Reader Settings

SEHEMU  YA 46.

Regina mara baada ya kuisikia hio kauli uso wake ulipata moto  kwa aibu  maana ni kama kitu ambacho hakutegemea.

“Bibi unaongea  nini , mimi siwezi kuolewa nae?”Aliongea Regina

Hamza hata yeye  alikuwa  kwenye kuchanganyikiwa , hatua hio aliona ni ya haraka sana  , isitoshe  hata mwezi haujaisha tokea afahamiane na Regina.

“Hutaki kuolewa nae , kwahio umetafuta boyfriend wa kucheza na akili  yangu ili niridhike  au ni kama  alivyosema  Lamla,  Hamza ni mpenzi wako feki”

“Sio hivyo bibi , mimi na Hamza ni kweli  ni wapenzi”Aliongea Regina kwa kusita sita.

“Kama ndio hivyo  nataka muone , sio lazima ya sherehe , kwasababu Hamza ni muislamu na wewe ni mkristo mnaweza hata kwenda kuandikisha ndoa yenu bomani  na kuanza kulala pamoja , mkishaona nimekufa  mnaweza kuachana kama  hampendani”Aliongea 

Regina alishikwa na wasiwasi mkubwa mno  na aligeuka na kumwangalia  Hamza  lakini kwa bahati mbaya  alikutana na uso uliokuwa na tabasamu zito  na kujiambia  hili lipuuzi mbona linatabasamu, au ndio mpango wake kutaka kunioa kwa muda mrefu, Regina alijihisi  kichaa kinakwenda kumshika.

“Bibi hali yako sio nzuri kwasasa , kwanini  tufunge ndoa wakati wewe unateseka , tusubiri ukishapona tutaanza kufikiria swala la ndoa”Aliongea Regina akijitahidi kutafuta kisingizio  cha aina  yoyote ile ili kumtuliza bibi yake.

Ukweli ni kwamba hakuwahi kuwaza kuolewa  na Hamza na sio hivyo tu  hakuwaza ingekuwa mapema hivyo baada ya  bibi yake kuija Dar kitu cha kwanza  anachotaka ni  kuona ndoa, yaani ilionekana mzee huyo hajaja kupona bali kumuozesha.

“Hivi  unadhani  na huu uzee wangu pamoja na kuumwa akili yangu haifanyi kazi , usisahau  ni mimi na babu yako tuliopigania kampuni  ya Dosam imesimama, hata kama nimekuwa mzee huwezi nidanganya kirahisi”Aliongea  na kumfanya Regina kuonyesha muonekano wa kukosa kujiamini.

“Bibi nathubutu vipi kukudanganya?”

“Regina usisahau hisa asilimia  hamsini na moja unazoshikilia  therathini na mbili ni za kwangu na kumi na tisa ndio zako , hisa zangu ni nyingi hata uunganishe na  saba za baba yako”Aliongea.

“Bibi najua hilo..”

Upande wa Hamza ndio kwanza alianza kushangaa ,  ukweli siku zote alijua Regina ndio  mwenye hisa nyingi ndani ya kampuni  lakini kumbe   ni bibi yake ndio mmiliki mkubwa wa  kampuni , sasa ndio anajua bosi mwenyewe wa kampiuni ya Dosam ni  Bi Mirium.

“Asilimia  kumi na tisa jumlisha asilimia  32 ya hisa zangu  jumla yake  ni  hamsini na moja , hii ndio  maana halisi ya kuwa bosi wa kampuni ya Dosam na kuwa na nguvu , wakati babu yako anafariki  aliweka wazi katika wosia wake  ukiweza kuolewa  na  kuanzisha familia yako ndio nitakukabidhi moja kwa moja asilimia  zangu zote , sasa kama hutaki kuolewa  nitampatia baba yako hisa zote therathini na mbili  na ndio atakuwa mmiliki halali”Aliongea.

“Bibi!!?”

