Reader Settings

Frida  alijua  kabisa anakwenda kufa na kifo chake kuja kuwa utata , aliweza kuona kilichokuwa kimemkaba kooni ni kivuli lakini hakuweza kufanya chochote.

Kwa mtu wa  kawaida unaweza useme  Frida alikuwa amepatwa na ukichaa au ugonjwa wa ajabu lakini ukweli ni kwamba kuna nguvu iliokuwa ikimkaba kupitia kivuli.

Wakati akiwa amekata tamaa  ghafla tu ule utulivu wa kile chumba ulitoweka , ilikuwa ni kama upepo umeongezeka kwa kiasi kikubwa  na kufumba na kufumbua kivuli kile kilipotea na kumfanya  Frida kuanza kukohoa kwa nguvu , mpaka anakuja kutulia alijikuta akishituka mara baada ya kugundua kuna mtu mwingine ndani ya chumba chake alievalia joho la rangi nyeusi, alitaka kupiga yowe lakini mtu yule alimpa ishara ya kutulia.

“Wewe ni nani?”Aliuliza Frida  kwa sauti ya chini huku akiwa ameshika shingo yake , ilikuwa bado hakuamini kama alikuwa amepona.

“Msimamizi wako na mlinzi wako mpya”Aliongea kwa lugha ya kingereza na kumfanya Frida kuchangayikiwa.

“Sikuwa na msimamizi na mlinzi , kwanini unajitambulisha kama  mlinzi wangu mpya , nataka kujua unatokea upande upi , Wiccan au Sinagogu?”Aliongea  Frida  kwa sauti kubwa kidogo.

“Mimi ni  mu’ alkemi kutoka  makao makuu ya Wiccan , nipo hapa kwa maagizo ya  Madame, mlinzi wako wa zamani amepoteza maisha”Aliongea na kumfanya  Frida kuzidi kuchanganyikiwa lakini mara baada ya kusikia mtu huyo  yupo  hapo kwa maagizo ya Madame alipata ahueni.

“Mlinzi wangu wa zamani , unamaanisha mlinzi gani?”

“Alietaka  kukuua  amemuua mlinzi  wako , kwanzia sasa  utakuwa chini ya ulinzi wa binadamu”Aliongea   huku akisogea karibu na mlango.

“Nilikuwa na mlinzi kivuli!!?”

“Wewe ni  wa muhimu sana kwa Madame kuwasiliana na waumini wa ulimwengu wa nje ya kivuli , kwa namna yoyote  unapaswa kuwa salama”Aliongea.

“Kwanini alitaka kuniua?”Aliuliza Frida, alikuwa akijua  mtu ambae alitaka kumuua  ni kivuli au watu ambao  wamepata umaarufu kwa jina la Night Shadows(Vivuli vya watu  vinavyoonekana usiku).

“Sina majibu kuhusu   swali lako lakini nina ujumbe kutoka makao makuu”Aliongea kama roboti.

“Ujumbe gani?”

“Hakikisha  anatumia  mshumaa kurekodi ndoto zake  ndio utakuwa salama, kadri atakavyoota bila ndoto zake kurekodiwa mtiririko wa  matukio utakosekana na mpango wote kuingia dosari”Aliongea.

“Unamaanisha  Ha…”

“Sikutajiwa  jina , huu ndio ujumbe kutoka makao makuu  unaopaswa kufanyia kazi”Aliongea yule bwana. Frida alitaka kuuliza swali zaidi  lakini alijua asingepata majibu.

Yule bwana alievalia joho la rangi nyeusi mara baada ya kuridhika  kwa kuona Frida alikuwa ameelewa aliaga.

“Wakati wowote ukiwa katika hatari na kuhitaji msaada wangu tamka neno , Grishav nitaitikia wito  wako”Aliongea  na palepale  bila  ya Frida  kujibu aliinama  chini  na kufumba na kufumbua alipotea.

