SEHEMU YA 58
Ajenti Alonzo mara baada ya kuona Amosi alikuwa akishangaa , alijua fika kile ambacho alikuwa akikitaka kutoka kwa Amosi amekiona.
“Mr Amosi unaweza kuniambia ni lini ulikuwa na mahusiano na Jasmine Mahmood?”Aliuliza na Amosi alifikiria kidogo na kisha alitingisha kichwa.
“Ilikuwa ni mwanzoni mwaka 2002, nilikutana na
Jasmine mwezi wa kumi na moja 2001
Amsterdam nikiwa katika msafara wa mheshimiwa Raisi kama Aide , Jasmine alikuwa mwandishi wa habari aliesafiri na mheshimiwa Festos Moga na ndio urafiki wetu ulianza , mwaka 2002 wakati anafika nchini Tanzania katika maonyesho ya riadha ndio tuliingia kwenye mahusiano rasmi ambayo yalidumu kwa muda mfupi sana”Aliongea Amosi.
“Kwanini mahusiano yenu yalidumu kwa muda mfupi?”
“Sababu kubwa ilikuwa umbali lakini pia kazi yangu ilinifanya kushindwa kusafiri mara kwa mara nje ya nchi kuonana nae”
“Hii picha Jasmine aliopiga na Neema Lindsery ilikuwa ni tarahe ishirini na tano mwezi wa kumi na mbili mwaka 2001 , siku nne kabla ya kifo cha Naomi, ni picha iliopigwa na Mattia Tommaso, mara baada ya kifo cha Naomi kutokea Jasmine alionekana nchini Tanzania kama mwandishi wa habari kutoka Botswana na kama ulivyosema ndio kipindi ambacho mliingia kwenye mahusiano , si ndio?” “Ndio”Alijibu Hamza.
“Ukiachana na mahusiano yenu unakumbuka chochote kisichokuwa cha kawaida kutoka kwa Jasmine?”Aliuliza Alonzo na kumfanya Amosi kufikiria kidogo.
Ukweli ni kwamba katika kipindi hicho ni kama matukio ya nyuma alikuwa akiyakumbuka kwa urahisi mno, kwake ni kama matukio hayo yalitokea jana.
Ubongo wake ulikuwa na nguvu sana ya kukumbuka mpaka vitu ambavyo alikuwa amekwisha kuvisahau, hata vile vitu ambavyo havikuwa na msingi sana katika kipindi alichokuwa na Jasmine aliweza kukumbuka, ki ufupi ilikuwa ni kama anaangalia tamthilia ya maisha yake na Jasmine.
“Nadhani nimekumbuka kitu?”Aliongea Amosi na kumfanya Alonzo kumkazia macho.
“Umekumbuka nini?”
“Nilikuwa na mahusiano na Jasmine kwa miezi mitatu pekee kabla ya kurudi nchini kwao Botswana , katika kipindi hiki tulikuwa na furaha wakati wote ila siku moja tu alionekana kunikasirikia sana kiasi cha kubadilika na kuwa mtu mwingine”Aliongea Amosi.
“Nakusikiliza , nini sababu ya yeye kukasirika?” “Nilishika mkufu wake uliokuwa na kidani chenye muonekano wa kipekee”Aliongea Amosi na kumfanya Ajenti Alonzo midomo yake kucheza kidogo.
“Unaweza kuelezea kidogo kuhusu huo mkufu hasa kidani?”
“Kilikuwa kidani flani ambacho kilitengenezwa kwa madini meupe kama kioo kwa juu na ndani kulikuwa na rangi za ajabu zilizojikunja kunja kama wingu linalozunguka na katikati kuna kitu kama kijishimo cheusi , upande wa nje kuna duara za vitu kama nyota , na eneo ambalo mkufu ule ulishikilia kuna alama flani hivi kama sikosei ni kama zile za miungu wa Misri ya kale inayowakilisha uhai na kifo”Aliongea Amosi na kumfanya Alonzo kuridhika.
“Kuna sababu yoyote ambayo ilimfanya kukasirika , jaribu kufikiria kila kitu na uelezee katika jicho la ujasusi”Aliongea na Amosi alifikiria.
