Reader Settings

Chimera.

Mvua ilikuwa ni kubwa mno  ndani ya jiji  la Paris chini ya anga jeusi, minunurisho ya mwanga wa taa katika maji ilikuwa imesambaa kila mahali. Jiji hilo la kimitindo  na  la mapenzi lilibadilika ghafla.

Pembezoni mwa Bar moja ambayo inauza vinywaji kama bia  na mvinyo alionekana mwanaume alievalia nguo nyeusi akiwa  amesimama  na mwanvuli wa rangi nyeusi.

Alikuwa amevalia koti refu lililovuka magotini( Trench Coat) la rangi nyeusi  na kofia ya hat  rangi nyeusi pia. Ukiachana na mwamvuli alikuwa ameshikilia  kibegi kidogo cha leather  rangi nyeusi , na muda ule alonekana kufungua kibegi kile na alitoa kitu kama mfuko wa nailoni hivi  ambao umetuna na kuutupia kwenye ndoo ya takataka.

Baada ya kufanya vile , palepale  hakujali mvua iliokuwa ikinyesha kwani na mwamvuli wake alitokomea  katikati ya nyumba mbele yake.

Dakika moja mbele  alionekana kijana mzungu mwenye nywele zilizojikunja kunja  akitoka  katika ile Bar akiwa amevalia Aproni.

Alisogelea ndoo ile ya takataka bila wasiwasi na  kisha alichukua  ule mfuko  na kuingia nao ndani ya Bar ile.

Zoezi hilo lilifanyika ndani ya  dakika mbili tu  na  kwa giza na mvua iliokuwa ikinyesha , ilionyesha hakuna mtu ambae ameshitukia.

Lakini  upande wa  mbele katika jengo refu kulikuwa na  mtu alieshikilia darubini akiangalia  jambo lile kwa umakini mkubwa bila ya kutoa sauti yoyote.

*****

Nusu saa mbele  katika makao  ya muda ya kikosi cha Malibu ndani ya hoteli.

Mkurugenzi wa kikosi cha Malibu kwa masuala ya kigeni , Balozi Rajabu , alionekana akiwa ameketi mbele ya tarakishi mpakato, alikuwa akivuta sigara lakini umakini wake wote ulikuwa ni kwenye monita ya tarakishi hio  na alionekana  kufikiria kwa kina pia juu ya kile anachoangalia.

Balozi  Rajabu alikuwa mlevi wa sigara ndio maana alichagua chumba cha peke yake ambacho kingemruhusu kufanya kazi huku akiwa anavuta sigara

“Ding Dong!

Mara baada ya Balozi  Rajabu kusikia  kengere ya mlango haraka sana alifunga laptop yake.

“Nani?” Aliuliza

“Balozi , nimekuletea  chakula”Alikuwa ni Rehema  sekretari na msaidizi wake, na baada ya kumtambua  Rajabu alisimama na kwenda kufungua mlango.

Rehema alionekana kuchoka kwa namna alivyokuwa akitembea na mkononi alikuwa ameshikilia mfuko ambao ulionekana kuwa na vyakula.

“Pole  Rehema kwa kutembea na mvua na asante”Aliongea Balozi Rajabu huku akipokea mfuko ule na tabasamu.

Rehema aliishia kufuta maji ya mvua usoni mwake  na kutingisha kichwa na tabasamu hafifu.

“Usijali balozi , hata mimi nilikuwa na  njaa”Aliongea huku akimuonyesha mfuko wake  wa chakula pia.

Wawili hao hawakupenda chakula cha kifaransa  hivyo  walienda  kwenye duka ambalo lilikuwa likiuza vyakula ambavyo vinaendana na radha ya kibongo.

 

“Basi sawa, kwasasa unaweza kwenda kupumzika  maana hakuna kingine cha kufanya , tutaonana asubuhi”

“Sawa! Usiku mwema  Balozi”Aliongea Rehema na kugeuka.

“Hebu subiri kwanza!”Aliongea Balozi  mara baada ya  kuona Rehema anatokomea nje.

