Reader Settings

 

Hamza alijikuta  akishikwa na soni , ijapokuwa  haikuwa makusudi  aliona pia  sio sawa , aliuliza ili kupata majibu na hakujua angemkasirisha Regina kiasi hicho, aliona pengine uelewa wake  juu ya wanawake una kasoro na anatakiwa kuanza  kujifunza upya.

“Toka  kwenye ofisi yangu sitaki kukuona!”Aliongea Regina  kwa kufoka.

Hamza aliishia  kushusha pumzi akikubali kushindwa maana hakutaka  kumwagia  moto  mafuta , hivyo  kimya kimya alitoka ndani ya ofisi  ya Regina.

Regina mara baada ya kuona  ni kweli Hamza kaondoka  aijikuta akipandwa na hasira mara  mbili zaidi  na kuanza kumlaani ndani kwa ndani   huku macho yakiwa mekundu, aliangalia  viboksi vya matunda alivyoleta Hamza na kwa hasira alivichukua na kwenda kutupia kwenye Dustbin kama kwamba  ndio anamtupa Hamza.

Upande wa Hamza alikuwa na mawazo , baada ya kutoka ndani ya ofisi ya Regina alikuwa akiipiga namba ya simu ya Eliza mfululizo lakini  ilionekana mwanamke huyo amezima simu.

Muda huo  alichotamani ni kwenda nyumbani  kwake kumuangalia  lakini alikumbuka ahadi yake  na Yonesi muda ule  kwa ajili ya kumuelekeza baadhi ya mafunzo hivyo hakutaka kuivunja na kuona aanzie huko  na kisha ndio akamtafute Eliza.

Muda ambao alifika ndano ya floor ya  kufanyia mazoezi Yonesi alikuwa amekwisha kufika na alikuwa akipasha mwili, alikuwa amevalia  mavazi ya mazoezi tayari   na ilionekana alikuwa akitegemea kujifunza  kitu kipya kutoka kwa Hamza kwa hamu zote.

“Kapteni wewe ni mwanamke , kwanini upo siriasi sana na swala la  mapigano?Aliuliza Hamza  mara baada ya kuona namna ambavyo Yonesi alionekana kuwa siriasi.

“Kwani ni vibaya, unadhani mwanamke hana haki ya kujifunza vitu ambavyo anaweza kujifunza  mwanaume?”Aliuliza na Hamza alitingisha kichwa kukubaliana nae , isitoshe aliuliza kumtania tu.

“Ngoja tuanze haraka  ili  tumalize, kuna sehemu nataka kwenda”Aliongea Hamza. “Kama una haraka kwanini tusifanye siku nyingine ,  mimi sio jiniasi  naweza nisikumbuke kila kitu   kwa  maelekezo ya muda mfupi”Aliongea Yonesi huku akiwa siriasi.

“Utakumbuka maana nakwenda kukufundisha   kitu chepesi sana , ndani ya saa tu utakumbuka kila  kitu”Aliongea Hamza na kisha alianza  kuonyesha  ufundi wake.

Yonesi mara baada ya kuona miondoko kadhaa kutoka kwa Hamza alijikuta akishangaa zaidi  huku akikunja sura 

“Hamza ijapokuwa uwezo wangu wa kimapigano ni  mdogo lakini huwezi kunitania na ulichonionyesha , hayo sio mafunzo bali ni kama kucheza mziki”

“Kapteni acha uharaka, wewe fanya kama nilivyokuelekeza  na uone kitakachotokea”Aliongea Hamza.

Yonesi aliishia kuonyesha kutoridhika  lakini alisogea kati na kuanza kujikakamaza kuigilizia kile ambacho ameonyesha Hamza.

“Mguu  wako  wa kushoto unatakiwa kuukunja zaidi kwenda nyuma  na viganja vya mikono  yako vigeuzie kuelekea juu  na mguu wa kushoto  upindishe  kwenda mbele…”

Hamza alianza kuelekeza huku Yonesi akifuatisha hayo maelekezo na kadri alivyokuwa amekaa katika  mtindo huo wa maelekezo uzito wa mwili wake ulianza kuongezeka kila dakika na alianza kuvuta pumzi kwa haraka 

“Bado kuna kitu  hukipati , mguu wako wa kushoto haujaunyoosha na wa kulia haujaupindisha  kwa angle sahihi,  ndio maana unaanza kukosa balansi ya mwili”

“Naupandisha kwa angle ngapi sasa?”

“Angalau  zifike sitini”

“Angle sitini!!”Aliongea Yonesi  akishanga kwa uona ni nyingi.

