SEHEMU YA 207.
Hamza aliweza kuona hali ya hofu katika macho ya Regina na kumfanya ahisi moyo wake kuuma na palepale hakujiuliza mara mbili na kumkumbatia kwa nguvu kumhakikishia usalama.
Aliishia kumpiga piga mgongoni kumtuliza huku akipapasa nywele zake kumfariji.
“Usiwe na wasiwasi mke wangu. Nitakununulia Donati zenye strawberry tukirudi nyumbani na utasahau kila kilichotokea hapa..”
Regina mara baada ya kusikia kauli hio ni kama ameshituka kutoka ndotoni na kugundua mwanaume aliemkumbatia hakuwa amebadilika. Ni yule yule mwanaume aliemzoea.
Ilikuwa ni kwasababu ya uhalisia wa maisha yake yaliopita ndio ulimduwaza mpaka kushikwa na hofu kwa muda.
Watu wengi mara baada ya kuona tukio hilo walijikuta wakipiga makelele mengi na makofi ya kumpongeza Hamza.
“Kumbe ndio ilikuwa plan yake , nilishangaa kwanini bosi ametumia nguvu nyingi kumaliza pambano kikatili kumbe…”Aliongea Mameni.
“Bosi amepitia mengi sana na ndio maana siku zote anafikiria hatua mbili mbele kuliko sisi”Aliongea Asmuntis.
Black Fog kuona namna Hamza alivyomkumbatia Regina kimahaba macho yake yalijawa na wivu mwingi.
Upande wa Regina aliweza kuhisi joto la kumbatio la Hamza na alijihisi utamu moyoni lakini kwa wakati mmoja aibu ya kike ilimvaa kutokana na macho ya watu wengi yalivyokuwa yakimwangalia.
“Wewe unanichukuliaje , nawezaje kusahau kila kitu kwa kula tu Donati?” Aliongea Regina huku akimsukuma Hamza. “Halafu hata hujajisafisha lakini unanikumbatia kwa kunibana hivi?”
Hamza muda ule ndio sasa anashituka na kugundua mikono yake ilikuwa na damu na kumfanya atoe tabasamu la kizembe.
“Samahani mke wangu , kwa jinsi ulivyopendeza na vazi la kijeshi nilishindwa kujizuia na kutamani sana kukumbatia”
Regina mara baada ya kusikia hivyo alishindwa kujizuia na kutabasamu. Kwa namna alivyopendeza ni kama ua linalochanua nyakati za kiangazi kirefu.
Mara baada ya kumuona Regina ametabasamu , hatimae moyo wake ulijawa na ahueni lakini bado hatia haikumtoka.
“Nilifanya makosa , sikudhania watakuteka , siku nyingine nitahakikisha..”
“Shhii… wewe sio malaika , huwezi kunilinda kwa asilimia mia moja. Siwezi kukulaumu bila sababu”Aliongea Regina , alijua kama sio Hamza angekuwa ameshakufa muda mrefu tu na hata kama angekufa awamu hio lisingekuwa kosa lake.
Pembeni, Gray na wenzake waliendelea kuomba kwa kubembeleza wakitaka Hamza aache hilo lipite na Hamza mara baada ya kuwageukia aliishia kuwaangalia kwa shauku.
“Kwanini bado tu hamjaondoka?”
Gray na wenzake mara baada ya kusikia kauli hio , wangewezaje kutokujua kauli hio inamaanisha nini . Haraka sana walisimama na kukimbia kutoka ndani ya eneo hilo.
Upande wa Regina muda ule aliweza kukumbuka jambo na kuanza kupiga makelele .
“Helena jamani! Hamza naomba usaidie kumuokoa Helena”Aliongea Regina kwa kubembeleza na kauli hio ilimshangaza Hamza. Alijikuta akiangalia upande wa chini Helena alipodondokea namna alivyolala akiwa katika dimbwi la damu.
“Unataka kumsaidia! Kwanini?”Aliuliza.
“Anatia huruma sana kwa namna alivyosalitiwa na wenzake , ukweli alichokuwa akifanya ni kutimiza kiapo chake , sidhani kama ni kosa”Aliongea Regina.
