Reader Settings

 

SEHEMU YA 76.

Baada ya kupandishwa kwenye gari walichukua uelekeo wa kurudi  Mbagala  na ndani ya dakika  chache tu walikunja kushoto na kuingia katika kambi ya jeshi.

Eneo hilo licha ya  kuhifadhia  maghala makubwa ya siraha za kijeshi lakini vilevile   lilikuwa na  gereza la siri  ambalo hufungia wafungwa  maalumu.

Ndio gereza ambalo  mara nyingi lilitumiwa na  kitengo cha  MALIBU na TISA  kwa ajili ya  kuhoji na kutesa  kupata taarifa.

Hamza mara baada ya kutolewa kwenye gari ndani ya eneo hilo  alipelekwa mpaka kwenye nyumba  ambayo ilikuwa imejengwa  kwa mawe,  jengo hilo lilionekana kama ngome ambayo haina madirisha.

Mara baada ya kupitishwa kwenye mlango mpana wa chuma hatimae aliingizwa kwenye chumba maalumu cha mahojiano ambacho kilikuwa kama sero.

Chumba hicho kilikuwa kimezungukwa na vioo vigumu ambavyo havipitishi risasi na  hata kuhimili mlipuko wa bomu la kawaida, kulikuwa na  kila aina ya  ufundi uliotumika eneo hilo kuhakikisha  usalama  na ilimshangaza Hamza huku akijiuliza kama kuna mtu ambae ashawahi kufikishwa ndani ya eneo hilo.

Hamza alikarishwa kwenye benchi  na kujikuta akigeuza macho na kugundua kulikuwa na kila tahadhari zilichochukuliwa ,  ilikuwa ni kama vile waliomleta hapo walikuwa wakimhofia na  kujikuta  kutamani kucheka.

Lakini kitendo cha  kuona  namna ambavyo chumba hiki kimejengwa aliamini pengine  Tanzania sio  nchi ya Amani kama ambavyo alitarajia,pengine kuna mambo mengi yanaendelea chini chini.

Ikumbukwe kwamba  kutengeneza chumba  kwa vioo ambavyo vina uwezo wa kuzuia  risasi  na  bomu  gharama yake ni kama  kutumia dhahabu,  sasa kama nchi  imeamua kutumia  kiasi chote hiko cha hela kujenga eneo hilo aliona   haiwezi kuwa bure.

Haikuchukua dakika  nyingi  wanajeshi kadhaa waliovalia kombati za jeshi waliingia , wakiongozwa na Afande Mdudu, mmoja kati yao   alikuwa amevalia kombati za jeshi la polisi zenye cheo cha Kamishina.

Afande Mdudu  alikuwa na tabasamu kama lote , kitendo cha kumwingiza Hamza kwenye eneo hilo  alijiona mshindi  na hakuwa na wasiwasi tena.

“Hamza huyu ni  Kamanda Wazo  mkuu wa kitengo cha Special Crimes,huyu mwingine ni mtaalamu  wa  mahojiano  alietumwa kutoka makao makuu ya polisi  , anaitwa Afande Maningi, Hawa ndio walikuwa bize kudili na kesi yako hivyo unapaswa kutoa ushirikiano kwa kuwajibu kila watakacho kuuliza bila kupindisha”Aliongea Mdudu.

Baada ya kuwatambulisha Afande Mdudu alivuta viti viwili na  kuwapa ishara wale ma’afande kukaa .

Wote walionekana kuwa na vyeo vikubwa kuliko hata Afande Mdudu, hata ambae alikuwa   na sare za jeshi la polisi alionekana pia ni  mwenye cheo kikubwa kutokana na  vyeo vilivyokuwa kwenye sare yake.

Afande Wazo  aliwapa ishara  ya kuondoka wanajeshi  wote waliokuwa wamefuatana nao.

“Mnaweza kuondoka , huyu  mfungwa  yupo kwenye selo yenye ulinzi mkali  hata kama ana uwezo mkubwa hawezi kufanya chochote”Aliongea Kamanda Wazo.

