Reader Settings

Unaweza kurudi ulipoishia kupitia Maktaba.

SEHEMU YA 205.

Gonzalezi alimwangalia Hamza  alivyokuwa akimsogelea na palepale alijua ni kwa namna gani  tatizo limekuwa kubwa. Akiwa na damu mdomoni , aliishia kusaga meno kwa nguvu  na kisha akaongea;

“Wewe.. ulifanya makusudi kuniigizia sio?”

“Iwe nimekuigizia  au vyovyote sio suala langu hilo, kama usingenisumbua hili lisingetokea”

“Lucifer kabla haujafanya chochote kwanini usiangalie  kushoto kwako eneo   F kwenye siti?”Aliongea Gonzalez akiwa na  mwonekano wa uovu kwenye macho yake.

Hamza alijikuta akikunja ndita na kusimama  kwanza huku akigeuka na kuangalia upande ambao   Gonzalez alikuwa akiongelea  na ile kugeuka tu sura  ya kwanza kuiona ilikuwa ni ya Regina aliekuwa amevalishwa mavazi ya  jeshi la  Metal Tide.

Wawili hao waliishia kukutanisha macho kwa umbali . Hamza alishituka  wakati huo Regina alijikuta akijawa na wasiwasi na kuishia kukunja ngumi yake tu.

Hamza muda ule ni kama makelele ya   watu kumshangilia yalimpotea ghafla na sio makelele tu ni kama  watu wote walitoweka na alibakia yeye aliekuwa kwenye steji  na  kipenzi chake Regina aliekuwa  katika siti za juu.

Kulikuwa na hisia nzito sana zilizopita katika kichwa cha Hamza.Hakudhania  uhalisia wake ungeweza  kufahamika kwa Regina kwa namna hio  tena katika Baraza la maksi.Alijikuta akishikwa  na hisia  nyingi  mchanganyiko  ambazo alitamani kuziweka wazi. Lakini katika muda huo alijihisi kuwa katika hasira zaidi ya kumdhibiti Gonzalez.

Hamza aligeuza macho yake na kumwangalia Gonzalez  katika mwonekano wa  ukauzu zaidi. Macho yake yalikuwa ni kama ya mnyama mkali  ambae anajiandaa kumrarua mtu.

“Umethubutu kumteka mke wangu?”Aliongea Hamza kwa sauti nzito sana. Muda ule ndio sasa anajua  taarifa ambayo Huge alitaka kumwambia ilikuwa ikihusiana na   jambo hilo , alijikuta  akimtukana ndani kwa ndani huku akigeuza uso wake na kumwangalia kwa  macho mabaya.

“Unaongea ujinga gani? Ninachokuonyesha ni kwamba watu wangu pia wananisaidia . Nitapigana na wewe kwa uwezo wangu wote kujiheshimisha   na kuheshimisha watu wangu”

Gonzalez asingekubali  kama  yeye ndio  alieruhusu Regina kutekwa. Vinginevyo hata kama akishinda  asingepata ujasiri wa kukalia kiti cha Ugwiji.

Lakini watu waliokuwa ndani ya eneo hilo walikuwa wakiangalia   kila tukio kwa uelewa wa hali  ya juu sana  na baada ya kumuona Hamza  mwonekano wake ukibadilika walihisi  kabisa kuna kitu hakipo sawa.

Kuhusu  Magwiji  licha ya eneo hilo kuwa na mekelele mengi lakini walikuwa na uwezo wa kumsikia Hamza na Gonzalez kwa urahisi kabisa.

“Gonzalez kamteka mke wa Lucifer? Huge unajua kuhusu  hili swala na umekaa kimya”Aliongea Oleg.

“Hatutoi taarifa bila ya kupata kitu , hio ndio sheria yetu”Aliongea Huge akiwa na tabasamu.

“Oh! Kumbe Lucifer kaoa?” Silvia alionekana kushangaa.

Nyakasura  aligeuza macho yake na kuangalia upande wa  mashabiki  na  kweli alifanikiwa  kumuona Regina.

“Ni kweli ni mke wake.  Hili furushi la chuma  ni lishenzi kweli”

“Mpaka hapa kama  Gonzalez akishindwa hatoweza kuvumilia aibu”Aliongea Mika.