“Ngoja nikusaidie kukuweka sawa”Aliongea Hamza  na licha ya Yonesi kuonyesha wasiwasi alimshika vizuri  paja na mikono na  taratibu akaanza kumnyoosha.

Licha ya kupokea  malalamiko  kutoka kwa Yonesi asiende mbali kwenye kumgusa maeneo nyeti  lakini Hamza alijifanyisha kuwa siriasi  zaidi na kutomzingatia lawama zake. 

Baada ya dakika kadhaa za kuchukua mazoezi ya kubalansi mwili alijikuta akishangaa, maana mwanzoni alidharau lakini aligundua ni kuna kitu cha upekee katika mafunzo hayo alianza kukipata.

“Hii ni aina gani ya mafunzo?”

“Hii ni mbinu ambayo nimeitengeneza mwenyewe  ili kurahisisha mazoezi ya  balansi  mwili , ukirudia  kujikunja  mara  mia moja  nitakufundisha  hatua inayofuata”

“Mara mia!!”

Aliongea Yonesi kwa  mshangao maana alikuwa amechoka kwa mzunguko huo mmoja tu na kuona mara mia itakuwa ni nyingi mno.

Kwasababu Hamza alikuwa na haraka  alimwambia awe siriasi na alichomwelekea ili amfunidshe hatua nyingne ,  licha ya Yonesi kujihisi kuchoka  aliishia kutingisha kichwa kukubali  na Hamza aliondoka haraka haraka kwenda kumtafuta Eliza.

*****

Ni muda wa saa nane kama na nusu hivi  alionekana  Kanali Dastani  akiingia ndani ya ofisi  yake akitokea  kwenye  kikao ambacho kiliitishwa na  Mkurugenzi mkuu wa kitengo.

Alionekana kuwa na  uso uliosawijika, mtu ambae ni kama amepokea taarifa ya kitu ambacho hajaridhishwa nacho lakini hana jinsi.

Akiwa  ana nyonga tai yake vizuri mlango wa ofisi yake uligongwa  na aliruhusu anaegonga kuingia na mara baada ya kugeza macho kumwangalia alieingia alionyesha tabasamu hafifu.

“Vipi Afande Mdudu kuna tatizo?”Aliongea  Kanali Dastani huku akimkazia macho.

“Afande  nilidhani utahitaji mtu wa kuongea nae ,  kwenye kikao hukupata mtu wa kukuunga mkono mawazo yako ,  kitu ambacho sio kawaida”

“Kwahio umekuja kuniunga mkono baada ya kikao kuisha?”Aliuliza Afande  Dastani huku akikunja sura.

Afande Mdudu aliishia kutoa tabasamu na kisha alisogea na kwenda kukaa  kwenye sofa.

“Hoja uliotoa ilikuwa ina mashiko  Kanali , lakini   unajua fika sisi ni wanajeshi , ijapokuwa mawazo yetu yanahitajika kwenye vikao lakini ikitokea kitu kishaamuliwa  kikao kinafanyika kutufahamisha kinachoendelea na sio  kusikiliza hoja zetu”Aliongea.

“Kama unachoongea unamaanisha basi ulipaswa kuuvaa ujasiri na kuunga mkono  hoja yangu”

“Hoja yako ilikuwa na  mantiki lakini haimaanishi ilikuwa uhalisia , swala la  kesi zote zinazohusiana na Hamza  kufungwa  halipo ndani ya kitengo chetu tu mpaka TISA  pia”Aliongea na kumfanya Kanali macho yake kuchanua.

“Mpaka TISA!!”

“Nimesikia taarifa hizi tokea juzi,Hamza alikuwa kwenye  rada za usalama wa taifa kwa muda mrefu sana, ukiangalia  hii kesi kwa umakini  haina vigezo vya kuwa chini  ya kitengo chetu ndio maana  nikasema imekosa uhalisia licha  kwa  jicho pana la  kichunguzi ilikuwa na mantiki” “Kama uhalisia wa hii kesi umekosekana katika kitengo chetu pekee kwanini Mshauri mkuu aingilie mpaka kwenye  idara nyeti ya  intelijensia ya taifa, hata kama ni swala la uchaguzi  haliwezi kufanywa na  watu wote wa kitengo”

“Swala  la uchaguzi kwasasa ni nyeti sana kwa usalama  wa taifa kosa kidogo  kunaweza kutokea  machafuko ,  swala la Jongwe  kufariki  limefanya  idara zote za usalama kuwa katika  tahadhari”

“Hio haikuwa hoja yangu Mdudu , najua

Uchaguzi ni swala la  juu kabisa kwa nchi   lakini  hili lipo chini ya  kitengo cha TISA na idara nyingine za usalama, Malibu ni Kitengo cha jeshi kazi yetu sio kuangalia  upande mmoja tu wa nguvu zizisokuwa za kawaida”

“Hoja yako nakubaliana nayo , lakini mpaka sasa zimebakia  siku  kumi na tano tu zoezi la kupiga kura lianze, Mshauri mkuu  ni mtu ambae hawezi kufanya maamuzi juu ya kitu kinachohatarisha usalama wa nchi”Aliongea  Afande Mdudu na  Kanali alionekana kufikiria kwa dakika   kadhaa   na kutingisha kichwa kukubaliaa nae.