“Nakumbuka nilimwambia kwanini amekasirika ilihali nimeushika tu bila kufanya chochote ila hakunipa jibu la kueleweka , moja ya kitu ambacho ni cha ajabu mara baada ya kuona ule mkufu roho yangu ilishikwa na kiu kubwa ya kutaka niouone tena kwa mara nyingine , ilikuwa ni kama nimesahau ulivyo na nilitaka kuuona ili kuanza kuufikiria upya , wakati Jasmine anaondoka nilimsihi kuuona tena ila alinijibu kwamba haukuwa wa kwake na alirudisha kwa mwenyewe na nisahau kama nimewahi kuuona kwake”Aliongea Amosi..
“Sitilii shaka maelezo yako kabisa , kwasababu kilichofanyika katika ubongo wako ni kukuwezesha iwe rahisi kwako kukumbuka matukio yaliopita, Je uliangalia upande wa pili wa Kidani, pia je ulipata nafasi ya kuangalia kidani hicho kwa umbali kidogo?”
“Ilikuwa ni kwa sekunde kadhaa tu na Jasmine alinipokonya, sikubahatika kuangalia upande wa nyuma wala kwa umbali”Aliongea Amosi na jibu lile lilionekana kumnyong’onyesha Alonzo.
“Umejibu vizuri kabisa na nimeweza kupata kila nilichotaka, naomba nikwambie ukweli sasa , sababu ya wewe kuwa katika hali hii ni kwasababu uliona kitu ambacho ni binadamu watatu tu duniani waliowahi kuona , siwezi kukuelezea ulichoona kina maana gani ila wewe ni mtu wa tatu, hii ndio sababu ambayo tulikupa kazi ya kumfuatilia Naomi Lindsey na Rosemary Macha mara baada ya kugundua uliwahi kuwa katika mahusiano na Jasmine Mahmood katika wakati ambao ulikuwa na maswali mengi na kutufanya kuona haikuwa bahati mbaya kwenu kuwa katika mahusiano”Aliongea Alonzo na Amosi alitingisha kichwa.
“Kwanzia sasa utaendelea na misheni yako kama
kawaida , ila malengo yamebadilika , ukishafanikiwa kujua uhusiano kati ya Naomi
Lindsey na Rosemary Macha tutataka kujua wapi Jasmine alipeleka huo mkufu, taarifa za awali zinaonyesha mmiliki wa ule mkufu ni Naomi , hivyo kazi yako ni kufanya uchunguzi je Jasmine aliweza kukutana na mwanamke aliefahamika kwa jina la Rosemary nchini Tanzania na je ndio mwanamke aliefariki kwa ajali ya radi mwaka 2002 , utafuatilia na kujua kila kitu na ndipo misheni yako itaingia katika sehemu ya tatu ya malengo makuu”Aliongea Alonzo na Amosi aliitikia kukubali.
Dakika chache mbele Alonzo aliweza kuachana na
Amosi na alirudi katika ofisi ya Profesa Maya Thema.
“Profesa viongozi walikuwa na wasiwasi na mafanikio ya hii operesheni , lakini kama ulivyowaaminisha imefanikiwa kwa asilimia kubwa”Aliongea Alonzo kwa Lugha ya Kihispania na kumfanya Dokta Maya Thema kutoa tabasamu.
“Nini kimekuaminisha Ajenti?”
“Katika kipindi chote nilichokutana na wagonjwa ambao wamepitia utaratuibu maalumu wa ubongo wao kurekebishwa , wengi wao
walitofautiana katika wingi wa maswali wanayouliza
, lakini kwa Amosi hajauliza swali hata moja”Aliongea.
“Ili kupima asilimia za mafanikio mara nyingi tunaangalia wasiwasi ambao anakuwa nao mgonjwa na tabia kuu ya kuonyesha ni kwa kiasi gani yupo na wasiwasi ni wingi wa maswali anayouliza , ikitokea hajauliza swali hata moja basi tunaweza kusema tumeudhibiti ubongo wake kimawazo kwa asilimia mia moja”Aliongea Profesa na Ajenti Alonzo alitingisha kichwa.
