Reader Settings

Katika ndoto ambayo aliota jana yake aliweza kuona  mwezi wa  ule ulimwengu wa ndotoni ulikuwa mwekundu ,sasa mara baada  ya kupewa mchoro uliokuwa kama picha  na kuona  mwezi huo ni mwekundu pia,ilimfanya kushangaa.

“Kwa  jinsi ulivyoshangaa nadhani tayari unajua  maana yake?”Aliuliza Frida akiwa na shauku.

“Sijui maana yake lakini   jana  kwenye ndoto niliona  mwezi mwekundu , unaweza kuniambia  nini maana ya huu mwezi na kwaninni umenionyesha hii picha?”Aliuliza Hamza , mbele ya Frida  aliamua kuwa mpole  ili kupata kile anachokitaka.

“Inamaanisha  mazingira unayoota  ni sahihi”Aliongea  na kumfanya Hamza kukunja ndita .

“Wewe umejuaje?”

“Nilipewa na dokta  Genesha  na alinimbia nikijisikia  ni muda sahihi wa kukuonyesha hii picha nikupatie , mwanzoni sikumwelewa alikuwa akimaanisha nini , lakini ulivyo uliza swali nilijua nini maana ya picha hii?”Aliongea .

Ukweli  ni kwamba licha ya Hamza kujihusisha na  Frida hakuwa akimwamini kabisa  haikuwa hivyo tu  hata kwa Frida alimuona Hamza kama mtu ambae hakuwa akimwanini.

Lakini  licha ya hivyo alipaswa  kumfanya  Hamza kumwamini kwa namna yoyote ile ili tu aweze kumshawishi kutumia mshumaa  wakati wa ndoto  la sivyo maisha yake yatakuwa hataini.

Hamza alionekana kufikiria  kwa dakika kadhaa huku akikodolea macho  ile picha , hakuwa na shaka  kabisa  juu  ya picha hio kwani ilionyesha kitu ambacho ameota yeye, alichokuwa akiwaza je haya yote yanayomtokea ndio njia sahihi ya kumpata Mzee kama  alivyosema  Dokta Genesha.

“Hamza  kwa ajili ya  hicho unachokiwaza  mshumaa  ni ufunguo wako , kumbuka maneno yangu niliokuambia juu ya uwepo wa Chumba cha nuru  na ni wewe pekee ambae unaweza fikia hiki chumba  kwa maelekezo ya Dokta, kadri  ambavyo  utachelewa kufanya maamuzi ndio unazidi kujiweka katika hatari  pamoja na watu wanaokuzunguka”,

“Una amini nikitumia mshumaa nitakuwa salama , sidhani  inaweza kuwa  hivyo , kwanzia sasa   kila ninachofanya  juu ya   hivi vitu ndio nazidi kujiweka katika hatari”

“Watu wanaokuwinda  kwasasa wanachotaka ni  kitu  ulichokuwa nacho ,  hata kama wachukue waondoke nacho hakina maana kwao,  wewe pia  umekishikilia kwasababu  bado hujajua maana yake halisi ni nini na kinaelekeza nini , ikitokea umejua kinachoelekeza  utakuwa ni wewe  tu   dunia nzima unaejua hilo  na  inabakia kuwa siri yako , hata kama  ukiwapatia kujiondolea  hatari  kwako na kwa  wapendwa wako, watakuwa wamekushikia tu  lakini maana unaijua  wewe tu”

“Na siri   hio ikitoka  inamaanisha nitazidi kuwa  hatari zaidi ya  mara  mbili ya kuwa na kitabu?”Aliongea Hamza huku akitoa tabasamu lililojaa uchungu.

“Ni mpaka  wakifahamu juu  ya  hilo  lakini  kwa  wakati huo utakuwa umejua namna ya kujilinda na kuilinda familia yako, sidhani  upo tayari kuruhusu  mwanamke  kama Regina kuingia   katika hatari kwa ajili yako”Aliongea.

