Reader Settings

SEHEMU YA 01..

 

Ni saa moja dakika saba  katika  website maarufu ya  JamiiForum  linaonekana tangazo  katika jukwaa la Connect  , tangazo ambalo limetolewa na ID yenye jina la Ngwena.

Ajira: Boyfriend anatafutwa.

“Husika na kichwa cha tangazo, mimi ni msichana wa miaka ishirini na nne natafuta mwanaume ambae ataigiza kuwa boyfriend wangu kwa mkataba wa mwaka mmoja, vigezo ninavyovitaka ni mwanaume wa miaka 20 mpaka 30 awe ni mwenye  kujiamini, dini yoyote, Mwonekano wowote lakini ukiwa mtanashati ni kigezo cha ziada, Elimu angalau ya chuo cha kati kuendelea, mshahara kwa mwezi si chini ya laki tano na maongezi yapo, kuhusu mimi zaidi utanifahamu  baada ya kukidhi vigezo, Kama umevutiwa  na  kazi hii njoo PM jielezee kwa ufupi na weka mawasiliano yako”

Jukwaa la Connect  mara nyingi  hutumika  kuunganisha watu ambao wanatafuta kuingia katika mahusiano ya aina mbali  mbali aidha yale ya urafiki wa kawaida au yale  ya  kupelekea uchumba hadi ndoa, hivyo  mwana jukwaaa  mwenye ID ya Ngwena alitumia haki yake kuweka tangazo la namna hio , ijapokuwa  tangazo limekaa kibiashara au kiajira  lakini  kwa namna moja ama nyingine lilikuwa likihusisha mahusiano.

********

Sifa yake kubwa ni mkimya lakini sio mpole, ni mtu mwenye kufikiria kila neno analolisikia na kulisoma mahali kwa kutumia akili nyingi, Hamza anaamini kuna zaidi ya maana katika kila neno analotamka binadamu na hii inampelekea kuwa  kati ya watu ‘Overthinker’ sana , kwa mfano Hamza unaweza kumtania ila ule utani yeye akauchukulia siriasi , ijapokuwa hakukasirika lakini  utani  ataugeuza na kuanza kujitafakari kwa nini  ametaniwa hivi na vile.

Hakuwa mchangiaji wa mada , lakini alipenda kusikiliza  michango  na maoni ya wengine ,  hakuwa  mpenzi sana wa  kuanzisha mada kwenye mitandao ya kijamii , lakini alipenda sana kusoma maoni ya  wengine na mada za wengine , huku akiamini kwa kupitia maoni yao angeweza kufahamu  tabia za watu mbalimbali  kwa kuchanganua zaidi ya  maana kwa kila maoni ya mtu mmoja mmoja , hayo ndio maisha ya Hamza na  alipenda sana mtandao wa Twitter na  JamiiForum.

Hakupenda kujichanganya na watu wengine, lakini alipenda sana mitandao  ya kijamii  kwa kiwango kikubwa sana  huku akijiaminisha kwamba  mitandao ya kijamii ndio sehemu ambayo watu wanaweza kuwakilisha uhalisia wao kwa urahisi kupitia maandishi kwani hawakuwa wakionekana kwani wengi wao walitumia utambubulisho feki,Kwa tabia yake hio unaweza kumuita  Jasusi wa mtandaoni.

Licha ya hayo yote lakini Hamza ni moja wapo ya vijana ambao unaweza kusema ni wenye moto unaowaka ndani ,  moto wa upambanaji, moto wa kutodharau fursa   iliopo mbele yake,  ni  kwamba tu kila fursa aliokutana nayo haikuwa kubwa ya kumtajirisha  lakini ilimfanya kusongesha maisha yake.

Sasa Hamza ndio moja wapo ya watu walioweza kuona tangazo la ajira ya kuigiza kama boyfriend, ilikuwa ni majira ya usiku wa kwenda saa mbili  na baada ya kusoma Tangazo hilo alivutiwa  sana , akiamini lazima kutakuwa na Maoni ya kuchekesha   na ndio alichokutana nacho.

Ni kweli Tangazo lilikuwa likijipambanua kwamba ‘Boyfried’ wa maigizo anahitajika   kama ajira isio rasmi, lakini  tangazo lilikaa sana  kitapeli kwa watu wengi , nani anaweza kuamini mwanamke wa kitanzania kuajiri mwanaume kwa kumlipa malipo ya laki tano kwa mwezi kwa  kuigiza kuwa boyfriend, ni jambo ambalo  sio kawaida  kabisa , hivyo  maoni mengi ya wachangiaji ilikuwa ni matusi na dhihaka huku ID(jina la utambulisho) feki ya jina la Mnyoo ukiongoza kwa dhihaka lakini upande wa mtoa mada hakujibu  chochote ni kama alitoa tangazo na kisha akapotea,watumiaji  wa mtandao huo  wanayo kauli ya kusema Uzi  unatembea  kwa kasi  mno na hiko ndio kilichokuwa kikiendelea ,wachangiaji wengi wakiwa ni wale wenye ID za kiume.