“Nitapeleka hizi taarifa makao makuu , zitaendelea kuimarisha nafasi yako katika umoja , lakini hata hivyo katika wagonjwa wote waliopitia taratibu wengi wao ni kutaka kujua kile ambacho wanajua na wamesahau lakini kwa huyu ni tofauti hivyo Profesa ili aweze kufanikisha kazi ambayo umoja inatarajia kutoka kwake tunataka arudi katika hali yake ya kawaida kwa muda”Aliongea Alonzo na kumfanya Dokta Maya Thema kushangaa kidogo.
“Lakini ni hatari kama tutafanya hivyo , anaweza kupoteza baadhi ya kumbukumbu za maisha yake ya kawaida yaliopita”Alionge.
“Profesa haya ndio maelekezo nilioweza kupata kutoka kwa Askofu , najua njia ipo ya kumrejesha katika wakati wake wa kawaida na kusahau baadhi ya matukio yaliomtokea wakati huo huo tukimdhibiti kihisia ili isitokee akawa msaliti kwa Sinagogu”Aliongea Alonzo na kumfanya profesa Maya Thema kufikiria kwa muda.
“Nilitamani sana kuona maendeleo yake katika mazingira ya kawaida , huyu ndio mgonjwa wangu wa kwanza kuwa na matokeo chanya kwa asilimia kubwa na kuna mengi niliohitaji kujifunza kupitia tabia yake , hata hivyo kwasababu ni maagizo ya Sinagogu siwezi kupinga lakini nikufahamishe njia iliokuwepo kama itafanyika hatoweza kuishi zaidi ya miaka mitano”
“Miaka mitano ni mingi sana kwa Amosi kuweza kutimiza makusudi ya umoja wetu Profesa , nadhani unajua ninachomaanisha”Aliongea lakini licha ya Dokta Maya Thema kuonekana kukubali alionekana kuwa mzito , wito wa kidaktari ulikuwa ukimfanya kuwa na hali ya hatia.Kama Daktari alikuwa na hatia ya kumfanyia Amosi operesheni bila ridhaa yake , lakini hatia ilimshika zaidi mara baada ya kuona anakwenda kufanya procedure ambayo itaweka ukomo wa uhai wa Amosi katika muda wa miaka mitano.
“Kwasababu tunahitaji matokeo ya haraka sina budi , lakini kama Daktari nina masharti pia”Aliongea “Nakusikiliza Profesa”
“Baada ya kifo chake awekwe kwenye orodha ya mpango Genesis 210”Aliongea Profesa Maya Thema na kumfanya Ajenti Alonzo macho yake kuchanua.
“Profesa hiki ni kitu ambacho siwezi kuidhinisha na hata kama nilifikishe kwa viongozi kuna hatua kwa hatua za maamuzi na inaweza kuchukua zaidi ya miezi miwili , nadhani unafahamu ni kwa kiasi gani Mpango Genesis 210 ulivyo nyeti , hatuna muda wa kusubiri mpaka ngazi za juu kufanya maamuzi la sivyo kile kilichosimamishwa kwa miaka mingi baada ya kujitoa kwenye Kanisa kuu kitapotea”
“Huna haja ya kuongea zaidi Ajenti , nimeomba kitu ambacho kinawezekana , mkataba wangu wakati nikiingia katika maabara za shirika niliweka masharti nitalinda haki ya mgonjwa kwa namna nyingine ikitokea umoja unachonitaka kufanya kinakiuka miiko ya kazi yangu , kama Askofu alikuwa mkweli na ahadi zake basi atanikubalia katika hili”Aliongea na kumfanya Ajenti Alonzo kutoa kitambaa na kufuta jasho. “Nitafanya mawasiliano”Aliongea.
******
Saa nne kamili asubuhi ilimkuta Kanali Dastani Mpiji ndani ya Wilaya ya kibaha sehemu ambayo ndio msiba wa Afande Mchuku ulikuwa ukifanyikia.
Watu walikuwa wengi japo sio sana na Dastani hakufika na usafiri binafsi bali alifika na Taksi na hio yote ilikuwa ni kuepuka macho ya watu.
Shida ilikuwa moja tu licha ya kwamba hakutaka macho ya watu mwili wake ulikuwa mkubwa na kumfanya aonekane kama bosi , hususani kutokana na Kitambi chake.
