FOR YOU 2
A Story by Elton Tonny
Familia, Urafiki, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Uhalifu, Mauaji, Visasi, Vita, Mambo yasiyotazamiwa
R-rated 18+
Enjoy!
★★★★★★★★★★★★★★★★
SEHEMU YA KUMI NA SITA
★★★★★★★★★★★★★★★★
Nora akawa amemaliza kuongea na aliyempigia na kurudi usawa wa Lexi. Alikuwa anataka amsemeshe jambo fulani, lakini akasitisha baada ya kuona Lexi alikuwa anadondosha chozi. Akamwangalia na Valentina, ambaye alikuwa anadondosha machozi pia huku Alexa akimuuliza nini tatizo.
"Lexi... what's wrong?" Nora akamuuliza.
Lexi akajifuta chozi haraka.
"Hamna kitu. Niko sawa," Lexi akajibu.
Valentina pia akajifuta machozi na kumwambia binti yake alikuwa sawa, naye akaendelea kumtazama Lexi. Nora alikuwa anawaangalia wawili hawa kimaswali sana.
"Mnafahamiana?" Nora akauliza.
"Ndiyo ni... rafiki yangu wa zamani. Ni kitambo sana. Sikudhani ningekuja kumwona... tena," Lexi akamwambia.
"Ooh... sawa. Habari yako dada? Naitwa Nora," Nora akamsalimu Valentina.
"Ah... safi. Naitwa Va..Valentina," yeye pia akajitambulisha huku bado akimtazama Lexi.
"Lexi... kuna dharura imetokea. Mdogo wangu... nahitaji kwenda kumwona, ila..."
"Usijali Nora. Wewe nenda tu," Lexi akamwambia.
"Lakini vipi kuhusu..." Nora akauliza huku akiangalia vitu walivyonunua.
"Usijali. Nitavipeleka kwa apartment yako. Sijui kama funguo una..."
"Oh, no, tunaacha. Nitawapigia kuwajulisha unazichukua. Asante, ngoja niwahi. Nita... nitakukuta siyo?" Nora akaongea haraka.
"Yeah... utanikuta," Lexi akamwambia huku akimtazama Valentina.
Nora akamwangalia kwa ufupi Valentina, kisha akawaaga kwa pamoja na kuondoka.
Kwa kuwa walitumia gari la Lexi kwenye matembezi yao, Nora akalichukua ili kwenda alikokuwa mdogo wake, naye Lexi angechukua taxi ili impeleke hotelini kwa Nora baadaye. Lexi na Valentina wakabaki hapo wakiwa wanatazamana kwa hisia sana. Kisha Lexi akakusanya vitu vyake vilivyowekwa kwenye mifuko sasa na kusogea pembeni bila kumsemesha Valentina lolote. Alexa akawa anamwambia mama yake maneno mengi kama 'huyu si ndiyo yule uliyenionyesha kwenye picha' na 'si ulisema amekufa,' naye Valentina akawa hawezi kujibu lolote lile na kubaki kumwangalia tu mtu aliyedhani kweli alikufa.
Lexi akamwonyesha Valentina ishara ya kichwa kuwa amfate, kisha akaanza kuondoka hapo bila kusema lolote. Valentina akajituliza na kumshika mkono bintiye, nao wakaenda sehemu ambayo aliacha kifaa cha kubebea vitu alivyonunua na kuanza kuvipeleka kwenye mahesabu. Mapigo ya moyo ya mwanamke huyu yalidunda kwa kasi sana, akiwa na maswali mengi na matarajio yaliyopita kiasi. Baada ya kumaliza kulipia, naye akabeba mifuko iliyowekewa vitu vyake na kuanza kuelekea nje.