Frida alijikuta akiingia katika maswali mengi na swali kubwa lilikuwa juu ya ule mshumaa , alijua maelekezo yale yalikuwa yakimlenga Hamza lakini alishangaa mara baada ya kuambiwa  Hamza anapaswa kutumia mshumaa ule ili kurekodi ndoto zake.

Swali  ambalo alijiuliza inakuwaje mshumaa ambao alipatiwa na Dokta  Genesha  kuwa na uwezo  wa kurekodi ndoto , kitu ambacho  Wiccan walitaka  iwe hivyo , inamaana  kuna mpango uliokuwa ukiendelea kati ya Dokta Genesha na  Wiccan kiasi cha kumkabidhi Mshumaa wa Nuru kwa ajili ya kumpatia  Hamza.

Frida alijiuliza ni kitu gani ambacho kinaendelea  yeye hakijui na kwanini amenusurika katika kifo.

Alikumbuka kwamba asipofanikisha Hamza kutotumia mshumaa basi atakuwa hatarini lakini swali lingine liliibuka inamaana Hamza alikuwa akiota bila  ya kutumia ule mshumaa.

Kitu ambacho  Frida alikuwa akijua ni kwamba mshumaa  ule ulikuwa ni kwa ajili ya kumletea Hamza ndoto  tu ili kujua  maisha yake ambayo ameyasahau , hayo ndio yalikuwa maelekezo kutoka kwa Dokta Genesha  na hakuelezwa kwamba  mshumaa ule ni kifaa cha kurekodi ndoto, alijiuliza kama ni hivyo kinarekodi vipi hizo ndoto , ni sayansi ya namna gani ambayo imetumika.

Alijikuta hata usingizi ukimpelea kabisa licha ya kwamba alijihisi uchomvu mkubwa , hofu ilimvaa na hisia zake zilimwambia pengine  anachofanya  sio kuhatarisha usalama wake tu bali anahatarisha na usalama wa Hamza.

“Sina jinsi kwasasa  lazima  nihakikishe Hamza anatumia  mshumaa ili kuwa salama ,  wakati nikitafuta  majibu ya maswali yangu yote.  Lakini nitafanya nini kumfanya atumie mshumaa kama  yeye mwenyewe haniamini  vya kutosha mpaka kuutumia?”Aliwaza Frida.

******

Hamza mara baada ya  Side  na wenzake kuondoka alibakia na mrembo  Dina , wote wawili hawakuwa na ile mudi  ya kwenda floor za juu kwa ajili ya  kulewa vileo  na kufanya starehe zingine kama kucheza  kamari.

Kitu pekee ambacho Dina alipenda  ndani ya Club hio ni  kutumia siraha kulenga shabaha na hata Hamza alikuwa akipenda kitu kama hiko , kwake hakuwa mpenzi sana wa  vileo na kucheza disco.

Walitumia zaidi ya lisaa limoja  na nusu  kulenga shabaha kwa kutumia  bunduki za aina mbalimbali.

Ilipotimia saa tano kasoro  njaa  zilikuwa zikiwauma na  Hamza alipendekeza warudi Kijichi ndio wakapate chakula huko  na Dina hakupiinga.

Mara baada ya kufika kijichi  chakula kiliandaliwa na wote wakaanza kula pamoja.

“Unaonaje  baada  ya hapa  ukaangalie maendeleo ya vijana wangu , tokea siku ile ulivyowafundisha  kiasi namna ya  kucheza Karate na Kung Fu hukuwaona tena”Aliongea Dina.

Hamza kipindi kabla ya kukutana na Regina alikuwa ameshawahi  kuwafundisha vijana wa  Dina mafunzo ya Karate na Kung Fu mara moja na hakuwahi kwenda tena kuwaona.

“Hakuna shida , kuna kitu pia nataka kwenda kukifanyia mazoezi”Aliongea Hamza.

“Kitu gani , ni kuvuna  nishati za mbingu  na ardhi au kitu kingine?”Aliuliza Dina kwa shauku  alikuwa  akijua Hamza ana mafunzo ya kuvuna nishati  za nguvu ya asili ya ardhi na mbingu na alitamani kujifunza pia siku moja.

