Reader Settings

Ilimchukua dakika kama kumi tu kwa Ajenti Alonzo kujitambulisha na Amosi kumuelewa , kwa wakati huo Amosi alionekana kuwa kawaida , ki ufupi hakuwa  na tofauti  sana kitabia , kitu kimoja tu ambacho kilikuwa  tofauti ni namna ambavyo alikuwa mtiifu kwa kile ambacho alikuwa akielezewa  na Alonzo.

“Mr Amosi kwasasa utafahamika  kwa jina la Ajenti Zuku  ikimaanisha  Askari  usie na chimbuko, umenielewa?”

“Ndio Sir”Alijibu  Amosi kwa utiifu akiwa ameketi kwenye kiti na kumfanya  Ajenti Alonzo kuridhika.

“Kilichofanyika  kwako haimaanishi kwamba jina lako katika mazingira ya kawaida linakwenda kuwa tofauti ,  ukitoka hapa unakwenda kuendelea na maisha yako ya kawaida”

“Ndio Sir”

“Vizuri  kabisa , mpaka sasa umefahamu nini katika misheni yako juu ya  Naomi Lindsey na Rosemary Macha?”Aliuliza na kumfanya Amosi kufikiria kidogo.

“Sijapata kufahamu kwa uhakika lakini hisia zangu zinaniambia Naomi na Rosemary  ni  mtu mmoja na kuna uwezekano  Naomi alidanganya  kifo chake nchini Italy  na kisha akakimbilia Tanzania  kwa uhusika wa  Rosemary Macha”Aliongea Amosi.

Hizo ndio zilikuwa hisia zake tokea siku kadhaa apewe misheni  na Chriss na katika uchunguzi wake  alikuwa akitaka kuthibitisha swala hili  na kisha kuliunganisha na tukio lililotokea mkoani  Rukwa huko Sumbawanga.

Hio ndio ilikuwa misheni yake   ambayo Chris alimpatia  , misheni ya kutafuta mahusiano yaliopo katika ya Rosemary Macha na Naomi Lindsey  msanii mkubwa aliefariki nchini  Italy.

Ajenti Alonzo alionekana kuridhishwa na jibu la Amosi  na muda ule alionekana kutoa kishikwambi katika mkoba aliokuja nao  na kupangusa kwa dakika kadhaa na kisha alimwangalia Amosi.

“Unajua nini kuhusu tukio lililotokea  Sumbawanga?”Aliuliza

“Sikuwa muhusika wa uchunguzi wa tukio hilo , Ajenti Sedekia  Shilla ndio alieweza kufanya uchunguzi  na nusu ya ripoti ilifika   makao makuu na  nusu nyingine haikuweza kufika kutokana na Ajenti Sedekia  kutoweka, taarifa ambayo alitoa  ni   mwanamke ambae  hakufahamika jina lake kamili  zaidi ya  jina la Chakwe ambalo alibatizwa na mmoja ya wanakijiji  wa Kizwite  aliweza kufika  ndani ya kijiji hicho akiwa na watoto kumi  wenye asilia ya makabila tofauti tofauti , aliishi ndani ya kijiji cha Kizwite kwa zaidi ya miezi sita  na aliweza kumudu mahitaji yake na watoto kupitia  kwa misaada  mbalimbali ambayo wanakijiji walimpatia , siku kadhaa  mara baada ya  kupatiwa msaada wa eneo la kuishi  ikiwa ni kipindi cha  Masika kuliweza kutokea ajali ya radi na kumuua  yeye na watoto wake tisa huku mmoja ambae inaaaminika alikuwa na asili ya Kizungu alitolewa eneo la tukio  na mtu asiefahamika  na kutoweka, Ajenti Sedekia  alikusanya  ushahidi  kutoka kwa mashuhuda wa tukio hilo na aliweza kuwasilisha taarifa hio makao makuu , lakini kutokana na kukosekana kwa ushahidi wa moja kwa moja kutokana na utata wa tukio hilo kesi  ilifungwa kama ajali ya asili iliomuua mama na watoto wake wote”Aliongea  Amosi.

“Unadhani ni kwanini Ajenti Sedekia alipotea!?”

“Sina uhakika,  lakini naamini utata wa tukio hilo ndio ulimpoteza” “Unamaanisha nini?”