Aliutumia uchangamfu wake kusalimiana na baadhi ya wanaume waliokuwa eneo la msiba huku akitoa pole , licha ya wengi kutomfahamu lakini walimchangamkia , isitoshe Afande Mchuku alikuwa mtu wa watu hivyo watu wengi walimfahamu.
Pembeni ya uwanja palipo wekwa maturubai kulikuwa na nyumba ambayo ilionekana haijamalizika kabisa na kwa haraka haraka fahamu zake zilimwambia lazima ndio nyumba ambayo Mchuku alikuwa akiizungumzia , aliishia kutingisha kichwa na kuona Afande Mchuku licha ya kutumia hila nyingi kujiongezea kipato lakini hela zake hakuzimaliza katika Starehe , ilikuwa nyumba kubwa mno ambayo tayari ishawekwa Grill , Milango na Plasta na kulikuwa na vitu vichache sana vya kumalizia ikiwemo madirisha ya Aluminium , kwa haraka haraka alipiga mahesabu na kujiambia kama Afande Mchuku angepata hela ambayo alitakiwa kumlipa kwa ajili ya kupata rekodi basi angeweza kumalizia jengo hilo moja kwa moja.
“Swahiba poleni na Msiba”Kijana mmoja alimsalimia Kanali Dastani , alikuwa ni bwana wa makamo kama miaka therathini hivi alievalia Kanzu na kibakrashia.
“Asante ostaz tumepoa”Aliongea Dastani na bwana yule alimpita na kuendelea kusalimiana na wazee wengine na mara baada ya kumaliza alirudi kukaa karibu na Dastani.
“Siamini Mchuku ametutoka , watu wema na tegemezi siku zote ndio wanaotangulia”Aliongea Kanali akianzisha maongezi.
“Binadamu siku ambayo anazaliwa mwisho wake umeshaandikwa, watu wote tunazaliwa tukiwa wema, dunia tu ndio inatubadilisha, mwisho wa siku tuwe wema au tuwe wabaya siku ikiwadia haichagui mwema au mtu muovu”Aliongea yule bwana huku akirekebisha kibarakashia chake.
“Nakubaliana na wewe , lakini muda mwingine katika jicho la kibinadamu tunatamani yule ambae ndio msingi wa familia kuendelea kuishi”
“Mwenyezi Mungu ni wa haki na anayajua yote ,
Anawajua Wema na waovu , anamlipa kila mtu na matendo yake , Labda Mchuku amepata kheri ya milele mbali na maumivu ya dunia hii”.
“Huzuni yangu ni kwa wale aliowaacha , alionekana mtu mwenye malengo makubwa ya kimaisha”
“Mwenyezi Mungu awape nguvu na amani katika kipindi hiki kigumu , awe faraja kwao”Aliongea yule Ostaz na kabla hata hajaingiza neno lingine la udadisi kuliibuka kilio cha mwanamke na kufanya karibia watu wote kugeuka na kutokana na kilio cha mwanamke huyo minon’gono iliibuka.
“Uwiii baba Nasra wee! , uwiii , mbona umeondoka mapema hivi mume
wanguu..”Kilikuwa kilio kilichowafanya wanawake waliokuwa wamekaa upande mwingine baadhi yao kumsogelea yule mwanamke.
Upande wa Kanali ni kama tukio lile lilimvutia , ukweli ni kwamba sio yeye tu ambae lilimvutia.
“Ostazi huyu ndio mke wa Mchuku!?”Aliuliza Kanali na kumfanya yule Ostaz kumshangaa kidogo.
“Nilijua una ukaribu na Mchuku”
“Ndio Ostaz, Mchuku ni rafiki yangu mkubwa na pia ni mfanyakazi mwenzake hatujawahi kuongea maswala yetu binafsi”Aliongea Kanali akiharakisha kujitetea.
“Inawezekana , wengi hapa ni watu ambao ni marafiki wa Mchuku , alikuwa mtu mwema, huyo ni mke wa pili ni daktari mwajiriwa huko mikoa ya Lindi”Aliongea yule Ostazi na kumfanya Dastani sasa kujibu kitu ambacho kilimvutia.