“Hutoelewa  hata nikikuambia ni kama maneno ya kutamka nataka kuyafanyia majaribio”Aliongea Hamza.

Ukweli ni kwamba  kitu ambacho alikuwa akienda kufanyia majaribio ni  yale maneno ambayo 

Yonesi alimtajia  wakati akiwa  hospitalini , siku ile wakati akifanya tahajudi kwa kupitia yale maneno aliona sura ya mwanamke ambae anamuona  katika ndoto , bado shauku yake juu ya tukio lile haikuwa imeisha na alitaka kwenda kujaribu tena.

Baada ya kumaliza kula  Hamza alitoka akiongozana na Dina pamoja na Lawrence  na kwenda katika  ukumbi maalumu ambao ni kama  eneo la mafunzo ya kimapigano.

Hakukuwa na matumizi ya siraha , ilikuwa ni  sehemu ambayo   watu wa Dina walikuwa wakijifunza  namna ya  kupigana kwa kutumia mbinu mbalimbali za sanaa ya mapigano , eneo hilo lilikuwa likitambulika hata kwa serikali na lilikuwa na kibali  kabisa.

Ni eneo ambalo  lilijengwa  katika mgawanyo wa sehemu mbili ,  sehemu ya kwanza ilikuwa ni   kwa kufanyia mazoezi ya kawaida kama Gym  na  mazoezi ya boksa, Karate  na Judo  upande mwingine ulikuwa ni wa tahajudi.

Katika  sanaa ya mapigano  tahajudi ilikuwa ni sehemu ya mazoezi kwa ajili ya kuujua mwili wako ulivo, ukifanya tahajudi kama binadamu utajuwa wapi  kuna udhaifu wako na wapi nguvu zako zinakaa kwa wingi na namna  gani ya kushinda udhaifu wako.

Hamza mara baada ya kuona vijana wa  Dina wakichukua mazoezi aliridhika , aliweza kuona wengi walikuwa wamepiga hatua kwa kufuata maelekezo yake.

“Bro , unapanga kufanya mazoezi ya namna gani , unataka kufanya tahajudi?”Aliuliza Lauwrence  mara baada ya  kumuona Hamza akichagua upande wa wanaofanya Tahajudi.

Dina na Lawrence siku zote walikuwa na shauku ya kutaka kumuona Hamza akichukua mazoezi hivyo walimwangalia.

“Kaa kimya  Lau acha maswali mengi”Aliongea  Dina akimzuia  Lau kutokumsumbua Hamza na maswali yake.

Kutokana na wale wanafunzi kumuona Hamza na wao wote waliacha na kumpatia Hamza nafasi , kwao ni kama kuna kitu ambacho walitaka kujifunza kwa kumuangalia ndio maana walisimama pembeni.

Wakati Hamza akiwa katika mkao wa kufanya tahajudi  huku midomo yake ikicheza  ghafla tu  watu wote walijikuta wakikumbwa na msisimko wa ajabu , ilikuwa ni kama kuna kiumbe cha ajabu kimefika ndani ya eneo hilo na kuwafanya kuanza kushindwa hata kupumua vizuri huku  eneo ambalo Hamza alikuwa amekaa  anga lake ni kama lilikuwa likitingishika.

Dina alijikuta jasho  la paji la uso likimtoka huku akimwangalia Hamza kwa wasiwasi , alipatwa na  hisia kama vile  Hamza amekuwa mfalme  ghafla na yeye ni kijakazi  wake.

Upande wa Hamza hakuwa hata akielewa kilichokuwa kikiendelea  kwa nje , kama alivyotarajia maneno yale  yalikuwa ni kama  anamwita yule mwanamke , mara ya kwanza wakati  alivyofanya kule wodini  alimuona kwa mbali yule mwanamke , lakini wakati huo kadri alivyokuwa akiimarisha umakini wake wa ubongo  na kuzidi kuyatamka yale maneno  alimuona ni kama vile yule mwanamke mchawi anaemuona kwenye ndoto alikuwa  akimsogelea kutoka angani kwa spidi ya ajabu.

