Reader Settings

 

SEHEMU YA 62.

Kitendo cha Hamza kuonyesha kuishangaa ile picha kama vile mtu  huyo anamfahamu ilimpa na   Dina shauku ya kutaka kujua  ni nani, baada ya kuangalia na kuona ni mwanaume wa kizungu aliekuwa amevalia mavazi ya  kifungwa huku akiwa na kipara  alimwangalia Hamza.

“Unamjua  huyu ni nani?”Aliuliza Dina.

“Naweza kusema ndio namfahamu , lakini hata nikuelezee ni nani  huwezi mfahamu, kinachonishangaza sio  kwamba huyu ni nani  bali ni  kuitwa mfungwa wa muda mrefu”Aliongea Hamza.

“Unamaanisha  nini?”Aliuliza Dina  akiwa hajamuelewa Hamza kabisa.

“Unadhani  kuwa mfungwa wa muda mrefu ni kama miaka mingapi hivi?”

“Inaweza kuwa  miaka ishirini na zaidi”Aliongea Dina na kauli ile ilimfanya Hamza kutabasamu , lakini tabasamu lake lilikuwa na maana flani hivi.

“Kama hii sura ni ya mtu ninaemfahamu mimi  basi huyu hajawahi kuwa mfungwa na kama ni kweli  alikuwa mfungwa hapa Tanzania basi aliamua  kulifanya  Gereza makazi  yake ya muda mrefu”Aliongea  na kauli ile ilimfanya Dina kushangaa na kujiuliza kuna mfungwa wa aina hio , yaani wa kuweza kukaa   ndani ya gereza  kwa hiari yake.

“Kwa unavyoongea , kama kweli kahusika kumuua mgombea wa uraisi , unadhani jeshi la polisi litaweza kumkamata?”Aliuliza Dina.

“Kwa asilimia tisini  nina uhakika  hawatoweza kukamata hata kivuli chake”Aliongea Hamza  na kumfanya Dina kumwangalia Hamza kwa shauku , alitamani kumjua huyo  mtu ni nani lakini kwa muda huo alishindwa kuuliza hata kwa Lawrence hivyo hivyo.

Keita yeye hakuwa akijua kiswahili, hivyo hakuweza  kusikia  wanachozungumza ni kitu gani.

Hamza alionyesha kuridhika na ile picha na kisha alimrudishia yule bwana aliemkabidhi  simu.

******

Upande wa  Las Vegas Big  alionekana kuwa na wasiwasi mno , zilikuwa zimepita dakika kumi na tano na kadri dakika zilivyokuwa zikiongezeka  ndio jasho lilivyozidi  kumtoka.

Mara baada ya simu yake kunguruma ikiashiria kuna ujumbe uliongia haraka haraka aliangalia na kukuta ni wa Keita.

“Bosi tumesamehewa…”Ndio ujumbe ulivyosomeka kwa liugha ya kingereza na kumfanya  Big kupumua kwa nguvu ikionyesha amepata  ahueni.

Ijapokuwa Keita alijiingiza mwenyewe katika anga za bosi wake lakini alikuwa akiomba  asiuliwe , katika watu ambao amefanya nao kazi na waliomwingizia pesa ndefu  na wenye ufanisi wa hali ya juu ni Keita, hivyo kama angekufa kwake ingekuwa hasara.

“Mr Mamen , huyo  mwanaume kutoka Tanzania ni muhimu  sana kiasi hicho , hii hoteli  pamoja na Casino vyote ni vyako , kwanini unamuogopa  sana?”Aliongea yule mwanamke wa kizungu , alikuwa ameshasikia mtu aliekuwa akiongea nae  yupo Tanzania.

“Acha kuongea ujinga , huna unachokielewa”Aliongea  Bonge kwa kufoka huku  akimsukumia pembeni maana mudi ilikuwa ishapotea tayari.

“Hebu kwanza ondoka , sitaki huduma yako tena”Aliongea Big na mara baada ya yule mwanamke kusikia kauli hio kama nyoka alijikumbatisha katika mwili wa  Big.

“Usifanye hivyo mpenzi , bado nina mbinu nyingi ambazo sijakuonyesha bado”

“Sitaki tena  mbinu zako”Aliongea Big huku akinyoosha mkono wake kwenye kimeza na kuchukua  sigara moja katika pakti na  kuiwasha kisha kuanza kuvuta.

Yule  kahaba  wa kizungu  aliona ni kama  mpango wake wa kupata maokoto umevurugika  na lawama zote alimpelekea Mtanzania aliekuwa akiongea na Big kwenye simu , isitoshe mpaka kupata nafasi ya kumhudumia Big   alikuwa amefanya juhudi kubwa za kujilengesha.