Alipotoka tu, akatazama huku na huku akimtafuta Lexi, naye Alexa akamwonyesha kwa kidole kwamba 'yule pale,' kana kwamba alijua mama yake alikuwa anamtafuta. Valentina akamwona Lexi akiwa amesimama nyuma ya gari fulani huku mifuko yake ikiwa chini, naye akaanza kuelekea sehemu hiyo huku Alexa akitangulia mbele. Lexi akanyanyua mkono wake mmoja kumwonyesha Alexa 'ice cream' ya maziwa na chokoleti iliyofunikwa kwa karatasi lake, naye Alexa akaanza kumkimbilia huku anafurahi. Akafika tu usawa wake na kuikwapua, kisha akaanza kuifungua na kulamba. Lexi akawa anamwangalia mtoto huyu huku anatabasamu, na baada ya Valentina kufika hapo karibu, wakatazamana kwa mara nyingine.
Valentina sasa alikuwa mtu mzima hata zaidi, mwenye miaka 38, lakini mwonekano wake bado ulikuwa mzuri kama wa kijana mdogo. Alipendeza. Wakati huu alikuwa amevaa blauzi nyepesi ya njano yenye uwazi katikati ya kifua chake, na suruali yenye rangi ya maroon iliyombana vyema. Uso wake mzuri ulipendezeshwa kwa make up ya kadiri, naye Lexi akatambua kwamba mwili wa Valentina ulikuwa umeongezeka kiasi, yeye hasa akifurahia zaidi hips zake. Akamshusha mpaka kwenye hips hizo na kutazama hapo zaidi, kwa njia ya uchokozi tu.
"Xander... au... I don't... sielewi... nini kinaendelea?" Valentina akasema.
Lexi akaona kwamba bado Valentina alikuwa na upole wake ule ule.
"Nitakueleza Valentina. Usijali," Lexi akamwambia.
Valentina akaendelea kumwangalia tu usoni.
Lexi akamtazama Alexa kwa umakini, kisha akamwangalia na mama yake pia. Valentina akaangalia tu pembeni kwa kuwa alielewa Lexi alichokuwa anauliza. Lakini ilikuwa ni ngumu kiasi kumjibu kwa ishara hasa ukitegemea tayari na yeye alikuwa na maswali mengi ya kuuliza.
"Umenenepa," Lexi akamwambia.
"Tunamwitaga bonge nyanya," Alexa akasema.
Lexi akacheka na kuuliza, "Wewe na nani mnamwitaga hivyo?"
"Na baba," Alexa akajibu.
Lexi akamtazama Valentina, naye akamwangalia. Kisha akaangalia kiganja chake cha kushoto na kuona pete.
"Alexa, shika funguo. Tangulia kwenye gari, nakuja," Valentina akamwambia.
Alexa akazipokea.
"Asante kwa ice cream aunty. Tutaonana tena unipe nyingine, si eti?" Alexa akamwambia Lexi.
"Hmmm... ningependa kama ungeendelea kuwa unamsumbua mama, ila sawa. Tuna dili," Lexi akamwambia.
Alexa akacheka na kuanza kuelekea kwenye gari lao.
"Aunty?" Lexi akamuuliza Valentina.
"Angalau nilimwambia kukuhusu," Valentina akasema.
"Mimi kama mwanamke au mwanaume?"
"Xander huyo ni mtoto. Angeelewa vipi kilichowapata nyie, si angeniona mwendawazimu?"
"Mmm... sawa. Naona kweli ume-move on. Unapendeza sana Valentina," Lexi akamwambia.
"Ona... nahitaji kwenda. Namba zangu hizi hapa..." Valentina akasema huku anampa kadi ndogo.
"Kirefu cha Alexa ni nini?" Lexi akauliza.
Valentina akamwangalia tu.
"Ilikuwaje... ilikuwaje uka..."
"Xander... kama wewe tu ulivyoniambia utanieleza... mimi pia nitakueleza, lakini si sasa. Tutaonana. Usiache kunitafuta," Valentina akasema.
"Na wewe usimwambie yeyote kuhusu mimi kuwa hai. Utaweza?" Lexi akauliza.
Valentina akatikisa kichwa kukubali ijapokuwa hakuelewa ni kwa nini.
