Reader Settings

SEHEMU YA 55.

USIKU WA JANA.

Hamza mara baada ya  kutoka  nje ya geti alisogelea moja ya gari  ya Mercedenz  iliokuwa imesimama mita kadhaa kutoka  katika geti la  nyumba yao na kisha aligonga kioo  cha mbele na muda uleule kioo kile kilishushwa na ndani ya gari hio alionekana  mwanaume alievalia suti, mweusi  mwenye makadirio kama ya miaka  therathini  hivi.

“Bosi pole kwa kusubiri muda mrefu?”Aliongea Hamza kinafiki  na kumfanya yule  bwana  kutoa tabasamu na kisha  aliangalia chini.

“Umejuaje nakusubiri Bro”

“Huna haja ya kujifanya mjinga, ilihali  umefanya kila hila ya kupata  ‘Attention’  yangu nijue unanifuatilia”Aliongea  Hamza  na kumfanya yule  bwana kutoa  tabasamu.

“Ni kama nilivyodhania umeniona , unaonaje ukiingia  ndani ya gari  Bro”Aliongea na kumfanya Hamza  kuzunguka upande wa pili na kuingia katika ile gari.

Kilichomfanya Hamza kujua gari hio  ilikuwa ikimfuatlia  ni mara baada ya kuiona zadi ya mara tatu katika safari nzima ya kutoka hospitalini mpaka kufika Kigamboni.

Wakati  alipokuwa akiongea  na  Regina  nje ya hospitalini karibu na maegesho ya magari aliweza kuiona  na wakati  wanasubiria  Taksi kuwachukua kwenda nyumbani iliwapita , Hamza mwanzoni hakuitilia sana  maanani kutokana na dereva kutoonekana kuwa na nia yote mbaya lakini mara baada ya kuona ikiwa imesimama  mita kadhaa kutoka    kwenye geti la nyumba yao  aliona kabisa  dereva wa gari hio alikuwa akifanya makusudi  ili kumjulisha kwamba anamtafuta.

“Bro wewe sio wa kawaida  , umeweza  kuwashinda wale  Maninja wa  kundi la Nyoka  na kisha kumuokoa Bosi Regina katika mlipuko wa  gari , uwezo ulioonyesha sio wa mwanajeshi wa kawaida aliepitia mafunzo  ya kikomandoo, naweza kusema wewe ni zaidi ya mwanajeshi. unaweza  kuniambia  mafunzo  yako ni ya namna gani  na uwezo wako kwa ujumla?”Aliongea yule bwana huku  akiwa na hali ya urafiki katika macho yake.

“Na wewe unaweza kuniambia ni  nani haswa na kwanini  umefanya kila hila nikutambue?”

“Oh , Samahani bro kwa kutokujitambulisha, Naitwa Norbert Geza  kutoka  kitengo cha  usalama wa nchi”Alongea  na kumfanya  Hamza kutingisha kichwa.

“Sawa bwana Geza , je kuna sababu yoyote ya  jeshi kunifuatilia?”

“Ni maswala ya  Usalama wa nchi  ndugu Hamza ,

tukio kama  la leo tuna kila sababu ya kukufuatilia”Aliongea na kumfanya Hamza amwangalie.

“Mnapanga  kufanya nini kuhusu tukio la leo , maana kama mlivyoona kuna watu wanataka kuniua  mimi na bosi  wangu, mpango  wenu ni nini au mnapoteza muda kunifuatilia ila  hakuna chochote mnachofanya”

“Tunapanga kulichukulia hatua swala hili  lakini hatua ya kwanza ni hii ya kuongea na wewe , nipo hapa kwa ajili ya kukutuliza na kukutaarifu kwamba  wote  waliohusika  hapa tutawaonya wasirudie tena kuyumbisha usalama wa nchi na raia wake”

“Haha.. mbona kama   kauli yako ni ya kimaigizo  na onyo kwa wakati mmoja, mimi ndio nimeshambuliwa lakini ninachoona hapa  unanipa onyo nisichukue  hatua kwa wale waliohusika, kama watu  wameweza kukodi kundi  hatari kama

hili  kwa ajili ya  kuhakikisha  tunapoteza uhai,  unadhani unachoongea hapa  kinaweza kutekelezeka?”

“Kama nilivyojitambulisha Mr Hamza ,  kupitia vitengo vyetu ya kiusaama vya nchi  tutafanya  kila linalowezekana , Tanzania ni nchi  inayoendeshwa kwa misingi ya haki na sheria , hatuwezi kumruhusu mtu kufanya anachotaka , hivyo  naomba usiingilie kazi ya  jeshi  na kusababisha matatizo zaidi , Idara ya usalama wa nchi haiwezi kufumbia  macho  maswala kama haya”

“Unaongea ujinga na upuuzi , nilikuona  kule hospitalini na nikakuona tena baada ya mlipuko , hii inamaanisha mlijua tukio kama hili litatokea , nyie kama kweli ni sehemu ya usalama wa nchi , kwanini hamkuzuia  tukio kama hili, hii moja kwa moja inaniaminisha kwamba  watu waliohusika  wapo ndani ya idara zenu na walikuwa wakiangalia nini kinachokwenda kutokea , sasa kwasababu umejileta mwenyewe unaonaje ukinitajia  kabisa wahusika”

“Hamza  unamaanisha  nini , kwahio unataka kwenda kinyume na  msimamo wa idara ya usalama wa nchi?”Aliuliza yule bwana na kumfanya Hamza macho yake kuchanua   na kumwangalia kwa umakini.

“Kama huna taarifa yenye maana  kwangu  basi naweza kusema  muda umeenda na nataka kwenda kulala”Aliongea Hamza na kisha alifungua mlango na kutoka  nje.

Norbert  aliishia kumwangalia tu , isitoshe alikuwa akimhofia kwa kile alichokuwa amekiona leo hivyo  hakuona haja ya kubembeleza.

Mara baada ya kumuona Hamza akirudi ndani  aliendesha  gari mpaka  mita  kadhaa kwenye moja ya nyumba iliokuwa  geti la njano   katika mtaa huo huo na mlango ulifunguliwa na  wanaume wanne  waliovalia mavazi ya kiraia na kisha kuingia ndani ya gari ile.

“Kapteni  vipi  kuhusu Hamza amekuelewa ?”

“Sina uhakika , huyu  dogo  inakuwa ngumu mno  kujua ni kitu gani anapanga kufanya , tunapaswa kuwa makini  tusiruhusu  akasababisha matatizo  hasa kipindi hiki cha uchaguzi”

“Haya yote ni kutokana na  tamaa za  mheshimiwa mstaafu  na familia ya Mzee Benjamini na kuendelea kumchokoza  Bosi Regina  kila siku , anadhani  kwasababu ya  kuwa mstaafu anaweza kufanya  chochote na kujimilikisha hii nchi”Aliongea mmoja  ya wale watu kwa chuki kubw.