“Kuna tatizo mheshimiwa!?”

“Hebu nenda  kaangalie kama  Mboma yupo  kwenye hii hoteli , nipe taarifa  baada ya kuhakikisha”

“Okey!”

Mara baada ya  Rehema kutoka , Balozi aliweka  chakula mezani na kuanza kula  taratibu na  dakika tatu mbele alipokea simu kutoka kwa  Rehema.

“Vipi Rehema , yupo?”

“Chief Mboma hayupo , msaidizi wake  Juma  anasema ametoka tokea saa kumi na mbili  kwenda kukutana na  marafiki zake”

“Okey! Asante kwa taarifa , nenda kampumzike sasa”

“Sawa Balozi”

Mara baada ya simu ile kukatwa , Balozi alifungua tarakishi ile ya mapakato na kisha  aliangalia kilichokuwa kikionekana na palepale alionekana kuingia katika fikra nzito.

******

Ndani ya chumba cha hadhi ya raisi katika hoteli ya Four Season , Regina mara baada ya kusikiliza mapigo ya moyo ya Hamza  kwa muda ,  sura ilimjaa aibu.

‘Sitaki tena kusikia , unaongea sana ila sikuamini”Aliongea Regina

“Wife nilichoongea ni kweli , mimi ni mpiganaji  na ni kawaida kuweza kudhibiti mapigo yangu ya moyo. Hata wakati  ninapopambana na jeshi kubwa mapigo yangu hayabadiliki namna hii . labda tu iwe nimefanya mazoezi makali sana . Lakini nikikukumbatia  na kukukiss  nashindwa kabisa kudhibiti mapigo yangu ya moyo. Ni aina ya hisia ambazo zijawahi kuzipata  tokea niwajue wanawake”

“Wewe umejuaje! Maana sio kama umekutana na  wanawake wote kwenye  dunia hii . Unajuaje pengine siku moja utakutana na mwanamke mwingine ambae anafanya mapigo yako yaende mbio”

“Ah!  Unataka nikutane na kila mwanamke dunia nzima , ili kujihakikishia nani anayabadilisha mapigo yangu ya moyo . Si itakuwa ni kupoteza muda na kama ingekuwa hivyo basi watu wasingeoa na kuolewa”

“Ila mimi sijawahi kupenda hapo kabla , sijui hata mapenzi yakoje… najuaje kama unanipenda kweli?”Aliongea Regina na kumfanya Hamza kuishia kunusa harufu ya marashi ya nywele ya Regina.

“Hata mimi sijawahi, likija swala la hisia hakuna kipimo  maalumu, hata mtu aseme mapenzi ni  sawa na kujumlisha moja na  moja na kisha kupata mbili, ukiuliza kanuni ya kuja na hesabu hio   hutopata majibu . Kitu pekee ninachojua ni kwamba  nikiwa na wewe hata kama unifokee , uwe na hasira za haraka na kununa  siwezi kukuchukia , haijalishi upoje  bado nakupenda.  Unajua  kumpata mtu unaempenda  na anaekupenda ni  kazi ngumu sana , kwanini unafikiria sana?”

“Jiangalie sasa ulivyokosa aibu , una wanawake kibao lakini unasema unanipenda , unaniona mjinga  eh! Mimi najua  umenioa kwasababu unajua mimi ni mjinga kati ya wanawake wote uliokuwa nao na ni rahisi kukubali kila unachofanya.  Unajua fika kama ungewaoa wengine wasingekuvumilia”

“Wife wewe sio mjinga, una busara kubwa  na  IQ yako ni kubwa vilevile , kwanini  uwe  mjinga?”

“Mh! Lazima utakuwa unaniona mimi mjinga mtu  rahisi kudanganyika na  kukubali  kila kitu”

“Wife kwanini unafikiria   mbali hivyo , kama ni kweli kulikuwa na haja  gani ya mimi kukuoa sasa?”