Zilipita kama dakika nne  tu yule mwanamke  aliweza kumuona kwa  ukaribu zaidi, lakini jambo  ambalo lilimshangaza Hamza  ni kitu ambacho alikuwa ameshikilia mkononi.

Kadri alivyokuwa akizidi kuongea yale maneno mwanamke yule alizidi kusogea , lakini ilifikia hatua ni kama hawezi kumfanya asogee zaidi  na yule mwanamke ni kama alijua Hamza hawezi kumuita karibu zaidi na alichokifanya ilikuwa ni kunyoosha kile kitu alichoshikilia mkononi mwake  na Hamza mara baada ya kuangalia vizuri alijikuta akipagwa , ulikuwa ni ule mshumaa ambao  Frida alimpatia akimwambia umetoka  kwa Dokta Genesha, Mshumaa wa Nuru.

Hamza alichanganyikiwa mshumaa wa nuru kwanini upo katika mikono  ya  huyo mwanamke , katika ndoto  yule mwanake alimuona kama  mchawi ambae anachomwa moto baada ya kukamatika lakini kwanini akashika kitu cha  nuru ilihali  nuru na uchawi ni vitu viwili tofauti.

Yule mwanamke ni kama alikuwa akitaka Hamza amsogeze karibu aweze kushika ule mshumaa ,  upande  wa Hamza alionekana kusita kuupokea  ule mshumaa  na yule mwanamke  ni kama aliliona hilo  na alitamka  neno kwa kunyanyua mdomo wake kwa juu bila kutoa sauti akihakikisha Hamza anasoma lipsi zake.

NISAIDIE!(Help me)

Ndio neno ambalo aliongea huku  akimpa ishara Hamza kupokea ule mshumaa.

Muda uleule Hamza aliacha kutamka yale maneno  na kitendo kile kilifanya yule mwanamke ni kama vile kuna nguvu iliokuwa ikimvuta na kuzidi kurudishwa nyuma mbali na yeye , lakini bado hakuacha kumnyooshea  ule mshumaa kama ishara ya kumuomba  amsaidie.

Muda ileule wakati kila mtu akiwa ameloa jasho  kana kwamba eneo lote limekumbwa na joto kali  Hamza aliweza kufungua macho yake  huku akionyesha hali ya kuwashangaa  waliokuwa wakimwangalia .

“Nini kimetokea, Dina  mbona upo hivyo?”Aliuliza Hamza mara baada  ya kumuona 

“Bado tu unapata muda wa kuuliza , ni kitu gani  ulichokuwa ukifanya?”Aliuliza  Dina na  kumfanya Hamza sasa kuelewa kilichokuwa kikiendelea , licha ya yeye mwenyewe kuwa na wasiwasi lakini aliishia kucheka.

“I am sorry !, hii ni mara yangu ya kwanza kujaribisha hiki kitu , sikuweza kujizuia kile kinachonizunguka”AliongeaHamza na kisha alipiga hatua kuondoka   katika eneo hilo.

Na wakati wakianza kutembea ndio sasa waligundua  paa la   jengo hili lilitingishika sana  na  kutokana   na mchwa kula mbao unga unga ulidondoka chini kwenye tailizi na kila walipokuwa wakipiga hatua walikuwa wakiacha nyuma alama za miguu.

“Muda umeenda sana , nataka nirudi nyumbani”Aliongea Hamza.

“Hamza ni mafunzo gani yale , ni nguvu ya ndani   au nishati ya mbingu na maji?”

“Ilianza mbingu ikaja  ardhi  halafu  mbingu ikaleta  maji na uhai , hizi ni kanuni za mafunzo ya nishati  za mbingu na ardhi na  ni kitu   ninachoweza kufanya pia , lakini kuhusu nilichofanya sasa hivi  hata sijui ni kitu gani , kama nilivyosema nipo kwenye utafiti”Aliongea Hamza  

“Hata jina lake hujui?”Aliuliza Dina kwa mshangao.