“Ni kwasababu  hakuna anaeweza kumfanya  chochote  Mstaafu , nchi ilimwacha afanye chochote na sasa mizizi yake ipo kila kona ya nchi kwanzia kwenye uchumi mpaka kwenye siasa, Familia ya Benjamini ni sehemu ndogo sana   katika Ngome yake”

“Ndio  maana wanadharauliwa na  huyu Hamza kwa kutumika kizembe”

“Hii ni misheni yetu ya kuhakikisha nchi inakuwa salama , sisi ni wanajeshi   na lazima  kila tunachofanya  kinazingatia sheria na katiba ya nchi , vinginevyo hatuwezi kuwa tofauti na  wahalifu”Aliongea mwingine.

“Haina haja ya kulalamika, kwasasa tokea tuanze kufatilia  matukio yote yanayoendelea hatuwezi kusema usalama  wa nchi upo hatarini , tunapaswa kuendelea kuwa makini  na kila hatua wanazochukua , lazima tutimize kila  wajibu ambao tumepewa na wakuu wetu”Aliongea Kapteni. “Ndio tumekuelewa Kapteni?”

“Ayubu vipi bado  hujampata Amosi?”

“Afande Rama anaendelea na  uchunguzi bado ,

Jasusi mara ya mwisho alionekana katika  Mgahawa Masaki  na baada ya hapo hajaonekana tena  na  hakuna alama alioacha nyuma inayoweza  kutufanya kupiga hatua  ya kujua alipo”

“Vipi  ndani ya Kanisa la Wabrazili , hakuna ‘Movement’ zozote za kutilia mashaka?”

“Kuna mtu wentu  ndani ya kanisa  na mpaka sasa hajawasilisha  taarifa yoyote  , nadhani bado hakuna  cha kutilia mashaka”Aliongea Ayubu  na kumfanya  Kapteni Norbert  kufikiria kidogo.

“Kuna kitu lazima kinaendelea, nimesikia na  Afande Danieli anamtafuta Amosi, Mzize wewe kwanzia kesho endelea kumfatilia  Kanali Dastani kila hatua anayopiga na kisha unipe  Ripoti. Fadhili  wewe utaendelea kumfuatilia  Hamza  pamoja na washikaji zako” “Sawa Kapteni”

“Hebu waulize kwanza tujue kama Hamza bado yupo nyumbani”Aliongea  na kumfanya  bwana alieitwa Fadhili kutoa simu palepale  na aliongea kwa dakika kadhaa na kukata.

“Bado yupo nyumbani  Kapteni , hakuna Kamera inayoonyesha akitoka”

“Vizuri, kama kuna lolote litakalotokea mtanijuza  naenda nyumbani”Aliongea  na  mabwana wale walikubali na kisha walishuka  katika ile gari na kuingia ndani ya nyumba ile yenye geti na  Kapteni Norbert alitoweka katika eeo hilo.

Sasa upande  mwingine wakati wakijua  Hamza yupo nyumbani  ukweli ni kwamba alikuwa ashaondoka muda mrefu  kwa kuzikwepa Kamera na hata simu yake aliacha hapo hapo  nyumbani maana alijua lazima Ma ajenti hao  wanafuatilia hadi simu yake.

Muda ulikuwa umeenda na  kuna maeneo ndani ya mtaa huo wa  Egret yalifunikwa na vivuli vya miti na ndio aliotumia kupotelea mpaka kwenda kutokea  katika mtaa mwingine kabisa.

Hamza mara baada ya kuona amefika mbali kabisa na nyumbani alitoa  simu ndoto ya batani na kisha alitafuta namba ya  Lawrence msaidizi wa Dina.

“Bro   muda umeenda sana , kuna kitu unataka nikusaidie?”

“Kundi la kininja la Black Eared Snake lipo Tanzania , nataka kujua eneo walipo?”

“Bro ! , Umejuaje wapo   Tanzania na kwanini unataka kujua  walipo?”Aliuliza Lau upande wa pili.

Hamza alikuwa akijua   moja ya kanuni kubwa ya  kundi hilo  la kininja ni kusafiri  kimakundi  , kwa  mfano ikitokea kazi  ya kuua mtu katika eneo husika  lazima na kiongozi wao asafiri kwenda kuweka makazi ya muda katika eneo hilo, Hamza alijua akimkamata kiongozi ndio atakavyyoweza kumpata mtu ambae anataka kumuua kwa kumsababishia ajali za mara kwa mara.

“Wewe niambie wapo wapi , kwa  Network yenu lazima mtakuwa na taarifa zote”

“Lakini Madam ashalala tayari , unaonaje nikimuamsha na kumwambia kwanza?”

“Ukiendelea kuongea ujinga  sitokutambua kama  Bro tena , sasa chagua kuniambia  au kwenda kumuamsha bosi wako”Aliongea Hamza kwa sauti ya kibabe.

Lawrence upande wa pili hakuweza kumkatalia kwani alimhofia Hamza licha ya kwamba  alikuwa ni kama rafiki yake hivyo aliamua kumtajia eneo walipo.

Hamza mara baaada ya kuambiwa eneo husika  aliona  ni umbali mrefu mno  hivyo aliona   hawezi kutembea zaidi ya kupanda Taksi ya kumfikisha huko. ******

Upande mwingine ndani ya  jumba la kifahari linalopatikana katika  eneo la Tegeta  walionekana  baadhi ya watu wakiwa wameketi  eneo la ukumbi.

Walikuwa ni mabosi  wenye pesa nyingi  na  walionekana kuwa na mabodigadi  waliombatana nao na kulikuwa na kikao kilichokuwa kikiendelea.

Alionekana Kanali Mstaafu Fanueli  Yowe akiwa amekaa  kwa kuegamia kwenye Sofa  akimwangalia  kwa macho ya ukauzu  bwana aliekuwa amekaa mbele yake , ambae amevalia  Jaketi la  leather , bwana huyo alikuwa mweusi tii  na amejaa makovu usoni.

“Mr Snake, umoja wetu umekuwa ukishirikiana na  kundi lako la Black Eared Snake kwa miaka saba sasa , katika kipindi hicho chote  tumeweza  kusimamia madili mbalimbali ya siraha ambazo  ziliingia nchini  kwako  na  umeweza kujiimarisha kwa kiasi kikubwa na kuweza  kufanya kundi lako kutambulika duniani kutokana na uwezo  wa juu  , lakini leo ndio mara ya kwanza umetuangusha  na kutukatisha tamaa kabisa”Aliongea Fanueli Yowe , huyu ndio bwana ambae  ni kiongozi wa  kundi la  watu wenye  ujuzi wa sanaa ya mapigano.