“Wife , huyo ndio mtu alietaka kukuua kumbuka”
“Mtu alietaka kuniua sio Helena ni kiongozi wake! Kwanini unakuwa hivyo, wewe si daktari? Haraka basi msaidie kumuokoa”Aliongea Regina akiwa na wasiwasi mkubwa.
Hamza aliishia kumwangalia mwanamke huyo na nia yake ya dhati ya kutaka kumsaidia Helena na alishindwa kujizuia na kuhisi kitu kisichokuwa cha kawaida katika moyo wake.
Pengine katika macho ya mwanamke huyo kila kitu kwake alichukulia kama vitu vyepesi mno. Alimuona kama mwanamke mfanyabiashara ambae siku zote alizingatia mahesabu lakini alishangaa kuona upande wake mwingine wa kitoto.
“Basi sawa , nitajitahidi kumsaidia kama ulivyosema” Hamza alijua hata kama atamsaidia Helena kupona hatokuwa na hatari yoyote kwake.
Hivyo licha ya watu kumshangaa aliishia kukimbia chini na kumbemba Helena juu na mkono mmoja.
“Nini kinaendelea! Wanataka kumuokoa?”
“Lakini si Helena alitaka kumuua mke wake?”
“Inaonekana mke wa Lucifer anataka kumuokoa Helena”
“Devil and Angels! What a couple” Aliongea mwingine akimaanisha Hamza ni shetani na Regina ni malaika na kushangazwa na mahusiano yao.
Upande wa Regina hakujali watu watafikiria nini , alichotaka kujua kwanza ni kama Helena alikuwa hai na anaweza kupona.
“Vipi , bado yupo hai , anaweza kupona?”
“Kama angekuwa hospitalini chumba cha upasuaji , pengine angeweza kupona ila kwa hapa naweza sema tumechelewa..”
“Kwahio unamaanisha amekufa?”Aliuliza Regina kwa masikitiko na Hamza alionekana kupata wazo.
“Kuna njia tunaweza kujaribu”
Mara baada ya kuongea hivyo bila ya kusubiri Regina kumuuliza ni njia gani , Hamza aliubeba mwili wa Helena ambao umekwisha kuwa wa baridi na kukimbia nao mpaka katikati ya uwanja na kumsogelea Silvia.
“Madam, hili ni ombi kutoka kwa mke wangu, naomba unisaidie”
Muda ule ndio sasa watu walikumbuka kulikuwa na Gwiji mwenye miujiza ya uponyaji kutoka kwa wavuna nishati wa ufunuo wa nuru.
“Pale sawa! White Queen anaweza kumponyesha”
“Lakini mume wake ameuliwa na Lucifer. Atakuwa tayari kumsaidia?”
Hadhira ilijawa na shauku nini kingetokea. Je White Queen angekataa kumsaidia Hamza kutokana na mume wake kuuliwa?.
Silvia alionekana kushituka kwa dakika kadhaa na kisha palepale alitoa tabasamu.
“Sijategemea Hamza umekwisha kuoa na unataka nimpatie mke wako zawadi , kama ni hivyo basi na mkono huu wa baraka ya miujiza na uwe zawadi kwake”
Mara baada ya kuongea vile alichaneli nguvu kumtoka kupitia mkono wake na ukaonekana mwanga mwepesi mweupe kama wingu ambao ulianza kuzingira mwili wa Helena kimaajabu.
Dakika ile damu iliokuwa ikimtoka Helena iliacha mara moja moja na hali ya joto ilianza kuurejea mwili wake
“Jeraha la moyo haliwezi kuponyeshwa na ufunuo wa nuru , lakini kupitia mkono wangu wa baraka ya muujiza , nimezuia hali yake kutokuwa mbaya zaidi na pengine utakuwa na muda wa kutosha kumfikisha hospitalini na kumfanyia upasuaji”Aliongea Silvia akiwa na tabaasmu.
“Mpaka hapa inatosha , na nitaondoka nae kwanza. Kwa hali ilivyo sidhani pia kama mkutano utaendelea”
Hali ya Arena ilikuwa mbaya sana , jukwaa maalumu limekwisha kuharibika na hata eneo la juu liliharibika pia , hivyo kwa Baraza hilo la maksi kuendelea ni mpaka maboresho yafanyike kwanza.
Hivyo Hamza palepale aliomba kuandaliwa gari na alimchukua Helena na mke wake na kwenda hospitali ya karibu ndani ya mji huo wa Limour.