“Unaonekana  kumchukia sana huyu Hamza, Norbert na  ujanja wake alishindwa kumkamata ilikuwaje  wewe mpaka Mshauri mkuu akaingilia?”Aliongea.

“Huwa  likija swala linalomuhusu Yonesi  nakuwa jasiri mno”

“Haha.. Afande  Yonesi!, kwanini?”

“Dastani acha kunikejeli ilihali unajua kinachoendelea”Aliongea Mdudu huku akiongeza usiriasi na kumfanya  Afande Dastani kutoa tabasamu  lilojaa ukejeli.

“Wewe na Amosi mmeteswa sana  na  penzi la Yonesi , ulienda mbali mpaka  kumtumia baba yako umuoe  lakini ‘kiko wapi’  kitisho kidogo  umeufyata”

“Usinilinganishe na Mzee, Amosi ni  mtu mzima aliejaribu bahati  yake kwa Yonesi , mimi ni kijana  ambae sikuwa nikibahatisha ila nilipigania kile ninachokitaka, mwanajeshi  mwenye busara ni yule  asiemdharau adui yake , natafuta namna ya kumrudia”Aliongea na kumfanya Kanali kutoa cheko.

“Likija swala la Yonesi unakuwa siriasi sana , anyway niambie   unachohitaji ,  nadhani hujaja kwenye ofisi yangu kupiga soga wakati ni muda wa kazi huu”Aliongea   na kumfanya  Afande Mdudu kukaa vizuri.

“Nataka  kujiunga na ushirika  Black 

Trinity”Aliongea  Mdudu  kwa sauti ya chini  na kumfanya  Amnosi kushituka 

“Unaongea nini Mdudu?”

“Acha hizo  kanali  najua wewe ni mwanachama  na  ili  nijiunge  lazima  nipate mwaliko kutoka kwa mwanachama”Aliongea  Mdudu na Ghafla  tu ni kama   Kanali Dastani  amebadilika na  kuwa  kivuli kwani alipotea alipokuwa amesimama na  kuja kusimama Mdudu alikuwa  amekandamizwa kwa nguvu kwenye  ukuta huku akiwa amekabwa shingo.

Kilikuwa ni kitendo cha maajabu mno na cha haraka sana alichokifanya  Kanali Dastani lakini ajabu Mdudu licha ya  kukabwa hakuonyesha hofu ya aina yoyote lakini upande wa Dastani  hakuwa wa kawaida, ni kama amegeuka na kuwa  kiumbe cha ajabu.

“Unajua unachokiongea!?”Alikoroma  Dastani  huku akimwangalia  Mdudu wa macho ya kuogofya.

“Kanali  huwezi kunifanya chochote , najua  wewe na Tresha Noah mpo  kwenye Uwili  na kama nitapoteza  maisha hapa picha zenu mkifanya mapenzi  ya rafu  zitasambaa mtandaoni , hebu fikiria kitakachotokea na kisha upunguze presha  tuongee vizuri , siri yako ipo salama  na mimi  kama utanipatia mwaliko, ombi jepesi sana”Aliongea Mdudu huku  akionyesha tabasamu  la kejeli  lililoambatana na macho kodo.

 

*****

Hamza  aliweza kufika  ndani ya Apartment anayoishi  Eliza na baada ya kugonga   kwa  dakika kama  moja hivi mlango ulifunguliwa na Eliza aliekuwa  katika mavazi ya nyumbani.

“Hamza ni wewe , unafanya nini hapa?”

“Eliza   nini kinaendelea , kwanini umezima simu  na umeomba   kwenda kufanya kazi nje ya nchi?”Aliongea Hamza akiruka hata salamu. Kwa jinsi ambavyo  mwanamke huyo alivyoonekana , ilikuwa ni dhahiri kabisa kuna kilichokuwa kikiendelea,  alionekana alikuwa na wasiwasi mno  kiasi cha kumfanya uso wake kupauka.