Mr Snake  ndio aliekuwa kiongozi wa kundi  la kininja la  Black Eared Snake ,  kutokana na  kundi lake kupewa misheni  ndani ya  Tanzania iliokuwa na malipo mazuri ndio maana alisafiri na  maninja wake kukamilisha kazi ya kumuua Hamza na Regina.

Genge la  mabosi wala keki ya taifa  ambao  wameamua kujipa jina la kuzugia la Martial Art Association  walikuwa  ni  washirika wakubwa  na  kundi hilo la kininja kwa muda mrefu ndio maana hata kazi ya kumuua Regina walipewa wao.

Unaweza kushangaa  kwanini kundi hili litake kumuua  Hamza na  Regina, ukiachana  na kwamba  Master Konki ambae alikuwa mwanachama kupewa kibano na Hamza kiasi cha kuwa na chuki  lakini upande  mwingine   kundi hili lilikuwa na sababu za kutaka kuona  Regina pia anakufa.

Mwanzilishi wa kundi hili  alikuwa ni Mheshimiwa Mgwenno ambae ndoto yake  kubwa  baada ya kuwa kiongozi  mkuu wa taifa ni kutaka kuimiliki Tanzania.

Mheshimiwa Mgweno  katika mbinu za kutaka  kuimiliki Tanzania  ndio alianzisha makundi  mengi  ambayo  hakujihusisha moja kwa moja   lakini alikuwa na nguvu ya kimaamuzi na moja wapo  ni kundi  hili la Umoja  wa watu  wanaojua  Mapigano, moja ya  sababu kubwa aliofanya  kuunda kundi hili ni kuhakikisha  katika kuendeleza kuwa na maslahi yake  anakuwa upande  mzuri na jeshi , isitoshe pia  alikuwa mwanajeshi Komandoo kabisa kabla ya kuingia katika  siasa hivyo ilikuwa rahisi kwake kushawishi  wanajeshi kutengeneza kundi hilo.

Sasa kutokana na wanajeshi hao kupata pesa nyingi  na pesa kuwanogea walitoka katika  miiko  ya kazi  na kuwa wahalifu wanaojilinda katika vazi la kujiita makomandoo na jambo hilo lilimfurahisha sana Mheshimiwa Mgweno  na katika kukamilisha mambo yake aliwatumia sana.

Sasa  mara baada ya swala la Hamza  na Regina kuletwa mezani na kiongozi wa kundi hilo Fanueli Yowe  akimwakilisha mheshimiwa  Mgweno  moja kwa moja waliona kazi ya kumuua Hamza wawapatie washirika wao wa muda mrefu  yaani Assassin wa Black Eared Snake kumaliza kazi hio, hayo yote ni kutokana na kuona  uwezekano ni mdogo wa  kupambana na Hamza ana kwa ana.

“Kundi letu la  Nyoka Mwenye masikio meusi  linahistoria ya miaka ishirini tokea kuanzishwa kwake  na  hatua kwa hatua tuliweza kutambulika kimataifa na ni juzi tu  hapa miaka kumi iliopita tuliweza kutambuliwa na Surety International Association  na  kupewa cheo cha daraja C katika  ulimwengu wa maninnja, uzoefu wa kazi za kuua  tunazo  ni kwamba tu  mtu ambae mmetupa kazi ya kumuua awamu  hii anaonekana kuwa na mafunzo ya juu  na pengine ashawahi  kuwa  mwanajeshi, Afande Yowe  huna haja ya kuwa na wasiwasi , kwasababu mmeshatulipa pesa nyingi juu ya hii kazi nina wahakikishia  tutaimaliza haraka iwezekanavyo”

“Unaongea ujinga , tulikuambia kabisa hili ni swala ambalo linatakiwa kufanyika mara moja , lakini angalia  mmefeli na kufanya  mkuu wa majeshi anatupa tahadhari , kazi imekushinda tunataka urudishe malipo tuliokupatia”Aliongea bwana  mmoja mwenye kitambi aliekuwa amekaa pembeni.

“Turudishe hela! Chochote ambacho sisi Noka wa Masikio meusi  tunameza hatuwezi kutapika”

“Kazi  imewashinda na mnataka kula pesa yetu ,  hamna aibu?”Aliongea yule bwana kwa hasira  huku akigonga meza , alifahamika kwa jina la Afande Sucre.

Maneno ya Sucre yalionyesha  kumkasilisha mmno  Mr Snake huku akionyesha nia ya  kutokubaliana nae kabisa.

“Mzee Sucre kaa chini  ili tuweze kusikia mpango B wa Mr Snake”

Muda uleule  Mr Snake alichomoa kisu  chenye kifimbo chekundu , kilikuwa kidogo mno  urefu wa kidole  cha mkono  na kilionekana chepesi na alitumia kisu kile kujikata kucha  huku akiongea.

“Wote hapa  ni wanajeshi lakini sijui kama mshawahi kusikia  neno maarufu katika vita  lifahamikalo  kama Original Strike?” “Unaongea  upuuzi gani ?”Aliongea  Sucre kwa hasira.

“Katika  ulimwengu wa kimasenari  ikitokea  umeshambuliwa  kitu cha kwanza unachopaswa kufanya ni kutafuta chanzo  cha shambulizi  kwani ndio  njia  nzuri zaidi ya kutatua tatizo , kama  hisia zangu ni sahihi  huyu kijana wenu  mnaemwita Hamza lazima atatafuta namna ya kututafuta  ili kulipiza”

“Unamaanisha nini , kwahio unasema  anaweza  kuja ndani ya hili eneo?”

“Sidhanin kama ni mjinga  kuja eneo hili  , maana itakuwa ni kujitafutia kifo”Aliongea bwana mmoja  mwwenye mwili mkakamavu.

“Mnakosea,  kwa taarifa mlizonipatia makisio yangu ni sahihi , anajiona  ni  mpiganaji mzuri  na  lazima  ataamini  anao uwezo wa kutudhibiti  , hivyo  atatudharau , isitoshe wengi  wenu hapa mnaonekana wazembe wazembe”Aliongea na kumfanya  Afande Yowe  macho yake kusinyaa,  ni kweli kabisa  katika mapigano licha ya kwamba wanajiita wanajeshi lakini  ni wanajeshi wa kutumia siraha na sio   kupigana.

“Mr Snake  kama kweli  Hamza akija hapa , unadhani vijana uliokuja nao  watatosha kudili nae?”Aliuliza na kumfanya  Mr Snake kwa kujivunia   kabisa kugeuza macho yake na kuangalia wanaume  waliosimama nyuma yake , walikuwa ni wanaume wenye miili iliojengeka kimazoezi  huku wakiwa wamenyoa vipara, hawakuwa na  ishara ya  uzembe hata kidogo. “Kama akijileta  ndio mtajua  nini kitakachotokea?”