“Kama ni hivyo , sitokuja kumchokoza Lucifer”Aliongea Sebastiani.

“Wewe Popo Mzee , si  Madhabahu yenu ya giza ina ushirikiano na  watu wa kuzimu. Kwanini usisaidie kumuokoa mke wa  Lucifer?”Aliuliza Oleg.

“Ingawa ni kweli sisi ni marafikii , lakini sio kihiivyo. Halafu huu  mchezo ni  kati ya watu wawili , tukiingilia haitokuwa vizuri. Mkumbuke  hata kama mbinu ya kuteka   ni ya kishenzi lakini  ni sehemu ya mbinu za kivita.Magwiji  pia wana udhaifu la sivyo   kungekuwepo na magwiji wengi ambao wapo hai” Aliongea Sebastiani na kisha akaendelea

“Jamani eh! Nimehudhuria  mabaraza mengi ya maksi tokea kuanzishwa kwake na nimeshuhudia marafiki zangu wengi wakipoteza maisha hapa hapa . Ni matumaini yangu nitaendelea kuwaona katika  mikutano ijao”Aliongea Sebastiani.

Sebastiani ndio Gwiji wa muda mrefu sana  , ambae pia amehudhuria vikao vingi vya baraza la maksi. Hakuna mtu wa kupinga maneno yake  kwa namna alivyoyaweka.

Uwanja wa vita ni kupigana kufa na kupona na kwasababu hio  mbinu nyingi zinatumika  na hakuna sheria rasmi ya  kimbinu,  iwe ni kuteka au mbinu nyingine jambo la kwanza ni kushinda mengine yanavumilika.Hivyo  ilikuwa juu ya Hamza kuweza kulimaliza swala hilo bila ya msaada wowote.

Mara baada ya kauli ya Sebastiani,  magwiji wengine wote walikaa kimya wakiwa hawana nia kabisa ya kutoa msaada na walimwangalia Hamza kwa shauku ya kutaka kujua ni jambo gani ataenda kufanya kumdhibiti Gonzalez na pia kumuokoa mke wake.

Chini  ya steji Azle na wengine   waliweza kusikia maneno ya  Hamza na walijikuta  wakipandwa  na  hasira mno.

“Damn it! Metal Tide ni kundi la wanahatamu ,  wanathubutu vipi kumteka shemeji  yetu?”

“Nilikosea . Nilipaswa kumuwekewa ulinzi shemeji tokea mwanzo”Aliongea Asmuntis akijilaumu.

“Bosi wetu   aliwachukulia wanawake kama chombo cha sterehe tu . Ila sasa hivi tuna shemeji   hakuna mwenye uzoefu kati yetu.. tulikosea kimahesabu”Aliongea Leviathani.

“Kwahio tunafanyaje sasa? Usiniambie bosi atakubali kushindwa hili pambano kwa sababu hii?”

“Hebu  acha kuongea ujinga  na fikiria namna ya  kumuokoa shem kwanza”Aliongea Mameni.

“Mimi naweza  kufanya nini  sasa kama sio kunionea tu” Berly alijikuta akilalamika.

“Master  unaonaje nikienda mimi kumsaidia”

“Haiwezekani. Anaemlinda pale ni Helena, kwa uwezo wake  kabla hujamfikia tayari atakuwa ashamuua. Hatupaswi kukurupuka katika hili   vinginevyo hatutofanikisha lolote”Aliongea Asmuntis.

“Kwahio tutafanyaje sasa.. Bro  sidhani kama ..” Black Fog alitamani kulia, akiogopa Hamza anaweza kupatwa na tatizo kwasababu hio.

Muda huo kwenye  steji , Gonzalez aliweza kumuona Hamza akisita kumshambulia tena   na alihisi uhakika wa kujipanga upya , hivyo palepale alisimama kwa kuchechemea na  kutema damu.

“Lucifer , kwasababu  kwa nia ya dhati kabisa unataka kuona uwezo wangu wote basi sina haja ya kuwa mpole tena. Nina  kwenda kukuonyesha leo hii kwanini naitwa  Goliathi”

Mara baada ya kuongea hivyo , Gonzalez palepale alichanua mikono yake juu huku akivuta pumzi nyingi  na kupumua. Mara baada ya  pumzi chache  alibweka kwa sauti kubwa.