“Haya yote ni kutokana na huyu  Mtanzania , yeye ndio kaniharibia  na kukufanya  kukosa mudi ya  kuendelea na mimi ,  Mr Mameni  wewe ni  mtu mzuri  sana kwake lakini kwanini inaonekana hakujali kama rafiki , kama ni kweli anakuheshimu asingekutafuta  muda mbovu kama huu”Aliongea akilalama

Kitendo cha kusikia kauli ile kutoka kwa huyo mwanamke , hasira  zilimvaa Big palepale na alimkaba shingoni.

“Arghhhhhh..!”

Kahaba  yule wa kizungu alijikuta akihangaika  kujinasua kutoka kwa Mamen lakini hakutaka kumwachia.

“Wewe mwanamke mpumbavu sana , wewe ni nani mpaka kumsema vibaya bosi wangu”

“Mr Mameni nisamehe , sikujua  unamheshimu kiasi hicho , naomba usiniue”Aliongea kwa  kuomba lakini Mameni hakuwa na mpango wa kumwachia kabisa na alizidi kumkaba.

“Kumheshimu? , huyo  mtu kwangu ndio imani”Aliongea  akimaanisha Hamza kwake ndio imani  yake na mara baada ya kauli ile alikaza mkono  na kuizungusha shingo ya yule mwanamke na palepale  alilegea.

Big hakuwa na hatia hata kidogo , baada ya kuona amekwisha  kumuua yule mwanamke aliupiga mwili teke na kudondokea chini kwenye Zuria la kiajemi  na kisha  bila ya nguo alitoka kitandani na kwenda kusimama katika dirisha huku akivuta  moshi mwingi wa sigara.

Katika macho yake alionekana kama mtu ambae ameingia katika kumbukumbu ya maisha  yaliopita.

 

******

Hamza alimsamehe Keita  na kumwambia aondoke  Tanzania na watu wake mara moja na  aachane na maswala ya  madili ya siraha katika  ardhi hii.

Keita alishukuru kusamehewa na kwa haraka sana aliongoza watu wake na  kutoweka  katika eneo hilo huku wakifuta ushahidi  wote  wa wao kuwepo nchini.

Kuhusu  maswala yaliobakia   alimwachia Dina adili nayo , kutokana yamekaa sana kisiasa na hakutaka kujiingiza huko.

Dina alitoa maelekezo ya Mzee Seif  kupelekwa Safehouse kwa muda  mpaka  mambo yatulie na vijana wake  walifanya kazi hio.

“Unapanga kufanya nini?”Aliuliza Hamza mara baada ya kungia kwenye gari , alitaka kujua ni hatua gani ambayo  Dina atachukua kuhusu swala la kifo cha  mgombea wa uraisi.

“Mpaka sasa  nimeshindwa kuamini kama Eliasi ameenda mbali  namna hii mpaka kumuua mgombea wa uraisi tena wa chama chake huku yeye akiwa mwenyekiti wa Chama, kuna  kitu kinaniambia hili hajalitekeleza yeye peke yake , pengine kuna nguvu ilionyuma yake”

“Unamaanisha nguvu ambayo inataka kumpindua  Mgweno?”Aliuliza Hamza.

“Ndio , Eliasi ninaemjua mimi sio jasiri kiasi hichi , ijapokuwa Mgweno  amekuwa  akiitawala hii nchi  nyuma ya pazia lakini  haimaanishi  ana nguvu kila mahali, katika uongozi wake alikuwa na maadui zake pia  na ndio namna ambavyo  hata mtandao wetu wa Chatu uliweza kuendelea kuwepo  licha ya kuupiga vita kwa kipindi kirefu akitaka kuumiliki”Aliongea Dina.

“Kwa ninavyoona kwasasa huu ni mpango ambao haujaisha bado ,  muuaji kakimbia  na sidhani kama wanaweza kumpata tena , pili  upande wa Keita mpango umevurugika kwa asilimia kadhaa , kama unavyosema ni sahihi basi  nina uhakika pengine  Keita alikuwa  Plan B  ya mpango mzima”Aliongea Hamza na kumfanya  Dina kidogo kushangaa.

“Unataka kumaanisha nini?”

“Wewe hebu chukulia , kazi kubwa ya  Keita ilikuwa  nini  katika huu mpango , ni kumtorosha  muuaji lakini Keita  amemkosa muuaji  hii maana yake walikuwa wakiujua uwezo wa muuaji  kujitorosha yeye mwenyewe”

“Vipi kitendo cha kutaka kunisingizia mimi kama muhusika?”Aliuliza Dina.

“Ni kukujulisha kinachoendelea kabla ya kukisikia kwenye  taarifa ya habari , yule  Pancho alikuwa chambo tu”Aliongea Hamza na kumfanya Dina kuanza kufikiri.

