Reader Settings

Brigedia Doswe aliishia kumwangalia Amosi kwa  macho ya maswali  bila ya kupokea salamu yake.

“Amosi  sina muda wa kuongea na wewe sasa hivi  , asubuhi kesho fika na ripoti kamili ya wapi ulipokuwa na  ulichokuwa ukifanya”Aliongea.

“Sawa Afande”Aliitikia kwa heshima na Doswe aliondoka akionekana kuwa na haraka  ya kuelekea kwenye kikao.

Dastani na Amosi waliishia kuangaliana , ukweli ni kwamba  Dastani alikuwa akimtafuta Amosi lakini  hakuweza kumpata  , hata  alivyoomba  kitengo cha usalama wa taifa kujaribu kumfuatilia  alishindwa na  hisia zake zilimwambia pengine  Tresha  kuna alichomfanyia  Amosi.

“Afande  Amosi nimekutafuta sana , nilidhani kuna kitu  kimekupata”Aliongea  Dastani.

“Na amini  ulifurahia kutokuonekana kwangu”

“Unamaanisha nini kusema hivyo  Afande”Aliuliza na kumfanya Amosi kutabasamu kifedhuli.

“Nani ambae aliniandalia  mtego mpaka kutaka kuwawa, Acha maigizo Kanali   nina uhakika  hata  kutekwa kwangu unahusika”Aliongea na kumfanya  Kanali kushikwa na hatia na mshangao kwa wakati mmoja.

“Unamaanisha nini  kuhusika na kutekwa kwako , inamaana kupotea kwako ulikuwa umetekwa!?”Aliuliza  na kumfanya Amosi kumwangalia kwa  macho yaliojaa chuki bila ya kuongea neno.

“Amosi licha ya kwamba sijawahi kukupenda  lakini huwezi kuongea  vitu ambavyo  havina  ushahidi kulingana na taaluma  yako”

“Umeshakiri kabisa hujawahi kunipenda ,  hio ni sababu  tosha, kama  niliweza kuingia katika mtego ulioniundia   kwanini nisikushuku na  hili lililonitokea”

“Kama  unachozungumza ni kweli  ulikuwa umetekwa, nipe sababu ambazo zinakufanya uone nahusika”Aliongea  Kanali huku  akionyesha hali ya usiriasi kwenye macho yake.

“Unataka sababu? , kama unataka  sababu nitakutajia  , unajua fika mimi ndio najua una mahusiano ya siri na Tresha  na niliwapiga picha , walioniteka  walinisurubu kwa kutaka niwatajie wapi  nimeficha  ushahidi wa picha”Aliongea Amosi na kauli ile ilimfanya Dastani mapigo ya Moyo kudunda  kwa nguvu,  kutokana na  kile ambacho Tresha  aliongea alijua fika  lazima   atakuwa amehusika kumteka Amosi  na kama ni hivyo moja kwa moja  hata yeye  anahusika.

“Kanali kesho naandaa ripoti ya mambo yalionikuta katika siku zote ambazo sikuwa nikionekana , juu ya kutekwa kwangu na walioniteka walichokuwa wakitaka , nitaelezea kila kitu katika hio ripoti  unapaswa kujiandaa katika hili”Aliongea Amosi , haikujulikana alikuwa akidanganya makusudi au    kutokana na kupandikizwa kitu kwenye ubongo wake inamfanya  adanganye , lakini kwa vyvoyte vile uongo  wake ulionekana kufanya kazi.

Upande wa  Dastani  alihisi hatari  , alijua  kama kweli  Amosi alitekwa na waliomteka ni watu wa Tresha  basi moja kwa  moja  swala hilo linamuunganisha na yeye , pili  faili la Tresha  kwa muda mrefu lilikuwa ndani ya kitengo chao akifahamika kama mfanyakazi kutoka  Binamu  na   ni juzi tu yeye pia alihusishwa kushirikiana na watu wa  Binamu, sasa kama Amosi  akiwa na ushahidi  wa picha  na pia ikionekana  kutekwa kwake  kuna uhusiano wa moja kwa moja na yeye, basi kuna uwezekano akaondolewa katika vitengo nyeti vya  kijeshi na kurudi kuwa mwanajeshi wa kawaida au  kufukuzwa kabisa maana ushahidi uakuwa wazi, sio hivyo tu alikuwa pia na kesi ya kuvunja vifungu vya utaratibu wa  kitengo cha MALIBU kwa kujichukulia kesi mkononi bila ya kuomba ruhusa  kwa wakubwa zake.

“Amosi  unataka nini kutoka kwangu?”Aliuliza Kanali Dastani akiwa siriasi.

“Unaniuliza nataka nini kutoka kwako , sina  ninachotaka”

“Kama huna unachotaka kutoka kwangu , usingeongea chochote na ungendaa ripoti moja kwa moja na kuikabidhi kwa   Brigedia”

“Kwahio unakiri   wewe na Tresha ndio  mlinniteka?”Aliuliza Amosi huku akiwa na tabasamu lililojaa uovu.