“Anachomaanisha kamanda  mahojiano  haya yanapaswa kuwa siri hivyo mtupe nafasi ya kufanya kazi yetu”Aliogea Afande Maningi na kufanya wale makomandoo na baadhi ya wanajeshi wengine kutoka ndani ya eneo hilo na kuwaacha.

“Hili gereza lenu  ni la kisasa mno mnaliitaje?”Aliuliza Hamza huku akichezesha miguu chini.

“Ukisikia  Dragon lair  ndio hili gereza , hakuna mtu ambae ashawahi kuingizwa  hapa akatoka  kwa hiari yake  hata kama ana uwezo namna gani  , tunao uwezo wa kukufungia hapa mpaka ukafa”Aliongea  Afande Mdudu huku akicheka.

“Kwa maelezo yako  hata mimi  naamini  hili gereza ni   la  hatari”Aliongea Hamza huku akitabasamu.

“Hamza huna haja ya kuwa na wasiwasi , sababu kubwa ya kukuleta hapa ni kutaka  majibu juu ya maswali yetu , kama huna kosa  hatuwezi kukusingizia”Aliongea Kamishina.

“Oh , maswali gani hayo afande?”

“Kwa muda mrefu  kidogo  tulikuwa tukifanya uchunguzi juu ya  maninja wanaojiita wawindaji kutoka Samar  ambao walikutwa  wameuwa wilaya  ya Bagamoyo , baada ya uchunguzi wetu tulibaini wewe  ndio muhusika, hawa watu wametokea nchi ya Ufilipino  na sio rahisi kuja Tanzania na kuuwawa hivi hivi  ,  siku ya jana tumeweza kukamata  wengine wawili ambao walijaribu kuzamia hapa nchini kama watalii  na baada ya  kuwafanyia mahojiano ya kina  wamesema kwamba 

wanafuatilia siri uliokuwa nayo juu  ya kitu kinachoitwa Ankh”Aliongea Kamishina  Maningi na kauli yake ilimfanya Hamza kukunja sura.

Hamza alijiambia inamaana wale wapuuzi hawakukata tamaa tu  au walikuja kufuatilia  kwanini wenzao hawakurudi, lakini hata hivyo aliona haiwezekani,  mara nyingi  wawindaji hao wa binadamu wakitumwa  katika misheni kuna mmoja  kazi yake ni  kufuatilia kisirisiri  maendeleo ya  misheni hio , hivyo Hamza aliamini kwa onyo  alilotoa lingefika kupitia huyo mwenzao.

“Hamza hawa  bounty hunters  inaonekana bado hawajakata tamaa na wamerudi tena nchini na kutaka  hiki kitu kinachotwa Ankh, kwa taarifa yako  hivi  unajua kwasababu yako  nchi imeingia katika hatari  huko mipakani  kutokana na  ongezeko kubwa la wahalifu kutaka kuingia nchini?”

“Hilo kundi ni daraja  B  na kwa taarifa nilzokuwa nazo kitengo chenu cha MALIBU  kinahesabika kama  Daraja A kwa kuwa na wataalamu wengi  wenye  mbinu  mbalimbali za kupambana  mpaka  na nguvu za giza , kinachowaogopesha nini juu ya hawa Wasamar?”Aliongea Hamza.

“Hili sio swala la sisi kuogopa ama kutokuogopa  , tunachotaka kujua   ni mzizi wa haya yote , mpaka sasa  ma Ajenti  wetu wanaendelea kuwahoji  hawa  Wasamar lakini  hatujapata majibu  , tunachotaka kujua kutoka kwako  hiki kitu kinachoitwa Ankh ni nini?, kwa maelezo yao wanachosema  Ankh ni kama dawa  ya  uzima wa milele , wengine wanasema Ankh  ni kitabu  cha ufunuo, sasa wewe tunataka utupe majawabu ya kipi ni kweli, pili sisi  kama serikali  utupatie hio Ankh  ili  tukutunzie , vinginevyo uwepo wako hapa nchini unaweka  usalama wa nchi rehani”

“Si useme  tu   na wewe unachotaka  ni Ankh, kwa bahati mbaya   hicho kitu wanachozungumzia ni uzushi  tu wa kinadharia  ila hakuna kitu cha  namna hio”Aliongea Hamza.