“Unajua nina mahusiano na Regina,  unaonekana kunifuatilia  sana”

“Wewe ni misheni yangu  kutoka kwa  Dokta Genesha , nipo kwa ajili  ya kukuelekeza, ukifeli kwa upande wako na mimi pia nafeli kile nilichomuahidi Dokta , lazima nijue watu ambao unajihusisha nao”

“Sishangai wewe kusema hivyo ndio maana  hata  mimi kuleta vyungu hapa  ulikuwa ni mpango wako na  haikuwa bahati mbaya kwa Alex  kunipa  kibarua”Aliongea Hamza.

Ukweli ni kwamba akikumbuka namna ambavyo amekutana na Frida  ilionekana kabisa ulikuwa ni mpango  wa Frida kukutana  nae.

“Siwezi kukataa na  tena  kuhusu Alex unapaswa kuwa nae makini?”

“Nina sababu ya kufanya hivyo?”Aliuliza Hamza .

“Alex  ni  shushu kutoka  watu wa  kisiwa cha  Binamu , maisha unayomuona nayo Alex  ni uwezeshwaji  na mbinu ya  kulinda kile ambacho  anafanya”

“Unamaanisha kusambaza vyungu?”

“Hupaswi kusema  ni kusambaza vyungu  bali ni kusambaza  teknolojia  mpya ya dawa  inayosisimua ubongo , nadhani unakumbuka nilikuambia  natumia vile vyungu kwa ajili ya utafiti  wangu?”

“Ndio nakumbuka , kwahio unamaanisha umekwisha kupata majibu?”

“Ndio majibu nimekwisha kuyapata”Aliongea na jambo   lile lilimfanya Hamza mwili wake kumsisimka  kwa furaha maana ndio kitu ambacho alitaka kujua  tokea mwanzo.

“Mpaka sasa sijajua  namna  dawa hii inavyotengenezwa , lakini  ni maarufu kwa jina la Stimula”

“Stimula!!” Hamza alionekana kuhangaa kidogo.

“Ushawahi kusikia?”Aliuliza  na Hamza alitingishwa kichwa kukubali.

“Zipo njia nyingi za usafirishaji  wa hii Stimula na haina kibali  chochote duniani   ni  kama madawa ya Kulevya , Njia  ya utumiaji  wa  chungu  ndio maarufu kwa hapa  Tanzania  na maeneo mengi  ya Afrika”

“Wanasafirisha vipi?”

“Ni rahisi sana , unatumia jiko la umeme  na  kukifanya chungu kipate  moto  na  dawa itaungua na kudhalisha harufu mfano wa marashi , hii harufu ukiivuta  inakulewesha na  baada ya hapo huelewi kinachoendelea  maana utakuwa ni kama  mgonjwa wa akili  na dalili ya kwanza utakayokuwa nayo ni uwendawazimu  kama vile  umetawaliwa  na roho nyingine , mtu anakuwa  ni kama sio yeye  kwani ataanza kuonge vitu ambavyo sio vya kawaida”Aliongea  Hamza na kauli hio ilimfanya  kukumbuka  swala la rafiki yake Amiri  juu ya harufu ya marashi  nyumbani kwa Mellisa  huku  akiongea vitu vya ajabu.

“Kwanini  haya yote , kuna faida yoyote  mtumaji anayopata?”

“Kwasasa  hakuna jibu sahihi  kama kuna faida yoyote , haijulikani ni kwa ajili ya starehe au kuna zaidi ya sababu, pengine kuna mpango unaoendelezwa ambao si ufahamu , ni ngumu kukupa majibu kwasasa”Aliongea lakini upande wa Hamza bado hakutaka kukubali kirahisi , alijua  lazima kuna kitu kinaendelea juu ya hicho kitu kinachoitwa Stimula.

Alitamani kutoendelea kuchimba zaidi lakini alimkumbuka Amiri rafiki yake na alimuahidi  atamsaidia , lakini kabla ya hivyo alipaswa  kujua kama Mellisa alikuwa moja ya  wateja wa Alex wanaonunua  hivyo vyungu.

Jambo la kwanza alipaswa kujua mtu aliempa kazi ya kufuatilia lugha  aliokuwa akiongea  amefikia wapi,  na pili  ndio  afanye maamuzi aidha ya kumwambia  Amiri  ili  ajue  cha kufanya ama alifuatlie  yeye mwenyewe .