“Maana yake ni kwamba  hata kama ningeenda mwenyewe ningeweza kuujua ukweli kutoka kwa Keita?”

“Nina uhakika huo licha ya kwamba ingekuwa ngumu, lakini kama ni kweli basi  nguvu iliopo nyuma ya Eliasi  inamtafutia udhaifu pia”Aliongea Hamza na upande wa  Dina  mara baada ya kuanza kufikiria  kimantiki, ni kama sasa anaanza kuelewa pointi ambayo Hamza analenga.

“Babu aliweza  kuulinda mtandao wa  Chatu   kwa kuushikilia  udhaifu wa mheshimiwa  Mgweno  lakini hili  lililotokea leo pia nimepata ushahidi wa  Eliasi  kupanga njama na kumuua  mgombea wa kiti cha uraisi  , hii maana yake  Eliasi  na Mgweno wote  wapo kiganjani  kwangu, kuhusu nani atarithi nafasi ya Jongwe lazima atakuwa  upande wa Eliasi na kuna uwezekano  pia amehusika  katika  huu mpango.Kama ni hivyo  basi napata picha nani yupo  nyuma ya  Eliasi” Aliongea Dina kana kwamba anajaribu kuunganisha matukio na kumfanya Hamza kutabasamu.

“Naamini atakuwa yule raisi wa Rwanda”Aliongea Hamza  huku akimshika Dina kiuno.

“Wewe umajuaje?”

“Babe si ushawahi kuniambia babu yako alifanikisha kumfunga  mikono Mgweno kutokana  na kumtengenezea udhaifu wa kashfa ya  kuuza rasilimali za nchi nchini China kwa ajili ya kumuokoa mtoto wake  na mpango ulisukwa na   rafiki yake mkubwa    raisi wa Rwanda”Aliongea Hamza  na kumfanya Dina kuitikia  kwa kichwa huku akimwangalia Hamza kwa macho malegevu.

“Huyu mzee anataka kuitawala Afrika mashariki nzima , naona anajaribu kumuweka raisi  anaemtaka madarakani huku wakati mmoja akiizima nguvu ya  Mgweno ambae ni adui yake mkubwa”Aliongea Dina.

“Mtu  wa nje anaweza  kuona ni kiongozi mwenye akili sana , lakini upande mwingine wa shilingi sababu ya kuwa na mipango mingi ni kutawala kwa muda mrefu na kuamini nchi  ni yake na anajaribu kila namna  kuiendeleza licha ya  kuwa na rasilimali chache”Aliongea Hamza huku akitabasamu na Dina alitingisha kichwa kukubaliana nae.

“Mbona huniulizi swali lolote  licha ya sura yako kuoneysha ina maswali mengi?”Aliongea Hamza mara baada ya kuona Dina alikuwa akimwangalia sana.

“Ndio nina maswali mengi kwa kilichotokea leo  lakini   kwasasa naona  ngoja lipite”

“Ukiuliza nitakuambia  kila kitu”Aliongea Hamza.

Ukweli aliona  Dina sio  Regina anaweza kumweleza kila kitu  na  wala asipate mabadiliko zaidi ya ushangaa tu.

“Kwasasa sitaki kujua vitu vingi , nahisi bado sina vigezo ,  siku za baadae nikijihisi  kustahili kukujua  nitakuuliza, sitaki kujua sasa hivi inaweza  kunifanya niwe na mawazo kwa kuona tuna gepu kubwa  kati yetu”Aliongea Dina na kumfanya Hamza kutabasamu , hakudhani Dina angekuwa na mawazo ya namna hio.

Mpango wa Dina ilikuwa ni kujiimarisha  zaidi  uwezo wake binafsi , alikuwa  akijua  kuna mbinu nyingi za kuwa na uwezo mkubwa ikiwemo  mbinu za kujifunza kanuni za  mbingu na ardhi , kuamsha nguvu ya ndani,  uchawi na  mengineyo.

Hamza alikwua ni mtu ambae anaamini ana mafunzo ya  nishati za mbingu na ardhi  na alitaka  ajifunze kutoka kwake  na kufikia  hatua ambayo atajiona yupo  tayari kumjua Hamza.

Kutokana na muda  ulikuwa umeenda Hamza hakupanga kurudi  nyumbani , ukweli ni kwamba   angetaka kurudi ingekuwa rahisi tu maana alikuwa karibu na  mji wa kisasa wa Egret  lakini aliamua kurudi Kijichi na mrembo   Dina.

Mara baada ya  kufika nyumbani hakukuwa na chakufanya zaidi ya kwenda kulala ,  kulikuwa na  vyumba vingi  vya wageni ndani ya  jumba la mrembo huyo lakini  Dina alilazimisha walale pamoja.