Yule mwanamke alionekana mrembo na pili ni aina ya wanawake ambao ukiangalia tu unaweza kujua hadhi yake ya kisomi. Jambo lile lilimfanya Dastani kumfikiria Mchuku kwa namna ya kumsifia, ijapokuwa hakumuona bado mke mkubwa lakini mke huyo wa pili alikuwa mrembo.
“Nasikia jamaa alimwambia mke wake mkubwa akifariki asimlilie”Moja ya Vijana waliokuwa nyuma ya Dastani walikuwa wakiongea na kauli ile ilimfanya masikio ya antena ya Kanali kunyaka mawimbi.
Aligeuka na kumwangalia Ostazi kama na yeye anasikia lakini aliweza kumuona Ostazi akiwa bize kusalimiana na mwanaume mmoja wa makamo ambae alionekana kama Shekh.
“Jamaa si alimwambia hivyo kwasababu alijua muda na saa yoyote ataondoka , licha ya huyu mwanamke kuwa mrembo lakini bado Mchuku alimpenda mke mkubwa”
“Tino wewe ndio huelewi , mchuku alimpenda huyu mwanamke lakini alishindwana nae kutokana na kutotulia , Mke mkubwa alikuwa mvumilivu na mwepesi wa kusamehe”Aliongea mwingine lakini Dastani ni kama hakuwa ameridhika hivi.
“Wadau kwani nini ilikuwa shida ya jamaa mpaka kupatwa na umauti?”
“Bro wewe ni mgeni?”Aliongea kijana mwingine na walionekana kuanza kumchangakia Dastani pengine ni kama wameona jamaa anaweza kuwapa fursa.
“Ni mgeni wa haya maeneo lakini Mchuku ni rafiki yangu wa kitambo , hatujawasiliana kwa muda mrefu na ndio nimesikia habari za kifo chake nikaona nihudhurie”Aliongea Kanali na kuwafanya wale vijana kumwelewa.
“Jamaa alikuwa na Kansa ya mapafu na alidondoka ghafla tu akiwa bar ndio ikawa hivyo”
“Ee bwana ee , sijujua kumbe jamaa alikuwa mgonjwa”Aliongea Kanali.
“Wengi hawakujua jamaa alikuwa mgonjwa , ila waliokuwa wakijua wakimkuta sehemu za starehe jamaa anawaambia anatumia siku zake vizuri za mwisho mwisho maana akhera hakuna bia’
“Jamaa alikiona kifo chake aisee”
“Ndio hivyo bro, jamaa ni kama alijua , nasikia mchana yake alienda kabisa na kumuaga mtoto wake wa kwanza shuleni”Aliongea mwingine huku zile kelele za mke wa pili hazikusikika kabisa.
“Alienda shuleni?”Aliuliza Kanali huku machale yakianza kumcheza.
“Kwa maelezo ya Abduli ndio alivyosema baba yake alimtembelea mchana”
“Dogo atakuwa ameshikwa na huzuni sana , ana miaka mingapi?”
“Ni chalii mdogo kabisa , umri wake sijui ila yupo pale St Joseph Mbagala kidato cha pili , Mchuku alikuwa akijisifia sana na Abduli kwamba ni jiniasi na amerirhi akili zake”Aliongea
“Dastani palepale akili yake ilifanya kazi na kwa haraka aliruhusu akili yake kutizama swala hilo kwa jicho la ujasusi.
“Mchuku alienda shuleni kumtembelea Abduli mtoto wake tena tarehe kumi ya huu mwezi, lazima kuna sababu ya kwenda kumtembelea Abduli katikati ya mwezi , nitaanza na Abduli lazima atanipeleka lilipo faili la sauti , lakini kwanza nijue kama kuna sheria ya kuruhusu wazazi kutembelea watoto katikati ya mwezi”Aliwaza Kanali na muda ule alitoa simu yake akiingia mtandaoni, ilikikuwa ni muda wa chakula na hata wale vijana walimpotezea kabisa na umakini wao waliweka kwenye chakula.
Dastani hakutaka kuungana na waombolezaji kwa ajili ya chakula na aliitafuta namba ya Tresha Noah na kuipiga huku akisogea pembeni nje ya maturubai.