Horn za gari fulani zikaanza kupiga sana, naye Valentina akatikisa kichwa huku akiondoka. Lexi akatabasamu akijua ilikuwa ni Alexa ndiyo anamwambia mama yake awahi eti, lakini tabasamu lake likageuka na kuwa simanzi nzito. Kitu alichokuwa amegundua wakati huu ni kitu ambacho hakuwahi kutazamia kabisa kwenye maisha yake kwamba kingekuja tokea. Alikuwa na mtoto. Akainamisha kichwa chake kwa kusikitika, kisha akabeba tu mizigo yake na kuelekea sehemu ya barabara. Akaita taxi moja, naye akaingia na kuanza kuelekea hotelini kwa Nora.
★★
Nora alikwenda mpaka kwenye nyumba ya mdogo wake, Asteria. Muda ule wakati yuko supermarket, alikuwa amepigiwa simu na rafiki ya mdogo wake ambaye alimjulisha kwamba hali ya Asteria kwa siku chache zilizopita haikueleweka. Alikuwa nyumbani tu, akinywa pombe kupita maelezo na kulia huku anafanya fujo nyingi.
Rafiki yake aliitwa Germana (kifupi Gema). Huyu alikuwa ni wale marafiki ambao wanang'ang'ania wenzao wenye pesa ili na wenyewe watoke, lakini alimjali Asteria, na hali hiyo iliyoendelea ilimtatiza sana. Aliamua kumpigia simu Nora kwa sababu sasa Asteria alikuwa amejifungia kwenye chumba chake tangu jana, na kila mara alipomwita hakumjibu. Kwa hiyo aliogopa na kumwambia dada yake ili aje kumsemesha.
Nora alifika na kuelekea ndani kule upesi. Kwa mara ya kwanza kabisa akaingia ndani ya nyumba hiyo. Hangejali tena nini kilifanya asitake kuingia hapo, kwa kuwa mdogo wake alikuwa wa muhimu zaidi kuliko chuki yoyote aliyokuwa nayo kumwelekea baba yao. Akafika getini na kupiga kengele, na baada ya sekunde chache Gema akafungua.
"Eh, afadhali dada... sh'kamoo?" Gema akamsalimu.
"Marahaba. Huyo vipi?" Nora akauliza huku akiingia haraka.
"Yaani hata sielewi kiukweli. Tokea majuzi amekuwa ovyo tu. Sijui mpenzi wake amemwacha... yaani sielewi," Gema akasema.
"Ah... yaani nyie watoto jamani!"
Nora akaongea hivyo kwa wasiwasi huku anapandisha ngazi baada ya kufika ndani.
Nyumba hii ilikuwa ya ghorofa moja, nayo ilikuwa pana yenye vyumba vichache tu lakini maridadi sana. Kwa kijana mdogo kama Asteria kuwa na nyumba tayari ilikuwa ni full kujiachia na kuburudika na marafiki tu hapo, kwa hiyo mpangilio wa vitu mara nyingi ungekuwa shaghaalabaghala mpaka siku yeye na rafiki yake wakiamua kufanya usafi wenyewe. Asteria bado alikuwa anasoma chuo kikuu, mwaka wa pili kwenye kozi ya kilimo. Na mbwembwe zake zote haikujulikana kwa nini alichagua kozi hiyo, ingawa kama ungemuuliza angesema tu anaipenda.
Baada ya Nora kufika nje ya mlango wa chumba cha Asteria, akajaribu kuufungua lakini haukufunguka. Akaanza kumwita sana, lakini hakujibu. Nora akamwambia kwa kumtisha kwamba endapo kama asingefungua basi angeuvunja mlango, na anajua nini kingefuata ikiwa Nora angechukua hatua hiyo.
Zikapita sekunde kadhaa za ukimya, na mlango ukasikika ukifunguliwa kwenye kitasa. Nora akaufungua na kuingia ndani, na hapo akakuta mambo mengi yakiwa yamekaa ovyo ovyo tu. Akamwangalia Asteria kwa ufupi, ambaye alikuwa amevaa khanga moja kutokea kifuani, huku nywele zake zikiwa zimevurugika sana kichwani. Sakafuni kulikuwa na chupa nyingi za pombe, naye Asteria akasimama usawa wa kitanda na kumwangalia dada yake.