Sasuti yake ilikuwa kubwa kiasi kwamba iliziumiza ngoma za masikio  za watu waliokuwa ndani ya eneo hilo na kutengeneza mwangwi. Muda ule kupitia sauti yake tu  eneo hilo lilianza  kutingishika kama vile   tetemeko la ardhi linatokea.

“Clang , clank!”

Steji ile  ilianza kuporomoka  na kufanya mpaka Magwji kusimama wakishangazwa na  kile kinachoonekana mbele yao.

“Nini kinaendelea , kwaninii  steji imeharibika   ghafla?”Watu walijiuliza kwa msahngao.

“Ni Gonzalez ana meng’enya chuma na kufanya elementi za madini mengine kushindwa  kuhimili uzito ndio maana steji imedondoka”Aliongea   mmoja wapo  na kufanya watu kuelewa kinachoendelea.

Upande wa  Gonzalez  ni kama alikuwa akipandiwa na wadudu  ambao wanajigandisha katika mwili wake  kwa spidi ya hali ya juu mno.

Eneo la tumbo lake palipokuwa pamebonyea  palianza kuvamiwa na madini ya chuma kwa kasi kubwa  na kuanza kupona. Ndani ya  sekunde chache tu  aliweza kurudi katika hali yake ya kawaida kabisa.

Haikuwa kupona tu  bali gamba  la chuma  liliongezeka upana wake  tabaka baada ya tabaka na  kufanya mwili wake kuwa mkubwa na wenye nguvu zaidi.

Mara baada ya kumeng’enya karibia madini yote ya chuma  yaliotengenezea steji  , kilichobakia ni baadhi ya madini mengine dhaifu tu na kufanya jukwaa na   Skrini kudondoka chini. Gonzalez hakumeng’enya  madini  katika juktwaa la magwiji kwa kuhofia kuwakasirisha.

Lakini hata hivyo chuma alichoweza kusharabu kilitosha kabisa  kufanya mwili wake  kuwa mgumu  mno na  mkubwa.

Mwanzo mwisho Hamza alikuwa akiangalia tukio hilo bila kufanya chochote , akiwa amesimama mbali na Gonzalez , hukua akimwangalia na macho yaliojaa ukauzu.

Licha ya Gonzalez kuendeleza  kunyonya chuma  Hamza hakuwa na nia ya kumzuia kabisa.

Magwiji pia walijikuta wakishangaa  baada ya kuona jitu likiwa limesimama  chini.

“Tsk tsk , huyu Gonzalez anaonekana  kuwa na  vimbinu vyake pia. Hilo gamba  lake si mchezo”Aliongea Oleg.

“Kama ataweza kuhimili uzito wa mwili wake na kuwa na spidi ileile , basi nitakubali uwezo wake sio wa kawaida”Aliongea Mikaeli.

“Uwezo huo anao  , vinginevyo  asingeendelea kunyonya chuma  na kuwa mkubwa zaidi”Aliongea Huge  na aliungwa mkono na wengine.

“Kwahio kuwa vile ndio nini! Kama ni mimi ningemuunguza  na kumgeuza kifusi cha  urojo”Aliongea  Nyakasura  kwa kajeli.

“Kipenzi wewe pekee ndio unaeweza kumuunguza , wengine wote hatuwezi”Aliongea Silvia  akicheka.

“Sijui Lucifer anapanga kufanya nini , ila anaonekana kutokuwa na wasiwasi”Aliongea Sebastiani.

Muda huo kimya kilitawala  , hata wale waliokuwa wakimshangilia Hamza walikaa kimya wakiangalia kwa   shauku kile kinachokwenda kutokea. Kila mtu alikuwa na hofu kutokana na mabadiliko aliokuwa nayo Gonzalez.

“Kweli hili ni jitu chuma , lakini atawezaje kupigana na mwili wote huo?”