“F**ck you  Hamza , jiafanye mjinga na ujilete hapa  nitampasua na  risasi moja tu”Aliongea Sucre na kitambi chake huku akikoki kwa mbwembwe bastora yake.

“Mkuu  mimi sidhani kama atakuja hapa  na muda umeenda , nadhani kikao kishaisha, nina miadi hivyo nitatangulia kuondoka”Aliongea  Afande Sucre  na kusimama  akifuatiwa na mabodigadi wake.

Lakini sasa muda ambao  anafikia mlango  ili kuufungua  ulifunguliwa kwa  kishindo  na mara baada ya kuangalia vizuri ni  mabodigadi waliokuwa wakilinda kwa  nje, walikuwa wamepoteza fahamu  wakiwa wamerushiwa  mlangoni.

Muda huo watu wote walikodolea macho mlango na waliweza kumuona kijana mdogo akiwa amesimama  kwenye mlango  huku akitafuna bublish na nyuma yake walionekana mabodigadi waliokuwa wakilinda  wakiwa chini wengine wakionekana  hawana fahamu  na wengine walikuwa wakiugulia maumivu.

Afande Sucre alijikuta akimeza mate mengi huku akimwangalia  Hamza kwa wasiwasi.

“Wewe ni nani?”Aliongea huku  mkono ukiwa umeshafika kwenye kiuno sehemu iliopo siraha yake.

“Naitwa  Hamza Mzee, mtu ambae unataka kumpiga risasi na hio bastora yako”Aliongea

Hamza akiwa  na muonekano uliojaa uzembe.

Afande Yowe macho yake yalimtoka , hakuamini Hamza angefika hapo kama alivyosema Mr Snake.

Afande Sucre alijikuta  akirudi nyuma  kwa namna ya kujihami  na kuungana  na wezake.

Upande wa wanajeshi wote  wa kundi hilo wanaojiita wanaojua mapigano walijikuta wakisimama  kwa wasiwasi na mshangao.

“Wewe ni jasiri  mno , hakika unasttahili  kuitwa mwanajeshi  kwa kujileta hapa”Aliongea Mr Snake akiwa na  tabasamu usoni  akijiambia  anakwenda kuimaliza kazi muda huo huo ndani ya eneo hilo.

Ukweli ni kwamba  licha ya kundi hilo kusikia habari za Hamza  wengi  wao hawakuwahi kuonana nae ana kwa ana zaidi ya  Master Konki ambae hakuwepo kwenye kikao hicho..

“Mr Snake  ulichoongea kimeonekana kuwa kweli , nipo tayari  kuona kile ambacho

umeandaa”Aliongea  Afande Yowe  na  wenzake wote walitingisha kichwa.

“Subirini kwanza?”Aliongea Hamza  akinyoosha mkono.

“Unataka kuongea nini , usije ukasema unaona woga wakati umejiingiza  kwenye  pango  la Simba”

“Sijaja hapa kupigana  wala kuibua mzozo na mtu , kwa ninavyoona hapa  wengi wenu mnaonekana kuwa na vyeo serikalini   hivyo sitaki kujiletea matatizo”Aliongea Hamza na kuwafanya wale  watu kumwangalia kwa mshangao.

“Kama hujaja hapa kupigana umekuja kufanya nini?”Aliuliza Mzee Yowe.

“Nimekuja kuwapa onyo,  leo baada ya kushambuliwa na maninja wa kundi la nyoka nilijua fika kuna mkono wa mtu wenye nguvu umehusika , hivyo  sitaki ugmvi  na mtu yoyote na muache kushambulia watu  wa karibu yangu”

“Onyo!! , Wewe ni nani wa kutupa onyo , unajua vyeo vyetu  katika jeshi , kwanini mtoto mdogo kama wewe tukubali onyo lako, ukiburi umekujaa”

“Kwamaneno yako naona kabisa haupo tayari kuikumbatia hii fursa ninayokupatia , hebu jifikirie

mara mbilimbili kabla ya kuendelea kunichokoza”Aliongea .

“Wewe mtoto ni kichaa  na  bora umejilera mwenyewe, kama  hukufunzwa adabu tutakufunza leo”Aliongea  Sucre.

“Upo siriasi?”

“Unadhani natania , unadhani naweza kuogopa panya mdogo kama wewe”Aliongea.

“Mr Hamza asante kwa kufika hapa kwa ajili yangu  ili niwaonyeshe ni kwa namna gani naenda kudili  na mtu kama wewe”

“Na mimi nimekuja kuona unadili vipi na mimi?”Aliongea  Hamza   na  muda uleule  Mr Snake alipiga  mluzi  na kufumba na kufumbua kundi la watu  waliovalia mavazi meusi walijitokeza  na kuingia katika ukumbi  huo huku  wakiwa wameshikilia siraha.

Kitendo cha watu wale kutokeza kiliwafanya  watu wote kushangaa akiwemo Mzee Fanueli.

“Mr Snake kumbe ulikuwa na kundi la watu wengi namna hii?”

“Nisamehee afande kwa kukutokutaarifu mapema , nilikuwa nimejiandaa kudili na huyu  mtu ndio maana nimechukua  kila tahadhari”

“Sidhani kuna haja ya kupoteza nguvu za vijana wetu , risasi  zinamtosha”Aliongea  Afande Sucre  na alitoa  bastora yake akifuatiwa a  mabodigadi  na bila ya kujiuliza mara mbilimbili walimfyatulia  Hamza mfululizo mpaka  bunduki zikaishwa  risasi lakini  kitu cha ajabu ni kwamba  risasi zile ni kama zilikuwa zikipiga hewa , Hamza walikuwa wakimuona mbele yao  lakini  ilikuwa ni kama holograph ya Hamza , ile wanamaliza Hamza alikuwa palepale mbele yao akiwa na tabasamu.

Swala lile liliwashangaza mno wale mabwana na  hofu na wasiwasi iliwavaa, walimuona Hamza kama mzimu.

“Wewe  ni  binadamu au Mzimu!!!”

Mr Snake  alijikuta akibung’aa huku akimwangalia  Hamza kwa hofu na kuna kila hali iliokuwa ikimwambia  Hamza aliwafanyia kiini macho ili waamini alikuwa mbele yao lakini muda mrefu alikuwa ashapotea na amerudi  baada ya  kuacha kushambuliwa.

Aliona kama  hisia zake ni sahihi basi njia moja tu ya kudili nae ni  kushambulia ana kwa ana na sio kwa kutumia  siraha  kama bunduki.