Ndani ya hospitali Hamza alifanya upasuaji kwa zaidi ya masaa mawili na nusu na hatimae alifanikiwa kuokoa uhai wa Helena. Ilikuwa rahisi pia kumuokoa kwasababu kwa uzoefu wa Hamza aligundua Gray hakudhamiria kumuua moja kwa moja Helena na badala yake namna alivyokizamisha kisu alitengeneza asilimia kadhaa za Helena kupona , lakini hata hivyo kama isingekuwa msaada wa Silvia ingekuwa ngumu.
Helena mara baada ya kutolewa chumba cha upasuaji , hatimae presha ilimshuka na kujihisi ahueni kubwa.
“Wife umeridhika sasa? Ila kama akiamka na kutaka kukuua tena sitokuwa na muda wa kumuokoa tena”Aliongea Hamza huku akicheka.
“Sidhani kama itatokea , ameshakufa tayari na ukamfufua, Sidhani atakuwa tena chini ya kifungo cha kutimiza kiapo chake kwa Gonzalez”
“Wife nimekuja kugundua muda mwingine una roho nzuri kiasi kwamba inakufanya uwe kama mgonjwa , nikifikiria swala la Lamla na la Helena, nakuona kama mama Teresa wa wakati wetu” Aliongea Hamza huku akitingisha kichwa kumuonea huruma mke wake kwa kuwa na roho nzuri kupitiliza.
Regina kusikia kauli hio alishikwa na haya kidogo na kuishia kumwemwesa lipsi zake.
“Nimemchukulia kama mwanamke mwenzangu aliesalitiwa na watu wengi na alieshindwa kujizuia , ndio maana..”
“Kwenye ulimwengu wa giza tendo la huruma moja tu linaweza kukufanya upoteze uhai. Naweza kuonekana mkatili lakini ukweli si kuzaliwa mkatili ni uzoefu ndio maana”
“Basi sawa, najua mimi ni mjinga lakini nilishindwa kujizuia. Isitoshe Helena si mtu wa kawaida tu mbele yako? Kama atageuka na kuwa mbaya kwangu unaweza kunilinda tena. Hata hivyo mimi sio mtoto mdogo , nimetekwa leo na kidogo tu niuliwe na nimechoka sana .. acha kuongea kama unanifokea basi”Aliongea Regina huku akionyesha hali ya machungu kwenye macho yake.
“Haya basi yameisha mke wangu, kwasasa hakuna namna, nitakuwa na wasiwasi ukirudi Paris peke yako. Kwanini usikae na sisi hapa , haitokuwa mbaya kama utashiriki katika mikutano iliobakia ..”Alishauri Hamza.
“Naweza kushiriki? Watu wa Baraza la maksi si watanizuia”
“Mpaka sasa ushajulikana ni nani kwangu , nani anaweza kuthubutu kukuzuia”
“Najua una nguvu na wanakuita mtawala wa kuzimu na Gwiji lakini sina vigezo vyovyote vingine mimi kama mimi”
“Wewe tayari ni mke wangu , vingezo vingine vya kwako vya nini?”
“Lakini hujanichumimbia na kunioa vizuri”Aliongea Regina kama mtoto huku akipepesa macho yake haraka haraka.
Hamza alijikuta akikosa usemi , mara baada ya kufikiria swala la kuchumbia tena na harusi kichwa kilianza kuuma. Sio kama hakutaka lakini bado hakupata wazo sahihi la namna ya kuchumbia.
“Wife nipe muda , nikishapata wazo zuri haraka sana nitakuchumbia na tufunge harusi”
“Usijali , unaweza kufanya taratribu taratibu , isitoshe sio kama nina haraka na harusi wala nini.”
“Hapana , hili swala linatakiwa kuharakishwa”Aliongea Hamza huku akijiambia namna ya kupunguza ukauzu wa Regina kwake ni kumpa kile kitakachomridhisha ili amuweka kifuani na kwa namna hio kidogo atarahisisha baadhi ya matatizo mengi yatakayojitokeza.
Wawili hao mara baada ya kutoka nje ya hospitali , watu wa Inferno walikuwa wakiwasubiria na kila mmoja alisogea na kumsalmia Regina kwa kumuita Shemeji.
