutosha wa kufikiria”

“Prisila   unasita sita nini , kufanya kazi  ndani ya kampuni ya Vodocum sio swala la mshahara tu, unajitambulisha kimataifa, pili  ndio nafasi pekee ya kuwa  karibu na bosi Side , unajuaje tunaweza kukuita Mrs Side haha..”Baada ya  baadhi yao kusikia kauli hio waliishia kutoa tabasamu  la kinafiki, lakini  kauli ile ilikuwa ni kama imemkera zaidi Prisila.

“Nyie mkiendelea kuongea ujinga , nitakasirika”Aliongea Prisila akiwa siriasi.

“Acheni kumtania Prisila ,ninachofanya ni kuhakikisha  Prisila  hadhi yake  inapanda ndio maana , hakuna zaidi ya hilo”Aliongea Side.

“Prisila  usimuangushe bosi , ni  bahati ujue kufuatwa na  bosi mwenyewe kutaka kufanya nae kazi, unaweza kuona sio maamuzi sahihi lakini  kumbe  ulioshikilia ndio maamuzi  mabaya”Aliongea Lidya.

“Lidya kuna haja gani ya kuzunguka zunguka , unamlenga Hamza , kwanini usimwambie  moja kwa moja “Aliongea  Dismasi.

“Sijataja mtu jina ,mnikome”Aliongea  na kufanya  watu kuanza kucheka  kinafiki huku wakimwangalia Hamza , hakuna ambae anajali kama Hamza anaweza kukasirika au Lah na jambo   lile lilimchosha  Prisila na kumshika mkono Hamza.

“Tuondoke , siwezi kuendelea kukaa hapa”Aliongea na kumshitua Hamza ambae alikuwa akimalizia  kubeba kipande  cha mwisho cha  nyama.

“Umekasirika kwasababu ya wao  kunicheka?”Aliuliza Hamza.

Prisila hakutaka kumfanya  Hamza kujisikia vibaya , ijapokuwa  alikuwa akitafuta hela kwa shida , lakini   hakuona ni tatizo tofauti na hao watoto wa matajiri ambao   wanadhani  pesa ndio kila kitu.

Upande  wa Hamza licha ya kwamba hakuwa

akijali , lakini   alihisi  furaha mara baada ya kuona  Prisila  hataki kuona  akiendelea kuchekwa.

“Nisisikie mtu anamuongelea tena Hamza , huyu ni braza  wangu kuanzia leo hii”Aliongea  Side , shida yake ilikuwa ni kutokumfanya  Prisila asiondoke maana alikuwa akifurahi kumwangalia.

‘Prisila usikasirike , leo ni siku nzuri na tumekutana na kumjua mpenzi wako hivyo anapaswa kupewa heshima yake”Aliongea  na kauli yake iliwafanya wote sasa kutulia.

Prisila  alikuwa  bado anasita sita kuendelea kubaki , lakini kwasababu Side ndio   kaongea aliamua kutulia.

Sasa dakika hio hio  mlango wa chumba hicho ulifunguliwa  na wafanyakazi waliovalia sare nadhifu  walitengeneza njia   huku wakionyesha heshima  juu ya mwanamke ambae alikuwa akiingia.

“Nini tatizo , mbona kama nahisi kuna mtu anataka kuondoka tayari?”Aliongea kwa kingereza ,  alikuwa ni mwanamke  mchangamfu.

Alikuwa amevaa  shati la mikono mirefu  la michirizi myeupe na mieusi  huku akiachia vifungo kadhaa kifuani , huku chini akiwa amevalia suruali  ya rangi ya kahawia   akimalizia na  koti la surti ya rangi ya  kahawia ,  mavazi hayo yalimfanya kuwa mrembo sana na kuchora umbo lake  la kuvutia.

Alikuwa  amesuka nywele zake  kwa mtindo wa Crochet  na kumfanya nyuzi nyuzi ndefu kumwagika begani , alikuwa na weusi angavu  rangi ya chocolate, hadhi yake ilikuwa ni ile  ya  mwanawake wa  daraja la juu.

Alikuwa mrembo mno  tembea yake kutumia viatu vya skuna  na harufu ya  marashi yake ya bei ghali ilifanya wanaume kumeza mate.