“Sijaja hapa kujibu  maswali , nimewapa nafasi mmeikataa”Aliongea Hamza huku akipiga hatua  lakini Mr Snake alifyatuka na kumsogelea Hamza kwa spidi  akiwa na  kisu  amekitanguliza mbele  kininja kwa kumlenga eneo  la shingoni.

Kitendo cha  Mr Snake kumfikia Hamza usawa wa shingo mkono wake  ulioshikilia kisu  ulidakwa kwa spidi  ya juu kiasi cha kushindwa kukwepa na kuzungushwa  kwa nguvu  na maumivu aliohisi  alijikuta akikiachia kile kisu mwenyewe.

Hamza hakuchelewesha  wakati kisu kule kinadondoka katika mikono ya  Mr Snake alikidaka na  mkono wa kushoto  na bila ya  huruma alimkita nacho Mr Snake katika paji la uso  na kuzama ndani kabisa.

“Master!!!”

Maninja wawili waliokuwa karibu na bosi wao mara baada ya kuona amekitwa na kisu cha paji la uso  walijikuta wakipiga yowe na kwa hasira kubwa waliinua  mapanga yao na kumsogelea Hamza  kwa spidi kana kwamba  wanataka  kumtenganisha shingo na kiwiliwili.

Wa kwanza  mara baada ya  kumsogelea  Hamza kwa spidi  kwa mtindo wa kutaka kumfyeka  shingoni ,Hamza alimkwepa kuinama chini na  upanga ulipita hewani  na kisha palepale  kwa ustadi wa hali ya juu aliachia ngumi  nzito iliompiga bwana yule eneo la moyo  na kilichoweza kusikika   ni mbavu zake kuvunjika  na alidondokea  mbali huku akikodoa  macho  na kutema damu kisha  akadondoka chini isieleweke kama amekufa au amezimia ,hakuzubaa baada ya shambulizi lile mwingine alikuwa ashamfikia  akinuia kutaka kumchoma  na upanga eneo la  tumboni lakini  Hamza alikuwa mwepesi kwani  alikwepa kisu kile na kupita  kwenye mbavu kiasi  cha kuchana  nguo aliovaa na palepale alimpiga  bwana yule  teke  la kigoti na kumfanya kupinda  na ilikuwa ni nafasi   ambayo Hamza aliitaka kwani alimtandika  ngumi   nzito ya  paji la uso iliomdondosha Ninja  yule  chini  na kuzima palepale.

Haikuwa kwa  Sucre na wenzake ama kwa kiongozi wao  Afande Yowe , wote walijikuta wakipatwa na mshituko usio  na kifani  huku hali ya woga ikiwavaa , Afande   Yowe Bastora yake ilikuwa na risasi lakini alishindwa kuchukua maamuzi ya kuitumia kutokana na kile alichoona  baada a Hamza kutoathirika na risasi.

Wale maninja wengine mara  baada ya kuona  wenzao walivyojeruhiwa walisita kufanya mashambulizi na kumwangalia tu kwa wasiwasi , isitoshe mkuu wao alikuwa ndio  mtaalamu wa hali ya juu na  mabwana wawili waliozimishwa kwa ngumi moja moja tu ndio walikuwa wakifuatilia kwa uwezo sasa   wanawezaje kumshambulia mtu ambae amemuua mkuu wao kwa shambulizi moja.

“Kajikundi  kadogo ka  daraja C  wanaona wanaweza kushindana na mtu kama mimi”Aliongea Hamza  mara baada ya kuona kazi yake ni njema na alipiga hatua kumsogelea  Fanueli.

“Unajua kwanini tumefikia hatua hii?”Aliuliza Hamza na kumfanya Afande Fanueli kutingisha kichwa kusema  hajui.

“Mmekodi watu kwa zaidi ya mara  tatu sasa  kwa ajili ya kuja kunishambulia   na hata kutuma hawa wapuuzi mkiamini wanaweza kunishinda, lakini   yote hayo  yaliotokea mmeshindwa kujiuliza swali moja jepesi  tu, na swali lenyewe mlipaswa  kujiuliza  mimi ni nani kwanza  kabla ya kuchukua hatua , tokea mwanzo nilijua  tu mnajitafutia matatizo  kwa kunichokoza , nilitaka kuwavumila lakini  inaonekana  nguvu yenu  hapa nchini imewapa kiburi na  hamuwezi kunusa hatari”

“Mr Hamza  tafadhali  tunaomba usitufanyie chochote , tupo tayari kufanya chochote , najua  unamahusiano makubwa na kiongozi  wa mtandao wa Chatu nipo tayari  kuongezea nguvu mtandao huo,  tumefanya haya yote kutokana na presha kubwa  kutoka kwa familia ya Mzee

Benjamini”Aliongea  lakini Hamza hakumjali  na muda uleule alimgeukia Afande Sucre.

“Wewe mzee njoo hapa”Aliongea Hamza  na kumfanya  Afande Sucre kutetemeka   lakini kwa hofu kubwa  alimsogelea Hamza.

“Mr Hamza kama kuna chochote unataka niambie   nitafanya”Aliongea  kwa kunyenyekea na kufanya wenzake kumwangalia  kwa macho yaliojaa dharau  kwa namna alivyonywea. “Nipe hio Bastora yako”

“Eeh!”

“Hutaki kunipa?”

“Hii hapa”Aliongea  Sucre kwa haraka mara baada ya kusika sita kumpatia Hamza 

Hamza mara baada ya kuishika ile bastora aliangalia ndani yake  kama ina risasi na ilionekana kuwa nazo  tatu na kitendo cha kuiweka sawa alikuwa ashaachia risasi  ambayo ilitoboa paji la uso la mzee  Sucre 

Sucre hata hakujua amepigwaje risasi  maana  mkono wa Hamza ulifyatuka kwa spidi kubwa  mno lakini ndio hivyo ilikuwa mwisho wake.

Hamza hakujali  maiti ile  na  alimgeukia  Fanueli ambae alikuwa akitetemeka kwa hofu   pamoja na kundi lake.

“Nilisema  kabisa sijaja kupigana lakini  ukaamua  kunidharau”

“Mr Hamza nilikosea  tafadhari naomba unisamehe  hili lipi…”

Kabla hata hajamaliza sentensi yake alikuwa ashachapwa lisasi  mbili  za kichwa  na kudondoka chini.

Ndani ya dakika chache Hamza alikuwa ashamuua kiongozi wa kundi la Nyoka Mwenye masikio  Meusi na   Kanali Mstaafu Afande Fanueli Yowe.