Hamza licha ya kukubali   alijitahidi asimfanye chochote mwanamke huyo, baada ya Dina kuuliza maswali kibao kuhusu namna ya  kuwa bora katika  eneo la mapigano na  kujua  nguvu iliojificha katika mwili wake hatimae alipotelea usingizini , lakini upande wa Hamza kama mwanaume  rijali ilikuwa ngumu kwake kulala , alijikuta akikaa macho mpaka   kunakucha.

*****

Wakati ikiwa ni siku nzuri kwa watu wengine  upande mwingine haikuwa siku nzuri kabisa kwa mheshimiwa  mstaafu Mgweno.

Taarifa ya kifo cha mheshimiwa  Jongwe aliweza kuzisikia usiku  wa manane saa saba  na  tokea apate taarifa hizo hakuweza kupata  usingizi kabisa ,  kwanza anaanza vipi kupata huo usingizi , kitendo cha  kuuwawa na bomu kwa   Jongwe  tena akiwa ndani ya  gari  ilimaanisha kuna mtu anataka kumpindua  ki nguvu ndani ya  Tanzania , jambo ambalo hakuwa tayari  kuona  likitimia, lakini  hata hivyo  kama ilikuwa kweli  aliona  wanaotaka kumpindua walikuwa wamepiga hatua.

Usiku mzima kwa kuambizana na msaidizi wake Jonathani  Machete  walipanga kila aina ya mpango wa kurudisha  hali  hio katika mstari wake. Hata mtoto wake ambae alikuwa  kwenye  siasa akifuata  nyayo zake alimpigia simu kumweleza kile kinachoendelea.

“Baba tunafanyaje  juu ya hili swala?”Kijana huyo  aliuliza  kwa  wasiwasi mkubwa , nafasi yake ya Uwaziri mkuu alikuwa akiona ikienda na maji.

Kitu ambacho Mgweno alikosea ni kukubaliana na Eliasi  Mbilu kwamba  kutokana na yeye kuweka mtu ambae ni chaguo lake  kuwania kiti cha uraisi  basi Mbilu yeye  ataweka  makamu wa raisi  ambae ni chaguo lake , sasa wakati huo alipokaa chini na kufikiria aliona   kabisa alijipiga risasi mguuni , ilionekana Mbilu tokea muda  mrefu  alikuwa na mipango ya kumuweka raisi anaemtaka madarakani kwa namna yoyote ile.

“Bakari   wahi  nyumbani asubuhi ,  kwasasa sina cha kukuambia”Aliongea Mheshimiwa.

“Sawa baba, nitapanda ndege binafsi kufika   asubuhi na mapema”Aliongea Bakari  Mgweno , alikuwa  nyumbani kwao  mkoani  ambako ndio jimbo   analogombea  lilipo , kama angetaka kuwa Waziri Mlkuu ilimpasa  kushinda kwanza ubunge.

Mheshimiwa usiku huo mara baada ya kukata simu  alimgeukia  Jona Machete ambae alikuwa bize.

“Vipi Machete  umefanikiwa kuwasiliana nao wote”

“Ndio mheshimiwa nimetoa taarifa na  wote asubuhi watakuwepo  kwenye kikao”Aliongea  Machete na kumfanya  Mheshimiwa  kukaa kwenye sofa huku akionekana kuwaza , bado hakuonekana kuridhika licha ya hatua ya kwanza  kuichukua.

“Kabla ya asubuhi kuingia wasiliana na  meneja wa Benki  wa Sychelles  napaswa kujiandaa kwa lolote”Aliongea Mheshimiwa.

“Sawa Mheshimiwa”

Mgweno kuna kila hisia mbaya ambayo ilikuwa ikimtawala, alijua  fika  Eliasi alikuwa akihusika katika hili lakini ushahidi wa moja kwa moja hakuwa nao.

“Mheshimiwa,  Bi Zalha anasema  ameshindwa kuunganisha mawasiliano na mheshimiwa Eliasi”Aliongea Jona  akipokea simu kutoka  kwa Zalha katibu wake  ndani ya ofisi ya mheshimiwa mstaafu Oysterbay.

“Ametoa sababu  ,inawezekana vipi raisi wa nchi kutopatikana hewani”

“Wanasema mheshimiwa kapata dharula ya kiafya, yupo chumba cha uangalizi  katika hospitali ya Rufaa  ya Gleneagles  nchini Malaysia”Aliongea Jona  na kumfanya  Mgweno kutoa tabasamu la kifedhuli.

“Eliasi ana maigizo sana , ila   hajui  kwamba  mimi ni mtoto wa mjini  na  ndio nilimwingiza Ikulu”Aliongea huku aking’ata meno kwa hasira na  Jona aliishia kukaa kimya.

