Reader Settings

Hamza alitegemea angemkuta tu Shangazi  nyumbani lakini ajabu yake ni kwamba alimkuta  Eliza na Regina wote wakiwa nyumbani.

Regina alikuwa ameketi upande wa kulia mwa Eliza akiwa ameshikilia glasi ya juisi na mara baada ya  Eliza kumuita Hamza kwa jina lake alishangaa. “Eliza , unafahamiana na Hamza?”

Ijapokuwa Eliza alikuwa katika mshangao na maswali kibao ya kwanini  Hamza yupo  nyumbani kwa bosi wake lakini aliitikia.

“Ndio nimefahamiana nae majuzi tu hapa , ndio mtu ambae alinisaidia wakati  Amosi na kundi lake walipotaka kunichukua kwa nguvu..”Aliongea Eliza.

Hakutaka kuelezea  kama  jana  Hamza alilala nyumbani kwake na aliondoka asubuhi, isitoshe uhusiano wao ni kama haukuwa wazi kama ni wapenzi au lah.

“Oh!”

Regina  hakutegemea kuona kwamba  Hamza ndio mtu aliemsaidia  Eliza wakati akidhalilishwa , hakuweza kujizuia kushangaa.

“Ilikuwaje  akakusaidia, mlifahamiana kabla?”Aliuliza mrembo huyo , alikuwa na mapozi hata wakati wa kuongea.

“Bosi , kwani sio kama yupo hapa kama fundi pia ? , ni mtengenezaji wa  AC na  kuna mama mmoja ndio  alinikutanisha nae  baada ya Ac yangu kupata hitilafu , wakati anakuja kutengeneza ndio  akanikuta nipo kwenye matatizo akanisaidia ,  mwenyewe anasema  ni fundi wa kila kitu kinachotumia umeme”Aliongea  Eliza bila kuacha kuweka chembechembe za kumsifia Hamza.

Lakini  kitendo cha kusikia kauli hio , mrembo Regina alijua  amedanganywa tena , na kuona ndio maana jana  alifika na kuanza kutengeneza TV yake  lakini haikuwa hivyo tu alikuwa mwanachuo na mwalimu kwa wakati mmoja na kujiuliza Hamza ana kazi ngapi anafanya.

Hamza upande wake alikuwa ameurudia ule muonekano wake kizembe uliomfanya kupigwa cha mbavu hadharani na Anitha  wa chuo,alijifanyisha  kutokumjua   Eliza kwa undani.

“Boss , umemuita kwa ajili ya  ufundi?”Aliuliza Eliza huku akimwangalia Hamza.

Swali lile ni kama ghafla tu lilimletea Regina maumivu ya kichwa ,hakutaka kabisa siri yake ifahamike , alijua kama itakuja kufahamika alikuwa ameajiri mtu wakuigiza kama  boyfriend  angeonekana mwanamke wa ajabu  mno.

“Unaonaje tukienda kuongea maswala ya kazi katika ofisi yangu kwanza , kuna baadhi ya vitu pia nataka ukavifanyie kazi”Aliongea Regina  akiwa na muonekano wa kibosi ,Eliza  alikuwa ni mwanamke ambae anajali zaidi kazi hivyo  asingeendelea kuuliza.

Kitendo cha wanawake hao kupandisha juu ,  ilimpa Hamza ahueni na haraka  haraka alikimbilia jikoni na kuchukua maji  ya baridi  vikombe vitatu na kushusha vyote  ili kuirudisha mudi yake.

Shangazi aliishia kumwangalia  tu Hamza , kuna namna flani mwanamama huyo alielewa kinachoendelea na kumfanya   hata Hamza kukosa utulivu.

“Regina alikuwa akionyesha kukujali  ndio  maana alikupigia , kwanini ulimkatia simu bila ya kuongea neno?”Aliuliza shangazi.