“Siwezi kukiri  wala kukataa kwasababu nina siku kadhaa sijampta Tresha hewani , ni kweli  nakiri nina mahusiano ya siri  na wewe una ushahidi, kama  Tresha   ndio kahusika  hili ni swala linaloniunganisha na mimi”Aliongea na kumfanya Amosi kutoa tabasamu.

“Kanali  licha ya kwamba  hunipendi lakini mimi nakuheshimu kama moja ya Ajenti wenye uwezo  mkubwa katika kitengo chetu, nakuheshimu kwa mafanikio  yako  nakuheshimu pia  kwa kunitangulia jeshini, lakini  matendo yako   ambayo ni kinyume na sheria  yanafunika mafanikio yako kwa kasi kubwa..”

“Amosi haina haja ya kuongea sana , niambie  ni kipi ambacho unataka kutoka kwangu  na katika ripoti yako usihusishe swala la mahusiano yangu na Tresha”Aliongea Dastani huku akionyesha hali ya wasiwasi.

“Nataka  ripoti yote ya  kesi  faili namba tisini na tisa  na juu ya muuaji  aliehusika na kifo cha Afande Mchuku  na  wapi  lilipo faili  la sauti ambalo ameacha, naamini kwa siku ambazo sikuwepo mengi yametokea kwenye uchunguzi wako”Aliongea na  Kanali hakubadilika muonekano , ni kama alitegemea  Amosi angeomba   kitu kama hicho.

“Jana kumetokea ajali  ya  gari la  Mheshimiwa Jongwe kulipuka na kupoteza Maisha, nilishuhudia hii ajali  baada ya kupata  intellijensia  kwamba yupo hatarini ,  muda huu nimetokea kuongea na  Brigedia  na sijamaliza  kumwelezea kilichotokea  na ameniambia naandae ripoti ,, nitaandaa nakala  mbili kwa wakati mmoja  moja nitakupatia wewe  na nyingine nitamtumia  Brigedia”Aliongea Kanali na kumfanya Amosi kutoa tabasamu.

“Vipi kuhusu rekodi ya sauti ambayo Mchuku alikuahidi  kukupatia?”Aliuliza  Amosi.

“Bado  sijaipata  ila kuna mwelekeo  wa kuweza kuipata   , katika ripoti ambayo nitaandaa  utaweza kuona”Aliongea.

Dastani hakuwa na jinsi ya kumpatia  kila kitu Amosi alichoweza kupata katika uchunguzi wake, kwake yeye ripoti ya aina hio haikuwa na umuhimu mkubwa kwani sio kwamba alikuwa akitafuta kupandishwa cheo  bali alikuwa na  mpango mkubwa na Tresha na hakutaka  kuona mpango huo ukiharibika  kwa  ripoti ambayo Amosi anataka.

Upande wa Amosi ni kweli alitekwa lakini hakutekwa na watu wa  Tresha bali alitekwa na  watu wa taasisi  ya Haliz  Foundation  na kufanyiwa upandikizaji wa kifaa kwenye ubongo wake.

Gia ambayo aliambiwa aitumie akiulizwa alikuwa wapi  kwa kutoonekana kwa kipindi chote ni kusema alitekwa , kuhusu   Dastani kuamini maneno yake  alipaswa kuamini  kwani   kabla ya  Amosi  kuchukuliwa na  watu wa Haliz  alikuwa akifuatiliwa na kundi linguine  la watu ambao walitumwa na Tresha kwa ajili ya kumuua , sasa haikueleweka ilitokea vipi ila kundi lile liliweza kukamatwa na  watu wa Haliz foundation  na hapo ndio sababu  ilipotokea ya  Amosi kuambiwa   akiulizwa alikuwa wapi kusingizia watu hao waliokuwa wakitaka kumteka.

Mpango wote huo ulikuwa  umeandaliwa na Ajenti Alonzo  na  Amosi baada ya kuambiwa mpango huo aliona pia  ni nafasi ya kutumia udhaifu wa  Dastani ili kujua ni wapi amefikia katika uchunguzi wa  kifo cha  Afande Mchuku na  wapi  alipoacha  faili la sauti ya  Wazungu wakiongea na Mfungwa Gerezani.

Ki ufupi ni kwamba Amosi alikuwa  katika akili yake lakini kwa wakati huo alikuwa mtiifu  kwa Umoja  wa Sinagogu.

Alikuwa na misheni moja tu  ya kufuatilia kujua  kwa undani tukio la  Ajali ya  radi iliotokea mwaka 2002  na pia  kujua wapi ulipo mkufu  ambao aliuona kwa  marehemu ex wake Jasmine.

Kwasababu  Brigedia alimwambia amtumie ripoti  ya  tukio zima la jana  Dastani hakuchelewa  kwenda ofisini kwake kuandaa ripoti hio na upande wa Amosi ilibidi asubiri mpaka apate ripoti , alikuwa  akifanya kazi kama roboti na alikuwa na siku chache za kukamilisha kazi aliopewa.

“Huyu  mfungwa  ndio amehusika  na   kifo cha mheshimiwa Jongwe   na vilevile ndio Mchuku aliekuwa akimzungumzia?”Aliuliza Amosi mara baada ya kukabidhiwa nakala yake  na Kanali.