Nora alimtazama mdogo wake kwa hisia kali sana. Alitaka kujua ni nini iliyokuwa maana ya haya yote aliyokuwa anafanya.
"Umechanganyikiwa?" Nora akauliza.
Asteria akabaki tu kumwangalia kwa njia fulani kama mtu mwenye usingizi. Gema akaingia ndani hapo pia na kusimama mlangoni.
"Ongea. Nini maana yake?" Nora akauliza tena.
"Kwani unataka nini Nora? We' si una kazi huko za kufanya? Niache tu mimi nitakuwa sawa," Asteria akasema.
"Unasemaje? Ndiyo nina kazi za kufanya, na isingekuwa ya huu upuuzi wako ningekuwa sehemu fulani sasa hivi. Utaendelea kujiendekeza mpaka lini? Kua Aste. Unajirarua namna hiyo kwa faida gani? Yote haya kwa sababu ya mapenzi?" akauliza Nora kwa hisia.
"Ndiyo! Nilikuwa nampenda sana. Hauwezi kuelewa ameacha pigo kubwa namna gani ndani ya moyo wangu," Asteria akasema kwa hisia.
"Kwa hiyo... ukifanya haya yote ndiyo atakurudia?" Nora akauliza.
"Hawezi. Lakini kama ni kuendelea nitaendelea tu...."
Nora akamkaribia na kumtandika kofi zito usoni!
Asteria akakaa kitandani huku akilia, na kuweka kiganja chake kwenye shavu huku ameinamia kitanda.
"Utaendelea kuwa mpumbavu mpaka lini? Eeh?" Nora akauliza.
"Nimekwambia hauwezi kunielewa," Asteria akasema huku bado analia.
"Nielewe nini? Nielewe nini?" Nora akauliza.
"Amekufa," Asteria akajibu.
Nora akatulia kidogo na kumwangalia tu.
Asteria akamgeukia na kusema, "Wamemuua."
"Nini?" Nora akauliza kimshangao.
Asteria akaendelea tu kulia.
Ikambidi Nora asogee karibu yake na kupiga magoti chini, kisha akamshika mikono na kumwangalia machoni kwa umakini.
Gema akaingia na kusogea mpaka karibu.
"Nini kimetokea?" Nora akauliza kwa kujali.
"Yaani hata sielewi. Nilikuwa naye... kidogo tu nashangaa ananiambia... nisimjue tena... hhh... Nikam..nikamtafuta... lakini sikumpata. Ndiyo nikaja kumwona... TV... eti amekufa...." Asteria akasema na kuanza kulia tena.
Nora akahisi vibaya sana kwamba alimpiga mdogo wake wakati alikuwa kwenye maombolezo. Akamkumbatia na kuanza kumbembeleza, huku akijitahidi kuyazuia machozi yake kumwagika. Akapanda kitandani na kukaa, huku kichwa cha Asteria kikiwa kifuani kwake akiendelea kumbembeleza.
"Pole Aste... pole sana dear," akasema Nora.
Asteria akawa anajitahidi kujikaza.
"Ulikuwa unasoma naye?" Nora akauliza.
Asteria akatikisa kichwa kukataa.
"I'm sorry. Sikuwahi hata kukutana naye. Pole sana mdogo wangu," Nora akamwambia.
"Pole Aste. Me mwenyewe sikujua," Gema akasema.
"Lakini Aste, umesema wamemuua. Inamaanisha nini? Nani amemuua?" Nora akauliza.
"Me hata sielewi. Wanasema ameuliwa na wale... Mess Makers," akasema Asteria.
Nora akashangaa. Akanyanyua kichwa cha mdogo wake na kumtazama usoni.
"Boyfriend wako aliitwa nani?" akamuuliza kwa umakini.
"Oscar," akajibu Asteria.