“Eliza ni nani anagonga?”Sauti  kutokea ndani  ilisikika na Eliza aliishia kurudi nyuma akimpa nafasi  Hamza ya kuingia ndani.

Muda  huo sasa Hamza alipata kumuona mwanamke  mtu mzima  hivi  ambae kwa haraka haraka ilionyesha umri umeenda.

“Mama shikamoo , naitwa Hamza  mimi ni mpenzi wa  Eliza”Aliongea Hamza  bila aibu  na kauli  ile ilimfanya  Eliza  kukakamaa mwili  na aibu juu kwani ilikuwa ni kama hakutegemea.

Haikuwa kwake tu hata kwa mama huyo alionyesha hali ya kushangaa maana  ni kama hajawahi kukutana na tukio  la mwanaume kujitambulisha kwa kujiamini na pili  hakuwa akijua kama Eliza alikuwa na mpenzi.

“Mama Mkubwa hapana huyo sio  ”

Hamza hakumpa hata muda wa kumaliza kuongea na  alimsogelea yule mama.

“Mama Mkubwa kama nilivyojitambulisha, napaswa kujua nini kinaendelea ama mpenzi wake ili kumsaidia   maana  Eliza hataki kuniambia, nimemtafuta sana kwenye simu”

Kauli ile ilimfanya  yule  mama kumwangalia Eliza kwa sekunde kadhaa  na ilionekana  alikuwa na uzoefu  wa kutosha kwani kuna kitu aliweza kukisoma tayari kutoka kwa Eliza.

Licha ya  kwamba alikuwa na mshangao lakini kwa wakati mmoja pia alionyesha kuwa na tumaini.

“Baba!,   wewe kweli ni  mchumba wa  Eliza?”Aliuliza yule mama.

“Ni kweli kabisa Mama Mkubwa , Eliza ni mpenzi wangu na nampenda sana, nipo tayari kwa lolote kwa ajili yake”Aliongea Hamza  ilikuwa ni kama  amepata  hadhira  ya watu kwa ajili ya kuelezea hisia zake.

“Eliza  ni kweli?!”Aliuliza Mama Mkubwa  kwa  shauku huku akimkazia macho  Eliza  lakini  mrembo huyo  hakujibu zaidi ya kuinamisha kichwa chini , ukweli ni kwamba alikuwa na  hisia   ambazo haikuwa rahisi kuzielezea  alikuwa akimpenda Hamza lakini tokea asikie Hamza ni mume wa bosi wake  hakujua  tena Hamza ni mpenzi wake au ni nani kwake.

Wahenga wanasema ukimya ni  jibbu  pia  , hivyo kwa  Mama Mkubwa yake  Eliza  aliweza  kujua watakuwa kweli ni wapenzi ila kuna  kinachoendelea kati yao.

“Baba nitakuelezea kilichotokea kama Eliza anagoma kukuambia unaweza  kuwa  na msaada”Aliongea yule Mama  huku akimuona Hamza kama mtu ambae ni kweli anao uwezo wa  kumsaidia kutokana na mwonekano wake wa kitajiri na kujiamini.

“Mama Mkubwa  hapana..”Eliza alitaka kumzuia  lakini Hamza  alimkatisha.

“Mama Mkubwa naomba uniambie, nadhani unamjua Eliza ni mwanamke  wa aina gani , asiponiambia  nitashikwa na mawazo mengi na sitojua namna ya kusaidia”Aliongea Hamza na Mama Mkubwa alivuta pumzi na kisha alikaa chini huku akionyesha kuwa katika hali  ya mawazo.

“Mama Mkubwa ngoja nimwambie”Aliongea  Eliza na kuingilia mara moja , aliona sio vyema kama  Mama Mkubwa akichukua nafasi yake.

Hamza maara baada ya kumsikia Eliza akiongea hivyo alijikuta akivuta  pumzi ya ahueni sasa maana alijua kama hatoambiwa kinachoendelea  ukichaa wa hasira  ungemshika.

“Baba amekamatwa..”Aliongea  kwa sauti hafifu. “Baba yako mzazi amekamatwa?”Aliuliza Hamza kana kwamba hajasikia vizuri na Eliza alitingisha kichwa kukubali.

“Imekuwaje baba yako akakamatwa  na waliomkamata ni  wakina nani?”

“Unakumbuka nilikuambia baba yangu ni mstaafu na yupo kijini?”

“Ndio nakumbuka?”

“Basi  baba baada ya kurudi nyumbani sikuwa  nikijua kinachoendelea , ubize niliokuwa nao juu ya  kumuuguza  mama umenifanya  nisifuatiilie yanayoendelea  kijijini , Baba alivyorudi  alishawishiwa na kaka yangu  kujiingiza katika  biashara ya  uchimbaji  madini huko Mkoani

Njombe…”

Eliza  aliendelea kumsimulia Hamza kilichotokea  na ilionekana  baba yake  alitapeliwa.