“Nina uhakika asilimia mia moja  ndio mhusika  na hisia zangu zinaniambia anaweza akawa ndio amemuua Mchuku”

“Kwahio unamaanisha ametolewa  Gerezani na  kukamilisha yote haya?,  kwa nilivyoweza kusikia mauzngumzo yako na Mchuku inaonekana  huyu ndio aliehusika  na kifo  cha Ajenti Sedekia”Aliongea  Amosi.

“Amosi  hii ni taarifa nyeti  ya serikali na kwa cheo chako  haikupaswi kujua haya ki undan”Aliongea  Dastani huku akiwa na  macho ya msisitizo.

“Afande huyu sio mfungwa tena , huyu ni muhalifu na anapaswa kudhibitiwa , kuna haja gani ya  kumlinda mhalifu wa namna hii , kamuua Sedekia na kisha kamuua  Jongwe na Martini  kwanini raia wasimjue?”

“Upo sahihi , huyu ni  mhalifu na anapaswa  kushughulikuwa lakini  hujiulizi kwanini anaweza kufanya haya yote tena  wakati huo  ikiaminika  ni mfungwa ndani ya Gereza la Silo  , lazima kuna mkono wa viongozi  hapa unahusika”Aliongea  na kumfanya  Amosi kutingisha kichwa.

“Kwahio  imekuwaje kuwaje umempoteza  wakati ukimfukuzia?”Aliuliza Amosi huku akisoma mwisho wa ripoti hio.

 Ilionekana    Dastani alikuwa na uhakika msababishi wa  ajali  iliopelekea kifo cha Jongwe alimfahamu ni Chendezi.

“Sikumpoteza Amosi , alikuwa akiendesha  pikipiki, mimi gari  unadhani  ni rahisi kumpata kwa  jinsi   mpangilio wa  mji ulivyo , kuna maeneo  gari haiwezi kupita lakini pikipiki inaweza kupita,  lakini  hata hivyo nishajua alipo kwasasa ”Aliongea.

“Una uhakika?!”

“Nina uhakika nimempata”

“Unamaanisha nini?”

“Siwezi  kukuambia  ninachomaanisha ,  nimekupatia hio nakala lakini picha  za mimi  na Tresha  unazo , sikuamini Amosi mpaka  nione umezifuta”

Amosi alitoa simu yake na kumpatia  Kanali  na kumuonyesha   picha hizo.

“Hizo hapo  unaweza kufuta lakini kumbuka  bado naijua siri yako, hivyo unapaswa kuniambia unamaanisha nini kusema umempata”Aliongea Amosi akiwa siriasi.

“Sina uhakika   kwa asilimia mia moja   ila  atakuwepo chini ya bosi Laizer makao makuu ya Dede , hiki  ndio ninachoweza kukuambia, Sikia Amosi hili swala lina mkono  wa viongozi wa juu   hivyo unapaswa  kulisogelea  kwa umakini mkubwa sana , sitaki uzembe wako uje kuniunganisha na mimi  , isitoshe hii ni kesi ambayo  haina vigezo vya kuwa chini ya kitengo chetu”

“Mimi ni Ajenti huru  na sifungwi na kazi   zilizopo ndani ama nje ya kitengo,  naweza kubeba majukumu ya  kitengo cha TISA na MALIBU muda wowote”Aliongea  na kumfanya  Dastani kutingisha kichwa.

Licha ya kwamba  Chendezi au Maddog  kuwa  makini sana  kuweza kumshinda  Kanali  katika mbio za pikipiki yake kitu pekee ambacho  kilimfanya  Dastani kumpata ni  kwamba alikuwa bado ni mfungwa.

Hivyo mara baada ya kwenda Gereza la Silo   na kumkosa  pamoja   na kumhoji nyapara juu ya mambo yanayoendelea hapo ndani ilikuwa rahisi kwake kujua lazima  Chendezi atakuwa   makao makuu ya Dede.

“Kuna kitu kimoja nataka tukubaliane baada ya hapa”Aliongea Dastani.

“Nakusikiliza”

“Kwanzia sasa  uchunguzi  wa kesi  faili  namba tisini na tisa tutashirikiana, kesho   unaonaje ukipendekeza hili  kwa  Mkurugenzzi, naamini kama tukishirikishana utaalamu wetu itakuwa rahisi kufumbua  fumbo lote kwa  wepesi”Aliongea Dastani  alijua  kwasababu Amosi alikuwa akiaminniwa sana na  Mkurugenzi akimpendekeza  hata swala lake la kuvunja vifungu  vya sheria za kitengo atasamehewa.

“Tokea ile siku uniingize kwenye mtego, nimetokea kukuchukia sana  Kanali lakini  kwa maslahi ya nchi  nipo tayari ya kuweka nyuma chuki yangu , nipo tayari tushirikiane lakini  tu  kama Mkurugenzi ataridhia”Aliongea  na kumfanya Kanali Dastani kutoa tabasamu.