“Pengine kuna kitu ambacho  Ajenti Sedekia  aliweza kupata  kuhusu utata wa tukio  hilo  na kuna watu ambao walitaka kuficha  taarifa hio ndio maana akapotea” “Kwanini unahisi hivyo?”

“Wakati nikiwa Ajenti  nimeweza kusikia  tetesi kuhitimishwa kwa  kesi ile kama ajali ya kawaida  ulitoka  kwa Kiongozi  wa juu kabisa wa nchi na kuna taarifa pia zinasema  kuna  nguvu ya nje ya nchi  iliohusika, hisia zangu nguvu hio ndio iliompoteza Ajenti Sedekia”Aliongea Amosi  kitiifu kabisa.

“Umesema wakati ukiwa Ajenti , sasa hivi wewe sio Ajenti?”Aliuliza na kumfanya  Amosi kutulia kidogo na kumfanya Alonzo kumkazia macho.

“Nilikuwa Ajenti  wa kitengo cha Intellijensia  za kimkakati cha  TISA  kwasasa mimi ni Ajenti wa siri  wa Kitengo cha  jeshi cha kupambana na nguvu zisizoonekana kiitwacho MALIBU”Aliongea na kumfanya  Ajenti Alonzo kutoa tabasamu. “Nielezee zaidi  kuhusu ulichopata  tokea kuanza kazi ya kuchunguza uhusiano wa Naomi Lindsey na Rosemary Macha?”Aliongea na kumfanya Amosi kufikiria kidogo.

“Katika uchunguzi  wangu nimeweza kugundua  watu wa kisiwa cha Binamu hawakutaka   niendelee na uchunguzi  sijajua kwasababu ni nini  lakini  kupitia  kazi hio niliwekewa mtego wa kuuwawa na moja ya mkuu wangu wa kazi  na kwa bahati nzuri niliweza kunusurika”

“Unadhani mkuu wako  alikuwa akishirikiana na  watu kutoka  kisiwa cha Binamu”

“Ndio ,  nina uhakika  ni mshirika na watu  kutoka Binamu”

“Kwa  ninavyojua  ufanisi wa  watu kutoka  kisiwa

Binamu  ulivyo mkubwa  usingeweza kuepuka kifo , hujawahi kufikiria  pengine waliamua kukuacha  hai makusudi  au kuna sababu nyingine ambayo wakaacha kukuwinda?”Aliuliza

Licha ya Amosi kuulizwa maswali mengi lakini alionekana kutokereka kabisa wala kuchoka , ilikuwa ni tofauti na tabia yake , pengine ni kile ambacho ubongo wake ulifanyiwa.

“Kuhusu hili nimefikiria pia ,  lakini mkuu wa kitengo aliniambia niendelee na uchunguzi na ameshaongea na Kitengo cha TISA kwa ajili ya Kinga”

“Kwa maelezo yako ulipokea kazi kutoka kwa Chriss sio kwasababu ya pesa , unaweza kuniambia kwanini ulipokea kazi hii licha ya kuonekana kuwa na uhatari?”

“Mwanzoni nilipokea kutokana na shauku , lakini  nilipata hamasa zaidi mara baada ya kujua ni kazi ambayo inahusiana  na  tukio  la mwaka 2002  lililomfanya Ajenti Sedekia kupotea, nimekuwa chini ya kitengo cha MALIBU  kama ajenti  hai kwa  miaka  saba, kabla ya kupewa misheni nyingine ambayo ilinifanya  kuwa Undercover  kwa kivuli cha kustaafu na kuanza kuwa mtumwa wa kazi za kihalifu za vigogo wa nchi”

“Misheni!,  ilikuwa misheni gani?”Aliuliza Ajenti Alonzo.

Licha ya Amosi kujua kabisa  anatoa siri za kitengo lakini alishindwa kujizuia kuongea.

“Nilipewa misheni ya kufuatilia  tetesi za uwepo wa  watu Vivuli  maarufu kama ‘Night Shadows’   na kuongezeka kwa wimbi la wagonjwa wenye ‘split Personality Disorder’”Aliongea na kumfanya Alonzo kutingisha kichwa na muda ule aliangalia kishikwambi chake.