Maana alijua kama swala hilo  Mellisa analifanya  kwa siri  basi ni dhahiri kuna sababu kwanini   Amiri hajui.

Hamza hakuwa na haja  ya kuendelea kubakia nyumbani kwa Frida , ukweli ni kwamba  swala la kutumia mshumaa ama kutokutumia   ilikuwa ni maamuzi yake.

Upande wa Frida alimwangalia Hamza mpaka anatokomea  na zilipita kama dakika kumi tu  ya Hamza kuondoka  aliingia mwanaume alievalia  suti ndani ya  jumba hilo , alikuwa mzungu..

Frida alionekana kumjua yule mtu  na hata hakumsalimia , ilikuwa ni kama vile mtu huyo anaishi ndani ya nyumba hio.

“Unaamini atautumia mshumaa kwa kumweleza alichotaka kusikia?”Aliuliza yule mtu na kisha alisogelea makaratasi yaliochanguka mezani  na kuchomoa karatasi  la   plastiki ambalo lilikuwa chini kabisa   mwa yale  makaratasi  na kulinyanyua juu kuliangalia huku akitoa tabasamu na  palepale alilikunja na kuliweka kwenye mfuko wa koti la suti.

“Umesikia mazungumzo yetu yote, hii inatosha  kuniamini juu ya kusimamia vyema utafiti wangu”Aliongea Frida akiwa siriasi.

“Hatuwezi kwenda huko haraka hivyo  Frida , upo  hapa  sio kwasababu  Sinagogu  wanakuamini  bali  tunamwamini  Dokta Genesha,  ulifanya kosa kubwa kumfanya Kuhani  kukutilia shaka  na sasa umejitengenezea udhaifu”Alionga  yule bwana huku akizunguka zunguka kana kwamba kuna kitu anatafuta kwenye hio nyumba.

“Unamaanisha nini kujitengenezea udhaifu?”

“KF  ni mtu  hatari sana  na kadri unavyokutana nae unazidi  kumdanganya, ulikuwa na ushawishi mkubwa katika maneno yako  ili kumfanya akuamini  ili hali kila kitu ni kinyume chake , unadhani akijua unamdaganya itakuwaje?”Aliongea   na   kauli ile ilimfanya  Frida kujawa na ukauzu.

“Kama  unalijua hilo haikuwa na haja  ya kuniuliza kama ameniamini, unaongea  kwa kujaribu kuniogopesha  lakini  unapaswa kujua kitu  kimoja, hii ni kazi ambayo nilifanya maamuzi mimi mwenyewe kuifanya , hivyo vitisho vyako hapa haviwezi  kufanya kazi, najua malengo ya kazi yangu”Aliongea  na kumfanya  yule bwana kuonyesha ishara ya kutabasamu.

“Frida kazi yangu ni kukuangalia na kukisimamia na kuhakikisha kila unachofanya  ni kama ulivyomuahidi  Kuhani , unapaswa kujua  Kanisa  halijawahi kukuamini bali tunaamini  kile unachofanyia  utafiti ndani ya taasisi zetu, wewe ni Wicca  na  kama ulivyo kwenye taasisi yetu  kwa ajili ya kutumiza malengo  ya   ushirika wako   na sisi tupo hapa kukutumia ili kutimiza malengo ya ushirika wetu,  hivyo haijalishi  nilichoongea unachukulia  kama tishio au onyo  hio ni juu yako, tutatonana tena baada ya kuona mafanikio,  Frida kumbuka naona kila unachofanya”Aliongea  na  kisha  palepale aligeuka na kutoka ndani ya nyumba ile huku akiangaliwa na macho makali  ya Frida.

Bwana huyo alikuwa ni yule yule ambae alikutana  na Frida juu  kabisa ya jengo la  Haliz Foundation  na ilionekana  chochote kila ambacho Frida anafanya anasimamiwa na huyo mtu na   pia ilionekana mazungumzo baina ya Hamza  na Frida yalifuatiliwa kupitia teknolojia  ya karatasi.

*******

Lisaa limoja na nusu  mbele  Hamza alikuwa akitoka kituo cha  Treni  ya Mwendokasi ndani ya mkoa  wa Morogoro na kuungana na abiri wengi  ambao walikuwa wakitoka eneo hilo.