 

*****                 

Hamza kabla hajapiga hatua kuingia ndani  aliweza kusikia sauti ya  Yonesi  katika hali ya kufoka.

“Naomba uondoke sitaki kukuona”Alisikika   Yonesi  na ilionekana   aliekuwa akimwambia ni mwanaume alievalia kombati za jeshi  zenye nyota tatu  ikimaanisha ni kapteni.

Regina ndio aliekuwa wa kwanza kutangulia kuingia  na  ndani hakukuwa na mwanaume mmoja tu , walikuwa ni wanaume wawili  wote wakiwa katika  sare za jeshi, mwingine akiwa ni luteni usu yaani nyota moja na jina la Diksoni J Mkandala lilisomeka  kwenye kifua cha kombati zake.

“Yonesi hawa  wanajeshi kwanini wapo hapa!!?”Aliuliza  Regina  mara baada ya kushikwa na wasiwasi kutokana na  muonekano wake..

“Bosi  kwanini umekuja mpaka huku hospitalini?”Aliuliza  Yonesi huku akiwa na  wasiwasi..

“Nilikuwa  bize sana kwenye siku hizi mbili na nikashindwa  kuja kukutembelea, vipi hali  yako?”

“Niko sawa kwasasa bosi , asante kwa kuja kuniona”Aliongea  na yule mjeda mwenye kombati  zenye jina la Johnson G Mdudu  aligeuza kichwa chake na kumwangalia  Regina kwa  macho yaliojaa kebehi.

“Lazima  wewe utakuwa ni  bosi wa kampuni ya Dosam , kwanini  umempa kazi ya ulinzi mchumba wangu na kumfanya aumie?”Aliuliza  na  swali lake lilimfanya Regina na Hamza kushangaa.

“Yonesi kumbe una mchumba tayari!!?”Aliuliza  Regina.

“Hapana  bosi , usimsikilizze anaongea ujinga”Aliongea Yonesi  na kugeuza macho yake na kumwangalia  huyo mjeda   kwa ukali.

“Mdudu  unaongea upuuzi  gani?”Aliongea.

“Yaani  naongea  upuuzi wakati ni kweli na umekimbia  harusi  hatua za mwisho na kuniabisha”

“Nilishasema sikutaki lakini unatumia nguvu ya baba yako kumpanikisha baba yangu ili  unioe , nimekimbia ndio na sitokaa niolewe na wewe”

“Wazazi wetu ndio wametaka kuunganisha familia zetu kupitia ndoa ,  ile siku uliokubali kupokea pete ya uchumba  rasmi ukawa mwanamke wangu na huwezi badilisha”Aliongea kwa hasira na kisha alimgeukia  Regina.

“Mchumba   wangu  namtoa hapa kumpeleka hospitali nzuri  ya hadhi yake, ole wako  nisikie umemfanya  kuwa  mlinzi tena”Aliongea  kwa  hasira.

Hamza mara baada ya kusikia kauli zake za kibabe alijikuta akicheka chini chini, kwa namna  Afande Mdudu alivyokuwa akiongea ilionyesha ni lazima anatokea katika moja ya familia  yenye nguvu la sivyo asingejiamini hivyo.

“Mdudu  siwezi  kwenda popote na wewe , nipo radhi kufa na sio kuolewa na wewe”Aliongea  Yonesi kwa hasira  na kumfanya Regina  aingilie.

“Yonesi  ni mfanyakazi wangu  na rafiki yangu  , siwezi kukuruhusu kumuondoa hapa kwa nguvu , hata kama wewe ni mwanajeshi huna mamlaka ya kumlazimisha”Aliongea  Regina  na kumfanya Mdudu kuanza kucheka.

“Unaanza kuongea maswala ya sheria mbele yangu , unanijua mimi ni  nani?”

“Haina  maana ya kujisifia wewe ni nani kama  matendo yako  ni ya kipuuzi”

“Una kauli mbovu kwa mfanyabiashara kama wewe , Hamza  kwanini unashindwa kumdhibiti mkeo?”

Regina na  Yonesi mara baada ya kusikia kauli ya Afande Mdudu  muonekano wao ulibadilika mara moja.

Regina alishangaa   imekuwaje  mjeda huyo kujua  amefunga ndoa na Hamza.

Upande wa  Yonesi  alishangaa kwa kutoamini kama Hamza na  Regina walikuwa na mahusiano ya aina hio.

Hamza yeye hakushangaa lakini muonekano wake ulikuwa ni wa kikauzu mno.

“Unanijua mimi?”Aliuliza Hamza  swali likienda kwa Mdudu.

“Nakujua ndio , najua pia wewe ndio uliemuumiza kapteni Norbert , unajiamini sana  mpaka kumshambulia mwanajeshi”Aliongea huku akiwa na mwonekano  usiokuwa siriasi sana , ni kama  alifurahia kitendo  alichofanya Hamza..

Hamza muda huo aliweza kujua lazima huyu  afande atakuwa ni moja ya  kikosi ambacho  kinamfatilia kama ilivyokuwa kwa   Kapteni Norbet, lakini hata hivyo hakujali sana , kama walikuwa wakimfatilia  ilikuwa rahisi kwao kuweza kupata taarifa za yeye na Regina kusajili ndoa Bomani.