Kingine cha kuvutia zaidi ni  kwamba  namna yake ya kuongea ilijaa  mapozi  na  cheo kwa wakati mmoja, ni aina flani ya haiba ambayo  mwanamke wa kawaida hawezi kuwa nayo, ni haiba ambayo mtu hufunzwa na sio kuzaliwa nayo.

Mwanamke pekee ambae alikuwa na uwezo wa kushindana nae  katika  muonekano  ni Prisila peke yake , lakini bado  haiba  yake na   utulivu  wa macho hakumfikia.

Kitendo cha  Hamza kumuona mwanamke huyo akiingia  muonekano wake ulibadilika na kuonekana wa usiriasi kidogo  na ghafla  ni kama  amekumbuka  kitu alichosahau kuona na kujikuta akitoa tabasamu ambalo limejaa uchungu.

Tatizo  pekee ambalo aliliona  ni  moja tu na kujiuliza imekuwaje huyu mwanamke  akawa Tanzania  tena katika mazingira kama hayo.

Upande wa mwanamke macho yake yote yalikuwa yamemkazia Hamza , huku akionyesha  ishara flani ya kuzuia hisia zake.

Upande wa watu waliokuwa hapo ndani pia walikuwa katika hali  ya mshangao , walishangazwa na  kivuli   cha mwanamke huyo kilivyokuwa  na nguvu na kuwasabibishia   msisimko.

Alieanza kusimama  kwa heshima alikuwa ni  Saidi Muhamehd au bosi Side.

“Bosi Yulia! , sikutarajia kama utakuwepo leo?”Aliongea Saidi.

Wengine wote mara baada ya kusikia jina la Bosi Yulia walielewa ni   nani anaongelewa na walijikuta wakisimama mara moja , huku maswali yakiwavaa ,wakijiuliza inamaana huyu ndio moja ya mataikoni wa kike  ndani ya taifa  la Tanzania, mmiliki wa makampuni ya Prima.

Hakuna ambae ashawahi kudhania bosi Yulia angeonekana kuwa kijana na mrembo hivyo, isitoshe  wanawake  ambao walikuwa ni matajiri  hawakuwa na muonekano wa kuvutia tofauti ya Regina na  Yulia.

Kila mmoja alionyesha heshima , huyo alikuwa ni bosi  zaidi ya  Saidi .

Bahati  alikuwa  na furaha mno kiasi kwamba  hakujua ni wapi aweke mikono yake , moyo wake ulikuwa umejaa furaha , mwanzoni    mpango wake ulikuwa ni kumtumia  Lidya ili kujenga  ukaribu na  Tajiri Side  ndio maana akalazimisha kushiriki kusanyiko hilo  lakini sasa  anamuona  Yulia shabaha yake ilibadilika mara moja.

Muda huo  wanadarasa hao walikuwa wakimuonea wivu  Saidi mno kutokana na kuwa na ukaribu na bosi mkubwa kama huyo tena mrembo.

“Kwahio kumbe ni wewe bosi  Side ndio umeandaa hii party , mniwie radhi kwa bughuza”Aliongea kwa lugha ya kingereza. Na maneno yake  mbele ya wasomi hao yaliwashangaza , ilikuwa ni kama wanajiuliza inamaana amefika kwa ajili ya kuangalia  party ambayo imeandaliwa  na Saidi , lakini sasa kilichotokea  mbele kiliwashangaza.

Bosi Yulia alizipiga hatua na kumsogelea  Hamza  huku akimwemwesa lipsi zake kama mtu aliekosa kujiamini.

“Sikuwahi kuwaza nitakuja kukutana na wewe hapa , nilidhani sitokuja kukuona kamwe”Aliongea na kulikuwa na ishara ya uchungu katika  sauti yake.

“It real is fate”Alijibu  Hamza  kwa  lugha ya kingereza  akimaanisha ni majaliwa huku akitoa tabasamu.

“Yaani , nilipokuona  pale kwenye  maegesho ya gari nilijiuliza ninaota au, hata kuja hapa sijaamini kama ni wewe, nimekuja kuhakiki , lakini  ni wewe kweli?”Aliongea bila ya kupepesa jicho.

“Bosi Yulia , unafahamiana  na Hamza  muda mrefu?”Aliuliza Saidi na kufanya kila mtu kutegemea jibu.