“Wasiliana  na IGP  nahitaji  taarifa kutoka kwake sasa hivi juu ya mshukiwa wa mauaji”Aliongea  na Jona  dakika ileile alifanya mawasiliano  na  mara baada ya simu kupokeleiwa alifowadi kwenda kwa simu ya mheshimiwa

“IGP yupo hewani mheshimiwa”Aliongea na Mgweno  alitoa simu yake  na kupokea   haraka  haraka na kuweka sikioni.

“Mheshimiwa nadhani tumewasiliana  dakika ishirini zilizopita”Sauti upande wapili iliongea.

“Sanga  tumekubaliana kila baada ya dakika  kumi unanipa ripoti , dakika ishirini zimepita naona kimya”Aliongea.

“Mheshimiwa   hakuna ripoti ya kukupatia  mpaka  sasa , vijana wapo eneo la tukio , maiti  ya mheshimiwa Jongwe  na Mzee Martini  pamoja na dereva zimefikishwa  hospitalini kwa ajili ya kuhifadhiwa”

“Nataka ripoti  Afande , kwanini  Jongwe alikuwa kwenye gari la Martini  tena usiku  akiwa hana  ulinzi  wa kutosha?”

“Msaidizi wake namba  mbili  hakuwa na taarifa ya mheshimiwa kutoka , kuhusu msaidizi wake namba moja mpaka sasa hatujapata taarifa zake, hakuwepo kwenye ajali ya  gari lakini pia nyumbani kwake hayupo”Aliongea IGP akiwa mpole lakini upande wa  Mgweno aliishia kung’ata  meno yake kwa hasira.

Katika taarifa ya tukio  hili ilisemekana  Mheshimiwa  Jongwe  alikuwa  nyumbani kwa  mzee Martini  na  wakati wa kuondoka alitoka na  Martini na ndipo  gari yao  ilipolipuka mara baada ya kusafiiri kwa umbali wa kilomita  nne kutoka nyumbani kwa Martini, swali   lilikuwa moja , licha ya kwamba inafahamika  Martini na Jongwe ni marafiki lakini ilikuwaje Jongwe akatoka nyumbani kwake  bila ya wasaidizi wake kujua  na akaenda kwa  Mzee Martini.

Mheshimiwa alijiuliza maswali mengi  lakini  aliamua kufuata ule msemo wa  ‘The dead  have no tales to tell’ yaani mfu hana stori tena ya kusimulia.

Sasa  akiwa ameshapanga mikakati ya kuchukua , hatimae asubuhi ikaingia akiwa hajalala kabisa  na muda huo  alikuwa akisubiria viongozi  waliokuwa upande wake ndani ya chama  kufika nyumbani kwake kwa ajili ya kikao cha siri na cha dharula kabla  ya kifo cha Jongwe kutangazwa,alikuwa amezuia kifo hicho kisitangazwe kabla ya muafaka wa kuamua nani  aingie  Ikulu.

Saa mbili kamili ilikuwa ndio muda wa kikao  lakini ajabu mpaka inafika saa  mbili na nusu  viongozi waliofika  kwa ajili ya kikao walikuwa saba tu  tena watatu kati yao wakiwa sio wale wenye vyeo vikubwa  kwenye Chama.

“Jona mbona  hawajafika  mpaka muda huu , una uhakika ulifanya mawasiliano nao?”

“Ndio mheshimiwa  na niliwapa muda sahihi  wa kikao ni saa mbili kamili”Aliongea Jona  na kumfanya  mheshimiwa kuanza kuzunguka  chumba kama vile amekuwa kichaa.

“Kuna  jambo   halipo sawa, hebu ongea na vijana wafuatilie sasa hivi unipe majibu”

“Mheshimiwa  pengine wamechelewa  tu  , kwanini tusiwape muda angalau nusu saa?”

“Jona  mimi sio mjinga kukuambia  ongea na vijana  wafuatilie , umeanza lini  kwenda  kinyume na ninachoagiza?”Alifoka mstaafu.

“Nitawasiliana na vijana mara moja mheshimiwa”Aliongea  Jona na kutoka katika   sebuleni  na muda huo alipishana na mke wa Mstaafu akingia akiwa amebeba  Trey.

“Mgweno punguza  wasiwasi , hebu  kunywa chochote kwanza  ndio  mengine yafuate”

“Mama  Bakari unadhani  kwa kinachoendelea  nina muda wa kuweka kitu mdomoni?”Aliongea akiwa  kakereka na kumfanya   Mama Rahma kuweka ile Tray kwenye meza na kuanza kuandaa.