Hamza aliendelea kusoma maoni huku mengine yakimchekesha sana, hakuwa na mpango wa kutoa maoni  lakini watu walivyocharuka  ilimfurahisha sana , baada ya kusoma karibia  maoni yote alirudia upya kusoma tangazo lenyewe  na kuanza kulitafakari kama ilivyokuwa tabia yake ya kutafuta zaidi ya maana kwa kila mtu anachoongea au anachokiandika kwenye mitandao, ndio tabia yake ambayo  kwa umakini  aliokuwa akitumia kuchambua mawazo    na maandishi ya watu ungedhania analipwa alichokuwa akitafuta ni kujua kwanini mtoa mada alikuwa akidhihakiwa kwa  kiasi kikubwa.

Hamza katika  siku zote alizokutana na matangazo ya ndoa na kutafuta wenza  hili kidogo lilikuwa na upekee , aligundua  kulikuwa na zaidi ya maana  , zilikuwa ni hisia ambazo  hata yeye mwenyewe  alishindwa kuzielewa , lakini ile tabia  ya kufatilia   maoni ya watu na mabandiko ilimwongezea utashi(Instinct) wa kuelewa hisia za watu kwa haraka zaidi kupitia kile wanachokiandika na wanachokitolea maoni  na ndio alichokutana nacho , wakati akiendelea  kusoma kwa kurudia rudia hilo Tangazo  ujumbe wa meseji kwenye simu yake ya Tecno Spark 5 uliiingia , aliufungua haraka sana na kuona ni muamala wa pesa.

“Huyu Mzee leo kanikumbuka” Aliongea   mwenyewe bila furaha huku akiangalia  ile meseji, sababu moja ya  kutokufurahia  ule mwamala ni moja  tu , hela iliotumwa haikuwa ikimtosha  kwa matumizi kabisa  achana na  madeni ambayo alikuwa akidaiwa  chuoni.

Kila ikifikia  hio tarehe ndio siku ambayo alikuwa akipokea  muamala kwa mwanaume anaemfahamu kwa jina la Mzee.

Miamala ambayo Mzee alikuwa akituma ni kwa kiasi anachojisikia yeye mwenyewe atume shilingi ngapi , mbaya zaidi ni kwamba Hamza hakuwa na uwezo wa kumpigia simu Mzee na kumwambia    amwongezee  kidogo.

Tusichokijua kuhusu Hamza ni kwamba   alikuwa ni Yatima  na kuna stori kubwa ya maisha yake iliomtokea  mkoani  Rukwa huko Sumbawanga  ambayo ndio ilimfanya kuwa mtoto Yatima lakini   pia kumkutanisha na mtu aliefahamika kwa jina la Mzee.

Maisha yake yote tokea  kupatwa na janga la  ajali huko Sumbawanga iliopelekea kupoteza ndugu zake na mzazi wake  mtu ambaye alimsaidia mpaka kufikia katika umri huo ni huyo Mzee..

Mbaya zaidi kuhusu Mzee ni kwamba alimuona mara moja tu na  ilikuwa ni  usiku  wa mvua  kali  na wakati huo alikuwa na miaka  tisa akiwa darasa la nne na mpaka wakati huu akiwa na miaka ishirini na tisa hakuwahi kumuona tena, miaka ya mwanzoni  aliwasiliana na mzee kwa barua , lakini mara baada ya ujio wa simu aliwasiliana nae kwa  jumbe za meseji tu na siku zote  Mzee angemtumia Hamza ujumbe kwa ‘Private number’(Namba ambayo huwezi kurudisha jibu) tena ikiwa ni  nyakati za usiku pekee.

Kwa maneno marahisi ni kwamba Hamza alisaidiwa  kimaisha na Mzee ambaye hakuwa akimfahamu kwa  sura  yake halisi  na ndio maisha yake yalivyokuwa mpaka kufikia umri huo,

Mzee alikuwa akimsaidia vitu vingi lakini hakuwahi kujionyesha kwake.

Hamza baada ya kupatwa na hasira  kwa kiasi kile kidogo cha pesa alichopatiwa na Mzee alijikuta akirusha  pembeni simu yake kwenye godoro ndani ya chumba chake alichopanga  katika eneo la  Gongo la mboto  jijini Dar es salam.

Chumba chake hakikuwa na vitu vingi kabisa , kilikuwa na godoro dogo kama yale ya wanafunzi, mtungi wa gesi na baadhi ya vyombo vichache pamoja na chandarua.

Alikuwa pia na mabegi mawili , moja kubwa kidogo la wastani na lingine ni la saizi ya kati ambalo hutumia kuwekea nguo zake, maisha yake yalikuwa ya chini sana huenda kuliko mwanafunzi yoyote anaesoma ndani ya chuo cha FEMU(Future Enterprise and Monetary University).