Regina alijikuta akishangazwa na maamuzi ya bibi yake  na kuishia kukunja sura.

“Bibi sio kama  nina tamaaa sana lakini wewe mwenyewe unajua baba hana uwezo wa kuiendesha kampuni , isitoshe kama akisikia  hivi  nina uhakika mtu mwenye nia mbaya atazikwapua hisa zote  na kampuni kutoka nje ya umiliki wa familia”

“Unadhani kwa umri huu najali sana  hela , kwangu vitu na hela  havina maana sana , ukifikia  umri wangu utajua ninachomaanisha , sababu babu yako kuacha wosia ule  ni kwasababu anataka  uwe  na familia, kwasababu ndio  kitu pekee ambacho kinaweza kukufanya kuwa na furaha na kuvumilia yote, wewe mtoto  kwanini huelewi , kila kitu ni kwa ajili yako  lakini unashindwa kukubali ,  babu yako anachotaka ni familia kuongezeka  na amenisisitizia hilo  na ndio ninachotaka kuona kabla sijaaaga”Aliongea na kumfanya Regina kushangaa , hakuamini babu yake Dosam alikuwa na  mpango huo kichwani.

“Sikutaka kukulazimisha swala la kuolewa kwasababu nilitaka wewe mwenyewe utafute mtu unaempenda bila ya kujali hali yake ya kimaisha wala dini , ndio maana  hata baba yako  aliposema anataka uolewa na mtoto wa mzee Benjamini sikuongea chochote , sasa  Hamza huyu hapa umemtafuta mwenyewe  lazima nihakikishe  mnafunga ndoa, au nimekosea, mimi sijakulazimisha kuolewa na mtu usiempenda , si umesema mwenyewe  Hamza ni mpenzi wako

?”Aliongea  mzee huyo , ilikuwa ni kama vile  ndio misheni yake ya mwisho anayotaka kuikamilisha kabla ya kufunga ndoa,

Regina alijikuta akikosa neno la kuongea , alitamani kusema Hamza sio mpenzi wake lakini hakuwa akiweza kufanya hivyo  na kumfanya kutamani kulia , isitoshe alijua Hamza ana mpenzi wake hivyo asingemlazimisha kuolewa nae.

“Halafu  ili uelewe vizuri kabla ya kufanya safari ya kuja hapa  nishaongea na mwanasheria  kwa ajili ya kuandaa nyaraka  za kusaini , muda wa kupoteza sina  ni aidha iwe sahihi yako au ya  baba yako ,

kila kitu kinategemeana na maamuzi  yako na Hamza mtakayoamua”

Mara baada ya kuongea kauli hio alifumba macho yake na kujifunika vizuri shuka akionekana kabisa hakutaka kuendelea kuongea.

Regina kihasira hasira alienda mpaka kwenye chumba chake cha kujisomea  na Hamza alifuata nyuma nyuma.

“Regina inamaana ni kweli tunakwenda kufunga ndoa?”Aliuliza Hamza kizembe.

“Ndio unachotaka?”

“Sijamaanisha hivyo , siwezi kufunga ndoa na wewe mimi,,  nadhani unajua hilo vizuri”Aliongea Hamza  lakini maneno hayo hayakuwa na radha nzuri

kabisa kwenye masikio yake, alijihisi  kuumia kuona Hamza hakuwa hata na wazo  la kumuoa.

“Kwannini unaongea hivyo , unaonekana kutonipenda kabisa, nachukiza sana?”Aliongea Regina huku akizidi kuwa kauzu.

“Sio hivyo , unajua wewe ni mrembo sana  na pia ni mwanamke tajiri , ni  bahati sana kuweza kupata mwanamke wa aina yako..”

“Hebu acha kuongea , mpaka sasa   hata sijui nani ni rajiri zaidi kati yetu”Aliongea , Regina hakusahau Hamza alikuwa akivaa mavazi ya bei ghali mno ambayo hajawahi kuyavaa kwenye maisha yake licha ya kutambulika kama mwanamke tajiri.