“Huyu malaya kapotelea wapi au kasafiri na Mheshimiwa , Kama kampoteza Amosi ataibeba kesi mwenyewe”Aliwaza Kanali huku aking’ata meno yake kwa hasira kwa kitendo cha Tresha kumzimia simu tokea mara ya mwisho alivyowasiliana nae.
Wakai akiwa pembeni aliona kabisa hana chakufanya lakini hakutaka kuondoka mapema , aliona atafute namna ya kusalimiana na mke mkubwa wa Mchuku pengine anaweza kupata kitu kingine cha ziada katoka uchunguzi wake wa kusaka mahali Mchuku alipoficha rekodi ya sauti.
****
Kapteni Norbert alikuwa haelewi vijana wake wamekosea kosea vipi kushindwa kujua kama Hamza ametoka na kwenda kuua na kurudi bila ya wao kuweza kumuona kabisa wakati akitoka na kurudi.
Jambo hili licha ya kwamba liliwafanya kuona Hamza ni mtu hatari lakini vilevile waliingiwa na hofu maana kwa jinsi Kamera walivyozitega ndani ya eneo lile ilikuwa ngumu kwa mtu yoyote kuweza kuepuka kamera hizo na kupita bila ya kunaswa , kubwa zaidi ni kwamba kijana wao mtehama alikuwa ameweza kudukua Kamera zote zilizokuwa ndani ya jumba la Regina.
Wakati akijua hali ni shwari na vijana wake kumwambia kuwa jamaa alilala kumbe alikwisha kutoka na kusababisha mauaji na kuondoka kimya kimya na asubuhi akiwa katikati ya kulifurahia tendo la ndoa anaanza kufokewa na wakuu wake wa kazi kwa kutokuwa makini kupitia simu kitu kilichomfanya kughailisha kumwagiliwa ua.
Licha ya kwamba Norbert aliona ni kosa kwa vijana wake kutokumuona Hamza wakati akitoka lakini vilevile aliona ni kama wakuu zake wanamuonea bure , maana ndio hao wakuu wanaomchekea Mstaafu akiendelea kumchokoza Hamza kupitia genge lake.
Hakupatwa na huzuni yoyote ya kifo cha Kanali mstaafu Fanueli Yowe wala Afande Sucre , ukweli ni kwamba alishaachaga kuwaheshimu tokea muda mrefu japo Afande Fanueli wakati akiwa mafunzoni ndio aliekuwa mkufunzi wake.
Norbert licha ya kwamba alikuwa akitumikia mfumo ambao ulikuwa umeharibiwa na watu wenye tamaa na siasa chafu lakini bado hakusahau wajibu wake kama mwanajeshi , katika jeshi iwe ni la polisi au ulinzi kazi yake kubwa ilikuwa ni kutii maagizo lakini licha ya hivyo hakuwahi kujichukulia kama mtumwa wa maagizo machafu ya wakubwa wake.
Wakati akitoka nyumbani kwake akielekea kazini alikuwa akimshukuru Hamza kwa namna moja ama nyingine kwa kufanya kazi ambayo ilipaswa mwanajeshi kama yeye ambae anapenda haki kuifanya, lakini kwa jicho la usalama aliona alichokifanya Hamza ni kosa na anapaswa kuadhibiwa.
“Muda mwingine tunahitaji vichaa kama hawa kuendelea kutusafishia nchi”Aliwaza wakati akiagana na mke wake.
Wakati akiwa njiani mkuu wake alimwambia haina haja ya kufika kazini bali aelekee moja kwa moja kwenda kumkamata Hamza na apelekwe kituoni.
Hilo halikuwa tatizo kwake na aliitikia kwamba atafanya hivyo , lakini ilimshangaza wakati akiwa ndani ya viunga vya hospitali pamoja na timu yake wakimsubiria Hamza na Regina kufika hapo kumuona Mgonjwa ili amkamate anapokea taarifa ya pili kutoka kwa mkuu wake.
“Achana nae”
“Mkuu ni achane na nani?” Norbert aliuliza akiwa kwenye simu mara baada ya bosi wake kuwa na kauli moja tu ambayo ilikaa kiswahili sana.
“Nimekuambia achana nae , kipi huelewi Norbert , rudi na watu wako kituoni mara moja kuna kazi nyingi za kufanya”Upande wa pili simu ilikatwa na kumfanya Kapteni Norbert kushangaazwa na kauli ile na muda uleule ni kama hakutaka kuamini
kauli ya mkuu wake wa kazi na alitoa simu yake ya kawaida na kuitafuta namba.