“Elezea kila kitu ulichofanya  ili kufanikisha uchunguzi wa Naomi Lindsey  na Rosemary Macha”

“Baada ya  kunusurika  kifo  niliweza kuendelea na uchunguzi  na kwa kumfuatilia Kanali Dastani aliekuwa mkuu wangu wa kazi  niliweza kugundua  kuna  mfungwa ambae kuna uwezekano mkubwa

alihusika  na kupotea kwa  Sedekia Shilla , niliweza kupata taarifa hii kwa kufuatilia mazungumzo ya simu kati ya  Dastani na moja  ya aliekuwa  Mkuu wa Gereza  la Silo, kwa kile nilichoweza kupata kusikia  ilionekana kuna watu walimtembelea  huyo mfungwa Gerezani  na  Mkuu wa Gereza  hilo aliweza kurekodi maongezi  kati ya  watu  hao na  mfungwa , kwa bahati mbaya katika harakati za kutaka kumfikia mkuu wa Gereza ili kujua walichoongea mkuu  huyo wa Gereza alikumbwa na umauti  na  imani yangu inaniambia  kifo chake kinahusiana na kitendo alichofanya cha kurekodi mazungumzo hayo”Aliongea na kumfanya  Ajenti Alonzo kutingisha kichwa.

“Katika maelezo yako umesema unadhani  Naomi

Lindsey  ni Rosemary macha , je unadhani pia  Rosemary Macha anaweza kuwa  mwanamke

aliefariki katika ajali ya radi akiwa na watoto wake?”

“Wakati nikiwa Ajenti  nilibahatika kuona  picha ya Chakwe  mhangwa wa  ajali ya radi na picha yake inafanana kwa asilimia mia moja na picha ya Naomi Lindsey na  Rosemary Macha , hivyo naweza kusema wote wanaweza  kuwa mtu mmoja”

“Kwa hitoria ya Naomi Lindsey hajawahi kabisa  kuwa na  mtoto  katika maisha yake  na pia kulingana na umri wake ni ngumu kuwa na watoto kumi , tena wa baba tofauti tofauti , lakini pia kuna historia ya kimatibabu ambayo inaonyesha  Naomi

Lindsey hawezi kubeba ujauzito kutokana na kukosa kizazi , kama  unachodhania ni sahihi unadhani  watoto aliokuwa nao  Chakwe  ni wa nani?”Aliuliza Alonzo na kumfanya Amosi akili yake kufanya kazi na sasa ni kama anapata kitu kipya  na kujiambia kwanini hakuwahi kufikiria hilo.

“Nadhani Mr Amosi  utakuwa na  maswali kwanini nakuuliza maswali yote haya , kabla ya  kujua unachokwenda kufanyia  kazi nilitaka kujua  unachojua  kwanza, nadhani  wakati unakutana na  Chriss  alikuelezea wewe  ndio mtu sahihi  katika misheni aliokupatia si ndio?”

“Ndio alisema hivyo  na ilinishangaza pia  kusikia hivyo?”

“Kuna  sababu  yoyote ambayo  unadhani kwanini tulikuchagua kwa hii misheni?”

“Sijui , labda ni kwasababu nishawahi kuwa chini ya kitengo  cha TISA  na kuhusika kwa namna moja na kesi hio ya Radi”Aliongea Amosi na Alonzo alitingisha kichwa kukataa na palepale  aliangalia tablet yake na alionekana   kupangusa pangusa na kisha alimpatia   Amosi.

Katika Tablet ile kulionekana picha  ya watu wawili , mwanaume na mwanamke  na kwa jinsi pozi lao lilivyo katika picha  ni aidha watu  hao walikuwa wapenzi au marafiki”Amosi alishangaa mara baada ya kuona ni picha ambayo alikuwa akiifahamu na yeye ni moja ya mhusika aliekuwa katika hio picha.

“Unaweza kuniambia huyu mwanamke  pembeni yako alikuwa nani kwako?”

“Huyu  ni Jasmine Mahmood  niliwahi kuwa nae katika  mahusiano kwa muda mfupi, alikuwa raia kutoka  Botswana aliwahi kuwa mwandishi wa habari wa kituo cha Aljazeera English nchini Qatar”Aliongea  na kumfanya Alonzo  kuchukua kile kishikwambi kwa mara nyingine na  kisha  alionekana kutafuta kitu na kumpatia.

Ilikuwa picha nyingine  ikimuonyesha  Jasmine Mahmood akiwa na  Naomi Lindsey katika pozi la tabasamu na picha ile ilimshangaza  mno Amosi.

Previoua Next