“Ongea  ukweli wewe”Aliongea  Afande Maningi huku akipiga kofi meza.

“Hawa  wazamiaji  wamesema  kitu ulichokuwa nacho  kimetoka kwa  mwanasayansi nguli  wa kihistoria  maarufu kama kichwa cha Tembo  au Dokta Genesha   na ndani ya maabara yake aliacha  anuani ya uelekeo wako  na ndio maana wamekupata kirahisi hapa  Tanzania. Kama  ni kweli unafahamiana na Dokta Genesha basi wewe sio mtu wa kawaida,  taarifa  tulizokuwa nazo mpaka sasa haijulikani kama kweli Dokta Genesha amekufa ama yupo hai  na hata  mara ya mwisho alipozushiwa kifo chake  iliaminika yupo hai baada ya kuwasiliana kwa siri  na wewe, kwa mantiki hio lazima utakuwa na taarifa ya siri ambayo hutaki kuongea”

“Ushasema taarifa ambayo sitaki kuongea , kwanini nikuambie sasa Afande?”Aliongea Hamza.

“Kuwa na adabu , endelea kuongea dharau  uone kitakacho kupata, unajua wewe ni nani hapa ndani? , wewe ni mfungwa na ukiendelea kuongea  uongo usije  kulaumu tukichukua  hatua nyingne kali zaidi?”

“Elezea  hizo hatua  kali zaidi?”Aliuliza Hamza huku mwonekano wake ukibadilika palepale.

“Tuta..”Kabla hajaongea alizuiwa na  Afande Maningi.

“Hamza huna haja ya  kuwa mkali juu ya hili,  sisi jukumu letu kama wanajeshi  ni  kuhakikisha  usalama wa  nchi unaendelea kudumu  na  kwakuwa wewe ni raia  wa nchi yetu tunapaswa  kujua hiki kitu  kinachoitwa Ankh ni nini ili tupate namna ya kukulinda bila kuathiri usalama  wa nchi , ukituambia kila  kitu  hatutafanya mambo kuwa magumu kwako , isitoshe tunajua wewe sio mtu wa kufanya vitu ambavyo vinaweza kuumiza usalama wa nchi”Aliongea na kumfanya Hamza kuwaangalia  kwa zamu.

“Kwahio  ni wewe unaetaka kujua hii siri ama   ni serikali inayotaka kujua?”Aliuliza.

“Sisi kujua  maana yake serikali imejua , wewe weka wazi Ankh ndio nini?”Aliongea  Afande  Wazo.

“Kama  serikali  ndio inayotakiwa kujua basi itifaki ya  vyeo inapaswa kuzingatiwa?”Aliongea na kauli ile ilimfanya   hata  Mdudu kushangaa. “Unataka kumaanisha nini Mr Hamza ?”

“Namaanisha kwamba taarifa unayotaka kujua  ni nyeti  mno na inaingia katika  taarifa za  juu za siri za nchi , hivyo kwa cheo chako  hutoshi, itifaki hapa ifuatwe nataka  kuonana na kiongozi wa juu wa jeshi Daraja  S?”Aliongea na kauli ile iliwafanya wote kutoa macho.

Katika nchi yoyote  licha ya Raisi kuwa na madaraka makubwa ya kujua siri nyingi za nchi haimaanishi kwamba anaweza kujua kila siri  ambayo anataka kuifahamu

Itifaki ya clearence ya siri za nchi  huanzia  dajara  E ambao hawa mara nyingi  ni  polisi  au wanajeshi  wa kawaida  tu  kama wa doria ,  siri ambazo hawa wanajua ni zile ambazo  mara nyingi zinahusisha matukio ya eneo  husika  ambazo  hazina athari kubwa  za ki’usalama hata zikiwa  wazi,  mara

nyingi maelekezo ya siri  hizi hutolewa kwa mdomo tu kama onyo  la kutoongea chochote.