“Isitoshe hata huyo Master Alex  fundi wako simfahamu vizuri ,  bado kuna  Dokta Ronica ambae siwezi hata kula nae sahani moja”

“Bosi Regina  hebu acha kunishangaza , mimi nipo chini yako ?”

“Nani unamaanisha haswa?”

“Utajua mwenyewe kama hujaelewa “Aliongea Hamza , hakuwa kabisa na mpango wa kujibishana nae , lakini kwa wakati mmoja alijikuta akifurahia ndani kwa ndani , sio kwamba alifurahia  kwasababu  ya pendekezo la Bibi Mirium , ila ni kwasababu  hakujua ni maauzi gani ambayo  Regina na ukauzu wake atayachukua, alitaka kusoma  mchezo hadi mwisho utakavyokuwa. “Hebu ondoka  kwanza nataka kufanya kazi”

“Bado unataka kufanya  kazi , umekuwa bize siku nzima  kwanini usipumzike”

“Jali mambo yako , Tokaa!”

Hamza alishia kujisikitikia na kutoka  kisha akafunga mlango , ukweli ni kwamba  kila ambacho alikisioma mtandaonni kuhusu Regina alikuwa akikishuhdia katika mazingira halisi.

Regina alitambulika mtandaoni kama mfanyabishara katili likija swala la kutengeneza pesa  na ndio ambacho  alikuwa akiona  na wengi walitafsiri hivyo  na  kuna wengine ambao walienda mbali na kuwaza Labda  Regina alikuwa ametengenezwa na Mzee Dosam kuwa roboti la kutengeneza pesa.

Hamza aliishia kumuonea huruma na kujiwazia kama  kampiuni  itakuwa katika mikono ya baba yake  moja kwa moja itamilikiwa na Lamla na familia ya James   na ikifikiria hatua hio  Regina  atakuwa katika hali  gani.

*****

Upande wa chumba cha Bibi Mirium , Shangazi alikuwa akimfunika vizuri

“Madam natoka kwenda kupumzika sasa , uwe na usiku mwema”Aliongea.

“Mariposa hebu niambie , unadhani  Hamza  anao  uwezo wa kumlinda  Regina?”Aliuliza na kumfanya Shangazi kugeuka.

“Ndio nina uhakika asilimia mia , ijapokuwa sijui ametokea nchi gani  na ni nani haswa  lakini  kwa kipindi chote nilichomfuatilia , sio mtu mwepesi”

“Kwa uzoefu wako  tokea  ukiwa kitengoni mpaka sasa , kama umesema sio mtu mwepesi basi naaamini asilimia mia,  mimi ndio nishazeeka hivyo , wasiwasi wangu  Wilsoni  na Regina watapata shida sana , wakati Mzee Dosam ananiambia nisije kumchagulia Regina  mume  na mtu  wa kwanza atakaemchagua nihakikishe wanafunga ndoa nadhani naanza kuamini alichokuwa akimaanisha , huu ni muongozo alionipatia  na naona umekuja nikiwa siku zangu za mwisho”

“Lakini madam licha ya kwamba  Hamza anaonekana kuwa na uwezo  lakini anaonekana kuwa na matatizo kidogo , labda ila sina uhakika..”Aliongea Shangazi akisita sita.

“Unamaanisha nini?”

“Kwa uchunguzi wangu wa kimya kimya nilioweza kufanya   nimeweza kugundua yupo kwenye mahusiano  ya kimapenzi na Eliza , mpaka sasa nashindwa kujua  kama Regina anafahamu hilo”

“Unamaanisha   huyu Eliza mtoto wa mzee Mlowe?”