Eliza anasema  kuna  wataalamu  wa utafiti wa maswala ya madini walifika mkoani Njombe  na kufanya utafiti  wa uwepo wa Dhahabu ndani ya maeneo ya msituni ya mkoa huo ,  moja ya watu  wa ndani ya mkoa walioshiriki katika utafiti huo ni  kaka yake  Eliza anaefahamika kwa  jina la Hebert Mlowe, baada ya watalaamu wale  kumaliza utafiti walitoa  majibu yao kwa  vijana wa mkoa huo ambao waliambatana nao ikiwemo Hebert  na walisema eneo x  katika shamba  la Mzee Mlowe kuna kiasi kikubwa cha  madini  ya dhahabu ambacho  kipo ardhini, majibu hayo ya kitaalamu yalimfanya kijana Hebert kupatwa na tamaa kubwa sana  huku  tamaa yake ikimpoza na kuamini kila kitu  ambacho wataalamu walisema.

Baada ya watalamu wale  kuondoka wakiahidi  kurudi kwa ajili ya  utaratibu wa  kuanza uchimbaji , Hebert  hakutaka  fursa ya kuwa tajiri impite hivi hivi  hivyo  aliwajumuisha na wale vijana wenzake walioshiriki na wataalamu hao kisha  walimpelekea  taarifa mzee Mlowe juu ya uwepo wa  madini  ndani ya shamba lao  la miti ya biashara , Hebert bila ya kuwa na uhakika  alimhakikishia baba yake  eneo hilo la shamba lao limebeba mali nzito itakayobadilisha maisha yao  kabisa   na Mzee Mlowe   alijikuta akishawishika na  kutumia kiinua mgongo chake chote kuwekeza katika uchimbaji  wa Dhahabu,  kiasi  cha hela ambacho kilikuwa  ni kidogo kutokana na kumaliza karibia ya robo tatu ya hela yote..

Baada ya kuchimba kwa muda wa mwezi mmoja hawakuambulia chochote na kiasi cha pesa walichowekeza   kiliishia kwenye mchakato na kununua vifaa, yalikuwa matokeo mabaya kwao lakini Mzee Mlowe hakukata tamaa baada ya Hebert   kumhakikishia wataalamu walisema madini yapo chini sana hivyo  wasikate tamaa na  kuendelea kuchimba..

“Nini kilitokea baada ya hapo?”Aliuliza Hamza huku akijua  nini ambacho kinaenda kutokea.

“Walichukua mkopo  kwa  ajili ya kuendelea  na aliewakopesha  aliwapa kiasi mara kumi ya kile walichoomba”

“Na  ndio kiasi gani?”Aliuliza Hamza  na kauli ile ilimfanya hata Mama Mkubwa kujiinamia kichwa chini kuna namna Hamza aliona pia huyo mama alihusika.

“Milioni mia tatu, baada ya kupewa  kiasi kikubwa  hivyo cha pesa ukichaa wa hela uliwavaa, mwanzoni wakati baba amewekeza kaka  na marafiki zake walihusika kwa  kuchimba lakini mara baada ya kupewa mkopo  hawakuchimba tena na waliweka vibarua , lakini hela yote hawakuitumia  kama  ilivyohitajika  kwani walianza kufanya starehe na kucheza kamari”Alingea Eliza huku akiona hata aibu ya kumwangalia Hamza  machoni.

“Kwanza inaoneana   kilichotokea ulikuwa  mpango  wa hao watalaamu na pengine hawana utalaamu wowote na  ndugu zako walikuwa wakiingizwa kwenye mtego , pia  kitendo cha wakopeshaji  kuwakopesha  zaidi ya mara kumi ya kiasi  cha hela walichotaka  inaleta mushikeli ya  matukio yote kuwa na muunganiko”Aliongea

Hamza na  Eliza alitingisha  kichwa kukubali.

“Sikujua  kinachoendelea, mbaya zaidi baba  ndio aliehusika  katika taratibu zote za kuomba mkopo”

“Waliahidi nini  kama dhamana ya mkopo?” “Asilimia hamsini ya faida itakayopatikana kwenye  kuuza madini watakayopata”Aliongea  Eliza na  kauli ile ilimfanya Hamza kukunja ndita huku akipatwa na msisimko wa kujua kwa undani  ni mpango gani  unaendelea.

“Kwahio  waliomkopesha baba yako baada ya kushindwa  kulipa mkopo  ndio hao waliokuja

kumkamata?”