Daraja  D hili ni  daraja ambalo   huhusisha polisi au wanajeshi pia lakini wale polisi  wa vyeo vikubwa  ambao wengi wao wanafanya kazi mpaka kwenye vitengo   vya usalama wa taifa , hawa  wanakuwa daraja  D kwasababu  watu wa  daraja E wote  huwasilisha hizi  taarifa kwao na kuamua  ni siri gani  iweke daraja lipi.

Daraja  C  hili linahusisha  siri zinazoendelea katika vikosi maalumu kama  vile  tukio la Hamza kuua Wawindaji kutoka Samar , hio  operesheni  inasimamiwa  na vitengo maalumu vya uchunguzi na  mara nyingi hapa unaweza wakuta polisi  au wanajeshi mfano wa Afande Mdudu  na kuendelea.

Daraja  linalofuatia sasa linakuja B halafu linafuatia  daraja  A , Daraja  A hapa anazungumziwa  raisi wa nchi , Amiri jeshi  mkuu na baadhi ya viongozi  wenzake wa juu,  mara nyingi  ikitokea   siri  ambayo  inahitaji  operesheni ndani ya eneo la  tukio  hapa wanahusishwa  watu wa Daraja B.

Daraja  B anaweza  kuwa mwanajeshi yoyote anaweza kuwa hata na cheo cha  Ukapteni lakini akawa na Clearence  ya kujua siri zote zinazoendelea katika daraja  B kwa  kibali maalumu kulingana na  kile anachofanyia uchunguzi.

Siri zote ambazo zinatokea katika Daraja A  yaani ngazi ya raisi  ambazo ni nyeti  hupewa  hadhi ya Top Secret na hizi  watu wanaopewa Clearence ya kuziona  ni Daraja S.

Sasa  daraja S  katika itifaki hio ni  daraja ambalo lijategemea kabisa na  hili  ndio  huwa na uwezo wa kujua  siri kubwa za nchi(Top Secret) siri ambazo hata kama raisi azihitaji  hapewi  au  kama akizitaka anapaswa  kuomba ruhusa kwanza  kwa watu wa hili  daraja.

Raisi anaweza kujua siri za daraja S lakini  ni baadhi  na mara nyingi siri hizo zote huwa zinatokea katika kipindi chake cha uongozi , lakini ikitokea  anahitaji siri ambazo zimetokea katika uongozi  uliopita ambazo zipo chini ya Daraja  S  ni mpaka apate kibali   ambacho kinaambatana na sababu maalumu  na ikitokea akikataliwa hana cha kufanya kisheria.

Bila shaka kuna baadhi ya taarifa nyeti sana ambazo  baadhi ya wanajeshi  wanajua siri hizo  wakati wa  uchunguzi lakini   hata kama walihusika kwenye uchunguzi  wakitaka taarifa hio  hawawezi kupewa ruhusa.

Hayo madaraja  ni  mfano tu ila   kila taifa  lina itifaki zake namna ya kutoa hizo Clearence lakini zinakuwa katika mtiririko huo  katika kuhakikisha usalama wa nchi unazingatiwa.

Lakini pia kuna itifaki ambayo  inahusisha  kujuana nani anaclearence ya daraja lipi , kwa mfano  asilimia  nyingi ya  wanausalama ambao wana Clearence ya daraja C hawajui  nani ana Clearence(Uwezo wa kufungua) ya daraja  S.

Kwa mfano kuna  matukio  ambayo yakawa  yametokea katika uongozi wa kwanza wa serikali , matukio kama haya  licha ya kwamba  kuna uwezekano wa kuyafuta  lakini serikali  kama serikali  haipaswi kuyafuta  kutokana na kwamba  kuna siku yanaweza yakahitajika hivyo  hutunzwa katika jalada la siri  nyeti za nchi.