Baada ya kujilaza kwenye godoro lake alijikuta akipotelea usingizini na  alikuja kushituka ni  siku nyingine kabisa  ya jumatatu , alijiandaa haraka haraka kwa ajili ya kwenda Chuo.

Baada ya kutumia  zaidi ya lisaa limoja na nusu kujiandaa kutokana na kusubiria zamu yake ya kuingia bafuni kufikia , hatimae aliweza kusogelea vituo vya daladala kwa ajili ya kupanda ambazo zingemwezesha  kufika chuoni.

Njia ilikuwa na foleni na  kwa bahati nzuri aliweza kupata siti ya kukaa , hivyo alitoa simu yake mfukoni na kuendelea kuperuzi peruzi mtandaoni huku Earphone zikiwa masikioni.

Hamza ni aina ya watu ambao hawakupenda   kabisa kusikiliza maongezi ya  abiria kwenye daladala na miezi  hio  habari za uchaguzi zilikuwa zikijadiliwa sana kwenye magari kwani ilikuwa  ndio mwaka wa uchaguzi na  ilikuwa kama miezi mitatu  tu hivi  siku ya wananchi wa taifa la Tanzania kupiga kura , lakini kwa upande wake yeye hakuwa  hata na mpango wa kupiga kura, kwanza hakuwa na chama na  wagombea wote hakuna ambaye alikuwa akimvutia  japo  mmoja wapo ya wagombea aliweza kusikia  akijinadi kwamba atakwenda kupambana  na rushwa pamoja na   Madawa ya kulevya nchini, kauli hio kidogo ilikuwa ni sera iliojitosheleza kulingana na  hali ya taifa kwa ujumla lakini Hamza  kwa mtazamo wake  hakuwa na uhakika kama sera hio ingeweza kutekelezeka.

Katika kipindi cha miaka mitano  iliopita madawa ya  kulevya yalikuwa yameathiri sana  vijana wa kitanzania , haikueleweka nini kinaendelea nchini kutokana na kuongezeka kwa wimbi la wagonjwa ambao wana uraibu wa madawa ya kulevya katika hospitali zenye vituo maalumu vya kusaidia wagonjwa hao.

Takwimu za kiserikali zilikuwa zikionyesha  kwa wastani  wa siku hospitali ya rufani ya Muhimbili hupokea zaidi ya wagonjwa wa tano  wapya wanaofikishwa kwa ajili ya kutibiwa uraibu wa madawa ya kulevya.

Inawezekana ikawa idadi ndogo  lakini  kimahesabu ni idadi kubwa sana na hilo lilimaanisha kwamba kuna zaidi ya  wagonjwa  wenye uraibu huo uraiani ambao  hawakufikishwa  hospitalini.

Sasa  Hamza kutokana na  kuishi uswahilini alikuwa akikutana na watu wa aina hio wanaotumia madawa ya kulevya kwa kiwango kikubwa , ndio maana  sera ya mgombea mmoja  wa chama fulani cha kisiasa  baada ya kutaja vipaumbele chake ni kupambana na dawa hizo  aliona angalau ana mantiki lakini kwasababu anazozijua yeye aliona  ni sera ambayo  ni ngumu sana kutekelezeka.

Hamza  akiwa kwenye gari kama hivyo  huwa ni mwenye kuyafikiria mapito  yake na asubuhi  hio  alipokuwa akielekea chuoni alijipa muda wa kufikiria nia ya mzee katika maisha yake.

Ukweli ni kwamba  maisha yake yote ni kama yameshikiliwa na huyu mtu anaejiita mzee ndio maana alikuwa akiwaza na alijiambia  huenda kama sio Mzee angetafuta uelekeo  mwingine wa kimaisha na  kuacha kuendelea  kuishi maisha ya kimaskini yaliojaa maigizo ndani yake.

Tatizo moja tu kuhusu Mzee ni kwamba alikuwa  anamtishia sana maisha yake pale tu asipotii maagizo yake, kwa upande wake huenda mtu ambaye anamuogopa katika maisha yake ni huyo  Mzee.

Kilichomfanya kumuogopa zaidi  ni kwamba ukiachana na  kumsaidia  kimaisha mpaka kufikia  umri aliokuwa nao Mzee hakuwa akionekana  na hata mawasiliano yake   yalikuwa ni nyakati za usiku  lakini kutokuonekana kwa Mzee mbele yake haikumaanisha  hakuwa na nguvu, alikuwa  na nguvu  kubwa ambayo Hamza mwenyewe ameweza kuishuhudia   kwa macho yake  katika kila hatua aliopiga katika maisha yake  akiwa chni ya uangalizi wa Mzee.

Kuhusu swala hilo lilikuwa likimfikirisha sana miaka na miaka  na  kujiuliza kuna siri gani  ya huyu mtu anaefahamika kwa jila la Mzee kumtafuta tu usiku.

Hamza  akiwa kwenye daladala   ambayo ilikuwa kwenye msongamano wa magari , palepale alijipa muda  wa kufikiria  maisha yake ya  nyuma namna alivyokutana na mzee.

 

Next