Kutokana na jua kali Hamza hakutaka kupanda pikipiki bali aliingia kwenye  taksi ambazo zilipatikana ndani ya eneo hilo.

“Nipeleke Tumaini mkuu?”Aliongea Hamza.

“Tumaini ipi mkuu?”Aliuliza yule bwana na kumfanya Hamza aone hakutoa maelezo ya kutosha.

“Tumaini kituoni kwa watoto Yatima kule”Aliongea Hamza.

“Nimekusoma bosi wangu”Aliongea mwendesha taksi kwa furaha na kisha aliondoa gari kuelekea uelekeo ambao ameelezwa.

Tumaini ni moja ya vituo maarufu   kongwe ambavyo hulelea watoto   Yatima na wale wenye ulemavu wa ngozi.

Kutoka  stendi mpaka kituoni ilikuwa  ni  umbali wa nusu saa kutembea na gari, eneo lote lilikuwa likimilikiwa na  taasisi moja ya kimisaada kutoka  Denmark  lakini baadae  waliacha ufadhili  na  kwa muda mrefu kituo hicho kipo  chini  ya taasisi ya  FOOT(Friends of orphans Tanzania).

Hamza mara baada ya kushushwa  na  taksi nje  geti la kuingia kituoni hapo alilipa na  kisha alisogelea chumba cha mlinzi  na  ilionekana  alikuwa akifahamika kwani hakuandika hata jina lake kwenye kitabu zaidi ya kuruhusiwa  kuingia.

 Ndani ya  kituo hicho kulikuwa na eneo kubwa mno , ijapokuwa  majengo yake hayakuwa ya kisasa sana kutokana na kujengwa zamani sana lakini mazingira yalikuwa safi na yenye utulivu wa hali ya juu.

Ilikuwa Jumamosi  hivyo   watoto wote   wanaoishi hapo walikuwa katika shunguli za usafi.

“Mr  Hamza!!”Sauti iliita kutokea upande wa kulia  wa bustani na kumfanya Hamza kugeuka .

“Madam Dorisi! Habari za siku?”Alisalimia Hamza.

Mwanamke ambae alifahamika kwa jina la Dorisi alikuwa  mfupi  na mnene  na alionyesha tabasamu kumuona Hamza.

“Ni nzuri kabisa, sijategemea kukuona leo  huku?”Aliongea  huku akimwangalia Hamza kwa kumchunguza  mavazi yake ni kama alikuwa akishangazwa na mabadiliko ya Hamza.

“Ulitegemea kuniona lini Madam?”Aliongea Hamza na yule mwalimu ni kama alijua  ameongea kitu cha kijinga   na kumfanya aanze kujibaraguza.

“Nilitegemea kukuona siku yoyote  kwanzia kesho ila sio leo?”

“Hayo ni maratajio au sio!?”

“Kabisa  , karibu sana , kama unavyoona  nawasimamia watoto kufanya usafi wao wa kimwili”Aliongea  na  Hamza alitingisha kichwa  kumwelewa.

Kila mtoto alionekana kuwa bize , wengine wakifua   wengine walikuwa wakiogesha watoto wadogo.

“Nipo hapa kwa ajili ya kuonana na  Mkuu wa kituo  nadhani sijamkosa maana nimekuja bila miadi?”

“Yupo  kuna wageni wengine anawasubiria leo”Aliongea na kumfanya Hamza kutabasamu  na kisha kumuaga  Madam Dorisi kuendelea na mambo yake.

Hamza alitembea  kwa mwendo usio  wa haraka sana na usiokuwa wa kivivu sana  akielekea jengo ambalo   ofisi za  walezi , mkuu wa kituo na  walimu zinapatikana.

Jengo la ofisi hizo lilikuwa limechakaa  kidogo   kutokana na stali yake ya  kizamani , kwa nje  usingejua kama ni jengo la  Ghorofa mpaka uingie ndani.

Hamza wakati akiingia eneo la  ukumbi  chini kabisa ya jengo hilo aliweza kuonekana mwanaume  mzee hivi kama miaka  sitini kwenda  therathini, hakuwa peke yake bali kulikuwa na mwanaume kijana ambae  ameshika  daftari kubwa   na ilionekana kuna kitu ambacho walikuwa wakishaurina kwa namna walivyokuwa siraisi.