Nora akaangalia chini akiwa amechoka akili. Mbona mchezo huu wote ulikuwa na mizunguko mingi namna hii? Aliwaza sana ni kwa nini mambo mengi yalikuwa yanatokea kwa njia hii tokea kundi la Mess Makers lilipozuka, lakini akakosa jibu. Sasa akawa anajiuliza ikiwa Oscar alikuwa anatoka na mdogo wake kimakusudi au la.
"Huyo Oscar... ulikutana naye wapi?" Nora akauliza.
"Mitaa fulani... zamani," akajibu Asteria.
"Zamani... yaani miaka mingi?"
"Kama miwili..."
"Kwa hiyo mli-date kwa miaka karibia miwili?"
Asteria akatikisa kichwa kukubali.
"Okay. Umesema... mara ya mwisho ulipokuwa naye nini kilitokea?" Nora akauliza.
"Hata sielewi. Tulikuwa wote... sijui nini kikampata akaanza tu kupasua simu, akaitupa chooni, halafu akaniambia nisimwambie yeyote kama ninamjua kwa sababu... maisha yangu yangekuwa hatarini. Sikumwelewa... yaani ni kama alijua kwamba siku hiyo angekufa... hhh... sielewi hao watu walitaka nini kutoka kwake, alikuwa kijana wa kawaida tu..." akasema Asteria kwa huzuni.
"Kwa hiyo ni kama kuna watu wengine wamemuua halafu polisi wakawasingizia Mess Makers?" Gema akauliza.
"Hata sielewi..." Asteria akasema.
Nora alikuwa anawaza mambo mengi, lakini kwa sasa alihitaji kwanza kumtuliza mdogo wake. Akamfuta machozi na kumwambia asiogope kwa sababu kila kitu kingekuwa sawa. Kwa sababu Asteria hakujua ikiwa dada yake alijihusisha na msako wa Mess Makers, Nora akamsihi kwamba afuate ushauri wa mwisho wa mpenzi wake, kwamba asimwambie mtu yeyote kuwa alitoka naye kimapenzi, na ikiwa ingetokea watu fulani wenye vyeo vya usalama wakamuuliza, basi angepaswa kumwambia yeye kwanza ili amsaidie kushughulika nao.
Dada mkubwa akaendelea kukaa hapo na mdogo wake, akimsaidia kuondoa mkazo na kumtia moyo zaidi ili afarijike.
★★
Lexi alirejea hotelini alikoishi Nora kwa sasa na kuelekea kwenye chumba chake moja kwa moja. Giza lilikuwa limeshaingia, ikiwa ni saa 1 sasa. Aliweka mizigo pembeni, naye akaketi sehemu ya kitanda akitafakari mambo mengi. Kukutana kwake na Valentina kulikuwa jambo ambalo hakutazamia hata kidogo. Na tena kuongezea utata wa hali hiyo ni kujua kwamba alikuwa na mtoto pamoja naye, ambaye hakujua kumhusu pia. Alianza kuwaza ingekuwa vipi kama kipindi kile mambo yote yale mabaya yasingetokea, inamaanisha labda leo angekuwa pamoja na binti yake na mama yake pia.
Kwa jinsi ambavyo maisha yao yalikuwa yamebadilika, nani angeamini sasa hivi ikiwa angekwenda na kusema yeye ndiyo "baba" wa huyo mtoto, wakati alionekana kuwa mwanamke? Alianza kumkumbukia Alexa, jinsi alivyokuwa mzuri na mashavu yake makubwa, naye akatabasamu kwa hisia. Lakini pia alithamini sana kwamba Valentina hakuficha ukweli kutoka kwake ingawa ndiyo walikuwa tu wamekutana baada ya miaka nane, naye akawa anatazamia kwa hamu kuja kuonana naye tena.