Sasa Hamza alikuwa  akitaka kutoa siri yake kwa  mwanausalama  ambae yupo daraja la juu kabisa ambalo  ni  S kitu ambacho kiliwafanya Mdudu na wenzake kumuona kama ana kichaa

“Unakichaa , wewe ni nani mpaka   mpaka tukutie mtu wa cheo hicho?”Aliongea Afande Mdudu huku akionyesha kutoridhishwa na Hamza kabisa.

“Hamza unapaswa kutuambia ukweli , haina haja ya kupotezena  muda  la sivo tutatumia njia za mateso”Aliongea Afande Wazo.

“Mimi nimekuona kama mtu ambae una akili , lakini hapa unaonekana kama mtoto mwenye  kiburi uliejaa sifa  kiasi cha kutaka kuonana  na kiongozi wa daraja la juu”

“Mnaongea sana ,  ila je kuna hata  mwenye fununu

kati yenu juu ya hicho  kitu kinachoitwa  Ankh?”Aliuliza Hamza 

“Kimya , kama hutaki kuongea ukweli   hatuwezi kuendelea kubembelea”

“Kwahio mpo tayari kutumia nguvu kwa ajili ya hili?,  kama ni hivyo msije kwenda  kinyume na maneno yenu”Aliongea Hamza kwa namna ya tahadhari

Mara baada ya kuona namna  ambavyo Hamza alionekana kutokuwa na hofu  , wote watatu walijikuta wakisaga meno yao kwa hasira.

Kwa yale matukio machache waliokwisha kuona walijua kabisa Hamza  uwezo wake sio kichekesho  , lakini bado  walishangaa kama  alikuwa kwenye  Gereza lao  la  Pango kwanini bado auaonyesha  ukiburi.

“Kama unataka kuonana na kiongozi ambae ana  Clearence daraja S ,  tukuambie tu  kwamba  hata sisi hatuwajui hawa viongozi  maana majina yao ni siri , pili  hata kama tunamjua mmoja wapo  ni watu ambao hatuwezi kuwaambia kiwepesi wepesi lazima  hatua za  maombi  pamoja na sababu za kueleweka zitolewe , kwahio  hili ombi ambalo unataka  halina mantiki, hivyo  hakuna namna tunaweza kulitimiza”Aliongea Afande Maningi. “Kwa ulichoongea  ni sahihi kabisa,  kwa vyeo  vyenu hapa sioni kama kuna amabe atakuwa anawajua hawa  watu wa usalama wenye madaraja hayo ya Clearence , mnaonaje tukifanya hivi,  kwa uelewa wangu katika kila  idara ya ulinzi na  usalama  hapa nchini  wapo  wawili au watatu”Aliongea Hamza na kauli yake ilimfanya  Afande Mdudu na  Afande  Wazo  kuonyesha hali ya wasiwasi maana hawakujua Hamza  imekuwaje akawa  na taarifa hio maana yenyewe ni siri ya daraja C.

“Kuhusu mtu ambae nataka aje hapa  kama sikosei cheo chake kitakuwa ni maarufu kama  Mshauri wa jeshi”Aliongea Hamza kana kwamba anajaribu kukumbuka jina  lakini  kauli yake iliwafanya wale wanajeshi kushituka.

“Unafaamiana na Mshauri  mkuu!!?”Aliuliza  Afande Mdudu  maana alikuwa akifahamu  mshauri mkuu  ndio huyo huyo mshauri mkuu wa jeshi.

“Mdudu  anazungumzia mshauri yupi?”Aliuliza 

Afande Maningi , sio kama hakujua ni kwasababu  kulikuwa na washauri wengi  na  wote walikuwa wanajeshi.