“Hamza leo  naona umetukumbuka?”Aliongea yule mzee  huku akionyesha hali ya   kutabasamu.

“Sijawahi  kukusahau mzee wangu, halafu naona hali ya hewa  Morogoro kidogo ni ya ubaridi na  upepo  mwingi , kwa mavazi hayo huogopi kuumwa?”

“Ni kweli hali imebadilika ,  japo naonekana kuwa na mvi tayari lakini  sijazeeka , Karibu  sana”Aliongea na Hamza alionyeshwa sehemu ya kukaa huku akisalimiana na yule bwana ambae alionekana kuwa  na  kaunta book,  kwa haraka haraka Hamza alimfahamu alikuwa ni Mgavi  wa hiko kituo.

“Dean  nitaenda kumalizia ili kubalansi  mahesabu , ikishindikana kabisa  kwa watu tunaowatarajia nifanye mawasiliano na Wizara”Aliongea yule mwanaume.

“Fanya  unachoona  kinafaa kwa utashi  wako , hakikisha  unagawa  pasipo ya kubadili utaratibu  licha ya kupelea kibajeti”Aliongea na yule bwana alitingisha kichwa.

Kwa namna ambavyo walikuwa wakiongea Hamza  alijua tu , kituo kitakuwa kinapitia wakati mgumu kwenye maswala ya bajeti na alijiambia  alifanya vizuri  kuja  siku hio.

“Nimesikia kutoka kwa Madam Dorisi   unasubiria wageni ndio maana hujatoka leo?”Aliongea Hamza.

“Amekuambia wageni!,  mimi nimemwambia kuna mtu namsubiri na sio wageni , Dorisi  bwana”Aliongea huku akitabasamu na kumfanya  Hamza kucheka.

“Tena una bahati kuja leo, ninaemsubiria   itakuwa unamjua kama kumbukumbu za utoto wako zinafanya  kazi vizuri, pengine anaweza kuwa msaada kwenye swala lako”Aliongea  na kauli  yake  ilimfanya Hamza macho  kuchanua.

“Ni  moja ya watoto waliolelewa hapa!?”

“Kama una kumbukumbu nzuri, unakumbuka  wakati unarejewa na  fahamu  kuna msichana mdogo  aliekuwa pembeni yako  akilia!!?”Aliuliza Dean huku alimwangalia Hamza machoni kwa matarajio.

Haikuwa ngumu  kwa Hamza kuvuta kumbukumbu  za  kituoni hapo wakati akiwa mdogo, ukweli ni kwamba  sehemu hio  miaka zaidi ya ishirini iliopira  ndio  sehemu  ambayo kwa mara ya kwanza alisikia jina la Mzee   na hio ni mara baada ya  kurejewa na fahamu akiwepo hapo huku akiwa hana kumbukumbu ya kilichomtokea nyuma , alijua tu alipata ajali ambayo ilimfanya kupoteza fahamu kwa kipindi cha miezi  minne.

“Nadhani kweli nakumbuka , kulikuwa na mtoto  kibonge aliekuwa na mashavu makubwa”Aliongea Hamza  na  kumfanya Dean kucheka.

“Ndio huyo,nilidhani umemsahau kabisa, ila naona umemkumbuka”Aliongea na kumfanya Hamza hamu ya kutaka kumuona huyo mtu kuongezeka.

“Mzee  kwa  jinsi unavyoonekana   nadhani amefanya vizuri sana wakati akiwa hapa?”Aliongea Hamza na  Mzee yule alitingisha kichwa kukataa.

“Hapa  hakukaa kabisa  na hapakuwa kwao , wakati unaondoka na yeye alichukuliwa na  baba yake, amefanya vizuri sana  akiwa kwa wazazi wake mpaka kupata elimu ya juu kabisa  na sasa  ni mwajiriwa wa  kampuni kubwa  hapa  nchini,  licha ya hivyo mpaka leo hajawahi kutusahau,  amekuwa moja ya wafadhili tegemezi hapa”Aliongea  na Hamza alitingisha kichwa kukubaliana nae.