“Ndio”

“Haha.. Hii inaonyesha ni kwa kiasi gani   Eliza amekuwa vizuri  licha ya changamoto alizopitia , huyu Hamza  inaonekana ana jicho  la  kuona mbali yule mtoto anafiti kila idara, lakini kama anataka kuendelea kuwa na Hamza lazima  akubali baadhi ya ndoto zake  kutotimia”Aliongea.

“Madam unamaanisha..”

“Wanaume siku zote  ambao  wana uwezo mkubwa , hawajawahi kuwa waaminifu , Dosam mpuuzi yule alinisaliti  mchana kweupe  bila hata ya kujutia , nadhani unajua  ninachomaanisha  Mariposa”Aliongea lakini kauli ile  ilimfanya  Shangazi kupiga magoti  mara moja.

“Madam samahani sana haikuwa nia yangu…”

“Inatosha sasa ,  wote tushazeeka sasa , japo mimi ndio naonekana kizee wewe bado kijana , mbinu yako imefanya kazi  nadhani ndio maana  Dosam alikupenda , lakini hayo yamepita kwasasa tumekuwa kama  dada, huna haja ya kuomba msamaha  wakulaumiwa ni Dosam sio wewe,ila bora alikupenda  wewe  ndio maana sikuwa  na tatizo , ingekuwa ni mwanamke mwingine  ningeachana nae mara moja”Aliongea Bi Mirium. “Asante sana  kwa kuniona mtu mzuri”

“Kuhusu  huyu Eliza muda si mrefu nitaonana nae na kumfanya  anitambue  mimi ni nani , kuhusu Hamza  kama uwezo anao sio kosa lake kuwa  na wanawake wawili watatu, isitoshe unajua fika   Regina sio rahisi kudii nae hususani ugonjwa wake ukiamka, kama akikubali  kuolewa na  Hamza naamini atakuwa na njia zake za kudili na michepuko ya Hamza, hili ni swala ambalo sisi tulioishi muda mrefu hatupaswi kuingilia”

“Madam upo sahihi , na mimi naona hivyo hivyo kwasababu ni watu wazima watafanya maamuzi yao wenyewe”

“Mariposa  hebu simama acha kuendelea kupiga magoti , nakutegemgea siku za usoni wewe ndio utakuwa  mlinzi wa  mtoto wangu na  mjukuu wangu , najua ni misheni yako kumlinda  Regina kwasababu ya  nafsi yake nyingine  lakini mimi awe

Regina au   yule mwingine  wote  ni wajukuu wangu.. nakuomba uhakikishe  Regina  anakuwa salama , ndio namna pekee ya Wilsoni  kuwa salama pia”

“Madam mimi Iris  nitaulinda ukoo wako  mpaka  hatua ya mwisho  ya uhai wangu”Aliongea  Shangazi akijiita Iris  huku akikakamaa kama mwanajeshi.

****

Hamza mara baada ya kurudi kwenye chumba chake alimtafuta kwanza mpenzi wake Eliza na kumuulizia swala la mama yake  lilivyoenda.

Eliza alionekana kuwa na furaha mno akisema kwamba Dr Ronica kamhakikishia  mama yake anaweza kupona  na kurudi  katika hali ya kawaida  na  mtu ataagizwa kuja Tanzania kwa ajili ya kusafiri  nae kwenda nje ya nchi.

Eliza pia alikuwa ashafanya utafiti wake na kujua 

Dr Ronicas anatokea Mayo Medical Center kutoka  Rochester Minnesota , akiwa kama daktari namba moja katika hospitali hio  yenye matawi  Marekani nzima  lakini pia namba moja dunnia nzima.

Sasa mara baada ya kujua Dokta Flora Ronicas ndio Dean  wa hospitali hio ya chuo  na pia CV yake kwa ujumla  alijikuta akishangaa na hakuwaza kabisa siku moja mama yake anaweza kutibiwa na mtu mzito  kama huyo , ilimfanya  kujawa na shauku ya kutaka kumjua Hamza  mara moja.