Wakati akiendelea kutafakari hayo, ujumbe wa Nora ukaingia kwenye simu yake, akiuliza kama bado alikuwepo hapo, naye Lexi akajibu kwa kusema ndiyo, ila aliboeka kukaa peke yake. Nora akamwambia angefika muda siyo mrefu; ampe kama dakika 15 tu. Baada ya Lexi kukubali, akafumba macho kwa sekunde chache, kisha akanyanyuka kutoka alipoketi na kwenda kwenye vitu vya Nora. Alianza kupekua vifaa vyake vingi, akitafuta hasa makaratasi au makablasha ili kuona kama angepata jambo lolote lililohusiana na kazi ya Nora ya kuwatafuta Mess Makers.
Alipekua na kupekua lakini hakupata taarifa zozote zenye kuvuta umakini wake. Ndipo akasikia sauti nyuma yake.
"Unafanya nini?"
Macho ya Lexi yakakaza huku akitazama mbele. Alikuwa amechuchumaa, hivyo akasimama akiwa anahisi hasira sana na kugeuka nyuma yake. Ilikuwa ni Luteni Michael.
"Unaingia vipi humu bila hodi?" Lexi akamuuliza.
Nyuma ya Luteni Michael walikuwa ni Mario na Hussein.
"Hodi siyo kitu ambayo wewe unajali, kwa hiyo tusipotezeane muda. Nataka useme unafanya nini ndani hapa," Luteni Michael akamwambia.
"Siwezi kukwambia nafanya nini hapa mpaka uniambie kwa nini hujapiga hodi," Lexi akasema.
Hussein akatabasamu na kusema, "I like you."
"Asante. Mimi pia," Lexi akamwambia.
"Mnaona jinsi hicho kiburi kilivyojaa usoni kwake? Nani ameshawahi kuwafanyia hivyo akijua kabisa nyinyi ni nani?" Luteni Michael akawaambia wenzake.
"Kwa hiyo kwa sababu wewe ni mwanajeshi ndiyo napaswa kutetemeka sanaaa? Cheo ulichonacho hakipaswi kuogopwa. Wewe upo kwa ajili ya wananchi, siyo kwa ajili ya kuogopwa," Lexi akamwambia kwa ujasiri.
Luteni Michael akamtazama kwa hasira.
"Kaa kimya, mshenzi wewe! Unaongea na sisi namna hiyo, nitakupasua sasa hivi!" akasema Mario.
"Oya, ndo' nini sasa? Swagger gani hizo kama makoplo, tena wale masharobaro wa chihaya?" Hussein akamwambia Mario kiutani.
"Em' niache na we' naye," Mario akasema.
Luteni Michael akamsogelea Lexi karibu zaidi. Lexi hakuonyesha woga wowote ule na kumwangalia tu usoni kwa njia ya kawaida.
"Wewe ni nani?" Luteni Michael akamuuliza.
"Naitwa Lexi," akajibu.
"Wenzako wako wapi?"
"Wakina nani?"
"Kama unajali sura yako, ongea kila kitu sasa hivi. La sivyo nitakuumiza," Luteni Michael akamwambia kiutulivu.
"Hivi wewe una shida gani? Unanitaka nini mimi? Au hii yote ni kwa sababu ya Nora? Kwa sababu amekukataa?" Lexi akamwambia.
Mario na Hussein wakaangaliana kimaswali.
"Ninakupa sekunde...."
"Hata usijisumbue. Kama unataka kunipiga anza. I dare you," Lexi akasema.
Luteni Michael akakunja ngumi kwa kuhisi hasira kali sana. Mario na Hussein wakawa wametulia tu wakisikilizia nini kingefuata. Luteni Michael akamsogelea Lexi mpaka karibu kabisa na mdomo wake akimwangalia kwa hasira, naye Lexi akanyanyua kidevu juu akimtazama bila hofu.
"Sababu moja inayofanya nisikuue hapa hapa sasa hivi ni kwamba haitaonekana kuwa haki, lakini hiyo haimaanishi siwezi kukutia dole. Hiki kiburi chako kitakwisha leo leo," Luteni Michael akamwambia hivyo.