“Bosi Regina kumbe umeolewa!?”Aliuliza  Yonesi kwa mshangao , licha ya kwamba Regina  alimchukulia kama rafiki  yake ulikuwa sio ule urafiki wa kufuatiliana maisha yao binafsi.

Regina aliishia kuangalia chini huku akiwa ameng’ata lips za mdomo wake, hakudhani  ingefahamika haraka hivyo juu ya ndoa yake na Hamza.

“Ndio tumesajili ndoa yetu , ila sikutaka watu wengi kujua”Aliongea

“Oh , kumbee…!”

Yonesi  alijihisi kama vile amekuwa mtupu na mjinga kwa wakati mmoja , siku ya kwanza aliomuona Hamza  na  kumpeleka nyumbani   hakutarajia Hamza angekuwa na mahusiano ya aina hio na Regina.

Kubwa zaidi kuliko yote ni kwamba alikuwa akimchukulia Hamza kama mwanaume muhuni , ambae  hana mipaka,  akikumbuka matukio kati yake na Hamza na taarifa hio alijikuta akishikwa na hasira.

“Hamza usijione  kidume  kwasababu  umeweza kumshambulia  KapteniNorbert ukahisi tutakuacha salama ,  una kesi  kadhaa zinazokukabili na tunakwenda kuzifanyia uchunguzi, kama una  akili ni kheri kujisalimisha mapema”

Regina alijihisi kupaniki  maana hakutarajia   serikali ingetuma watu kwa ajili ya kumchunguza Hamza na alijiuliza inamaana Hamza anakwenda kufungwa kwa kumuua mtu.

“Kwangu  bora kapteni Norbet kidogo naona ana weledi , ila wewe unachojua ni kuongea   tu , kama unao uwezo  wa kunikamata huna haja ya kunipiga mikwara  hapa”Aliongea Hamza  na  kauli  yeke ilimfanya  Afande Mdudu kujaa sumu , lakini licha ya hivyo alikuwa akimhofia Hamza    hivyo hakufanya chochote na hakutaka kuzidi kumkasirisha.

Lakini hata kama alikuwa akimuogopa aliamini kama  akiamua kumkamata   ataweza.

“Wapo  watalamu wengi wa mapigano ndani ya hii nchi ambao  wanaweza  kukushinda , hivyo acha  ukiburi , hatujaamua tu kukuchulia hatua kwasababu tunaangalia muda sahihi wa kufanya hivyo”Aliongea.

“Kama umemaliza kuongea  ondoka maana hakuna anaonekana kukukaribisha hapa”Aliongea Hamza.

“Unanifukuza kama nani ,nilivyosema Ypnesi ni mwanamke wangu hujanielewa , wewe ndio unatakiwa uondoe  hapa”

“Kama una  uwezo jaribu kumchukua Yonesi kinguvu uone”

“Wewe ni mjinga kuleta ukiburi mbele ya mtu ambae hata hujui nguvu yake?”

“Ndio sikujui na sitaki kujua”Aliongea Hamza  huku akitingisha mabega.

Yonesi mara baada ya kuona wawili hao wanaanza kupandishiana alijikuta  akiingiwa na wasiwasi.

“Hamza acha kujibishana , Bosi  nitaondoka  nae tu”Aliongea Yonesi,  japo majeraha yake yalikuwa yamepona lakini bado alihitaji muda wa  kupumzika  kwanza zaidi.

“Yonesi kwanini, si ulisema hutaki kuondoka nae?”

“Kwa ajili yangu sitaki kukuingiza kwenye matatizo”Aliongea na hapo Regina alijua lazima itakuwa  ni  kuhusu  nguvu ya  Afande Mdudu ndio maana ameamua  kwa hiari yake kuondoka ile isijetokea wakaingia kwenye ugomvi na Hamza.

Regina hakuwa mtu wa kukurupuka   hata hivyo , alikuwa akijaribu kupima faida na hasara , hata kama   alikuwa akimiliki  kampuni kubwa lakini  bado ataishia kuwa mfanyabiashara tu mbele ya wanasiasa  na  wanajeshi.

“Yonesi hukuona unaisababishia familia yako matatizo kwa  kukimbilia  huku , huu ni muda wa kurudi nyumbani na usiwe na wasiwasi kabisa, tukifika  nyumbani  nitaongea na baba yako ili tuweze kufunga ndoa haraka haraka  na  tuanze kufikiria swala la  Watoto”

Wakati huo  akiongea alikuwa akikiangalia kifua cha Yonesi kwa macho yaliojaa uchu  wa kimatamanio.

“Endelea kuota , siwezi kukubali kuolewa na  mtu mwenye majigambo kama wewe”

“Hehe , hilo sio juu yako kuamua, tukisharudi kila kitu  kitaenda kutokana na mipango ya familia, baba yako amekuvumilia muda mrefu na licha ya kujua unaishi hapa Dar hakuchukua  hatua y a kukulazimisha  kurudi , alikuwa akikupa muda ili mwisho wa siku  uelewe kwamba mimi ndio mwanaume sahihi wa kukuoa, ni mimi pia ambao  sikutaka wakusumbue  niliwaambia wakupe muda”Aliongea   kwa majingambo.