“Shangazi  mbona unatania , Regina anijali mimi?, si  ndio yeye alienifukuza  hapa  usiku usiku”

“Ni kweli ,lakini baada ya kumwambia   maisha yako yalivyo  na kwanini uliongea vile  alionekana kukuelewa”Aliongea Shangazi , kwa namna moja  alionekana kama vile alikuwa akitaka  wawili hao wapatane.

Hamza  na yeye alionekana kuelewa , na aliona  Regina pengine ni tabia yake , ana  kauli  zenye ukali mno  na mwenye kubadilika badilika  ila ni mwenye roho nzuri , kwa  alichosema  Shangazi kilimfanya aone haina haja ya kuondoka.

“Tutabanana hapa hapa mpaka kieleweke, haondoki mtu hapa”Aliwaza Hamza akisahau  mkataba wa kuishi maisha mazuri  karibu na mrembo wa matawi ya juu  unaisha ndani ya miezi  mitatu  tu.

Baada ya  lisaa kupita , hatimae  Eliza alishuka sebuleni  na kumuaga Shangazi kama anaondoka , Hamza muda huo alikuwa akiangalia TV huku miguu ikiwa juu ya sofa   na Eliza upande wake hakuonyesha hata kujali , kuna namna flanni ilimuambia  Hamza anaishi hapo kwa namna alivyokuwa  amejiachia kwenye sofa.

Hamza mara baada ya kuona mrembo huyo ameondoka kabla ya kumuaga alimuwahi.

“Eliza  naomba unisikilize”Aliongea  kabla hata hajaingia kwenye gari lake

“Unataka kuongea nini?”Aliuliza akiwa na uso usiokuwa na masikhara kabisa.

“Sio kama unavyofikiria  mimi na Regi..”Hamza alisita kuendelea mara baada ya kukumbuka kipengele cha mkataba kilimtaka   uhusiano wao kubakia kuwa siri.

Eliza aliendelea kumkazia  Hamza  huku akimwangalia namna ambayo anajikuna kichwa kwa kukosa kujiamini  lakini  kitendo cha kuona mwanaume huyo anavyohangaika kujielezea alitoa kicheko.

“Eliza mbona unacheka, inamaana unajua tayari?”Aliuliza kwa  wasiwasi 

“Uitana ukifanyia surprise sio , kuna haja gani ya kuficha sasa , nishajua  tayari umekuwa mwajiriwa wa kampuni  yetu na unaanza jumatano”Aliongea  Eliza  na kauli ile ilimuacha Hamza mdomo wazi.

“Ajira gani  tena?”Ndio wazo  la kwanza lililomjia  Hamza akilini.

Kabla hata hajaongea chochote sauti kutoka ndani  ilimwita.

“Hamza njooo  kwenye chumba changu cha kujisomea”

“Tutaongea siku nyingine,  nenda haraka bosi anakuita nawahi  mwendokasi kwenda  Morogoro kikazi  bye”Aliongea  Eliza huku akimwangalia Hamza kimahaba na kisha aliingia kwenye gari  yake na kuondoka.

Hamza hakuwa akielewa chochote na  ni kama alikuwa amechanganyikiwa ,  na  kimya kimya alienda mpaka chumba cha kujisomea cha Regina.

Baada ya kuingia ndani  akiwa na muonekano wake wa kizembe alifunga mlango na kuanza kujikuna kichwa kama mwanaume ambae  amekosa kujiamini. “Regina  umemuambia nini Eliza juu yetu?”

“Nimemuambia mimi  na wewe  tulikuwa marafiki wakati tukiwa wadogo  katika kituo cha kulelea Yatima   na tumekutana  majuzi tu hapa , kwasababu ya   maisha yako  kuwa magumu sana na unasoma nimeamua kukufanya msaidizi  wangu binafsi, kuhusu kuishi  hapa nimemuambia ni kwa ajili ya kumsaidia saidia Shangazi  kazi za nyumbani na kumpeleka sokoni na gari”

“Na ameamini hayo maneno?”Aliuliza Hamza  huku neno ‘maisha magumu sana’ likijirudia rudia kwenye kichwa chake na kufanya midomo yake kucheza.