“Kuna mwingine anataka  kufa?”Aliuliza Hamza  huku akiwaangalai waliobaki  na kila mmoja alionekana kuwa katika hali ya kutetemeka huku baadhi wakitaka kujikojolea na waliishia kutingisha  vichvwa vyao  wakitia  huruma.

Hamza hakuwa na mpango wa kumuua mtu 

wakati anakuja hapo lakini uchokozi ulizidi  hivyo alilazimika kutoa fundisho.

“Mimi ni kijana mpole  sana tena mwanachuo , lakini naomba niwaambie tu Sipendi

Uchokozi”Aliongea Hamza na kisha alirusha ile bastora chini  kisha  alitoa simu yake  ya batani na kuangalia saa na aliweza  kuona muda ulikuwa umeenda sana.

“Nadhani taarifa zitamfikia anaewapa  kiburi cha kutaka kufanya chochote ndani ya  nchi hii, mwambieni ajifikirie mara mbili mbili kabla sijamchukulia hatua”Aliongea   Hamza  na kisha  aliondoka ndani ya eneo hilo.

*****

“Wakati ulipokuwa umelela sijafanya chochote mbona?”Aliongea Hamza akiwa katika simu na  Dina.

“Bado  unaongea kimatani tu , asubuhi nimesikia  taarifa umemuua  Mzee Fanueli Yowe,  mstaafu Mgweno   ametoka kunipigia hapa anaomba yaishe”Aliongea Dina na kumfanya Hamza kucheka , ilionekana onyo ambalo alitoa jana limefanya kazi.

“Kuna onyo nilijaribu kutoa jana usiku  na limefanya kazi , tumia nafasi hii kujiimarisha”Aliongea Hamza.

“Unajua kusababisha matatizo  sana , sidhani  pia kama  ameomba kuyamaliza kwa nia ya dhati , kuna  uchaguzi mwezi ujao  ndio maana kaamua kujishusha, Mgweno ninaemjua mimi sio mtu wa kukubali yaishe kirahisi’

“Kama hajanielewa   muache aje hata baada ya huo uchaguzi, mimi sipendi uchokozi  ni hivyo tu basi ,  nitapambana kulinda amani yangu”Aliongea

Hamza na upande wa pili ulionekana kuwa kimya.

“Vipi baadae unakuja  kunisalimia , sijakuona muda mrefu?”

“Muda mrefu wapi  wakati ni juzi tu hapa?”

“Hata kama  hakikisha unakuja usiku la sivyo nitakuja kuruka ukuta  na kuingia ndani ya hilo  kasri  unaloishi siku hizi”Aliongea na kumfanya Hamza kuishia  kukubali tu.

Hamza  mara baada  ya kumaliza kuongea na Dina alikata simu mara moja  na muda huo ndio alikumbuka  alikuwa ameghairisha  mara kibao kwenda nyumbani kwa  Eliza  na pia kulingana na ratiba za siku hio aliona  ingekuwa ngumu pia kwenda hivyo alimpigia simu  na kumwelezea kuwa  hatoweza kumtembelea.

Baada ya kuoga   alivaa nguo  na kisha alishuka chini sebuleni   na aliweza kumkuta  Regina akiwa bize jikoni akitengeneza Sandwich kwa kutumia kutumia Sausage.

“Regina unatengeneza  Sandwichi au kitu gani?”Aliuliza Hamza.

“Sio lazima kujua ninachotengeneza”Aliongea huku akizidi kuwa bize, alionekana kujivunia kwa kile alichokuwa akifanya.

Kutokana na Shangazi kutokuwepo nyumbani aliona aingie mwenyewe  jikoni.

Hamza alikumbuka Shangazi akimwambia  Regina hakuwa akijua  chochote kuhusu kupika  hivyo alishangaa kumkuta jikoni.

Alijua  Regina  atatengenea utopolo wa chakula hivyo alifungua friji na kutoa  mayai, tambi na  nyama , vitunguu  na pilipili hoho. “Unafanya nini , utachafua vyombo tu”

“Nitaviosha baadae nikirudi”

“Unadhani kula sana ndio afya , kwanini usisubiri  tule hiki ninachopika?”

“Haijalishi  nakula sana , sijui nitaishi kwa miaka mingapi mbeleni ,  mtu unapaswa kula kila unachojisikia  maana  hujui ni lini utashindwa kula”

“Mawazo yako   yanasikitisha , kwahio unadhani  kwasababu huwezi kuishi muda mrefu unachopaswa  ni kula tu na sio kufanya vitu vingine ya  msingi?”Aliongea huku akikunja sura lakini Hamza alikuwa mvivu kujibishana nae na alianza kusaga saga ile nyama.

Muda huo  vipande viwili vya mkate vilichomoka  ndani ya kibaniko.

“Aiyaa..”Regina alijikuta akishangaa   huku akikunja ndita.

“Nini tatizo?” Aliuliza Hamza  na huku akimgeukia na mara baada ya kuangalia  kilichokuwa  kikimshangaza Regina alijikuta akianza kucheka 

“Haha.. Regina huo ni mkate au ni pande la mkaa?”

Vipande  hivyo vya mkate vilikuwa vimegeuka kuwa  vyeusi  tii  na sio  Brown kama alivyotarajia.

“Unacheka nini sasa ,  nimezidisha moto ndio maana umeungua”Aliongea  na kumfanya Hamza kusogea karibu na kuangalia

“Aina ya hii mikate inahitajika  nyuzi tatu tu za joto  kuubanika, sasa wewe umeweka  sita unadhani nini kitatokea?”Aliongea  na kumfanya  Regina kuangalia mashine hio ya  kibaniko  na kuona kweli aliweka  joto la juu mno.

“Nilikosea”Aliongea  huku akirekebisha na kuanza kubanika upya vipande vya mikate ili ajazie na  Sausage.

“Nilijua  ni mzoefu wa kutumia hizo mashine za kupikia”

“Endelea na unachokifanya achana na mimi”Alimsukumia  pembeni huku akiendela kuwa bize. 

Baada kama ya nusu saa kila mtu alikuwa ameshamaliza kutengeneza kile alichokuwa akitengeneza , Hamza alitengeneza tambi za mayai nyama na kuweka na Regina alikuwa ametengeneza Sandwich zake za Soseji.

Baada ya kukaa mezani kila mtu alikula kile alichoandaa mwenyewe.

Sasa Regina ile anapeleka mdomoni kung’ata kipande cha  mkate  alijikuta akikunja sura na alitema palepale.

“Hizi Soseji nadhani zilikuwa zimeshaharibika ,  ni chachu mno”

“Kwahio ulipika   bila ya kuangalia kama  muda wake umeisha?”Aliuliza Hamza na kumfanya Regina kuwaza kwanini hakuangalia kabla.