“Ni Generali, Afande Himidu Siwa , unaweza kumuita mkuu wa vitengo  vyote, kwanzia  kitengo cha  TISA, Malibu na kuendelea, hana cheo maalumu ila  anafahamika kwa jina la  code kama Mshauri Mkuu, kwa muda mrefu watu wanajua mshauri mkuu wa  jeshi ni mkuu wa majeshi lakini yeye ndio mshauri  mkuu sasa ,  kwa mtu  ambae  upo nje ya jeshi huwezi kuelewa, Afande Himidu   alipaswa kuwa mkuu wa Majeshi  mara mbili mfululizo lakini  alikosa kigezo cha umri na  kuishia  kutoa ushauri wa  majina ya nani awe mkuu wa majeshi  huku yeye akijipachika cheo cha ushauri  mkuu”Aliongea Mdudu.

Viongozi wengi  wakisiasa walikuwa wakimheshimu  Afande Himidu  kutokana na kwamba ndio ambae alikuwa  na cheo kikubwa katika utunzaji wa siri za nchi , hivyo kwa lugha  nyepesi alikuwa akijua siri nyingi mno.

Kwa namna ambavyo Hamza alikuwa akiongea ni kama Afande Himidu alikuwa akimjua  na hatanii katika hilo na ndio maana iliwafanya   Afande Mdudu na wenzake kuwa na wasiwasi  wakijiuliza amemjuaje.

“Unatuthibitishia vipi kama  Afande Himidu anakufahamu  na kwanini  akubali kuonana na wewe?”Aliuliza Afande Wazo.

“Akigoma kuja  kwa jina  la Hamza, mwambie Murphy anataka kuonana na wewe”Aliongea Hamza.

“Mafiii!?”

Afande Wazo ,  Afande Maningi na Mdudu hawakujua jina hilo lilikuwa linamaanga gani ila limekaa  kwa kingereza.

“Fanyeni haraka maana najua yupo  makao makuu ya nchi , mimi nitatumia huu muda kujipumzisha kidogo  mpaka akija maana mmenichosha bure tu”Aliongea Hamza  na palepale  alipandisha  miguu kwenye  benchi  na kujinyoosha  akiwa  amejiagamiza  na kufumba macho.

Ilikuwa sawa kupumzika  maana kama kweli 

Mshauri mkuu atatoka Dodoma mpaka  kufika Dar basi inaweza kuchukua angalau masaa mawili mpaka kupanda  ndege na kuanza safari.

Walikuwa hawajaridhika na maelezo ya Hamza lakini Afande  Wazo alikuwa makini sana na cheo chake , hakutaka kukurupuka  mpaka  awasilishe ripoti kwanza kwa mkuu wa kitengo chake na kisha mkuu wa kitengo chake  atoe taarifa  kwenda kwa Mshauri mkuu.

“Nitawasiliana na Afande  Msuya  na  atajua namna ya kumfikishia taarifa  Afande Himidu, weka watu hapa wawe wanamwangalia”Aliongea Afande Wazo huku akitoka.

Kesi hio  ya Hamza ilikuwa chini ya  Mkuu wa kitengo msaidizi Afande Msuya  na  kwa kufuata itifaki  hata kama Afande Wazo alikuwa na namba ya   mshauri mkuu basi asingempigia simu moja kwa moja.

“Fanya hivyo  afande , huyu haina  haja  hata ya kumuwekewa watu wa kuangalia , hii sehemu hawezi kutoka hata kama a na uwezo kiasi gani”Aliongea Afande  Maningi na wote walikubaliana nae.

*****

Mji kuu wa kiserikali licha ya kuwa na vumbi  la kuchafua pamoja na jua la saa tisa mchana kwenda saa kumi kuwa kali   kwa  watu wenye vyeo  na  matajiri hawakusumbuliwa na hali hio ya karaha ya   mji.

Haikuwa nyumba kubwa sana wala ndogo sana , ilikuwa ya wastani lakini  yenye mazingira ya kuvutia  ambayo yaliwakilisha hadhi ya mtu  anaeishi ndani ya hilo eneo  katika mtaa maarufu wa Mji mpya.