“Nimefahamiana   na Eliza kwa muda mrefu  ukiachana kuwa mkubwa kwangu ki umri  na uwezo wake mkubwa  kazini  lakini  anapenda kuishi maisha ya kawaida  na sio mtu wa kufikiria fikiria watu vibaya bila sababu ,   ili mradi sikuongea kitu ambacho hakina maana nina uhakika ameamini”

“Huoni kwamba ni vibaya kumdanganya mtu anekuamini?”

“Kwahio vipi sasa kama nimemdanganya , au unataka kila mtu kujua mimi na wewe ni  wapenzi feki , halafu inakuuma nini  kama nimemdanganya , haya ni mambo yangu  binafsi  haina haja ya kumwambia kila mtu kinachoendelea  kwenye maisha yangu”

Hamza alijikuta akishikwa na bumbuwazi , dakika chache zilizopita aliona Regina ukauzu ulikuwa wa nje tu  lakini   muda huo  anaona kabisa  ni mpaka ndani.

“Ni kheri uache kujali ya wengine  na usaini hii nyaraka”Aliongea akimpatia Hamza karatasi  na 

Hamnza aliangalia kilichokuwemo kwenye karatasi. “Kwahio  ni kweli unataka niwe msaidizi wako , unadhani ratiba zangu  za chuoni zinaniruhusu kuwa   kazini masaa yote hayo?”

“Mimi na wewe uhusiaon wetu  ni wa kikazi zaidi na ili kuficha kazi yako  ya  kuigiza  ni kheri tuwe na namna ya kujitambulisha  pindi tutakapoonekana pamoja , isitoshe huu ndio uongo niliomwambia  Eliza , hivyo  lazima uongo  wangu uwe kweli, kingine una vikazi vingi kibao mara fundi mara sijui  mwalimu, nani anajua kesho utakuwa unafanya kazi gani nyingine ,  ili usije kujiingiza  kwenye matatizo  ni kheri kuwa  na kazi ya kueleweka inayoendana na usalama wako

Nilikupigia muda ule lakini ukawa  kama vile hujataka kupokea simu yangu, nikajua labda upo  na tatizo , mimi kama bosi wako usalama  wako pia  ni kipaumbele changu”Aliongea  bila ya kuwa na hisia zozote usoni.

“Regina muda ule wakati ukiwa unapiga nilikuwa sehemu mbaya … sikuona  kama  itakuwa vizuri tukiongea ndio maana nilikata simu” “Sijakuambia ujielezee na sijali unachofanya  , hayo ni maisha yako binafsi , ninachotaka ni usaini mkataba  huu wa kazi”Aliongea  kibabe  kana kwamba anajaribu kumuogopesha na Hamza  akiwa katika muonekano wa kizembe alichukua  karatasi na kusaini haraka  haraka.

“Watu na bahati zetu bwana , mshahara milioni moja , ukijumlisha na zile … nani wa kukataa kusaini mkataba mnono  aina hii”Aliongea Hamza mara baada ya kusoma karatasi  hio   na kutia saini kwa mbwembwe zote huku akiwa na tabasamu zito usoni , alionekana mtu anaependa pesa mno kuliko kitu chochote..

Laki tano  kwa mwezi kuwa boyfriend feki  ukijumlisha marupurupu ,milioni  moja nyingine ya kuwa msaidizi binafsi , ki  ufupi ni kwamba ndani ya  miezi hio  mitatu aliona atakuwa na kitita cha kutosha.

“Huyu mwanaume muonekano wake ni mzuri , anaonekana kuwa na akili  na pia anajua kuongea kifaransa , kinachosikitisha ni kwamba udhaifu wake hufichi hata kidogo  , yupo tayari kufanya lolote kwa ajili ya hela”Aliwaza Regina.

“Bosi  kwanzia sasa mimi ni msaidizi wako binafsi , lakini vilevile ni boyfriend wako wa maigizo”Aliongea  Hamza kijeshi huku akipiga saluti akiwa na tabasamu pana usoni na kitendo kile kilimfanya Regina kutoa tabasamu.