“Mimi sijui , lazima  uliona kwasababu ya ujinga wangu sitokusumbua na kujihisi ni kama upo bachela tu”

“Unachofikiria sio sahihi mke wangu”

“Utajua mwenyewe , muda umeenda na nataka kuosha uso  kuondoa makeup”Aliongea Regina akijiondoa kwa Hamza.

“Wife kwani umepaka make up! Mbona haionekani?”

“Wewe ni mjinga! Unadhani kwa sherehe ya leo ningeenda bila ya kujipodoa , huwezi kuona  ndio lakini  nilijipaka foundation kidogo  ili  macho yangu yaonekane vizuri. Macho yamenikauka sana , nitaenda kununua lensi nyingine nzuri ili yawe mazuri”Aliongea huku akifikicha macho yake na muda huol Hamza aliishia kucheka baada ya kuona Regina  anataka kupendeza macho na lenzi.

“Wife unajua una macho mazuri sana, ni kama umechanganya  damu ya mzungu na mwafrika kama mimi”

“Wewe  mshenzi huaminiki! Unasema unanipenda lakini umeshindwa kujua  nimepaka makeup. Hujali mwonekano wangu kabisa wewe ,  hebu toka chumbani kwangu kwanza”

“Wife  ni kwasababu   ya uzuri wako  ndio maana  sizingatii kabisa mabadiliko madogo”

“Kamdanganye mtoto wa darasa la tatu ndio atakuamini sio mimi”

“Kweli mke wangu , umejaliwa uzuri na silika nzuri, ukiachana na uzuri wako wa sura  namna ulivyo tu inatosha kuwapiku wanawake wengi”

“Nilivyo kivipi?”aliuliza Regina.

“Mwonekano wako umegawanyika katika matabaka  kadhaa ,yaani kawaida sio kawaida , ni kama upo katikati ya  kila aina ya uzuri , ukivaa vizuri ndio  unabadilika kabisa , Aura unayosambaza ni kama vile ni malkia kutoka falme  ya kufikirika”

“Kadri unavyoongea ndio unavyoonekana muongo , unanisifia kama vile umekula asali, kwa taarifa yako siwezi kulainika kwa kuzidisha kunisifia,hebu toka  kwanza nataka nioshe uso”

Hamza aliishia kujiambia moyoni  , kwani amemzuia kuosha uso au ndio hivyo tu hataki  kukaa uchi mbele yake , lakini  alijua fika Regina hakutaka kutengeneza mazingira ya  kugawa kitumbua chake.

“Wife  usiku mwema , mimi naenda”.Aliongea  Hamza huku akipiga hatua  na Regina aliishia  kumwangalia tu huku kwa namna flani akijisikia vibaya.

“Kesho sitoenda kazini” Aliongea Regina  baada ya Hamza kufikia mlango na baada ya kusikia sauti hio aligeuka.

“Basi nitakutoa out kesho tukatembee!”

“Sawa! Asubuhi tutaongea vizuri. Uwe na usiku mwema”

“Na wewe pia mke wangu”

Hamza aliongea   akiwa na furaha  na kisha alitoka na kufunga mlango.

Hamza mara baada ya kutoka nje alijikuta akihema  kwa nguvu , ukweli ni kwamba  kipindi cha nyuma hakufikiria sana  namna ya kuongea anapokuwa na mrembo , lakini ilikuwa tofauti na alipokuwa na Regina , alijitahidi  akili yake ifanye kazi kwa kiwango kikubwa , Lakini  hata hivyo  aliridhika na namna alivyomsifia.

Hamza alijihisi ni kama  amegeuka kichaa  ambae anayafurahia maumivu Regina anayomsababishia, maana kadri Regina anavyomwekea ngumu na kumfanya ajisikie vibaya ndio alivyozidi kumpenda.

Hamza hakuwahi kuyafurahia mapenzi na ndio kwa mara ya kwanza alijihisi kupenda kweli, alijua alikuwa amependa kweli maana alivyokuwa akijisikia akiwa na Eliza  na Dina ni tofauti sana alivyokuwa na Regina.

Ijapokuwa aliona sio haki kwa wanawake wengine kuchanganywa na mwanamke mmoja , lakini hakuweza kujizuia kufurahia hisia hizo.