Alijikuta akitia huruma huku akiangalia  kitafunwa alichoandaa kilichokuwa kimeshachacha na  kujikuta akiangalia  sahani ya Hamza iliojaa tambi za mayai kama vile ni Pizza, alijikuta akimeza mate kutokana na harufu yake nzuri.

Hamza aliweza kujua mwanamke huyo alikuwa akitaka   cha kwake  lakini alikuwa akishindwa kuongea.

“Regina  nadhani  haitakuwa  vizuri kuharibu   chakula ,  unaonaje tukiambizana kumaliza hiki cha kwangu”Aliongea Hamza akimaanisha wasaidiane kula na kumfanya Regina kusafisha koo.

“Kwasababu umeniomba nikusaidie nitafanya hivyo  , nitakula kidogo kukupunguzia mzigo”

“Asante kwa  msaada wako bosi”Aliongea  Hamza huku  akimpunguzia kwenye sahani yake.

Kitendo cha Regina kuonja alijikuta macho yakimtoka  na palepale  alijiambia inakuwaje Hamza anajua kupika namna hio , japo tambi hizo zilionekana za kawaida kwa kupikwa na  nyama pamoja na mayai  lakini hakuamini zingekuwa na radha tamu kama hio.

“Hey! , hivi ushawahi kuwa mpishi?” Regina alishindwa kujizuia na kuuliza.

“Hapana”?”

“Sasa inakuwaje unajua kupika  namna hi”

“Labda ni kwasababu sio rahisi  kuishi, ndio maana ni vizuri kuhakikisha unajua namna ya kuridhisha tumbo lako”Aliongea Hamza lakini jibu lake ni kama halikumridhisha  Regina na  shauku  kubwa ilimvaa.

“Regina unanisifia?”

“Kidogo tu”Aliongea  Regina kwa sauti ya chini na kumfanya Hamza kutabasamu.

Baada ya kifungua kinywa  walindoka kwa pamoja wakiwa na nyaraka  maalumu na kuelekea Bomani kwa ajili ya kukitafuta cheti cha ndoa.

Kwasababu  Lexus ilikuwa imelipuka walitumia Mercedenz Benz Maybach , ilikuwa gari nzuri ambayo haikupitisha risasi.

Kutokana na  ukubwa wake  katika jamii swala zima la kupata cheti halikuchuwa muda , mwanadada ambae alikuwa amesimamia swala zima alijikuta akimuonea wivu Hamza kwa kuweza kupata mwanamke mzuri kama Regina.

Mara baada ya kurudi kwenye gari , Regina alionekana kuwa na hisia mchanganyiko  mara baada ya kuona picha  zao katika cheti 

Hamza aliishia kumuangalia kupitia kioo cha nyuma na kuona ni kwa namna gani Regina alionekana kuwa na wasiwasi.

“Vipi sasa ,  unahisi   kuna chochote kilichobadilika?”

“Sioni chochote cha ajabu ,   nimefanya yote haya kwa ajili ya kumridhisha bibi  tu  ili anipe hisa zake”Aliongea Regina.

“Ndio unaona ipo  hivyo , muda  ni fumbo kubwa mno sikudhania nitajikuta katika hali kama hii , ila  inanifanya niwe na furaha bila sababu ya msingi”Aliongea Hamza.

“Hiki ni cheti tu , unaweza kuoa muda wowote unaotaka , hili likipita tutafuata taratibu  na kufuta hiki cheti , hakikisha mpenzi wako hajui sitaki matatizo”

“Swala la kufuta cheti ni  mimi kuamua kama nakubali au lah , lakini usijali sana , muda una majibu  mengi”Aliongea Hamza , lakini licha ya kuonekana ana furaha upande wa Regina hakuwa na furaha na alimtaka  Hamza kuendesha gari kuelekea hospitalini ili kumuonyesha  bibi yake  cheti aridhie kumkabidhi hisa zote za kampuni.

Lakini sasa wakati wanafika ndani ya  maegesho ya magari  katika hospitali hio ni kama Hamza alikuwa akisubiriwa kwani  walikuwepo Polisi  wakiongozwa  na  Nobert.

“Mr Hamza upo chini ya ulinzi  kwa makosa  ya mauaji yaliotokea jana usiku”AliongeaNobert akiwa siriasi  na polisi wenzake walimzingira kutaka kumfunga pingu huku wakiwa  katika hali ya tahadhari na siraha zao.

Regina   alijikuta  akitoa macho mara baada ya kusikia kauli hio,  ilikuwa ni kama hajasikia vizuri.

*****

Upande mwingine ndani ya makao makuu yya

Taasisi ya Haliz Foundation katika  floor ya nne kwenda chini ya  vyumba vya Ardhi, Amosi  alionekana kuwa macho licha ya  kwamba bado  mikono yake ilikuwa imefungwa na  vitu kama pingu katika kitanda na kumfanya ashindwe kusimama.

Alionekana kuwa na utulivu wa hali ya juu na alikuwa kama mtu ambae  alikuwa akisubiria mtu aingie kwenye wodi hio.

Upande mwingine nyuma ya chumba alicholazwa Amosi  kulikuwa na watu  wanne  waliovalia makoti ya kidaktari  mmoja wapo akiwa ni Sister Maya Thema na mwingine alikuwa ni Frida ambae alionekana kuwa   na mshangao akiangalia Skrini iliokuwa ukutani ikimuonyesha Amosi.

“Profesa  kama hili  lingekuwa swala  ambalo jamii inapaswa kuambiwa basi katika historia  Tanzania inaingia katika nchi tatu ambazo  upandikizaji wa Chip  kwenye ubongo wa binadamu umefanikiwa kwa asilimia mia moja”Aliongea Frida  na kumfanya Dokta Maya Thema  kutingisha kichwa kukubaliana nae.

“Kwasasa hii teknolojia  wakuu  hawataki  ikitangazwa kwa  jamii  ya watu mpaka kukamilisha mipango yao , lakini licha ya hivyo imenipa hali ya kujivunia kufanikisha  operesheni hii kwa mara ya kwanza katika Ardhi ya Afrika”Aliongea.

“Nini  hatua inayofuatia baada ya  hapa?”Aliuliza Frida huku akiwa na macho yaliojaa  shauku.

“Sisi ni wanasayansi pekee na kazi yetu ni kukamilisha kile ambacho wafadhili  wetu wanataka kufanya,   hatua inayofuatia  ipo chini ya Ajenti  wa umoja wa Sinagogu”Aliongea.

“Profesa kwahio kwasasa  pale yupo  imara kiakili , hakuna  athari zozote nje ya zile zilizotarajiwa zilizoweza kuonekana kupitia tabia yake?”Aliuliza  Frida.