“Namuona kama kifaru tu! Kwa haraka haraka uzito wa mwili wake ni tani kadhaa pale”

“Mimi kwangu naona Lucifer ana hali ngumu , kwa mwili ule hata  umlipue na bomu ni kama kumtekenya tu”

Watu  waliendelea kujadili  na wasimamaizi wa Baraza la maksi walijikuta wakiwa katika hali ya wasiwasi , maana hawakutegemea  hali ingefikia hatua hio.  Angalau walipata ahueni mara baada ya Gonzalez kuacha kunyonya chuma zaidi.

“Lucifer sasa nipo katika  nishati zangu zote za mwili ,  huu ndio muda wa pambano la uhakika sasa. Awamu hii nakuruhusu  uanze kushambulia  hahahaha..”

Gonzalez alicheka kama  kichaa  huku akipiga hatua moja mbele na kufanya Venue yote kutikisika.

“Huyu  jamaa sio wa kawaida , kwa  ukubwa wa  miguu yake na  mikono  nani anaweza kuhimili uzito wa ngumi yake?”Aliongea Berly

“Bosi hana nishati za mbingu na ardhi  ila Gonzalez ana ulinzi mkubwa wa mwili wake. Sio rahisi kudili nae”

“Bosi!  Usimdharau huyo”Aliongea Mameni kwa  sauti ya juu.

Watu wote wa upande wa Hamza   hisia zao zilikuwa juu mno. Mkandamizo wa  Gonzalez ulikuwa umefikia habari nyingine.

Wanajeshi wa kundi la  Metal Tide walirudiwa na hali ya furaha  na kuanza kumshangilia bosi wao.

“Lucifer bado tu unashangaa , hutaki kushambulia? Usipo anza  nitakukanyaga na kukugeuza chapati”

Hamza aliishia kutoa pumzi nyingi , huku akigeuza sura yake na kumwangalia Regina.

“Nadhani utakuwa hujui ni mtu gani unamjaribu?”Aliongea Hamza kwa sauti yenye kitetemeshi.

“Oh!”

Gonzalez aliishia kuchezesha mboni za macho yake huku akihisi kuna kitu hakipo sawa.

Muda huo huo  ghaflt tu mwili wa Hamza ni kama unachemka  na kufanya utoe msisimko ambao  hakuna aliewahi kuuhisia.

Ni  kama vile muda wowote dhoruba kubwa itatokea  na kuwafunika watu wote waliokuwa katika eneo hilo.

Muda ule  Hamza mwili wake ulionekana kutawaliwa na kivuli  kikubwa na kumfanya aonekane kama jitu, haikuwa hivyo tu misuli  ya mwili wake ni kama ilikuwa ikituna na kusinyaa kama moyo.

“Nini kile!!” Mikaeli alijikuta akibung’aa.

Magwiji wengine pia walijikuta wakishindwa kuelewa , mabadiliko yale ya Hamza hususani kivuli cheusi kilichozingira mwili wake na kufanana nae.

Ilikuwa ni Nyakasura pekee ambae hakuonekana kushangaa ,  na hio yote ni kutokana na kuonja  uwezo huo wa Hamza wa ajabu.

“Mwili wake ni kama umetawaliwa na mnyama mkali .. hapana ni  kama kivuli cha jini” Sebastiani alijikuta akichanganyikiwa.

“Incredible!” Auland aliishia kuongea kauli hio huku  akilinganisha uwezo wa Hamza na  Gonzalez na kutoa mchanganuo wake.

“Inaonekana kupotea kwa Lucifer kwa zaidi ya miaka mitano  , amerudi na mbinu mpya..”Aliongea Oleg huku akicheka.

Hata kwa Mchawi  mkuu  Skeletoni  , ambae hakuongea neno tokea afike hapo  alijikuta akishangazwa  na kiwingu  cha umbo la mtu kilichomzingira Hamza.

Kama magwiji  tu walikuwa katika mshangao , haikuwa hata na haja ya kuelezea kuhusu  watu wengine waliokuwa wakiangalia.

Watu wa upande wa  Hamza walijikuta wakiwa katika bumbuwazi , hakuna  aliethubutu kupepesa macho  wakiogopa watakosa  maelezo muhimu.

“Mmeona  kile kivuli cheusi .. ni kama vile kimemfanya kuwa na nguvu zaidi”

“Achana na kivuli  , mwili wake haujaongezeka sana” Watu walijikuta wakipagawa.