“Usichokijua ni kwamba  hadhi ya msaidizi wangu

binafsi mshahara wake ni milioni  nne na nusu  kwa mwezi…”

“Nini!!.. kwahio unanifanyia dhuluma?”

“Hii ndio njjia ya kudili na  mtu kama wewe mpenda hela kupindukia , ambae unaongea kama bila tuo , hii kitaalamu inatiwa jino kwa jino , hakikisha unazingatia vipengele vya  mkataba, utakatwa nusu ya mshahara wako kila unapokiuka vipengele”

Kauli ile ilimnyong’onyeza  kabisa  Hamza na kuona  alimchukulia poa  huyo mwanamke lakini anazo mbinu za kimafia za kumdhibiti.

Siku iliofuata Hamza alienda chuo kama kawaida na alikuwa na test , alifanya na akamaliza  na kisha aligeuza  zake  na safari yake haikuwa  nyumbani bali alienda Kijichi kumuona Dina lakini bahati mbaya hakumkuta hivyo  alichukua baiskeli yake  na kuanza safari ya kurudi  Kigamboni.

Saa kumi kamili ndio muda ambao alifika  na Shangazi alimshangaa sana  Hamza kurudi akiwa na baisikeli ambayo ilikuwa imechakaa lakini hata hivyo hakuongea sana  na Hamza alienda kupaki  usafiri wake pembeni na ile Maserati ya Regina tena kwa kuigamiza.

Muda wa jioni wakati  Regina anarudi  kazini  na kukuta ile baiskeli alikasirika mno mara baada ya kugundua alieileta hapo ni Hamza na kumwambia  aitoe  nyumbani kwake lakini  Hamza aligoma na kumwambia ana koneksheni ya kiroho na hio baiskeli hivyo haiendi popote , mgogoro ulikuwa mkubwa mpaka Shangazi akaingilia  na Regina akatulia.

Siku iliofuata  Hamza hakuwa na kipindi kabisa chuoni , ki ufupi wiki hio hawakuwa na vipindi mpaka wiki inaofuata maana walikuwa mwishoni mwa semista  na wangefunga moja kwa moja  ingekuwa ni field na Hamza aliona  ni kama kupiga ndege wawili na jiwe moja  maana anao uwezo wakuomba field moja kwa moja ndani  ya kampuni  ya Regina.

Asubuhi ya jumatano  hio ndio siku ambayo  Hamza  anaenda kazini na Regina kama  msaidizi  binafsi 

Nguo zote ambazo alikuwa amevaa alipatiwa  na Regina , kuanzia viatu mpaka tai , haikueleweka  hata   leseni  ametolea wapi lakini  Hamza alikabidhiwa leseni ya jina lake kabisa.

Hamza alishindwa kujizuia  na kuishia kutoa  pumzi nyingi ya kushangaa na aliona namna ambavyo pesa ilikuwa na nguvu , mwingine kufuatilia leseni ingechukua hata mwezi lakini kwa  Regina ilikuwa ni  masaa tu alikuwa nayo mkononi , gepu hilo halikuwa dogo hata kidogo.

Akiwa  kama dereva ndani ya  gari ya Lexus  570  nyeusi, Hamza alikuwa akiboreka kwani foleni ilikuwa kubwa mno , yaani hata baiskeli yake aliona spidi yake  ilikuwa kubwa.

Hamza aliangalia kupitia kioo cha nyuma na aliweza  kuona  Regina alikuwa bize na Mackbook yake  akifanya kazi , hakuonekana kuathirika kabisa na foleni ya magari.

Kwa jinsi ambavyo alikuwa amevalia na kupendeza ni kama vile hakuwa akielekea kazini , alikuwa  amevaa gauni  ambalo  limevuka magoti  pamoja na  blazer ya rangi ya ugoro hivi na alikuwa amepiga nne  na kufanya miguu yake ilionona kuwa  nje nje.