*******

Hakujua hata ametumia masaa mangapi  tokea  apoteze fahamu , lakini mara baada ya kushituka aliweza kujua alikuwa katika  chumba ambacho kilikuwa ni kama hospitali.

Amosi alijikuta akivuta kumbukumbu zake  vizuri na kujiuliza ni nani  ambae amemkamata  kwa kumzimisha na kumleta katika eneo hilo ambalo  lilionekana  kama hospitali  lakini kwa upande mwingine lilionekana kama maabara.

Alikuwa amefungwa  katika kitanda ambacho mara nyingi aliviona katika  filamu  za kisayansi , juu yake kulikuwa na kitu  kama helmeti ambalo lin vidole vilivyokuwa katika muundo wa chuma , ilikuwa ni kama roboti  na  ni harufu  hafifu  tu ndio  iliompa  nafasi ya kuona eneo hilo sio la kawaida hata kidogo.

Kutokana na kufungwa vizuri hakuweza kukagua eneo lote  kwani  hakuweza kuangalia nyuma , vitu ambavyo aliweza kuona ni mbele yake  na  kulia na kushoto kwake.

Alijaribu kufurukukta lakini ilikuwa ni ngumu mno  kujitoa, alikuwa amefungwa na chuma  na sio pingu.

Alijikuta akiishia kutoleta ukinzani na hio ni mara baada ya kuona kuna Kamera ambazo zilikuwa zikimmulika na moja kwa moja alijua kabisa kila anachofanya kinaonekana.

Na kweli  ndani ya dakika chache  alisikia mlango kuslide , ijapokuwa hakuweza kuona  kutokana   na kwamba hawezi kuangalia  vitu vya jyuma yake lakini alihisi uwepo wa mtu.

Dakika ileile akiwa na matarajio makubwa  ya kumuona mtu alieingia na  kumuuliza kwanini amefungwa hapo alishangaa baada ya kuona sura ya mwanamke mrembo  alievalia  Hijabu , macho

yake hayakuwa yakimdanganya mwanamke aliekuwa mbele yake alikuwa ni Sister  kutokana na mavazi yake.

“Sister naomba unifungue , hapa ni wapi?”Aliuliza  Amosi  huku akiwa na wasiwasi, ukweli ni kwamba 

alijihisi   hayupo Tanzania na kuna hisia zilimwambia  pengine amelala muda mrefu akiwa hajitambui.

“Kuwa mtulivu Mr Amosi , kadri unavyohangaika  ndio unavyojiumiza , isitoshe  kidonda bado hakijapona vizuri”Aliongea Yule Sister na kumfanya Amosi kushangaa.

“Kidonda , unamaanisha kidonda gani?”Aliuliza Amosi huku akijaribu kudhibiti mwili wake kujihisi kama kuna maumivu sehemu , lakini hata sehemu ambayo alipatwa na jeraha la risasi palikuwa pashapona  na  hakusa  na maumivu.

Sister yule alionyesha kutoa tabasamu  na  dakika ileile  alipiga makofi mawili  na  kitanda alicholalia Amosi kilianza kubinuka  taratibu na kumfanya  akae kitako na  baada ya pale kiti kile kiligeuka  kama kiti cha saluni na kumgeuzia upande mwingine.

Hakukuwa na kitu cha kushangaza  zaidi ya Runinga iliokuwa  mbele yake, ki ufupi  alikuwa wodini  , utofauti ni kwamba wodi aliokuwa ilikuwa imeendelea zaidi .