“Haha.. nahisi  huu ni ujinga ila napenda radha yake”Aliongea Hamza mwenyewe huku akijicheka.

Hamza alijiambia njia rahisi ya kumega tunda ni kuharakisha zoezi la kumchumbia Regina , lakini aliona  zoezi hilo lazima lifanyike kitaalamu zaidi. Vinginevyo matokeo  yanaweza kuwa tofauti kwa mrembo huyo.

Wakati akiendelea kufikira , bila kujijua alikuwa ashafika kwenye mlango wa chumba chake na kabla ya kupitisha kadi  alihisi kuna mtu alikuwa amefika kumtembelea  na aliishia kutoa tabasamu la kifedhuli  na kisha  bila kujali chochote alipitisha kadi  na kufungua mlango  na kuingia ndani.

Mara baada ya kuingia ndani aliweza  kuona kivuli cha mtu kikiwa kimekaa kwenye kiti dirishani. Mtu huyo  nywele zake ndefu zilikuwa zimefunika uso wake  na mavazi yake machafu yalionekana kuloa  na  maji  ya mvua.

“Aah! Mchafu ya nini kuja kwenye chumba changu  usiku wote huu  kuniogopesha”Aliongea Hamza akijifanyisha kushituka baada ya kuwasha taa.

Alikuwa ni Asmuntis , kama ninja namba moja duniani  kuingia  katika chumba kama hicho bila ya kuwa na ufunguo ilikuwa ni rahisi sana kwake.

“Bosi , uko sawa!”Aliuliza  Asmuntis  huku akiruka kutoka kwenye kiti.

Hamza aliishia kutoa tabasamu na alisogea mpaka kwenye kimeza na kutoa  sigara kwenye pakti na kumpatia Asmuntis  na kisha alimsaidia kuiwasha.

“Naona umenitembelea usiku usiku?”Aliongea Hamza  muda huo akiwasha ya kwake sigara  na kufungua mlango wa kutokea kwenye balkoni na wote waliangalia upande wa nje ya jiji.

“Nani mwingine kajua kuhusu mimi?”Aliuliza Hamza , haikuwa na haja ya kuuliza kwanini Asmuntis amefika  hapo.

“Ni watu wa Metal Tide. Inaonekana  Gonzalez amekosa uvumilivu  wa kutaka kupata cheo cha Ugwiji. Isitoshe  vikao  vya  magwiji ni adimu sana  kama hivi , nadhani anataka kutumia nafasi hii kuthibitisha mbele ya watu wote  kwamba ana hadhi ya  kuwa katika orodha ya magiwji kumi wa dunia”

“Kama ana  shida sana na cheo hicho  ningemwachia tu , kulikuwa na haja ya kutuma watu kunijaribu?”

“Bosi hatuwezi kuruhusu  Gonzalez kuchukua  cheo cha hadhi yako . Hata kama umepoteza uwezo wako wa nishati , sisi tupo . Inferno ni jamii iliokamilika, wewe ndio uliotutoa  kutoka kuwa Clubs  na  kuwa umoja. Nimekwisha kuwasiliana na Azzle, tutakusindikiza kwenda  kuhudhuria  kilele cha  magwiji . Muda ukiwadia  tutakuwa chini ya maagizo yako na kupigana kwa ajili yako. Hatuwezi kumruhusu  Gonzalez kushinda”Aliongea Asmuntis akiwa sirasi mno.

“Pepo mchafu , nashukuru  sana kwa  kunijali . Kwa muda mrefu nilikuwa nikidharau sana hiki cheo , ila kama ndio hivyo basi nipo tayari kuwakaribisha wakibisha hodi.  Ukweli mpango wangu ni kustaafu  moja kwa moja katika ulimwengu wa siri na kuishi kama binadamu wa kawaida anaeonekana na mke wangu  na wapenzi wangu na  mengine yatajidhihirisha yenyewe. Malengo yangu mengine ya kimaisha ni kumuamsha malaika , kuhusu mengine yote  sitaki kuyazungumzia”

“Bosi bado  tu hujamkatia tamaa Malaika?”Aliuliza Asmuntis  akiwa amekunja sura.