“Ndio ila kwasasa  nitaiita hii kama Wito, kwasababu ukiifanya ni kama kuna kitu unakiiita”

“Huwa haifurahishi  kusikiliza pekee”Aliongea  Dina kwa  macho yaliojaa  huzuni  na shauku.

“Usiongee hivyo , hiki ni kitu ambacho siwezi  kukuruhusu ufanye kabla sijakipatia majibu , nguvu yake ni kubwa kiasi kwamba ni kama sijakula kabisa”Aliongea Hamza  huku akijihisi ni mwenye njaa kali.

Dina alimwambia twende ukale na Hamza hakuwa na aibu ya kukataa kwani alikuwa na njaa , muda huo hawakurudi  kwenye mgahawa bali Hamza alienda mpaka  yalipo makazi ya Dina  mita kadhaa kutoka mgahawa wake ulipo na  mfanyakazi aliagizwa kuandaa chakula na Hamza alikaa chini na kuanza kukifakamia huku  Dina akimwangalia kwa macho yaliojaa  mahaba.

“Unajua  nilishangaa baada ya   mstaafu Mgweno kunipigia simu  akisema yaishe”Aliongea Dina. “Kwanini yeye ndio kakupigia simu?”,

“Unaweza kushangaa , licha ya kwamba  kwa nje inaonekana familia ya  Benjamini  ndio inataka Regina kuolewa na  James lakini  upange mwingine  ni mipango ya  Mheshimiwa Mgweno”Aliongea Dina.

“Unataka kumaanisha nini?”

“Labda utakuwa  hujui  tu , ila kampuni ya Dosam  ni kubwa Tanzania  na inachangia  zaidi ya asilimia tatu ya pato lote la Taifa , imeshikilia  uchumi  wa nchi katika maeneo nyeti, Benki namba  moja  ya  kibiashara inayoongoza kwa Tanzania  na Afrika  mashariki yote ni Dosam Commercial  Bank  huu ni  kama utawala wa mzunguko wa fedha nchini , hapa bado hujazungumzia usafiri wa anga ,  mahoteli  na usambazaji wa bidhaa  mbalimbali kwa  matumizi ya  majumbani, Kabla ya mheshimiwa Mgweno hajaingia  madarakani  Kampuni ya Zena ilikuwa   ya kawaida tu kulinganisha  na  Dosam lakini  baada ya Mgweno kuingia madarakani ilikua kwa spidi ya hali ya juu na yote hii ilikuwa ni  uwekezaji mkubwa ambao  mheshimiwa alifanya kwa kuiba hela za wananchi”Aliongea Dina.

“Kwahio unachomaanisha ni kwamba  kampuni ya 

Zena inamilikiwa na  Mheshimiwa mstaafu Mgweno?”

“Ndio  kwa asilimia zaidi ya  arobaini na tisa, ukifuatilia wana hisa wa kampuni ya Zena utagundua  wengi wanaomiliki hisa hizo ni kampuni kutoka nje ya nchi , ukifuatilia kampuni hizo nje ya nchi utagundua  kwamba  ni kampiuni ambazo zimepewa haki kisheria ya kumiliki  hisa hizo na kampuni nyingine , mzunguko unaendelea hivyo hivyo, zote ni njama za Mgweno kuficha  wananchi kwamba anaimiliki Zena , sio  kampuni moja tu , kila  kampuni  kubwa ana ushawishi wa kimaamuzi”

“Zote hizo ni hela za rushwa!?”

“Ndio lakini hakuna ushahidi wa kuthibitisha kama ndio mmiliki,  sehemu pekee ambapo amekosa  umiliki na ushawishi ni kampiuni ya Dosam peke  yake na hii ni kutokana na msimamo wa aliekuwa   kuongozi wa kampuni  yaani babu yake Regina”Aliongea Dina na sasa ni kama Hamza alikuwa akipata picha.