“Hello Mr  Amosi , naitwa Dokta  Maya Thema   kutoka kitengo cha tiba ya fahamu  ilioendelea  chini ya Sinagogu , unachokwenda kuona  ni hatua kwa hatua za  operesheni   ya kupandikiza Chip kwenye ubongo wako  bila  kufungua  kichwa chako ,  tunatumia teknolojia maalumu ambayo  ina uwezo wa kutengeneza Chip ndani ya  ubongo wako kwa kukuingizia mionzi isiokuwa na madhara ambayo  huambatana na madini  maalumu , kazi kubwa ya  chip  hii ni kuushitua ubongo wako na kutengeneza daraja la kimawasiliano kati ya  ubongo wako na vifaa vyetu vya

kielektroniki..”Amosi alijikuta akishangazwa na 

kauli ile , sauti iliokuwa ikisikika ndio ya Sister aliekuwa ndani ya chumba hicho japo  kwenye Skrini alionekana kuvalia  barakoa  na PPE. “Sister nani anakwenda kufanyiwa  hio operesheni ya kupandikizwa Chip?”Aliuliza  Amosi huku akiwa na hali ya kuchanganyikiwa.

“Mr Amosi  operesheni imekwisha kufanyika , unachopaswa  ni kuangalia  na majibu  ya maswali yako yote utayapata”Aliongea  yule Sister na kumfanya Amosi kugeuza macho yake kwenye Runinga.

Hazikupita dakika  chache  Skrini ilianza kuonyesha taaarifa za mgonjwa  ambae amefanyiwa  operesheni, kitu cha kwanza ambacho kilimfanya Amosi kushikwa na mshituko ni  mara baada ya kuona jina lake , Amosi Sembe..”.

“Hapana , haiwezekani”Aliongea Amosi na kuanza kufurukuta kwa nguvu  akitngisha kile kitanda   na kumfanya yule Sister kumwangalia  kwa macho ya masikitiko na palepale aliangalia Kamera  na kutoa ishara flani  na ni ndani ya sekunde tu Amosi alishikwa na usingizi  na kulala tena.

“Tutaendelea baadae akionyesha   kuukubali ukweli ,ninachowahakikishia upasuaji umeenda  vizuri kwa asilimia mia moja na baada ya hapa atakuwa Agent mahili na kukamilisha misheni zenu zote”Aliongea yule Sister huku akionyesha ishara ya heshima kwa kuangalia zile Kamera , ilionyesha ni dhahiri kuna  watu ambao walikuwa wakiangalia, haikueleweka Amosi alikuwa wapi.

*********

Siku iliofuata  Regina  na Hamza hawakuenda kazini  bali walimchukua bibi yao  kumpeleka hospitali ya chuo  ya Muhimbili .

Kwasababu Ronicas alitarajiwa kukutana na wanafunzi  wote wanaosomea udaktari  na kutoa  hotuba yake  ilibidi wapelekwe kabisa katika upande wa   wodi za watu mashuhuri kwa ajili ya kusubiri.

Bibi Mirium alitumia nafasi hio  kumuuliza 

Hamza kuhusu maisha yake kwa ujumla  wapi alipotokea na familia yake ilipo , lakini alishia  kutunga uongo ulioenda shule  lakini upande wa

Bibi huyo alionekana kuamini na kuishia kufurahi.

Wakati wakiendelea kusubiri  mlango  ulifunguliwa na akaingia mwanaume mrefu  alieenda hewani alievalia  shati  la mikono mirefu, alikuwa mweusi  aliependeza kwa kufuga nywele zake na kuwa ndefu.

Mara baada ya kuingia tu alionyesha hali ya furaha katika uso wake na kumsogelea Bibi Mirium.

“Grandma , I missed you so much”Aliongea  kwa sauti laini isiokuwa ikiendana na  muonekano wake , ukweli Hamza alidhania bwana huyo angekuwa na sauti nzito lakini alivyoongea alionekana kama aina ya wale watoto walioharibiwa na wazazi wao kwa kudekezwa.

“Naona  hatimae umezileta ngula zako  hapa Frank”Aliongea Bibi Mirium huku akitabasamu.

Upande wa Regina  kwa namna ambavyo alionekana ilikuwa ni dhahiri kabisa hakuwa na mpango wa kusalimiana na  Frank.