Upande wa eneo la bustani ndani ya  nyumba hio walionekana   watu wawili  mwanamke na mwanaume wakiwa wamekaa katika  eneo la bustani la kupumzikia pembeni ya Swimming pool.

Mwanaume alikuwa amevalia  tshirt ya rangi ya ugoro  , jeans na  American boot , alikuwa  na kipara na muonekano wake ulikuwa wa kawaida  lakini macho yake  yalijaa umakini ulioonyesha utulivu wa akili..

Upande wa mwanamke  aliekuwa nae alikuwa mrembo haswa alievaa akapendeza , nywele zake  ambazo haikufahamika ni za bandia au asili zilikuwa  ndefu na nyeusi zilizomfikia mgongoni , alikuwa amevalia  kana kwamba ni mgeni ambae yupo ndani ya hilo eneo kwa ajili ya kumpagawisha mwanaume aliekuwa pembeni yake.

“Ni watu wachache sana ambao wanaweza kucheza mchezo wa Chess hapa nchiin  na mmoja wapo ni wewe Sophia . ijapokuwa nakwenda kushinda hii mechi lakini niseme umezidi  kuimarika tokea  mara ya mwisho tulivyocheza pamoja , sio mbaya licha  huwezi kunishinda  pengine siku zijazo utafanikiwa ukiendelea na mwendo huu huu”Aliongea  yule mwanaume kwa sauti nzito na kisha alichukua  chupa ya maji na kunywa kidogo huku akimsubiria yule mwanamke mrembo  kucheza.

Wawili hao walikuwa makini katika kucheza mchezo maarufu wa Chess.

Mwanamke yule mrembo  alionekana kukodolea  ubao ule wa kuchezea kwa macho yenye hali ya kutafakari kwa  kina,  upande wa mwanaume simu yake  ya  batani  iliokuwa na mkonga mkubwa  ilianza kuita  na aliichukua na kuipokea.

“Ongea!”Alitikia  akiwa sirasi , mara nyingi akipokea simu kupitia  simu hio basi ni ya kikazi  ndio maana anakuwa siriasi.

“Mshauri mkuu , jina langu ni  Afande Msuya..”

“Hebu  acha kuzunguka nishakufahamu , nenda moja kwa moje  kwenye pointi”Aliongea kwa sauti ya amri  kama mtu ambae hakupendezwa kupigiwa simu hio.

“Sawa afande , ipo hivi  kuna operesheni maalumu ya ki uchunguzi ambayo inaendelea hapa kitengoni chini yangu  , katika operesheni hii tumeweza kumkamata   mtuhumiwa anaefahamika kwa jina  la Hamza Mzee , nimepokea simu kutoka kwa  wanausalama  wakiwa wanamfanyia mahojiano na amekataa kutupa taarifa  na anataka kuonana na wewe  Afande”Aliongea .

“Hamza Mzee!!”Aliongea yule bwana huku akionekana kama vile  anawaza wapi amesikia hilo hina lakini hakukumbuka.

“Simfahamu mtu wa jina hilo mimi , hili  swala mnaweza kudili nalo wenyewe sidhani linahitaji ushauri wangu , sitaki ripoti za namna hii  kuripotiwa kwangu”Aliongea na  muda ule wakati akitaka kukata simu upande wa pili uliropoka.

“Anasema  Murphy  anakuita”Aliongea  na  jina lile  lilimfanya yule bwana  mwenye  sura  ya maji ya kunde kukunja sura  kiasi cha kumfanya mwanamke mrembo aliekuwa pembeni yake  kumwangalia kwa wasiwasi.

“Wewe.. umesemaje hebu rudia vizuri?”

“Amesema kama humtambui  kwa jina la Hamza, nikuambie  Mafi…. Murphy anakuita”Sauti upande wa pili ilirudia na kumfanya  yule bwana kuvuta pumzi nyingi na kuzishusha.