Hamza  alijikuta akimeza mate mengi na kujiambia inakuwaje mwanamke huyu kuwa mrembo namna

hio , kwanini ngozi yake inaonekana laini hata kabla  ya kuigusa.

“Pipii..!!Papaaa!!”

Sauti ya honi ya gari iliokuwa nyuma ilianza kupiga honi mara baada ya gari ya Hamza kutosogea mbele licha ya foleni kuisha. 

Regina ndio aliekuwa wa kwanza kushituka na alikunja sura mara baada ya kujua Hamza alikuwa  akimwangalia kwa kupitia kioo cha nyuma na  kushindwa hata kuona  taa ya kijani ilikuwa ishawaka.

“Hamza , unaangalia nini, taa ya kijani ishawaka”Aliongea  Regina kwa kukaripia na hali ile ilimfanya  Hamza uso kupata moto  huku akiwahi kuendesha kusogea mbele , alikuwa amejisahau  akimakinika na urembo wa Regina.

“Kwanini unanikodolea mimacho yako?”Aliuliza  Regina huku  akionekana hana masikhara hata kidogo 

“Sikuwa nikikuangalia  nilishikwa na ka usingizi ,niliamka mapema”Aliongea Hamza akiwa na sura  ya mikausho  kabisa kama hakujatokea kitu.

“Muongo sana ,mbahiri ,  tamaa zimekujaa  na umekaa kihuni huni  tofauti  na muonekano wako , wewe ni mwanaume  jitahidi hata kujizuia , huoni hata aibu”

“Mbona unanibebesha tabia ambazo sina , mimi nakubali  ni mbahili ndio  na napenda hela , nani hapendi hele dunia  hii , kama shida nikukuangalia, ndio nilikuwa nikikuangalia , unadhani  ni mwanaume gani rijali  asiependa kuangalia wanawake warembo”

“Bado tu unautetea ushenzi wako? Haya nimeacha kuongea  kuhusu  baiskeli yako , vipi kuhusu hizi..”

Aliongea na  palepale alirusha mfuko  wa nguo mbele ya  Hamza , ilikuwa ni mfuko ambao ulikuwa na nguo chakavu za Hamza ambazo alivaa siku ile wakati anaenda kukutana na   wazazi wa Regina , sasa alizisahau kwenye gari.

“Kama sio mbahili wewe ni mtu gani ,nguo ikichakaa  unabadilisha lakni  wewe  jana  uko bize mpaka kuzipiga pasi , mpaka nguo za kazini  nimekuandalia mimi , chuo ulikuwa ukienda na nguo gani , inamana hizo kazi zako hazikutoshi hata kununua  nguo  za bei rahisi ,halafu  unaongea kwa kujiamini mbele yangu”

Ukweli ni kwamba  Regina alikuwa na kisirani cha asubuhi, wakati  Hamza anashuka  asubuhi kwa ajili ya kwenda kazini  alikuwa amevaa suruali ya pundamilia  ya  mtumba  na tisheti  ya jezi  yenye bonge la chata la MoExtra.

Shangazi  licha ya kwamba  alikuwa  mtu mzima na ambae hakujali sana mavazi lakini  alichovaa Hamza kwa ajili ya kwendea kazini kilimfanya kucheka.

Kama isingekuwa  Regina kuandaa  nguo kwa ajili ya Hamza  asingekubali kuondoka nae.

Hamza aliishia kumuona Regina kama mwanamke ambae hachuji maneno kwenye kumwambia vitu  na  kujiona kama mtoto mdogo.

Lakini hata hivyo hakutaka kujibishana nae, kama ilivyokuwa asubuhi alivyofokewa kwa kuvaa jezi na suruali yake pendwa ya pundamilia   ndio ambavyo aliona awe mtulivu  asiendelee kujibishana nae.

Hamza alijiambia yeye ni mwanaume  na  haina haja ya kujibishana na mwanamke, kwake nguo  sio kupendeza bali  ni athari  za faida za nguo husika katika  ulimwengu wa kiroho.