Hamza pia ilikuwa mara yake ya kwanza kuonana na  mdogo wake Regina  na kwa kumwangalia tu bwana huyo licha ya kubarikiwa mwili mzuri  lakini  alikuwa dhaifu mno  kiasi kwamba ilionyesha  alikuwa  akifanya sana ngono.

Frank mara baada ya kusalimiana na  bibi yake alisimama na kumwangalia Hamza huku akiweka tabasamu bandia.

“Kwahio huyu ndio boyfriend wa dada yangu , Shemeji yangu  sio?”Aliuliza.

“Habari yako mzee”Aliongea Hamza  huku akionyesha kutotaka kuendelea zaidi kuongea nae.

“Wewe Frank ni lini utaanza  kufanya intership yako  ndani ya kampuni , ongea na dada yako akupatie nafasi uanzie chini kabisa”Aliongea bibi  lakini kauli ile ilimfanya Regina kukunja sura , ilionyesha dhahiri hakupenda.

“Bibi mimi pia ni  mwanafamilia , sidhani kuna haja ya mimi kufanya intership , unaonaje  ukinikopesha  bilioni mbili  napanga kuanzisha kampuni ya Mutual fund”

“Yaanni huna hata uzoefu wa kufanya kazi  ndani ya kampuni unataka kuanzisha kampuni?”Aliongea  Bibi Mirium huku akimkodolea macho  Frank. “Lakini tayari  Dada ashakuwa  CEO , sihitaji uzoefu kwani  nina uwezo wa kuajiri watu wazoefu ambao wanaweza kuniongoza , bibi nadhani unanijua mwenyewe mjukuu wako ninaweza kujifunza haraka , sihitaji uzoefu kabisa”

“Usinione kichaa wewe mtukutu ,  ni aidha ukatafute kazi  au ukaanze kufanya kazi ndani ya Dosam katika ngazi ya chini kabisa, unadhani dada yako amekuwa CEO kwa kupendelewa  , wakati akiwa chuo  ashaanzisha kampuni yake  na kuipa thamani mpaka akafanikiwa kuiuza kwa  Bilioni kumi  na ndio tulitumia nafasi hio kushawishi wakurugenzi kumpigia kura kuwa CEO, lakini wewe ni tofauti , unachoweza ni kucheza tu na hutaki hata kutumia  ujuzi  na akili   halafu unataka nikupe hela yote hio uongoze kampuni , unadhani mimi kichaa”Aliongea na kumfanya  Frank kutabasamu  kwa kufosi.

“Basi bibi yaishe , mwakani namaliza chuo , utanipa hisa zako lini?Aliongea na  kumfanya  Bi Mirium kumpiga konzi.

“Yaani mimi nikosiriasi   unaanza kufikiria kuhusu hisa zangu , ni lini utajifunza , kama nikitoa hisa zangu itakuwa ni aidha  kwenda  kwa baba yako au kwa dada yako, sio zamu yako”

“Bibi unachofanya ni upendeleo , Dada anakwenda kuolewa muda si mrefu  na mimi ndio  mtu pekee wa kuendeleza ukoo , Da Regina tayari ana hisa  kumi na tisa ila mimi hata hisa moja sina”

“Hela ya matumizi unayopewa ni zaidi ya bilioni moja , unataka hisa za  nini?”Aliuliza  Bi Mirium huku akionyesha hana furaha.

“Bibi..”Frank alijikuta  akishindwa kuendelea kuongea zaidi  na alikuwa na hasira mno  kiasi cha kusugua meno yake kwa hasira.

“Basi bibi  haina shida nitakusikiliza kwasasa  chochote unachoongea”Mara baada ya kauli hio alimsogelea Hamza.

“Shem , unaonaje tukienda  kuongea kidogo hapo nje?”Aliuliza na kumfanya Hamza kushangaa na kujiuliza huyu bwana anataka nini.

Previoua Next