“Kwahio  anajaribu  kuitumia familia ya  Benjamini

kwa ajili  ya kuingiza ushawishi wake  katika kampuni ya Dosam?”

“Ipo  hivyo , mwanzoni walijua  mambo yataenda sawa kama  Regina atakubali kuolewa na James  lakini mambo yamekuwa magumu , Regina karithi tabia zote za  waanzilishi wa ile  kampuni”

“Unamaanisha  bibi yake na babu yake,  unachoongea kinaonekana kuwa sahihi”Aliongea Hamza.

“Mgweno anachotaka ni kuimiliki  Tanzania katika kila nyanja , kwanzia  mtandao wa biashara  haramu , biashara  halali na  kisiasa , hii itaifanya familia yake kuwa  ya  kifalme  na raisi ni kama waziri mkuu tu anaepokea maagizo kutoka kwao”

“Kama ndio anachowaza  anajidanganya , kuna mifano  mingi ya kihistoria  ni ngumu sana kuuchimba msingi wa nchi  na kutengeneza nyufa   pasipo kushitua wamiliki wake”

“Pengine anaelewa  ila  anaona ni kheri kujaribu kuliko kufa bila ya kujaribu”

“Kwahio baada ya kuona   familia ya mzee Benjamini imekwama  njia pekee alioona ni kumuua Regina maana  urithi  utaenda  kwa mtoto  wa pili?”

“Ndio lakini mipango  yake inaonekana kukwama  kutokana na uwepo wako , niseme tu umetibua  mambo mengi sana , najua  hata kunipigia simu ni kutokana na kujua ukaribu wetu na anatangeneza mazingira ya kujihami, lakini kwa wanaojua  Mgweno  kuna kitu lazima anapanga, walijaribu  hadi mbinu ya  kutaka  kumtengeneza  mtu wao ambae yupo karibu zaidi na Regina”Aliongea Dina na kumshangaza kidogo  Hamza.

“Unamaanisha wale wazee ambao Regina amewafurumusha?”Aliuliza.

“Huo haukuwa mpango ,  wale wazee walikuwa wakifahamika tokea  kipindi kirefu wapo kinyume na uongozi wa  Regina”

“Ni nani ambae walikuwa wakimlenga?”

“Mchepuko wako alieniingiza kwenye matatizo”Aliongea  huku akivuta midomo”

“Eliza!?”

Dina alitingisha mabega  lakini kabla  ya Hamza hajauliza swali lingine  mlango wa kuingilai uligongwa kwa nguvu  na Lawrence alionekana  akiingia kwa pupa.

“Kuna nini Lawrence?”Aliuliza.

“Nimeletewa taarifa muda huu  na vijana ,

Mheshimiwa Jongwe  amefariki  dunia kwa  ajali ya gari  na  jeshi la polisi limeishikilia familia ya Mzee  Seif  kama  washukiwa namba moja”Aliongea  Lawrence na habari ile ilimtoa  macho  Dina. “Unamaanisha  mgombea  wa kiti cha uraisi kupitia chama tawala , Jongwe amefariki, tena kwa ajali , kwanini familia ya mzee  Seif ihusishwe kama ni ajali?”Aliongea Dina.

“Inawezekana sio ajali ya kawaida”Aliongea  Hamza.

“Kwa maelezo niliopatiwa gari ambayo alikuwa amepanda imelipuka na ndani yake alikuwa ameambatana na Mzee Martin”Aliongea  Lawrence na  alivyoongea ni kama alijua taarifa ile itamshitua bosi wake na ilikuwa  kweli kwani  Dina alijikuta akisimama  akiwa kama haamini.

“Mzee Seif na Mzee Martini mbona kama ushawahi kunitajia hawa watu?”Aliuliza Hamza.

“Ndio Bro hawa ndio  washirika wetu wakubwa, japo  mara nyingi inaaminika  Mzee Seif  ana uadui wa kisiasa  na  Mzee Martini”Aliongea Lawrence.