Mara baada ya kufika  katika eneo la maegesho ,

Valet alimpa ishara  ya  eneo maalumu ambalo   CEO ndio gari yake inaegeshwa  na Hamza alienda kuisimamisha hapo , ilikuwa ni ndani kabisa ya jengo.

“Kumbuka masharti mawili  niliokusisitizia jana”Aliongea Regina kabla ya kutoka nje ya gari.

“Nakumbuka bosi ,  sipaswi kukuita Regina bali nikuite bosi  na vilevile  nisitoe siri juu ya mahusiano yetu feki”Aliongea

Mara baada ya  Regina kuridhika alishuka kwenye gari na akafuatia Hamza  na kisha walizisogea lift maalumu ambazo hutumiwa na wafanyakazi wa  ngazi ya juu wa kampuni.

Pembeni ya lift hio kulikuwa na  mdada ambae alikuwa amesimama,makadirio ya umri  miaka

ishirini na sita hivi.alievalia suti  nyeusi.mfupi wa wastani hakuwa  mrembo sana lakini alikuwa mtanashati.

“Goodmornining Madam”Alisalimia yule mdada kwa heshima na Regina aliishia kutingisha kichwa kupokea salamu yake.

“Huyu  ni Linda , msaidizi wangu namba moja , hakikisha unajifunza kutoka kwake”Aliongea Regina akimtambulisha  Hamza.

“Hello , naitwa Hamza Mzee natumaini kujifunza mengi kutoka kwako”Aliongea Hamza akimpatia mkono  Linda.

Linda alionekana kusita kwa sekunde kadhaa lakini aliishia kupeana mkono  na Hamza ukweli sio mkono bali aligusanisha vidole tu  na mkono wa Hamza , hakuonekana kumchukulia siriasi kabisa Hamza.

Hamza aliona  ndio maana  ni msaidizi wa Regina , wanaonekana kufanana  kabisa wote ni makauzu na  maringo yamewajaa.

Linda muda uleule alishikilia kishikwambi chake vizuri na kuanza kumsomea Regina ratiba yake ya siku hio.

“Madam , leo  ratiba yako ya asubuhi  ni  saba , tisa , kumi na tanu ,  kumi na nane , ishirini   , ishirini na moja  na ishirini na mbili..”

Aliongea Linda  na ilimfanya Hamza kushindwa kuelewa anachomaanisha  lakini aliishia kufuata

nyuma nyuma mara baada ya Regina kuingia  kwenye lift 

Sekunde ambayo   lift inajifunga  , muonekano wa Regina ulizidi kubadilika na sasa kuwa na usiriasi mno kama vile  ni mkuu wa  nchi , hali ile ilimfanya  hata Hamza kumeza mate mengi na kujiambia kwahio huu ndio muonekano wake akiwa kazini, kwanini  ni kama vile ni mtu tofauti na yule  Regina  wa nyumbani.

Regina  alibinya namba mfuluulizo akianzia saba , tisa , kumi na tano na kuendelea bila kukosea kulingana na  maelezo aliotaja Linda , jambo lile lilimshangaza Hamza kwani  Regina alisikia mara moja tu lakini alikuwa akikumbuka  vizuri , muda huo ndio sasa Hamza alielewa herufi zile zilikuwa zikimaanisha  floor za jengo hilo.

“Boss , floor ya ofisi  yako si  mwisho kabisa , kwanini unabonyeza floor za chini?”Aliuliza  Hamza ,jana yake alishasoma maelezo ya mwanzo  juu ya mazingira ya kazi ya Regina hivyo alikuwa akijua ni floor ipi  ofisi ya CEO inapatikana.

“Kila Floor CEO anakuwa  na kikao , atatatua baadhi ya shida katika idara husika , kwa njia hii ndio namna anavyookoa muda  wa wafanyakazi kupanda na kushuka kwenda ofisini kwake  hivyo kuongea ufanisi wa kazi”Aliongea Linda.

Previoua Next