Na  wakati huo  wakiongea Madam Dorisi alijiiunga nao na stori ziliendelea .

Zilipita dakika  chache tu  mgeni ambae alikuwa akisubiriwa  aliweza kufika , Hamza  alikuwa na hamu kubwa  ya  kumuona kweli maana  hata Madam Dorisi alionekana kumsifia kama ni  mrembo sana  huku akimtania  akimwambia  aangalie asije kupagawa.

Shida ilianza pale  Hamza alipo ona  gari ambayo iliingia ndani ya eneo hilo,gari hio ni kama alikuwa akiitambua vizuri,  kabla hata hajashuka mgeni  alimtambua vizuri  alikuwa ni Prisila.

Hamza  hakuwa hakuamini na alihitaji  uthibitisho kutoka kwa Mzee Hizza na alitingisha kichwa  kwamba ni yeye huku akiwa na tabasamu. Mzee huyo mara baada ya  kuona wawili  wakionyesha ishara kama wanafahamina  baada ya kuangaliaana kuna kitu aligundua.

Prisila alikuwa amependeza licha ya kwamba alikuwa amevalia kistaarabu sana  ,  hakuvaa mavazi ya kumfanya aonekane  wa matawi ya juu sana wala wa  hali ya chini sana , alikuwa katikati.

Baada ya kumuona Hamza ndani ya hilo eneo hata yeye alishangaa   maana ni kama hakuwa ametarajia kumuona.

Prisila  alikumbatiana  kwanza na Dorisi huku akimpatia Mzee Hizza  mkono  na  kisha ndio alimsogelea Hamza.

“Ningejua unakuja huku nisingepanda treni , ungenipa lift tu”Aliongea  Hamza huku akijifikiria kwanini kila anapomaliza kikao chake na Frida  mtu anaekutana nae   baada ya hapo ni Prisila , ilikuwa ni kama mara ya pili   hio inatokea.

“Kumbe mnafahamiana?”Aliuliza  Dorisi aliekuwa na tabasamu na mshangao.

“Nafahamina  nae  huyu ni mfanyakazi wetu , nimeshangaa kumkuta  huku”Aliongea Prisila huku akiongea  kwa macho yaliojaa wasiwasi na jambo lile  hata Hamza aliliona.

“Hapa ni nyumbani, amekuja kusalimia”Aliongea Mzee Hizza na kumfanya  Prisila kushangaa kidogo.

“Njooni  tukae kwanza  ili tujue mmekutana lini tena kwa mara ya pili mkiwa wakubwa”Aliongea akicheka  na kauli  ile ilimfanya Prisila kushangaa zaidi na kujawa na maswali mengi.

“Dada Dorisi ongea na Agustino, kuna oda nimeweka  Msamvu dukani kwa  Mzee Salum , sikutaka kununua vitu  bila ya kujua kipi kimepelea”Aliongea   na Dorisi aliitikia na kuondoka na kubakia  Hamza  na Prisila.

“Prisila yule bwana niliekuambia ni huyu na yeye anaonekana kukumbuka, Hamza huyu ndio  Prisila uliesema ana mashavu makubwa  akiwa mtoto”

“Dean  mimi sikuwa na mashavu”Aliongea Prisila huku akionyesha kushangaa   japo alikuwa na furaha  lakini pia alikuwa na wasiwasi.

“Hamza  kasema kitu kilichomkumbusha ni  mashavu yako , ni maneno yake sio yangu”Aliongea huku akicheka.

“Mzee Hizza  nadhani  imepangwa tukutane tukiwa ukubwani ,  mimi na Prisila tunafanya   kazi kampuni  moja  ila kumbe  tulijuana tukiwa watoto?”Aliongea Hamza.

“Kila  jambo lina sababu yake , kama ambavyo sikutegemea ungerudi  kwenye kituo chetu kunisalimia  ni kama hivi  wewe na Prisila”Aliongea na kumfanya Hamza  kukumbuka siku   ambayo alifika  Tanzania na kukutana na  Mzee Hizza kama mtu  wa kwanza kumjua.