“Hamza!! , kumbe ndio jina lako?”Aliongea yulia  na kufanya watu kuzidi kushangaa huku wakijiuliza wanafahamina vipi huku hawajuani majina au Hamza hakuwa na jina hapo  kabla.

“Ndio”

“Umefika lini  na kwanini Tanzania?”Aliuliza Yulia.

“Ni stori ndefu”Alijibu Hamza na kumfanya Yulia kutabasamu.

“Niambie taratibu taratibu , sio rahisi kukutana na wewe hapa , awamu hii nadhani  haitakuwa haraka , bado hata sijakushukuru kwa kilichotokea  wakati ule  kama isingekuwa wewe ning….”

“Miss Yulia , its not convinient to talk  about it here “Aliongea Hamza akimaanisha kwamba sio vizuri kuongelea hilo hapo.

“Nini tatizo , kwanini umebadilika sana , wewe katika kumbukumbu zangu sio  mpole hivi”Aliongea Yulia.

Watu wote waliokuwa hapo walijikuta wakishangaa kwa kuwaangalia wawili hao na maongezi yao , ilionekana ni kama vile  Hamza amemfanyia Yulia kitu cha ajabu  nje ya nchi , ndio walivyotafsiri.

Yulia alionekana kuelewa  na hapo hapo alimsogelea Hamza karibu  kabisa, huku  akiona  hali hio  aliokuwa nayo Hamza inamvutia mno ,  walisogelena karibu kiasi kwamba mpaka  pumzi zao zinagusana ngozi ya kila mmoja.

“Then do you want  to come to my house ?, just me and you alone , we can have a good chat”Aliongea akimaanisha  au anataka  aende nae  kwake wakiwa wawili tu  na  kufanya maongezi yawe mazuri zaidi.

Alichokuwa akifanya  Yulia ni  kumpagawisha  Hamza mazima tena bila ya kificho.

Sasa fikiria  bosi  mkubwa  kama Yulia anamfanyia hivyo   Hamza  ambae sisi tunamjua ni mzembemzembe.

Kauli hio ilimfanya  Prisila  na wenzake wote kutoa midomo kiasi kwamba ukiwawekea yai linapita.

Walijiuliza Hamza ana nini mpaka mwanamke wa aina hio kumwalika  kwa  kimitego namna hio.

Tajiri Side hata yeye muonekano wake ulibadilika , ulikuwa muonekano mzito , hasa baada ya kupotezewa kabisa  na Yulia.

“Just who is Hamza!!?”Ndio swali ambalo lilimvaa mara moja.

Prisila alikuwa akimjua Yulia vizuri kwa kumsikia ,  lakini kitendo cha mwanamke huyo kumfahamu  Hamza ilimfanya awe na shauku ya kutaka kujua kwanini   Hamza anafahamiana nae , ukweli ni kwamba hio ni mara ya pili kwa Hamza kumsahngaza , mara ya kwanza ilikuwa ni  mwanasayansi nguli wa hisia za kibinadamu  wa  taasisi ya Felizi yaani Frida na  leo ni tajiri  Yulia.

Kitendo cha  Hamza kuwa katika  hali kama hio na mwanamke tajiri na mrembo kama huyo ilikuwa ni vibao chapuchapu kwa kila mtu ambae alikuwa akimbeza kuwa fundi.

Watu hao ambao waliona hawawezi hata kukaa

meza moja kula chakula na Yulia  na sasa  walikuwa wakimbeza mwanaume ambae alionekana ana historia nae.

Wale wote ambao walicheka sana walianza kumwangalia Lidya  kwa macho ya hasira, walijiambia kama sio  Lidya kuongea upuuzi wake  na umbea umbea wasingejiweka upande mbaya na Hamza na pengine wangeweza kupata  walau nafasi ya  kujipendekeza kwa Yulia.

Upande wa Hamza hakuwa na mawazo  hayo kabisa , alijua kama  Yulia ataendelea kuropoka itamletea shida  kabisa  hususani katika matukio ambayo yamekwisha kupita 

Hivyo Hamza bila kujifikiria mara mbilimbili alimshika  Yulia  mkono na kisha akamvuta kumtoa katika chumba hicho.

“Niufuate” Aliongea.

Previoua Next