Kisha akaishika sehemu ya Lexi ya siri na kuiminya kwa nguvu. Lexi alikasirika sana! Akampiga kichwa cha pua na kufanya Luteni Michael arudi nyuma kidogo. Kisha mwanaume huyo akamfata Lexi tena na kumpiga kofi zito usoni, naye Lexi akadondokea kitandani akikunja ngumi kwa kuhisi hasira kali. Mario na Hussein wakawa wanamwambia Luteni wao asimfanyie mwanamke huyo jambo lolote baya, lakini Luteni Michael akamfata kitandani hapo na kumshika shingoni kisha kumvuta kuelekea uso wake.
"Unajifanya mbabe, si ndiyo? Sasa ngoja nikuonyeshe!" Luteni Michael akamwambia.
Kisha akamvuta na kumsukuma upande ambao Mario na Hussein walikuwa wamesimama, naye Hussein akamwahi na kumdaka kabla hajaanguka chini vibaya.
"Asante..."
Lexi akamwambia hivyo Hussein, naye Hussein akamwonea huruma kiasi.
"Mwachie," Luteni Michael akamwamuru Hussein.
"Luteni... hivi unavyofanya siyo sawa. Hata kama angekuwa mmoja wa Mess Makers, huyu ni mwanamke, hupaswi kumpiga hivi. Na vipi ACP aki...."
"Nimesema mwachie!" Luteni Michael akamwambia kiukali huku amemnyooshea kidole.
Hussein akamwachia Lexi na kusimama, ambaye pia akasimama na kumgeukia Luteni Michael.
"Unataka kupigana? Come to me," Luteni Michael akasema.
"Oh, no. By all means, ring's yours (hapana... kwa mambo yote, ulingo ni wako)," Lexi akasema kwa ujasiri.
Luteni Michael akatabasamu na kuwaambia wenzake, "Hivi mnaweza kuamini kabisa mwanamke huyu anani-challenge mimi?"
"Kwani wewe ni nani? Wewe ni binadamu kama wengine tu. Hakuna chochote kilicho chenye ubora kuhusu wewe kinachopita kile cha mtu anayekaa kuombaomba pesa barabarani. Tena naweza kusema hata mtu wa namna hiyo ni bora kuliko wewe, kwa sababu ijapokuwa ana hali ngumu, angalau anajua anapotakiwa kuwa. Wewe je? Unajua unapotakiwa kuwa? No. Kwa sababu unafuata tu kila unachoambiwa na viongozi wako kama mbwa!" Lexi akasema.
Luteni Michael akamfata na kwa hasira akampiga ngumi usawa wa mdomo wake. Mario na Hussein wakashangaa sana na kusogea pembeni, kwa kuwa Lexi alianguka na kuanza kutambaa kuelekea mlangoni taratibu. Luteni Michael akamfata na kuzishika nywele zake kwa nguvu, akimvuta kumsimamisha juu. Kisha akamsogelea sikioni kwake huku mkono mmoja akiuweka kwenye shingo yake.
"Nani unamwita mbwa, malaya wewe?! Umekosa mwanaume wa kukupa watoto ukahamia kwenye mashine za usagaji, si ndiyo? Sasa kuanzia leo uta...."
Kabla hajamaliza kuongea, mlango wa kuingilia ndani ya chumba hiki ukafunguka. Ilikuwa ni ACP Nora! Alifika tu ndani hapo na kukuta Lexi akiwa ameshikiliwa namna hiyo, huku uso wake ukionyesha maumivu. Alichoka!
Luteni Michael akashtuka moyoni, naye akamwachia Lexi, ambaye alidondoka chini huku akipumua kwa nguvu. Yaani Nora alishindwa hata kuongea, alishindwa hata kujongea, alishindwa kuelewa nini kilikuwa kinaendelea. Mario na Hussein wakatazamana kama kuambiana 'haya sasa,' naye Lexi akamtazama Nora usoni huku mdomo wake ukitoa mchirizi wa damu.
★★★★★★★★★★
ITAENDELEA
★★★★★★★★★★
Comments