“Kwanini inaaminika hivyo ?”

“Kwasababu wote ni wanasiasa wa vyama tofauti , 

Mzee Seif ni  kutokea chama cha upinzani na 

Martini ni kutoka chama tawala na  wamekuwa  wakipishana kama wabunge katika  jimbo moja kwa zamu , uchaguzi huu akishika mzee Martini  mwaka mwingine  anashika   Mzee Seif , awamu hii  inayoisha  Mzee Seif  anamaliza muda wake lakini  uelekeo wa kura  upo   upande wa Mzee Martini ,

siasa zao   mara nyingi ni za kurushiana maneno”Aliongea Lawrence.

“Kwahio jeshi limemkamata Mzee Seif kwa kuamini kwamba  ametegesha bomu katika gari la  Mzee Martini ili ashinde  uchaguzi , kama ni hivyo  mgombea wa uraisi wa chama tawala  kwanini  amekufa pamoja na   Martini?”Aliuliza Hamza lakini   ni kama alikuwa akiipata picha.

“Lazima kuna kitu Mgweno anajaribu kufanya , hizi zote ni hila za kutaka kubomoa  mtandao wa Chatu”Aliongea  Dina kwa hasira.

“Lakini Madam  Mheshimiwa Jongwe  ni mgombea ambae amepata sapoti kubwa kutoka kwa  mheshimiwa Mgweno ,  kwanini afanye hila  ya kumuua mgombea ilihali zimebakia wiki chache kabla ya wananchi kupiga kura”

“Kesho kutwa pia ndio ilitarajiwa  mkutano  wa mwisho wa chama tawala kufanyika ili kufunga kampeni”Aliendelea kuongea  Lawrence.

“Kuna picha inanijia akilini”Aliongea Hamza lakini upande wa  Dina alionekana kuwa katika majonzi ya kumpoteza Mzee Martini, alikuwa ni moja ya mhimili wa mtandao wake.

“Lawrence polisi wanamshikilia  kituo gani Mzee Seif?”

“Nasikia hawajamkamata  bali  wameizingira nyumba yake huko Kigamboni Mbutu B”Aliongea Lawrence.

“Yaani  baada ya  dakika kadhaa mlipuko kutokea  na kuua watu, tayari washafikia   maamuzi  Mzee Seif ndio muhusika , mbona haingii akilini , hii lazima ni njama ya kutaka sisi twende tukamsaidie”Aliongea  Dina.

“Tena nina uhakika  hata hao wanaoitwa polisi  ni feki”Aliongea  Hamza huku akiweka kijiko chini.

“Madam tunapaswa kufanya nini?”Aliuliza  Lau. “Kama ninachofikiria  ni sahihi lazima hili linahusiana na kikao  nilichofanya  na mheshimiwa  Mgweno siku kadhaa zilizopita ,  mtandao wetu wote unajua ni kwa namna gani Mzee Seif  alikuwa mwaminifu , nisipoingilia   na kulifanyia hili  maamuzi unadhani nitaonekanaje ,  Lawrence kusanya  vijana  wote  ambao hawako mbali tutaenda kuangalai kinachoendelea”Aliongea Dina.

“Lakini Madam ulitoa  maelekezo ya vijana karibia wote wakae chimbo , waliopo  karibu na mjini  hawazidi hata hamsini?”

“Haina haja”Aliongea Hamza huku akisimama.

“Watu hamsini ni wengi sana na  hili linaweza kuwa ni mtego , hebu ita wale  kumi  kutoka  jumba la mazoezi  waje hapa , wanatosha sana” “Bro unataka  na wewe…”

“Hamza na wewe unataka kwenda?”

“Nataka nikajionee kinachoendelea , kama  kweli  huu  mpango kaupanga Mgweno basi  atakuwa katumia akili ,  unadhani  kwa katiba yao ya chama nini kinafuata mara baada ya mgombea  mkuu wa chama kufariki ghafla?”Aliuliza Hamza.

Previoua Next