“Mume wangu hivi  sio namna nilivyokuzoea, tumekuwa pamoja kwa muda mrefu na tumepitia makubwa kuliko hili  na kipindi chote hicho  hukuwahi kupoteza  utulivu  wako , wewe mwenyewe unamwambia Bakari kila siku hatua ya kwanza  ya kutatua tatizo ni kujipa utulivu lakini naona unaenda kinyume na maneno yako”Aliongea  na muda ule  ni kama amekumbushwa  kuhusu  Bakari.

“Kuhusu Bakari mpaka sasa hivi hajafika  tu?”Aliuliza

“Baba nipo hapa , hebu kwanza angalia taarifa ya habari”Sauti ya mtu kuingia   ndani ya  sebule hio mkuku mkuku ilisikika.

“Bakari kuna  nini?”Aliongea mama yake lakini Bakari alikuwa mwepesi mno kuikimbilia rimoti  ya TV na  kuweka taarifa ya  habari.

Kitendo cha  Mstaafu Mgweno kuona ile habari alijikuta vigoti vya miguu  vikilegea , ilikuwa ni habari  ya kifo cha Jongwe  mgombea wa Chama,  licha ya kwamba  Mgweno hakuruhusu  taarifa hizo kutolewa  kilichomlegeza ni sababu ya  kifo cha  Jongwe.

Kulingana na   uchunguzi wa jeshi  la polisi   wanasema ni kweli mheshimiwa Jongwe amefariki na  wamethibitisha  mhusika  mkuu ni  Yohana Kamote  msaidizi namba mmoja wa mheshimiwa  Jongwe, polisi wanasema wamemkuta Kamote  hotelini akiwa amejinyonga na kuacha  wosia , akisema kwamba mheshimiwa Jongwe  alimuiba mpenzi wake  Janeth yaani mke wa  Mheshimiwa  Jongwe , Kamote anadai alikuwa kwenye  mapenzi na Janeth kabla ya kuolewa na  Jongwe  na mapenzi yao yaliendelea  hata wakati Janeth  akiwa  ameolewa tayari  na wamezaa mtoto mmoja ambae anafahamika ni wa Jongwe , Kamote anasema Janeth alianza kubadiika baada ya  mume wake  kupewa dhamana  ya kupeperusha  bendera ya Chama  na  kutokana na wivu  ameamua  kumuua  Jongwe na  kujiua yeye mwenyewe kumkomoa  Janeth, Polisi wanasema Janeth  ameshikiliwa na jeshi la polisi kwa ajili ya  mahojiano kuthibitisha  kama  kuna ukweli juu ya  maneno ya Marehemu  Kamote.

Mstaafu Mgweno alijikuta akinyong’onyea , upande wa Mama Rahma pia hata ile mudi ya kumlazimisha  mume wake kunywa chai haikuwepo kabisa.

“Jamani mama Lebroni nili…!!”

Mke wa Mstaafu alijikuta akiropoka  na kumfanya Bakari  na  mume wake kumwangalia kwa macho yaliojaa maswali.

“Mama  unajua nini?”Aliuliza  Bakari na  Mama Rahma alianza kumwangalia  mume  wake kwa wasiwasi.

“Mama Bakari unajua nini ,  mbona huongei unaniangalia , usiniambie kinachosemwa na Polisi ni cha kweli?”

“Mume wangu naomba unisamehe  sikukuambia  kuhusu hili maana sikuwahi kuona ni muhimu , ni kweli nimejua muda mrefu  Janeth alikuwa akitembea  na Marehemu …”Alijikuta akishindwa kuendelea kuongea na kuanza kulia.

Mgweno   alitamani kumvamia  mke wake  kumdunda  lakini  Bakari alionekana kuwa makini na baba yake  kumsogelea mama  yake , sio kwamba alikuwa akimtetea mama yake , lakini  baba yake alikuwa na tabia ya kumpiga mama yake na hakuwa akipenda.

Mgweno  hakutaka kusikiliza neno lingine na alitoka ndani ya sebule hio na kuelekea  moja kwa moja kwenye  ukumbi wa  mikutano lakini mara baada ya kuona hakuna  ambae ameongezeka alijikuta hofu ikimwingia.

“Mheshimiwa  kuna ujumbe wako”Sauti ya  Jonna ilisikika na  kumfanya  mstaafu na  wale waliokuwa ndani ya  ukumbi  kumwangalia   Jona kwa shauku.

“Taarifa imefika ofisini kwako  asubuhi hii ,  unahitajika kwenye kikao  cha  dharula cha Halmashauri kuu  ya Chama , saa tatu kamili  ndio kinaanza ukumbi wa makao makuu”Aliongea Jonna.

“Kikao  saa tatu kamili  taarifa naeletewa saa  mbili na nusu , Jona  nini kinaendelea?”

“Mheshimiwa hata mimi nimeshangaa ila  ni Zalha ndio kafikisha hii taarifa”Aliongea  Jonna  na  mheshimiwa alimwangalia  msaidizi wake kwa  udadisi na hakuongea neno alihisi harufu kubwa ya usaliti kwa vijana  wake aliowaamini.