Mzee Hizza alikuwa   ni kama mmiliki wa  hicho kituo   na karibia ujana wake wote ameumalizia kukiendesha , hata kipindi ambacho wafadhili waliondoka ni yeye aliepambana  kuendelea kukisimamia mpaka kuja kupata wafadhili wengine.

Kwa muda huo mzee huyo hakujua  chochote juu ya Hamza kuandishika  ndoa na maswala mengine, hivyo  alijua pengine kukutana kwa Prisila  na  Hamza kutafungua milango mingine.

Stori ziliendelea  ndani ya eneo hilo  na kutokana na uchangamfu  wa  Mzee Hizza  hata  Prisila ambae alikuwa na wasiwasi alichangamka.

Baada ya maongezi machache Prisila  yeye alienda kusalimiana  na  watoto na Hamza na mkuu wa kituo walibakia  kuongea.

Moja ya vitu muhimu ambavyo Hamza  alimuuliza ni kama kuna kitu chochote amekumbuka  juu ya  aliemleta kituoni hapo wakati akiwa mtoto, lakini kauli ya Mzee Hizza haikubadilika.

Kauili yake ilikuwa ni ileile  ya siku zote kwamba  Hamza aliachwa kituoni na mtu aliejitambulisha kwa jina la Mzee  huku  akitoa maelezo  Hamza angekuja kuchukuliwa na  mzazi wake.

Hamza alikuwa  akijua  kauli hio ilikuwa ikimaanisha nini, lakini  alitamani kumjua mtu ambae alimuacha hapo kituoni , kuna kila hisia mtu huyo  alikuwa ni Mzee anaemjua   maisha yake yote  lakini hakuwa na uhakika  kwasababu Mzee Hizza hakumuona vizuri na  mtu ambae inasadikika  alimuona kwa macho  kasema  keshafariki  muda mrefu.

Kwahio  Hamza katika kipindi chote alichofika   Tanzania alikuwa akitembelea kituo hicho  mara kwa   mara

Prisila alionekana kutokuwa na muda mrefu wa kukaa hapo hivyo aliaga na Hamza hakutaka  kumuachia aondoke , isitoshe  walikuwa na mengi ya kuongea hivyo aliomba  lift  na Prisila.

Hata  Mzee Hizza  licha  ya kutaka  Hamza abaki kwa chakula cha mchana lakini alitaka  waondoke pamoja na Prisila ili wapate muda wa kuondoka.

Hamza kabla ya kuondoka alitoa  cheki ya kiasi cha pesa ambacho  alikipata kwa bosi Laizer na kumpatia  Mzee Hizza.

Ilikuwa cheki ya hela  nyingi mno  hivyo ilimfanya mkuu huyo kusita kupokea, isitoshe  alimuona Hamza bado hakuwa ameyapatia maisha kama  Prisila , hivyo alishangaa kupewa cheki ya hela nyingi kiasi hicho.

Lakini Hamza alimwambia  sio  kwa ajili yake bali  ni ya watoto  na Mzee Hizza alipokea kwa  unyenyekevu huku  akimshukuru  sana  Hamza kwa kutatua changamoto  ambayo ilikuwa ikiwasumbua, alimuona Hamza kama malaika.

Upande wa  Prisila aliona tukio hilo la Hamza kutoa kiasi kikubwa cha pesa , kilikuwa kiasi kingi mno na hajawahi kutoa kiasi hicho , sio kama  hakuwa  na roho ya kutoa hiko kiasi  ila ukweli ni kwamba   uwezo wa kutoa kiasi hicho mara moja  hana.

Kutokana na kitendo kile kidogo alionyesha  hali ya wasiwasi kwenye macho yake kupungua.

“Prisila kuna kitu kimetokea , najua  hatukufahamiana sana utotoni  kiasi  cha kuwa na furaha baada ya kujuana  ukubwani  lakini  kuna hali ya wasiwasi kwenye macho yako tokea unafika hapa” Aliongea Hamza wakati wakiwa kwenye gari  Hamza akiwa  ameomba kuendesha.

“Ukiachana na kazi yako   kama  msaidizi wa Regina  ni kazi  gani nyingine unafanya?”Aliuliza Prisila  akiwa siriasi na swali lile lilimshangaza Hamza.

Previoua Next