Moja  ya sifa ya Mdudu ni kuwa mpole mbele ya  wakubwa zake kijeshi  , lakinni ukimkuta mbele ya watu waliochini yake  ni mjivuni wa kiwango   cha daraja  A.

Regina mara baada ya kusikia maneno hayo na kuona namna Yonesi alivyokuwa katika hali ya huzuni   alijikuta akimuonea huruma , hata yeye alikuwa akiyajua machungu ya kulazimishwa kuolewa.

Kwake aliona licha ya  Hamza kuwa na  mapungufu yake lakini alikuwa afadhali kuliko Mdudu.

“Eunice  kama hutaki kwenda haina haja ya kujilazimisha , ndoa ni swala la hiari  na  ukiona  hupati haki yako shirikisha hata  wanasheria wa mambo ya haki za binadamu”Aliongea Regina.

“Ashirikishe wanasheria!  ,  Regina  wewe ni mjinga kutaka kuingilia mambo yetu”.

Yonesi  mara baada ya kuona  Regina alikuwa akimtetea alijisikia vizuri ,ni mara ya kwanza kwake  kutetewa kama hivyo , nyumbani  wakati analazimishwa kuolewa hakuna ambae alimkingia kifua mpaka alipofanya maamuzi ya kukimbilia  Dar es Salaam.

“Mkurugenzi asante sana  kwa kusimama upande wangu  na kunijali  mwanamke kama mimi ambae ninachojua ni kupigana tu kwa miaka  yote mitatu tokea tukutane , nisamehe  siwezi kuendelea kufanya kazi chni yako tena”Aliongea  Yonesi  kwa  sauti iliojaa huzuni na maneno yake yalimfanya Regina  kuzidi kushikwa na huzuni iliochanganyika na hasira.

Muda huo Yonesi alikuwa ashatoka  kitandani  kwa ajili ya kuondoka,hakutaka hata kumwangalia Hamza ambae alikuwa amekaa nyuma.

Kitendo cha Yonesi kutaka kuondoka bila ya kumuaga , kilimtoa Hamza aliposimama na kwenda kumzuia kwa mbele.

“Yaani tumekula  chakula cha mchana mara kibao halafu unataka kuondoka bila hata ya kuniaga”Aliuliza Hamza.

Kauli yake ilimfanya Yonesi kukumbuka siku ambazo alifahamiana na Hamza mpaka kuzoea kula nae chakula kwenye meza  moja.

“Wewe ni muongo siku zote kumbe  ni mume wa  bosi halafu  umenikalia kimya , nimekasirika sitaki hata kukuaga mimi”

“Sawa Kapteni,  lakini haina haja ya kujilazimisha kuondoka”

“Kuna baadhi ya mambo kwenye dunia hii  yapo nje ya  hiari yetu”

“Ndio yapo mambo mengi ambayo hatuna hiari nayo, ikiwemo kifo  na kuumwa , lakini swala la kuolewa na  mtu kama  huyu ni kuamua , kama hutaki   hutaki”

“Hamza acha kuniongelea vibaya ukidhani siwezi kukufanya chochote , hujui hata  kipi ni kizuri  na kibaya kwako  kwa kujaribu kuingilia mambo yangu na mchumba wangu”

“Eti wewe na mchumba wako, bro   unaziabisha hizo kombati za jeshi kama unashindwa kujua ndoa ni makubaliano ya watu wawili , wewe unamwita mchumba lakini Kapteni   hakutaki  Zaidi ya kufosi”Aliongea na kumfanya Afande Mdudu  kumsogelea Hamza karibu na kumwangalia kwa macho makali.

“Sitaki kupoteza muda wangu na mhalifu  kama wewe ,ukiendelea na mbovu zako nitakufanya ulazwe hapa hospitalini”

“Acha hasira bro ,  sina mpango wa kuingilia mambo yako , kinachonipa wasiwasi  ni juu ya mke wang  tu”

“Hili linahusiana vipi na mkeo?”Aliuliza Mdudu.

“Wewe  ndio uniambie , unadhani ni kitu gani muhimu cha kuzingatia kama mwanaume  kabla ya ndoa?”

“Kwanini nikujibu?”

“Huwezi kunijibu kwasababu kwa macho yako unadhani kuoa ni  kama kunfunga  kondoo  Kamba na kumpeleka nyumbani , unachotaka kufanya hapa  ni  kumchukulia  Kapteni ni kama mnyama ambae unaweza kumuweka nyumbani  bila ya kujali hisia zake”

“Unataka kumaanisha nini?”Aliuliza , sio kama hakuelewa ila hakutaka kuelewa.

Sababu ya  Mdudu kumlazimisha  Yonesi  kuolewa nae ni kwasababu ya uzuri  pamoja na familia anayotokea , hakujali  hisia zake , pengine  hayo yote yalichangizwa na namna  ya familia zao zilivyo, kwao  ndoa ni kama biashara ya kuunganisha familia mbili  zenye nguvu.