“Ahirisha hiki kikao , tunaelekea makao makuu”Aliongea Mgweno huku akitoka  ndani ya eneo hilo  kwa  pupa.

Kuna  jambo alikuwa akiliwaza katika akili yake lakini  hakutaka kulipa kipaumbele  kwa wakati huo ,  alitaka kuwahi kwanza maana kama akichelewa na maamuzi yakifanyika hata  kama  ana ushawishi mkubwa hatokuwa  na uwezo wa kupinga maamuzi ya watu wengi.

*****

Hamza  asubuhi na mapema  alikuwa ashaondoka  nyumbani kwa Dina.

Siku hio mpango wake ni kwenda kazini na kisha akutane na Eliza amweleze kuhusu ndoa feki aliofunga na Regina.

Hamza  hakutaka kabisa kumkosa Eliza lakini aliona sio vizuri pia kumdanganya.

Baada ya kufika  ndani ya kampuni   alikuwa amewahi sana na hata Eliza hakuwa amefika bado , hivyo  hakuwa na chaguzi zaidi ya kwenda ofisini kwake  na kuangalia kazi ambazo anapaswa kufanya.

Na mara baada ya kufika tu Linda alionekana kumtafuta  na alimwangalia Hamza kwa ukauzu  mkubwa.

“Umekuwaje wewe , unasiku ngapi  hujaripoti kazini na kwanini unachelewa , yaani  bosi kafika wewe ndio unaingia kazini?”Aliuliza  Linda kana kwamba yeye ndio bosi.

Hamza alitaka kumwambia  mwanamke huyo yeye ni nani wa kumpandishia ilihali   amemuoa  bosi wake  ila  alijizuia.

“Nilikuwa na maswala binafsi ndio maana?”

“Hii ni tabia gani unayojaribu kuonyesha,  maswala binafsi ni ya kwako na  hayapaswi kuingiliana na maswala yako ya kazi , usijione kwasababu unajua  watu  maarufu  ndio unaweza kufanya  chochote kile unachotaka”Hamza alifokewa na  alijifanyisha mzembe kama kawaida na kutingisha kichwa lakini upande wa Linda  ni kama hajaridhika aliishia kuchukia mara baada ya kuona hakuna dalili ya woga  kabisa kutoka kwa Hamza.

Alikuwa na  kila haki ya kukasirika, wote na Hamza walikuwa nafasi sawa  lakini yeye muda wote alikuwa bize kuhakikisha  ratiba za bosi  wake zinaenda sawa , sasa  Hamza ambae wapo nafasi sawa anafanya   anachotaka , aliishia kumwangalia  Hamza kwa  macho mabaya  na kisha aligeukia  ofisi ya bosi wake na kwenda ndani.

Regina  muda huo alikuwa ameshafika kazini  tayari  na aliwahi kwani  alikuwa na viporo vingi vya  kufanyia kazi.

Hata pale  jana aliporudi na kutokumkuta Hamza nyumbani wala hakujali kabisa  na kila alipohisi kupandwa na hasira alijiambia  cheti chao cha ndoa ni kwa ajili ya kupata hisa za bibi yake tu na hakuna kingine.

“Bosi…”Aliita Linda kwa unyenyekevu mara baada ya kuingia katika ofisi ya Regina na aliongea mara baada ya Regina kumwangalia.

“Kuna tatizo nataka kukushirikisha”

“Tatizo gani?”Aliongea Regina huku akirudisha  macho yake kwenye karatasi aliokuwa akiangalia.

“Ni kuhusu Hamza”Aliongea  Linda na kauli yake ilimfanya  Regina mikono yake kutetemeka kidogo na kisha alimwangalia  Linda kwa shauku.

“Nini kimemtokea?”

“Anaonyesha  tabia ambayo si nzuri kazini ,  kwanzia siku ziliozopita anafika kazini kwa kuchelewa na siku zingine haonekani kabisa na hakuna taarifa , tukimuacha akiendelea kama hivi  ni taswira mbaya kwa kampuni”

“Unaona  tumfanye nini sasa?”Aliuliza  Regina lakini   Linda kidogo alishangaa maana   ni mara chache sana kwa Regina kuuliza swali kama hilo , ki ufupi alikuwa na majibu kwa kila kitu.

“Naona ni vizuri tukimfukuza tu”

“Hapana”Aliongea Regina  haraka na kumfanya Linda kuinamisha kichwa chake  chini kwa  kusikitika

“Bosi  ni  kwasababu anafahamiana na Master Alec?”