“Bado sijajua , waliomkamata baba walijitambulisha kama polisi, lakini baada ya ndugu kwenda kituo cha polisi  hakukuwa na  taarifa zao  jambo ambalo  lilishangaza  , baada ya  kusumbua sana polisi  wamesema Baba amesafirishwa  kuja  huku Dar es salaam , lakini mpaka sasa  tumeshindwa kupata kujua baba ameshikiliwa  gereza lipi  na polisi hawataki kutoa ushirikiano..”Eliza alikuwa akitia huruma kweli.

Hata Hamza alimuonea huruma , isitoshe  ilikuwa ni kama  kila matatizo ya familia Eliza  ndio aliekuwa akihusishwa kwa kiasi kikubwa kuyabeba, kwanzia swala la mama yake mpaka swala hilo la familia yake.

“Kaka yako yeye yupo wapi?”

“Herbert ametoroka  na milionni therathini  zilizobakia na mpaka sasa hajulikani alipo”. “Poleni sana,  hili swala nitalifanyia kazi ndani ya  muda mrefu nitapata majibu , niambie ni watu gani ambao wametoa mkopo”

“Hamza unataka kufanya nini?”Aliuliza Eliza kwa wasiwasi.

“Hili swala mkiliendea kisheria hamtopata majibu  kwa uharaka , hapa  sio swala la  mkopo kuna kitu kingine kinachotafutwa”

“Hamza sitaki  kukuingiza kwenye matatizo yangu ya kifamilia, nimeenda benki  kwa ajili ya kuomba mkopo  kwa ajili ya kulipa mkopo  huo na baada ya hapo  nimeomba nafasi ya kwenda  kufanyia kazi  nje ya nchi, kule malipo ni maradufu  zaidi ya hapa ,ndani ya miaka mitatu nitaweza kurudisha kiasi chote”Aliongea Eliza  huku akionyesha hali ya usiriasi  kwenye macho yake.

Licha ya kwamba Hamza alikuwa na hasira ya Eliza kutomhusisha katika matatizo yake lakini vilevie alizidi kumpenda , alikuwani mwanamke ambae hakosi njjia ya kutokea , lakini alijua kama akiruhusu swala hilo litokee basi  mrembo huyo ataishia kupoteza ujana wake tu kwenye ulipaji wa madeni.

“Eliza unajua  kabisa huu ni mtego umewekewa  kwanini unataka kulipa kirahisi , ni  kweli  ndugu zako waliingizwa kwenye mtego lakini hujiulizi ni

kwanini  iwe ni kwa familia yako tu?”Aliongea Hamza

“Najua  lakini bado nashindwa  kuelewa  kwanini haya yanatokea?”

“Hatua ya kwanza ya kutatua tatizo ni  kujua kiini chake ni nini , unaweza ukaenda  nje ya nchi  , unadhani kila  kitu kitaishia hapo?”Aliongea Hamza huku akipandisha sauti na Eliza aliishia kuinamisha kichwa chini.

Ukweli Hamza alikuwa  kuna kitu ambacho Eliza hamwambii na alijua kuna uwezekano wa hicho kitu  ndio kilichoifikisha familia   yake katika hatua hio ya kutengenezewa mtego.

“Eliza  niambie  kila kitu  ili  nipate kukusaidia , kukubali matatizo bila ya kujua chanzo  sio  njia sahihi ya kuyatatua”Aliongea Hamza  huku akimwangalia Eliza.

Kitendo cha kuangaliana  kwa sekunde kadhaa na Hamza  machozi yalianza kumtoka mfululizo  na haikuchukua hata sekunde alianza kulia kilio cha kwikwi  jambo ambalo  si tu kumshangaza Hamza lakini pia lilimshangaza na Mama Mkubwa wake.

Hamza alijikuta akihisi  hisia mchanganyiko kwenye moyo wake , ilionyesha Eliza alikuwa akipitia wakati mgumu mno na kujitahidi sana kuficha kile ambacho anapitia na hali hio ilimfanya Hamza  kuona licha ya kwamba  walikuwa na muda mchache tokea wajuane  ila hakuwajibika vya kutosha.

Aliishia kumkumbatia  pekee  na kumfuta machozi  tukio ambalo lilionyesha kumgusa sana Mama Mkubwa.

“Eliza nyamaza na niambie nini  kimekutokea”Aliongea Hamza kwa kumbembeleza lakini  ilikuwa ni kama anaongezea mafuta kwenye   moto.

Dakika chache baadae  Eliza aliweza kutulia sasa na kuanza maongezi.