“Mimi sijui wengine wanachowaza ila kwangu kitu cha kuzingatiwa   kwa mwanaume  kuoa ni ule utayari wa mwanaume  kubeba majukumu yote  ya kifamilia , ndoa inaweza isiwe kamilifu   lakini  uwajibikaji  ni lazima , kwa mke wangu mimi  anamchukulia Kapteni kama Rafiki yake  wa karibu,  kama  Kapteni hana furaha na  mke wangu hawezi kuwa na furaha,  na kwasababu sitaki kumuona Regina  akiwa na huzuni  Yonesi anabakia hapa  , haendi popote”

Regina licha ya  kutopendezwa na Hamza kumuita mke , lakini bado moyo wake ulilainika kwa namna ambavyo  alionekana kuwa siriasi kujali kile ambacho anataka.

Hata kwa Yonesi ilikuwa ni hivyo hivyo  alikuwa na hisia mchanganyiko , aliguswa na  namna Hamza alivyoonekana kusimama  mbele yake kumkingia kifua

Kauli ya Hamza ilimfanya  Afande Mdudu  kuchomoa bastora kiunoni  na kumuwekea  Hamza kwenye paji la uso.

*******

Saa nane za mchana ndani ya  dhehebu la kiimani la The Chosen Faith’s, maarufu kama Kanisa la Wabrazili  alionekana Ajenti Alonzo  akiwa amekaa kwenye  benchi ndani ya kanisa hilo.

Kanisa hili lilikuwa likipatikana Bunju  B ndani ya jiji la Dar  es salaam, kwasababu ilikuwa ni mchana  hakukuwa na waumini  wowote wa Dhehebu hilo.

Alonzo alionekana  kukodolea skrini iliofungwa  juu ya  dari  ikionyesha  ratiba  mbalimbali za ibada.

Moja ya sababu kubwa ya kanisa hili kujipatia umaarufu  duniani kote ni kutokana na taratibu zao za ibada , lilikuwa dhehebu  ambalo  linakaribisha kila aina ya Imani kasoro  waumini wa Wiccan pekee.

Yaani kila kitu ndani ya kanisa hilo   kilikuwa kikifanyika  kinyume , ilikuwa  pia sio sahihi kuliita kanisa kutokana na utaratibu wao.

Kama ni muumini wa  Rastafarians  kulikuwa na  ratiba yake ya ibada,  kama ni muumini wa Kibudha kulikuwa na ratiba yake ya  ibada , kama ni muumini wa kikristo kulikuwa na ratiba yake ya Ibada, kama ni muumini wa Caodaism  kulikuwa na ratiba yake ya ibada , ki ufupi  ni kwamba  dhehebu hili lilikuwa likitilia mkazo kila Imani ya mtu bila kumbagua, kasoro tu wapagani wa kisasa ambao  maarufu hufahamika kama Wicca.

Inasemekana kwamba licha ya kanisa hili kuwa na ibada  ya  kila Imani  lakini  siku moja ambayo ni Jumamosi wanakuwa na ibada ambayo inawakutanisha waumini  wa  Imani zote  na  mafundisho yanayotolewa katika siku hio  ni  kufundisha elementi  ambazo  zinaunganisha dini zote.

Yaani kwa lugha nyepesi  kinachoangaliwa  ni  vipi   Imani ya Rastafarian inafanana na Imani ya Kibudha , hivyo  hivyo ni vipi  Imani ya Kihindu inafanana na  ya Kiyahudi , sasa   hizo sababu zote ambazo zinatengeneza mshahibiano  ndio msingi   mkuu  wa  Imani ya kanisa hilo la Wabrazili au  The Chosen faith’s.

Mbele ya  Madhabahu ya kanisa hilo  kulikuwa na kila aina ya  vitabu vya dini  ambavyo hutumiwa na Imani tofauti tofauti  kwanzia  Satanic Bible, Black Book , Mishefa na vinginevyo.

Baada ya dakika chache kupita pembeni ya Alonzo aliweza kufika mwanaume  wa kizungu alievalia joho  la rangi nyekundu  na kukaa pembeni yake.

“Shalom Shalom!”Alisalimia yule  mwanaume wa kizungu  alievalia  joho.

“Merry meet , Raeli”Aliitikia Alonzo  kwa Imani yake na kumpa heshima yule mtu kwa Imani yake.

Merry meet ilimaanisha  kuitikia salamu kwa  muumini wa kipagani ambae sio Wicca  na Raeli ni  cheo cha mtumishi  kutoka Imani ya Raelism.

“Tupo na kipi cha kuzungumzia leo?”Aliuliza

“Nipo kwa ajili ya kuripoti kazi  yangu nchini Tanzania imekamilika”Aliongea.

“Kuhani  alinipa  taarifa juu ya ushawishi wako mbele ya  Profesa Maya Thema, kazi nzuri Ajenti”.

“Asante  Raeli  kwa kunitambua”Aliongea  Alonzo akionekana kufurahia kusifiwa .