“Ndio! Ni swala ambalo siwezi tu kuliacha. Nimekuja kugndua kupitia Earth Axis ambayo serikali ya  Tanzania imeshikiria , kuna  tumaini  kubwa la kumuamsha malaika na hata kumfahamu mzee. Ndio maana nimekuwa na ukaribu na kitengo cha Malibu”

“Bosi Kama kweli Malaika ataamka , ataweza kukulinda kwa hakika  na unaweza  kupata   majibu ya maswali yako mengi” Aliongea na Hamza alitingisha kichwa.

“Angalau leo mchafu umeongea vizuri. Halafu  vipi kuhusu huyu msichana wetu.. nini kimetokea juu ya hii mbinu ya Hundred Shadow?” Asmuntis mara baada ya kusikia kauli ile macho yake yaliwaka.

“Ametumia  hundred Shadows?”

“Usiwe na wasiwasi , kaniambia nisikwambie  lakini mimi na wewe hatuna haja ya kufichana ndio maana nasema sasa hivi  mbele yako. Yule  ni kama mdogo wangu wa kike hivyo nataka kumsaidia , hivyo kabla sijachukua hatua nataka kusikia  kutoka kwako  na mtazamo wako juu ya mbinu hii ya hundred Shadows”.

“Bosi ukweli  mimi niliishia kumfundisha tu , lakini kuhusu  uwezo aliopata  sina uhakika kama unatokana na mbinu yenyewe , ni kama vile ni kitu ambacho amezaliwa nacho”

“Duh! Unataka kumaanisha nini? Mbona hata mimi sijui . Hundred Shadows ni mbinu ya kumuwezesha mtu asionekane katika macho ya kawaida , lakini  alichopata kupitia hii mbinu ni spidi kubwa  kitu ambacho ni ngumu  wewe kumfundisha. Hebu niambie  unachojua kuhusu chimbuko la Rhoda kwa ujumla”Aliongea Hamza.

“Wakati nilivyomuokota na kuamua kumlea . hakuwa akikumbuka wala kuelewa chochote zaidi ya jina lake tu. Miaka kadhaa iliopita baada ya  kufikia  daraja la juu la mafunzo nilimpa ruhusa ya kufuatilia chimbuko lake.  Baadae alikuja kujua  ufunuo aliopata baada ya kufika levo ya nafsi, ilikuwa ni  asili ya ufunuo   uliokuwa ukifundishwa  katika shule moja iliofahamika kwa jina la Night Shadows. Ajabu ni kwamba watu ambao walikuwa wakivuna  nishati kwa ajili ya kugeuka vivuli, kambi yao imeteketezwa yote  na mtu  ambae  alitumia shambulizi la radi na  inaonekana  katika shambulizi hilo ni Rhoda peke yake alisalimika mpaka  mimi kuja kumuokota na kumwasili”

“Unasema wanafunzi wote wa mafunzo ya Black Shadows  waliuliwa?”

“Ndio  na muuaji alitokea nyakati za usiku  wa mvua kubwa kama hivi na hakujulikana  ni nani. Mama yake Rhoda pengine alikuwa ni ninja  na pengine ni yeye aliemuokoa”

“Lakini bado mpaka sasa nina swali ,  kwa nilichosikia kutoka kwa Rhoda ana asili ya ki Afrika na Ugiriki , ilikuwaje ukamuokota Japani?”Aliuliza Hamza.

“Hata mimi nilijiuliza hivyo mwanzo! Ila baada ya kufuatilia kwa umakini  niliweza kupata habari za  biashara ya viungo iliokuwa ikiendelea  kutoka  bara la Asia na Afrika , wanawake wengi  kutoka Afrika walikuwa wakisafirishwa kwenda  Asia. Pengine mama yake  alikuwa ni  moja ya  Wa afrika waliongizwa Japani”

Hamza hatimae aliweza kuelewa mbili tatu , ndio maana  Rhoda alikuwa akikwepa kuongea  kuhusu chimbuko lake.