“Unakumbuka siku  ambayo ulinikuta   kwa mara ya kwanza  nikidhalilishwa na watu ambao niliwakopa??”Aliuliza na Hamza alitingisha kichwa kukumbuka.

“Wale  uliowakuta hawakuwa wahusika wakuu?”

“Unamaanisha kuna muhusika mwingine?”Aliuliza Hamza  akiwa na utulivu na Eliza alitingisha kichwa kukubali.

“Kuna  mwanaume   nilikuja kukutana nae kipindi  mama amelazwa hospitali ya taifa , hii ilikuwa ni siku kadhaa baada ya kupata mkopo kwa  ajili ya kulipia matibabu ya mama , nakumbuka kwa mara ya kwanza nilikutan nae hoteli ya Serena  akiwa  pamoja na aliewahi kuwa   Dokta wa hospitali ya taifa  ambae alijaribu   kunitaka kingono  ndio mama afanyiwe matibabu , bahati nzuri nilikutana na  Dokta  mmoja  ambae sasa hivi  ni  mkufunzi wa chuo cha Uchumi ,  ndio alienisaidia  kufichua ushenzi ambao alikuwa akifanya yule Mkurugenzi kwani kesi  zake zilikuwa nyingi kiasi cha serikali kumuwekea mtego”

“Ilikuwaje ukakutana nae Serena?”Aliuliza Hamza.

“Wakati  mama anapatiwa matibabu  huyu dokta aliniita ofisini kwake  na kuanza porojo zake za kunitaka kimapenzi, nilikuwa nimechanganyikiwa kipindi kile  na sikumpa jibu , siku kadhaa mbele aliniita  hotelini na ndio  nilikutana  nae”

“Hili ni  tukio la pili anaombwa rushwa ya ngono  na daktari?”Aliongea Hamza  ndani kwa ndani huku akikumbuka tukio lile la Kigamboni.

“Kwahio unaamini huyo mwanaume ambae ulikutana nae huko hotelini ndio chanzo?” “Ndio chanzo cha kile ambacho kilikuwa kikiendelea kwa Amosi na genge  lake , Amosi ndio alienikopesha hela kwa ajili ya matibabu , kipindi kile nilikuwa desparate  kumtibia mama na sikuwa na kazi ya kueleweka mpaka nilipokutana na Regina, baada ya kupata mkopo  baadae ndio nilikuja kukutana na huyo mwanaume ambae alichokuwa akitaka  kwangu ni kilekile , nilale nae  kwa siku tano  kisha afute mkopo wangu , nilimkatalia na matokeo yake yalikuwa ule udhalilishaji ulionikuta nao na nilishangaa hawakuja tena kunidai na  kuomba msamaha kabisa”Aliongea Eliza.

“Wale  niliwapa onyo mimi ndio maana hawakukusumbua tena  , kama ulivyosema ni kweli basi huyu mtu  bado hakuwahi   kukata tamaa juu yako , lakini inafikirisha sana , kama yeye  kweli ndio  mhusika na ameenda mbali mpaka kumwingiza baba yako kwenye mtego  basi kuna cha ziada”Aliongea Hamza.

“Wewe ndio uliewazuia kipindi kile? , kama ni hivyo kwanini unaamini kuna kitu cha ziada?”Aliongea  Eliza huku akionyesha mshangao na  macho ya shukrani kwa Hamza , hakuwahi kujua kama  Amosi  kutokumsumbua  Hamza ndio alihusika lakini alipatwa na woga baada ya kuona  pengine mzee yule  sio  ngono pekee  anayotaka kutoka kwake.

Hamza kuna kitu ambacho alikuwa akifikiria  lakini hakuwa na uhakika kama ni kweli na  alipaswa kulitafutia  hilo swala ufumbuzi, aliwaza hilo kutokana na uzoefu wake.

Hamza muda huo  alikuwa ameweka umakini kwa Eliza na alisahau hata kuna mama aliekuwa pembeni  na baada ya kugeuka aligundua Mama Mkubwa  alikuwa ameloa machozi , ilionekana alikuwa  ameguswa sana na maswaibu ambayo Eliza alikuwa akipitia.

“Bado sijajua ila  naamini nitalifanyia ufumbuzi hili swala  na lazima nitapata kitu”Aliongea  Hamza  lakini kwa Eliza licha ya kuwa na shukrani  lakini bado  alikuwa na wasiwasi na kile ambacho Hamza anakwenda kufanya , maana kwa  alichokuwa akijua mtu huyo hakuwa mdogo  , alikuwa tajiri ambae vigogo wengi wa kiserikali walikuwa wakimkingia kifua.