“Kutokana na uwezo  wako  wa  hali ya  juu  unapaswa kuendelea kubakia nchini Tanzania kwa kazi nyingine”Aliongea Raeli na kumfanya Ajenti kushangaa.

“Kazi nyingine!!”

“Ndio , kazi hii ni muhimu na kama utaweza kuifanikisha  nafasi yako ndani ya umoja itapanda , Ajenti Alonzo upo tayari kupokea kazi  nyingine?”

“Moyo  wangu ni kwa ajili ya Umoja , nipo tayari kwa kazi nyingine”Aliongea   na kumfanya  Raeli kutoa tabasamu.

“Kama Sinagogi tunaamini  uwepo  wa viumbe wengine ambao  wanaishi hapa duniani pamoja na sisi , uchunguzi wetu wa kisayansi umeweza  kuthibitisha uwepo wao , lakini  jamii za kimataifa zimekataa kuamini kutokana na kutokuwepo kwa Ushahidi wa kuonekana kwa macho, Shukrani kwa Dokta Genesha  kwasasa tuna teknolojia ya  kunasa  nguvu zisizoonekana”

“Raeli unamaanisha hawa Night Shadows!!”Aliuliza Alonzo na Raeli alitingisha kichwa kukubali.

“Kwa taarifa iliosambazwa na Kuhani mkuu  duniani kote inapambanua Viumbe hawa  wanaweza kujidhihirisha kwa binadamu  kwa kutawala kivuli  chao,  tunaamini  viumbe hawa wamekosa miili  ya kibinadamu ndio maana tunashindwa kuwaona , Kuhani kupitia  andiko lake anasema viumbe  hawa wapo kila  sehemu ndani ya dunia , lakini viumbe waliopo  America  hawawezi kuvuka bahari  na  kufika  bara la Afrika , hivyo hivyo  kwa mabara mengine ambayo utenganisho wao ni maji”Aliongea na kauli ile ilimfanya Alonzo kuwa katika hali ya mshangao kana kwamba alikuwa amepata  taarifa ambayo hakuwahi kuisikia ,  yeye kama ajenti wa Sinagogi alikuwa akijua uwepo wa hao walioitwa Night Shadows  lakini  hakuwahi kupata uzoefu wa kivuli chake kutawaliwa na  hao viumbe.

“Ndugu Raeli,  maelezo yako   ni  yenye kunishangaza  mpaka sasa ,  na sijajua  ni  kazi  gani nyingine nakwenda kufanya”

“Naelekea huko  Ajenti  wakati nikimalizia  kukusimulia  barua ya Kuhani, kwa maelezo ya  Kuhani anaamini  kuna njia za mawasiliano baina ya hawa viumbe kutoka  bara lingine kwenda bara lingine  na Nadharia ambayo  imeibuliwa  na haadhi ya watafiti wetu  ni juu ya matumizi  ya kinachoitwa Stimula”

“Stimula!!”

“Ndio  ni  kama aina ya  moshi   wa harufu ambao  humfanya binadamu  kupata msisimko wa hali ya juu wa ubongo wake na kufanya kazi  kwa uwezo wa juu kabisa, Hapa Tanzania imegundulika  kuna matumizi ya siri sana ya hizi Stimula  ambazo  husafirishwa  kwa njia ya vyungu”Aliongea  na kauli ile ilimfanya  Alonzo kushangaa.

“Hizi Stimula zinatokea wapi kama zinatumika dunia nzima?”

“Kwasasa  hakuna  Ushahidi wa moja  kwa moja  wapi  zinatokea na  kipi kipo nyuma ya  teknolojia ya udhalishaji wake , wanasayansi wetu wanaendelea na utafiti ,  uchunguzi wa awali tunahisia  hizi Stimula zinatokea  kisiwa Cha Binamu”

“Binamu!!”

“Ndio,  nadhani sina haja ya kukuelezea kuhusu   Binamu?”?Aliuliza na  Alonzo alitingisha kichwa kukubali.

“Kazi yako  nchini Tanzania sio kujua  wapi hizi Stimula zinatokea  wala  juu ya kazi yake, unachokwenda kufanyia kazi ni  kujua   watu wote wanaotumia hizi Stimula , Kuhani anaamini   wateja wa hizi  Stimula ndio njia ya mawasiliano ya hizi roho ambazo hujidhihirisha  kwa njia ya kivuli”Aliongea na kauli ile ilimfanya  Alonzo kutingisha kichwa.

“Kwa maana kazi yangu itakuwa ni   kuwatambua na  kuwafuatilia  hawa watu  wanaotumia hizi Stimula  na kuona kama kuna mawasiliano yanayofanyika?”

“Hakika umeweza kuelewa ninachomaanisha  Mr Alonzo ,  ninachokukumbusha kazi hii inapaswa kufanyika kwa siri sana   na isitokee  ikagundulika  unafuatilia hili swala , kazi yako kubwa  ni  kujua kama  kuna mawasiliano yoyote yanayofanyika  wakati wa matumizi ya hizo Stimula na kama yapo ni kipi kinaongelewa”Aliongea na Alonzo alitingisha kichwa kuelewa.

 

Previoua Next