“Inawezekana , ndio maana  wakati unamuokota alikuwa mdogo  sana, lakini spidi yake ya  kuvuna nishati ni kubwa sana kiasi cha kunishangaza”

“Bosi kuna swala lingine pia sikukuweka wazi, pengine ndio linalochochoa uwezo wake wa kuvuna nishati”

“Swala gani?”

“Rhoda ni Chimera”

“Chimera! Unamaanisha ana wazazi  watatu?”Aliuliza  Hamza kwa mshangao. Kama  mtu mwenye mafunzo ya utabibu alikuwa akijua  nini maana ya Chimera au Chimerism , mtoto ambae  anakuwa  na  baba wawili kwa wakati mmoja , ni  binadamu adimu sana wa namna hio ambae hutokea  baada ya  mwanamke akiwa katika siku za hatari kuzalisha mayai mawili  kwa wakati mmoja kutoka katika ovari zake na hayo mayai  hutungishwa  na mbegu  za wanaume wawili tofauti na baadae  ya hapo  mayai hayo huungana  na kutengeneza mtoto mmoja na kumfanya mtoto kuwa na  vina saba vya  wanaume wawili kwa wakati mmoja , ukijumlisha na Mama anakuwa mtoto mwenye wazazi watatu. Mtoto wa aina hio huitwa Chimera.

Kwa lugha nyepesi unaweza kumpima  Rhoda  vinasaba vya damu  kwa kulinganisha na vya  Hamza  akafanana kwa asilimia  kubwa na  ukapima damu yake tena kwa kulinganisha na Asmuntis pia ikaonyesha ni baba yake, japo pia inategemea na aina ya kipimo.

“Ninachomaanisha bosi ana  chimbuko la watu wa damu ya Aikido , pengine ndio maana spidi yake ya  kuvuna nishati ni ya juu  sana”Aliongea Asmuntis.

“Inawezekana  pia , ukijumlisha na changamoto alizopita , moyo wake umejaa moto  , pengine ni wa kisasi ya juu kilichotokea.”Aliongea Hamza.

“Nadhani pia linaweza kutokuwa swala zuri , kuna hisia zinaniambia pengine mtu ambae alihusika na kuimaliza kambi  hio , sio mtu  wa kawaida  kudili nae”

“Haha , mara nyingi ikifikia hatua kama hii , wewe kama mwalimu huna chakufanya zaidi ya kumwelekeza mwanafunzi wako nini chakufanya”

‘Sidhani kama anaweza kupokea maelekezo yangu , mimi namjua vizuri”

“Basi sawa , tutaongelea kuhusu hili vizuri . Vipi kuhusu taarifa juu ya watu tuliowaweka kufuatilia wanajeshi wa  kitengo cha Malibu?”Aliuliza Hamza.

“Ni kama ulivyotea bosi , mtu ambae ulimshuku  anaonekana kuwa tatizo lakini  kuna zaidi ya  watu wawili ndani ya Malibu ambao wana matatizo”

“Ni hivyo , basi napaswa kukusikiliza kwa umakini ..”

*****

Katika anga moja , kulikuwa na jengo kubwa lenye  bango kubwa la chuma ambalo limebandikwa  juu kabisa ya jengo hilo.

Bango hilo la chuma lilionekana kama la pembe sita  lenye mchoro wa  ishara ya dhoruba.

Sehemu hio ndio yalikuwa makao makuu ya  kundi la kimasenari kwa nchi ya Mafuvu maarufu kama Metal Tide. Katika  Command Room  alionekana  jitu kubwa  la miraba minne na urefu wa mita mbili  akiwa amesimama  mbele ya dirisha akiwa amevalia koti.

Ingawa ngozi  ya nguo zake  ilikuwa imefunika mwili wake vyema , lakini  haikutosha kuficha  namna misuli ya mwili wake ilivyotuna.