Upande wa Hamza palepale alitoa kilio kama vile amepandwa na wazimu  na  ni kauli moja tu iliosikika.

“Mgawanyiko!”

Hamza aliacha kusita, mbinu mgawanyiko  mwanzoni ilikuwa ikimletea shida  na kumfanya  ajione ni kama yupo katika ile ndoto , lakini  mara baada ya kuibobea wakati akipambana na Nyakasura hakuogopa tena kuitumia. Ikumbukwe mbinu hii ni ileile ambayo haikukamilika alioipata  kutoka kwa Yonesi  na alivyoanza kujifunza aliona sura ya mwanamke  aliekuwa akimuota ndotoni , mwanamke mchawi.

Gonzalez  aliweza kuhisi miguu yake ni kama inamtetemeka , licha ya kuwa na mwili chuma lakini msisimko ambao alikuwa akiusikia ulitawala kila  pande ya mwili wake  na kuanza kuhisi kuwa mdhaifu na kushindwa kutawala gamba la chuma  nje ya mwili wake.

Alipanga kumuacha Hamza  afanye shambulizi  kwanza , lakini muda huo hakujali tena kwa hofu ya kuona jambo ambalo halikutabiliwa lingemtokea.

Gonzalez palepale  alijikuta akipiga  makelele mengi  na kumsogelea  Hamza  huku akiinua  mkono wake mzito wa chuma  akielekezea  ngumi kumlenga Hamza.

Angle aliotumia  ililenga kutumia muunganiko  wa mwili wake wote  ili  iwe na nguvu ya kusambaratisha. Watu waliokuwa wakiangalia mara baada ya  kuona shambulizi lile la ngumi waliona ilikuwa na uzito mara nyingi zaidi kuliko ile ya mwanzo.

Mpaka hatua hio ilikuwa ngumu kwa watu kutabiri nani anakwenda kushinda katika hilo pambano , lakini sasa ile  kila mtu akiwa amekakamaa mwili  wakijua Hamza anakwenda kujeruhiwa vibaya ,  Hamza alikuwa ni kama  radi , kwani palepale alikanyaga  chini   kwa nguvu  huku akiwa amekunja ngumi yake na kumsogelea  Gonzalez  na kwenda kugonganisha nayo mkono kwa mkono , ngumi kwa ngumi  na  kufanya watu washindwe kuona  kinachoendelea kutokana na Hamza kuzibiwa  na mwili wa Gonzalez lakini vilevile vumbi la hatua  za Gonzalez.

Boss!!

Watu wa upande wa Hamza walijikuta wakiita kwa sauti kubwa  huku wakiwa wameshikisha vidole vya mikono yao kwa nguvu kutokana na wasiwasi.

Ilikuwa ni muda mchache sana  wa shambulizi hilo  lakini  kutokana na wasiwisi ni kama ilikuwa ni mwaka. Ila sasa ile wakiwa na wasiwasi na kupiga makelele  ghafla tu  Gonzalez aliekuwa  akionekana  kutawala alitoa  ukulele  mkubwa.

Mkono wa Gonzalez ulionekana kusinyaa  na kuwa mdogo huku  matabaka ya  ngozi ya chuma yakiachia  kama magamba ya mti.

Clang ! Clang! Clang!”

Hamza alionekana kusukumiza ngumi yake katika mkono wa Gonzalez akiwa hajarudishwa nyuma hata kwa  inchi moja  na alikuwa akisambaza nguvu ya uharibifu   na kufanya kile  kivuli cha ajabu kilichomzingira  kuzingira  mkono wake.

Gonzalez alionekana kukosa mhimili  na  kufanya mwili wake kunesa nesa ukionekana unataka kudondoka huku upande wa Hamza alionekana kutopoa.

“Clank!”

Kishindo kizito kilisisikika  na hio ni mara baada ya Gonzalez kupoteza balansi na kudondoka chini kama furushi  la chuma.

“Haaaaa!!!”

Jambo lile lilifanya  watu kutoa  ukulele wa juu mno wakionekana kupagawa na kutoamini.

Previoua Next