“Hapana , ni  kwasababu hawezi kuachishwa kazi”

“Lakini…”

“Unaonaje tukifanya hivi .. muandalie kazi  ambazo zinahitaji muda na nguvu ,  wewe mpe  kazi  hakikisha muda wote ana kitu  cha kufanya”Aliongea  Regina  na Linda alikubali na kutoka ofisini.

Linda  akiwa  kwenye  ofisi yake alikuwa ashaona ni kazi gani ambayo  anapaswa kumpatia  Hamza, kulikuwa na kesi mbalimbali ambazo zimetoka  kwenye kampuni tanzu   na moja ya kesi  iliokuwepo  ni kutoka  idara ya Sales and Business development  , walikuwa wakitoa  taarifa juu ya kampuni ya  Dede kutoka  Bagamoyo  wamepitiliza siku za kulipa pesa wanaozodaiwa na  walijaribu kufanya  mawasiliano na kampuni hio lakini  wametoa taarifa kwamba watalipa  kwa Cash  na  anaepaswa kufuata hayo malipo ni Eliza  meneja wa idara ya mauzo.

Kipindi ambacho kampuni  ya Dede inaingia  katika tenda ya kibiashara  na  Dosam dili hilo lilisimamiwa na meneja wa idara ya mauzo yaani Eliza, lakini kutokana  na  Dede kukosa  kiasi chote cha pesa waliomba  kufanikishiwa tenda  yao  na watalipa  kiasi kilichobakia katika muda wa  miezi   mitatu na Eliza aliweza kuidhinisha.

Ilikuwa ni ngumu  kuona  kampuni inamuwekewa masharti mtu ambae amemkopesha , hii ni  kwasababu ya nguvu ya kampuni hio ya Dede , ndio kampuni ilioaminika  kuongoza  kwa utapeli , ilikuwa kampuni ambayo inamilikiwa na Mmasai  na huyo mmasai alikuwa akiaminisha wamasai wenzake kwamba hio ni kampuni ya kabila lao.

Sasa  ilishangaza wamiliki wa kampuni hio kumtaka  Eliza ndio akachukue  malipo , ilionekana ni kama kuna mtego, sasa mara baada ya Linda kukumbuka Hamza anajua  mbinu kadhaa za mapigano aliiona ni kazi ambayo  inamfaa sana.

“Linda   kuna kazi ninayopaswa kufanya?”Aliuliza Hamza  mara baada ya kumuona Linda akiingia ofisini kwake.

“Ndio ila sio kutafsiri kama ulivyozoea , leo kuna kazi nyingine nje ya ofisi, kuna malipo yetu ya mwisho ya mwisho ya mauzo  na tunaowadai wanataka  twende tukachukue  Cash”

“Kwanini mimi nikamilishe hayo malipo , hii ni kazi ambayo  inapaswa kufanya na idara ya mikopo  , ya fedha au  mauzo kwanini  niwe mimi?”Aliuliza Hamza.

“Upo sahihi lakini  kampuni tunayoidai kidogo ina upekee wake , hivyo tusipomtuma mtu ambae  sio makini anaweza kupata matatizo, umeonyesha una  uwezo wa kupigana , hivyo  utaenda kama bodigadi   kuhakikisha  Meneja Eliza hapati shida”Aliongea Linda.

“Ni kampuni gani?”Aliuliza Hamza  maana  baada ya kusikia ataenda na Eliza kidogo aliingiwa na utayari wa kwenda lakini alitaka kujua ni kampuni gani kwanza.

“Inaitwa Dede Entertainment”Aliongea na kumfanya Hamza kuona huyu Linda ni kama anamtafutia matatizo, Hamza aliwahi kusikia kuhusu hio kampuni  mtandaoni lakini hakuwahi kuingia , kulikuwa na  taarifa  za malalamishi kibao kwenye mitandao zikiilalamikia serikali kuhusu watu wengi kupotea ndani ya kampiuni hio na hakuna  hatua zozote zinazochukuliwa.

“Hili swala wameweka masharti  watalipa Cash  tunataka kuona kama kweli wanayonia ya kulipa  na kama hawana   tuchukue hatua  za kisheria kuwadai ,  lakini   kama tukiwashitaki  itachukua muda mwingi mpaka kushinda kesi  hivyo kama wapo tayari kulipa kwa Cash haina haja ya kukataa kwenda kuzichukua hizo hela”Aliongea Linda.

Hamza mara   baada ya kumwangalia huyu  mwanamke alivyokuwa akimpa  maelekezo aliona  ni kama anataka kumwingiza matatizoni.

Lakini kwasababu hakuwa na mpango wa  kuendelea kubishana na huyo mwanamke ambae ni kama anamuonea wivu  kwa kula bata kazini aliamua kukubali  na  alitoka ofisini kwenda kumtafuta Eliza.

Previoua Next