Mtu huyo ndio mwanzilishi wa kundi hilo la kimasenari la Metal Tide. Alikuwa pia ni  mtaalamu wa kimapigano ambae alikuwa akikaribia kuingia katika daraja la Ugwiji, Aliitwa Jitu Chuma  au Gonzalez.

“Kwahio unasema  mwanzo mwisho mtu aliezuia mashambulizi ya kumuua Lucifer ni Black Fog?”Aliuliza mtu huyo kwa sauti ya  chini.

Nyuma yake alikuwa amesimama  mwanaume na mwanamke. Walikuwa ndio viongozi wakubwa wa  kundi hilo , watu ambao Hamza alikutana nao  yaani Helena na Gray.

“Ndio, Kapteni. Nadhani  sio suala la kawaida  kwasababu kwa kile nilichoona  Lucifer hakushituka kabisa”

“Halafu pia tumeweza kugundua  maninja kutoka  Baffodil  wameingia mjini . Makisio yetu ni kwamba wapo kwa  ajili ya kumpa ulinzi Lucifer”Aliongea Gray.

Gonzalez  aligeuka na misuli mingi ilionekana katika uso wake  kama vile ni mizizi  ya mti  uliozeeka.

“Kipindi kile baada ya Lucifer kuondoka , nilijua tu kuna kitu hakipo sawa . Kimsingi baada ya kumuua Mr Black  angejitokeza hadharai kupata sifa zake , lakini akaamua kwenda kujificha , ili nichanganya  na kuona  ni mtu gani ambae ana sifa  nyingi namna hii  kuamua kwenda kuishi maisha ya kawaida? Lakini naona  yote haya ni kwasababu  hana nguvu yoyote iliobakia katika mwili wake. Sasa  mtu hana nguvu na anajaribu kutaka kushiriki katika Baraza la maksi. Hizi ni dharau na  sisi Metal Tides hatuwezi kuchukulia hili kiwepesi .

Nataka  kuona nani  atasogelea  kundi letu baada ya  kuwatia uvilema mashetani wote wa  Inferno! Natamani kuona namna watu watakavyoniangalia baada ya pambano”

“Hongera sana Master , hatimae  ndoto  yako ya kubeba cheo cha hadhi ya nyota kumi , inakwenda kutimia”Aliongea Helena na Gray huku wakiwa na  msisimko wa hali ya juu sana  kwa kiongozi wao.

Muda ule mwanga wa radi ulitokea na kufanya  sura ya  Gonzalezi iliofunikwa na giza kuonekana , alikuwa katika tabasamu la uovu  na  halikumlenga mtu mwingine bali Hamza.

******

Saa tatu kamili za asubuhi Hamza na Regina  walimaliza kupata kifungua kinywa na kuanza safari ya matembezi kuzunguka jiji hilo la Paris.

Hamza alikuwa mzoefu wa jiji  na alikuwa akijua historia ya maeneo mengi , hivyo  alikuwa kama tour guide kwa siku hio  na uwezo wake wa kuongea kifaransa  ulimpa maksi nyingine.

Mara baada ya kufika katika Eiffel Tower , waliweza  kuona  wapenzi wengi wakipiga picha , hivyo na yeye alitoa simu akitaka kupiga picha na Regina.

“Wife  ngoja tuweke kumbukumbu”Aliongea Hamza huku akimshika Regina bega na kuanza kupiga selfie , lakini Regina alionekana hataki.

“Wewe hujui kupiga picha vizuri, unanifanya naonekana mbaya”

“Mke wangu kwa uzuri wako huo , unaogopaje kupiga picha? Vipi kufanananisha na hawa wengine ambao ni wakawaida lakini wanajitahidi  kuonekana wazuri?”

Hamza hakujali ubishi wa Regina na alimshika kwa nguvu na kuanza kupiga selfie za kutosha.

Muda huo , mwanaume alievalia katika  mavazi ya mtindo wa mpiga picha aliwasogelea , akiwa na tabasamu pana usoni.

“Excuse me, may I bother you two for a few minutes?”Aliongea yule mwanaume  kwa lugha ya kingereza , huku akiwaangalia  Regina na Hamza.

 

 

Previoua Next