“Eliza pole  sana mwanangu , hakuna aliekuwa akijua unapitia wakati mgumu  kiasi hicho?”Aliongea Mama Mkubwa yake Eliza na kumfanya Eliza kutingisha kichwa.

Ukweli ni kwamba katika familia  nzima ya Eliza Mama Mkubwa  wake Merieta  ndio ambae alikuwa akimjali mno na ndio yeye aliefunga  safari kutoka kijijini kuja mpaka Dar kwa ajili ya Eliza , shida tu  ni kwamba  katika ukoo wote yeye ndio aliekuwa  na hali ya chini ya kiuchumi , utajiri wake ulikuwa ni ukarimu na busara pekee  lakini mbele ya  ndugu zake hakuonekana wa maana.

Hata baba yake Eliza hakujali kabisa kuhusu mke  wake wa kwanza kuumwa kwake , baada ya kupata kiinua mgongo alihamia  mkoani kwa mke mdogo ambae ndio  mama yake Hebert hivyo kumfanya  Eliza kuhangaika  mwenyewe kumtibia mama yake, uzuri wake  tu  ilikuwa ni  kwamba licha ya kumtelekeza Eliza hawakujihusisha nae   kwenye  mambo  yoyote  na hata hela hawakumuomba baada ya kuajiriwa.

Licha ya yote Eliza alikuwa akiijali familia yake  sana  na  alikuwa ndio kama kichwa cha familia  na  asingemuacha  baba yake kuchukuliwa na watu bila kufanya chochote.

“Mama Mkubwa nadhani mpaka  hapa nimepata pakuanzia , Eliza umesema  ni  watu gani  wamemkopesha baba yako, kama ni shirika nitajie jina lake?”Aliongea Hamza na muda ule  Eliza alimwangalia Mama Mkubwa  akionekana ndio  mwenye  kujua jina hilo .

“Kwa ninavyojua sio  kampuni wala benki , ni shirika  la  kukopesha watu kwa riba nafuu , wanajiita  Utatu?”

“Utatu!!”Aliongea Hamza kwa kushangaa.

“Unawajua?”

“Sina uhakika lakini kuna umoja wa siri wa giza   wenye washirika waliosambaa dunia nzima , unafahamika  kwa jina la Black Trinity,  huwezi kuelewa ila nadhani nishaanza kupata picha ya kile kinachoendelea”Aliongea Hamza.

“Nini kinaendelea Hamza  mbona

unanitisha?”Aliuliza Eliza huku wasiwasi ukizidi kumvaa.

“Huna haja ya kuogopa kwanzia sasa , ili mradi nishaanza kupata picha ya kile kinachoendelea , hili ni swala ambalo napaswa kulishughulikia”Aliongea Hamza huku akipatwa na hisia mchanganyiko, alijua kama kweli ni Black Trinity  ndio wanaojiita  Utatu basi Eliza alikuwa  kwenye hatari kubwa mno.

Hamza  aliwahakikishia hakuna kitakachowapata na atamtafuta  baba  yake  na kumrudisha  salama na kisha aliaga na kuondoka.

Hamza mara baada ya kuingia kwenye gari   alitoa simu yake haraka na kupiga simu kwenda kwa Dina  na  baada ya salamu  alienda moja wa moja  kwenye lengo la simu hio.

“Dina  kuna kitu nataka  unisaidie , Eliza yupo  kwenye matatizo, unakumbuka ile siku uliniambia  Eliza alikuwa shabaha inayolengwa kwa ajili ya kuingizwa ndani ya kampuni ya Dosam?”Aliuliza Hamza.

“Ndio, nini kimemtokea Eliza?”Aliuliza  Dina na Hamza alimwelezea  kwa ufupi kinachoendelea.

“Nataka uniambie nani  alikuwa  nyuma  ya mkopo wa Eliza , sitaki kusikia ni yule Amosi  najua  kuna  wa nyuma yake”Aliongea Hamza.

“Ni  kweli kuna waliopo nyuma  ya Amosi”

“Waliopo!?”

“Ndio  ni swala  nyeti sana  ambao  kwa kipindi kirefu nimejitahidi kukaa nje na kutokufukunyua , ila  uzuri ni kwamba najua mmoja  wapo  na  nadhani ndio huyo”Aliongea  Dina na Hamza tabasamu lilimvaa palepale.

“Ni nani?”

“Acha  haraka , ulivyoanza kuzungumzia hili swala umenifanya mwili wangu kusisimka , njia   rahisi ya kumjua ni kupitia tukio la leo”Aliongea Dina.

“Tukio la leo!! , unamaanisha  ninI?”

Previoua Next