“Umefanikiwa?”Sauti upande wa pili ilisikika.
“Nimepokea maagizo mengine , Mkuu anasema niachane nae”Aliongea.
“Kwanini!?”
“Sijajua ila nimepewa kauli moja tu na anaonekana kukasirika sana”
“Kukasirika ni lazima , Fanueli alikuwa rafiki yake wa karibu sana”
“Najuua lakini Afande hili ni swala la kisheria pia , kwanini niache kuondoka na mhalifu?”
“Norbert nadhani unapaswa kumsikiliza mkuu wako wa kazi kwasasa , kama amekuambia achana nae lazima ni maagizo kutoka juu, unatakiwa
kutii ili kulinda uhusika wako mwingine, mimi pia namuunga mkono”
“Lakini Mkuu”
“Hakuna cha mkuu Norbert fanya hivyo”
“Sawa Afande”
“Vizuri”Sauti upande wa pili ilisikika na simu ilikatwa palepale, muda huo huo ndio Norbert aliweza kuiona Mercedenz Benz Maybach ikiingia hospitalini hapo na aliweza kujua moja kwa moja lazima ni bosi Regina maana ni Watanzania wachache wa kutembelea magari ya bei ghali namna hio.
“Hata kama wakuu wanamuogopa siwezi kumuogopa, pengine bosi wake hata hajui alichofanya usiku”Alijiwazia Norbert huku akishika pingu zake na kuwapa ishara wenzake na kumsogelea Hamza na Regina , sio kwamba alikuwa akikiuka maagizo bali alitaka kumpiga mkwara Hamza na pili kuhakikisha Regina anajua kama mtu anemwita msaidizi wake ni muuaji.
Ukweli ni kwamba licha ya Norbert kuona matukio kadhaa ya Hamza akidhihirisha uwezo
wake lakini bado nafsi yake ilikuwa ikipinga kwanini dogo mzembe mzembe kama huyo anatikisa hadi watu wazito , kila akikumbuka mafunzo makali aliopitia jeshini na kupewa nishani za kila aina kutokana na ukakamavu wake alijikuta akipandwa na hasira kumuona Hamza mzembe mzembe ndio anaabudiwa, hali ya ujivuni kwa kujilinganisha na Hamza ilimvaa.
“Mr Hamza upo chini ya ulinzi kwa kosa la mauaji’Aliongea kibabe akitaka kumfunga Hamza pingu lakini Hamza hakuwa mzembe wa kukubali mikono yake ifungwe pingu kizembe.
Regina ambae alishitushwa na kauli ile ya Norbert alijikuta akirudi katika uhalisia , alikwisha kumjua Norbert ni polisi pamoja na wenzake licha ya kuvalia kiraia.
“Afande subirini kwanza”Aliongea Regina huku uso wake ukizidi kuwa na usiriasi na alimkinga Hamza kwa mbele.
“Madam unazuia jeshi la polisi kufanya kazi yake”Aliongea Norbert huku kwa namna flani akionyesha heshima mbele ya Regina , peingine uzuri wa mwanamke huyo ulimfanya kukosa kujiamini kiasi, pengine siku hio ndio mara yake ya kwanza kuona uso mzuri wa Regina kwa ukaribu hivyo, kwenye maisha ya kiraia Regina alihesabika kama mtu adimu kuonekana.
Ilikuwa ni ngumu sana kumuona Regina kutokana na kwamba akitoka kazini maegesho ya magari yapo chini ya jengo na gari lake lilikuwa na vioo visivyompa mtu nafasi kuona aliekuwa ndani.
“Kama wewe ni polisi nadhani unajua ni kosa kisheria kutaka kumkamata mtu bila kibali , isitoshe Hamza hawezi kuwa muuaji . bila Waranti hamuwezi kumkamata na hamuwezi kuongea nae chochote pasipo ya kuwepo mwanasheria wangu , hii imekuwa tabia yenu polisi kukiuka haki ya uhuru wa raia”
“Sheria hio hio inatuambia tunaweza kumkamata Muuaji bila ya kibali , mbele ya muuaji kwanini tujali uhuru wake”Aliongea Norbert huku hali ya kuanza kujiamini mbele ya mrembo Regina ikirudi upya.