“Leo ni siku yake  ya nne tokea  kufanyiwa  operesheni , siku ya kwanza  alikuwa  kwenye  hali ya kawaida ya  mshituko na kuikataa hali aliokuwa nayo , lakini kwa kushitua mishipa yake ya  fahamu eneo la hisia  tumeweza  kufanikisha  kumfanya  kuwa  katika hali ya mazoea , kuhusu tabia ambazo  zipo nje ya matarajio bado hatujaona na hatuna budi kumfuatilia  hata akiwa katika mazingira ya kawaida”

“Profesa  hii sio operesheni ya kwanza kufanyika , mbili ziliweza   kufanyika nchini  Uingereza na  moja  nchini Marekani na  mbili Israeli na  ni zaidi ya miaka kadhaa imepita tokea kufanikiwa kwa  operesheni hizo , kwanini tusitumie Follow up  ya

data za wagonjwa waliopita?”Aliuliza Dokta John moja ya wanasayansi  wa taasisi hio.

“Kila operesheni inayofanyika katika upandikizaji wa Chip katika Ubongo inabeba malengo  tofauti  hivyo matokeo ya kitabia kuwa tofauti pia , Katika historia ya Dunia Operesheni ya kwanza ya kupandikiza kifaa kwenye ubongo  ilifanyika  nchini Ujerumani chini ya Usimamizi  na ufadhili wa  Nazi  , malengo ya upasuaji ule yalilenga kufanya wanajeshi kuwa imara zaidi  katika  kubuni mbinu  za kumshinda adui , unachopaswa kuelewa utofauti wa operesheni ile  na wa leo ni kwamba ule ulifanyika katika kufunua kichwa cha binadamu na kisha kuweka kifaa  lakini huu  umefanyika bila ya kufungua kichwa cha binadamu ikimaanisha dunia ilipiga hatua kutoka wakati ule  , tulichelewa miaka  mingi  kuendeleza sayansi ya upandikizaji Chip tokea  vita ya pili ya Dunia  mpaka sasa kutokana na  Josef Mengele  kumuua Dokta Douglas kwa sumu  akiwa katika maabara   ambae  ndio alibeba  jukumu kubwa la  tafiti za ubongo wa  binadamu, hakuishia  kumuua Dokta Douglas tu bali  alichoma tafiti zake zote na kitendo kile kilirudisha dunia hatua  moja nyuma katika  maswala ya tafiti za kibailojia”Aliongea Dokta Maya na jibu lile kidogo lilionekana kumshangaza na Frida.

“Profesa unamaanisha Joseph Mengele huyu  ambae katika historia  alifahamika kama Malaika wa kifo ,  sijawahi kusikia jina la Dokta  Douglas katika historia  kwanini alimuua?”

“Hakuna ambae  ashawahi kumsikia Dokta Douglas kwasababu alikuwa ni mwanasayansi ambae anapiga hatua  na  hakukuwa na matokeo ya wazi ya tafiti zake , mgonjwa wake wa kwanza ambae alimpandikiza  kifaa katika Ubongo hakuonyesha  matokeo  makubwa sana kama nadharia ilivyokuwa, pengine alifanikiwa au pengine hakufanikiwa ndio maana  Josef Mengele alimuua na kuchoma tafiti zake”.Aliongea Dokta Maya Thema.

“Imekuaje ukawa na  taarifa ya swala hili , Profesa kwa umri wako…”

“Frida  si kila kitu ndani ya  dunia hii kipo wazi  na sio kila mwenye umri mkubwa anafahamu kila kitu , historia ipo leo kwasababu imetunzwa , kabla ya

kuwa muumini wa Sinagogu nilikuwa  mwanasayansi nchini ya Kanisa kuu”Aliongea Maya na kumfanya Frida kutingisha kichwa.

Alielewa  watu wengi ambao walikuwa na historia kubwa na Kanisa kuu walikuwa wakijua mambo mengi.

Muda  ule wakati wakiongea  katika Floor hio  aliingia bwana mmoja alievalia suti , alikuwa ni kijana  ambae  ana muonekano wa kidominikani  au kilatini  kwa lugha nyepesi, ikimaanisha kwamba  alikuwa na asili ya makabila matatu yaani  Mzungu kwa asilimia hamsini , Mwafrika kwa asilimia  arobaini na  mlatino  kwa asilimia kumi.

“Ajenti Alonzo  karibu sana”Aliongea Maya Thema alionekana kumfahamu yule bwana ambae tembea yake ilionyesha  ni kwa jinsi gani alikuwa mkakamavu.

“Asante sana Profesa”Aliongea  na kisha macho yake yalitua katika sura ya Frida na kumfanya ProfesaMaya kuchukua jukumu la mara moja kumtambulisha Frida na Dokta John.

“Mr Alonzo huyu ni  Dokta Frida Franklin  mkuu wa idara   ya CST , kutana pia na Dokta John mtaalamu wa Neva”Aliongea  na Ajenti  Alonzo alisalimiana nao.

“Nimefurahi kukutana na wewe Frida , nimelisikia jina lako  mara kadhaa na imekuwa heshima kwangu kukutana na mwanasayansi  kama wewe”

“Asante sana”Aliongea huku akitoa tabasamu la ukarimu na muda uleule  Ajenti Alonzo  macho yake yalitua katika Skrini iliokuwa ikimuonyesha Amosi.

“Nimeambiwa kila kitu kwa upande wako kimekamilika , nipo hapa kwa ajili ya kukamilisha hatua ya pili, kwanini bado amefungwa kwenye kitanda?”Aliuliza.

“Tumeamua kuchukua tahadhari , lakini kutokana na utendaji kazi wa ubongo wake sidhani  kama anaweza kuwa   hatari ”Aliongea Dokta Maya.

“Operesheni hii sio kwa ajili ya kumfanya  kuwa mwanajeshi mwenye uwezo bali  kuwa  Ajenti mtiifu  na Muaminifu kwa Sinagogu  ambae anaweza kutuambia kila kitu, kama kutakuwa na   matumizi ya nguvu  kumuweka sawa , basi  mimi  ni mwanajeshi”Aliongea  na kumfanya  Dokta Maya kukubaliana nae na aliongozwa kuelekea mpaka kwenye chumba alichokuwemo Amosi.

Ajenti Alonzo  akiwa ameingia  na Dokta Maya Thema kabla ya salamu aliomba  Amosi afunguliwe mikono na awe huru na Dokta Maya alifanya hivyo.

“Profesa  kwanzia hapa nitaendelea  mwenyewe ,  naomba  Kamera zote  kuzimwa”Aliongea.

“Bila shaka Ajenti”Alijibu Profesa na kisha palepale  Profesa alitoka na kumuacha Amosi na Ajenti Alonzo.

Previoua Next