“Waambie wanisubiri wasifanye chochote , narudia huyo mtu ambae  umesema anaitwa Hamza  asichokozwe , nitafika hapo ndani ya lisaa limoja au mawili  yajayo  kwa kutumia chopa  ya jeshi”Aliongea kwa msisitizo.

“Mshauri  ni kweli unafahamiana na huyu  Hamza?”Upande wa pili uliuliza kwa namna ya mshangao.

“Hata mimi simjui  ni nani  mpaka nimuone  mwenyewe”Aliongea na kisha palepale alikata simu.

“Sophia  nataka kwenda Dar es salaam mara moja , nina haraka , vipi  tuongozane wote?”

Mwanamke huyo mrembo alievalia nguo za rangi nyekundu aliishia kutingisha kichwa kukataa  bila ya kusema neno.

“Naona  kwa leo  mechi yetu inaishia hapa ,

isitoshe  sikuwezi  na  nakufanya  usifurahie mchezo,  nakuombea apatikane mtu wa kuendana na uwezo wako”Aliongea kwa namna ya  kuvutia  kana kwamba anamtega.

“Nadhani kuna kitu kingine tunaweza kupimana uwezo”Aliongea na kauli yake ilimfanya  yule mrembo ukauzu kumvaa palepale  na ghafla tu aliinua mkono wake  wa kulia na kuanza kuchezesha vidole katika muundo  wa  ajabu na hazichukua sekunde  vitu kama moshi moshi ulitawala vidole vyake.

“Upo sahihi ,  siku nyingine nitakuonyesha   ufunuo niliopata kwenye kuvuna nishati za mbingu na ardhi”Aliongea .

“Naisubiri hio siku kwa hamu kubwa”Aliongea  Afande Himidu  na  yule mwanamke  alitingisha kichwa na  kisha akasimama  na kitendo cha kuinama  kama mchawi alipotea palepale.

********

Masaa  kama mawili  mbele   katika eneo la kambi  ya jeshi walionekana  Afande Mdudu na  wenzake wakipiga saluti mbele  ya Kamanda  Himidu anaeshuka kwenye chopa  huku wakijitahidi kupotezea wasiwasi wao na tabasamu la kulazimisha.

“Afande  umetokea  ghafla sana , tulikuwa tukipanga kuja kukupokea na escort”Aliongea Afande Wazo lakini upande wa Afande Himidu hakuwa na muda wa kuongea nao  kwani baada ya kutoka kwenye chopa  aliwapita.  “Huyo Hamza  yupo wapi?”Aliuliza

“Yupo ndani ya  Dragon Lair  Afande”

“Nini!, yaani mmefungia ndani ya hilo  gereza, vipi hakuwaletea ukinzani wowote?”Aliongea huku akionyesha mshangao kidogo.

“Afande hakuleta ukinzani pengine ameogopa  wingi wetu , anaweza kutushindwa mmoja mmoja

lakini  kwa wingi wetu hawezi kufanya chochote”Aliongea Afande Wazo  kwa  majigambo.

“Una akili kweli wewe , unajua hata ninachomaanisha , nakuuliza je mpo salama?”Aliuliza  lakini  swali lake liliwachanganya.

“Afande unauliza nini kuhusu usalama?”Aliuliza lakini Afande Himidu hakutaka hata  kuwaelezea kile anachoataka kumaanisha.

Afande huyo mara baada ya  kuingia ndani  na kumwangalia Hamza kupitia kioo  kizito kilichokuwa mbele yake  mshangao ulivaa palepale huku   pumzi yake ikiwa nzito ni kama vile  ameona mtu  ambae hakutarajia kumuona.

“Mshauri  yule ndio Hamza”Aliongea Afande Maningi.

“Nani alietoa wazo la kumfungia  pale?”Aliuliza akiwa siriasi  na kuwafanya Afande Wazo  na Afande Maningi kuangaliana , wao sio ambao walikuwa wamemkamata Hamza  Afande  Mdudu  ndio alifanikisha hilo  na wao walipewa jukumu la kumhoji pekee.

Previoua Next