Regina kabla ya kuendelea kubishana na polisi alimgeukia kwanza Hamza na kumwangalia , ukweli ni kwamba kutokana na namna ambavyo Norbert alikuwa akijiamini na vilevile siri ambazo Hamza alikuwa akimficha alijikuta akipatwa na wasiwasi kidogo na kupoteza msimamo.
“Kamuua nani , kwanini mnasingizia watu asubuhi asubuhi , mnadhani kuua ni rahisi?”Aliongea
Regina na Hamza kauli ile ilimfanya aone kama Norbert ataendelea kuropoka basi itakuwa ni taarifa kubwa kwa Regina.
“Regina tangulia kamuone bibi kwanza , nitadili na hii hali”Aliongea Hamza na kumfanya Regina kukunja mikono yake na kumwangalia hamza kwa macho ya kikauzu.
“Wamesema umemuaa mtu ni kweli?”
“Sikia Regina tangulia kwanza kwenda ndani , tutaongea vizuri baadae”
“Kwanini , kama hujaua kuna haja gani ya kuongea na mimi baadae?”Aliongea Regina alikuwa na wasiwasi mno na alitaka Hamza aseme hajaua.
Ijapokuwa alimuona Hamza kama mtu ambae alikuwa na maisha yake kabla ya kukutana nae na historia yake kwa ujumla haijawa wazi lakini kitendo cha kuandikisha ndoa yao ni kama alijihisi kutaka kuwajibika kwakile ambacho kinamzunguka Hamza.
Nafsi yake ni kama ilikuwa ikimwambia hakuwa tayari kuwa karibu na mtu ambae ni mbalifu tena sio mhalifu wa kawaida bali mhalifu wa makosa ya kimauaji.
Upande wa Hamza aliona yupo katika wakati mgumu , ukweli ni kwamba tokea afike nchini amekuwa akijitahidi kujificha ili asionekane sio wa kawaida hata kujipa usumbufu na kuanza masomo ya chuo ambayo hayakuwa na faida yoyote kwake zaidi ya kupoteza muda.
Alitaka kuwa na maisha ya kawaida kabla ya kukaribia kupata kumjua mzee ni nani , historia yake ya maisha ilianzia Tanzania ndio maana alifika nchini Tanzania lakini kama mwenyewe alivyosema muda ni fumbo, saa na siku hio alikuwa kwenye mtego mwingine.
Hakuua makusudi iwe amefanya kama mfanyakazi wa Regina au kama mtu wake wa karibu yote juu ya yote hakutaka kuona mwanamke huyo akiendelea kukumbwa na hatari , alitaka kutoa onyo ambalo linaweza kueleweka kwa wale wanaomuwinda, kama amekubali kuandikisha cheti cha ndoa na mwanamke huyo na bibi yake kulazimisha swala hilo kufanikiwa basi ilikuwa pia ni jukumu lake kumalizia kila kitu na sio kufanya vitu nusu nusu , alikubali kuandikisha cheti kwa ajili ya kumlinda lakini hata kama amefanikisha hilo bado kuna hatari nyingine ambazo ni yeye ambae alipaswa kuzimaliza.
“Ndio nimemuua mtu jana”Aliongea Hamza huku muonekano wake ukitoka katika hali ya uzembe na sasa kuwa kama mtu mwingine ambae amekuwa mtu mzima ghafla , hata Aura yake ilibadilika mara moja.
Jambo lile lilimfanya Afande Norbert kushangaa na kujiuliza inakuwaje mtu anaweza kubadilika kwa dakika chache namna hio , lakini kitendo cha Hamza kukiri ilimfanya hasira kumvaa na kupata kibali cha kumkamata.
Upande wa Regina mara baada ya kusikia kauli hio ya Hamza alijikuta akipiga hatua kadhaa kurudi nyuma kana kwamba alikuwa ameona hatari mbele yake.
Kichwa chake ni kama hakikuwa kikifanya kazi vizuri na ghafla tu kilimsahaulisha na kuanza kujiuliza Hamza ni nani.
Comments