Jina hilo lilimfanya Regina kuhisi aibu na kufanya sura yake kuwa ya moto na hio yote ni kutokana na kwamba watu hao wengi walikuwa ni wazee kuliko Hamza, lakini waliokuwa wakifanya ni kama Hamza ndio aliekuwa mzee.
“Wife ngoja nikutambulishe , huyu ni Azzle, unaweza kumuita tu Aziza kurahisisha, ni mhunzi anapenda sana kugongelea vyuma, Huyu hapa ni Asmuntis au mtu mchafu, pepo lake linamruhusu kuoga mara moja tu kwa mwaka. Huyu Bonge hapa tunamuita Mameni , anajishughulisha na biashara za siraha , anapenda sana kamari na wanawake . Huyu hapa Braza tunamuita Leviathani a.k,a Ngisi mkubwa kwasababu bendera ya meli zake zina chata la Ngisi , ana mtoto mdogo wa kike na sio mtu wa kunyoa kipara , alikuwa na rasta ndevu na ngumu kama maganda ya mua. Kuhusu huyu mrembo wa sura hapa ni mshikaji wangu Berly , ni mvivu kupindukia , ukiachana na kupenda kwake kula vinono lakini vilevile ana swaga hatari mbele ya wanawake. Ujuzi wake mwingine ni kujua kukopa mpaka wanaomdai, hana sifa nyingine kubwa..”
Regina mara baada ya kusikia utambulisho huo alijikuta akichanganyikiwa , alijiuliza kwanini kila alietambulisha katika kundi hilo hakuna anaeonekana kuwa wa kawaida. Lakini hata hivyo alijua watu hao walikuwa maarufu zaidi katika ulimwengu wa giza na walikuwa marafiki wa Hamza wa kufa na kuzikana . Hivyo hakuwadharau na alijitahidi kufahamiana nao vizuri.
Mara baada yakufikia zamu ya Rhoda , Regina alionekana kushangaa.
“Dada na wewe ..”
“Samahani sana Dada Regina kwa kukudanganya ile siku, Master wangu ni Asmuntis na mimi kazi yangu ni kuua”
“Wewe ni muuaji!?” Regina alishangaa maana hakutegemea msichana mzuri na mwenye sura ya kipole kama huyo angekuwa muuaji.
“Ndio” Alijibu Black Fog bila ya kuwa na aibu kuhusu kazi yake.
Ijapokuwa Regina alijikuta akijisikia furaha hatimae kumjua mume wake , lakini mara baada ya kukutana na watu hao wasiokuwa wa kawaida alishikwa na wasiwasi.
“Bosi , watu wa Baraza wanasema kazi ya kuweka mambo sawa imekaribia kumalizika , unaweza kujunga kwa ajili ya kumalizia kikao cha leo”Aliongea Asmuntis.
“Okey! Napaswa kuwakabidhi tuzo leo , hivyo twendeni maana sitaki hili swala lipite”
Mara baada ya kurudi ukumbuni watu wengi waliwaangalia , asilimia kubwa walimwangalia Hamza , tofauti na mwanzo sasa walionekana kumheshimu zaidi.
“Hehe.. bosi ndondi ulioonyesha leo imekuongezea mashabiki wengi sana. Unaonaje tukirudisha umoja wetu wa Inferno. Nitatamba sana mjini”Aliongea Bellie.
“Hebu acha zako Belli , hii ndio mara yangu ya mwisho kuhudhuria Baraza la maksi , kama isingekuwa kitengo cha Malibu kunishinikiza nisingeshiriki”Aliongea Hamza kwa kingereza na kufanya wenzake kukubaliana kinyonge , lakini upande wa Regina alionekana kunyaka baadhi ya maneno.
“Una uhusiano gani na kitengo cha Malibu?”
“Mke wangu ni stori ndefu, nitakuambia tukifika nyumbani”Aliongea Hamza.
Kila mmoja alirudi katika siti yake huku Regina akizungukwa na watu na kuwa kama malkia.
Mara baada ya kila mtu kupata muda wa kupumzisha akili kidogo ndio sasa waligundua takataka na mchanga vilivyokuwa vimechafua eneo hilo vimesafishwa . Lakini hata hivyo jukwaa ambalo liliharibiwa halikutengenezwa upya.
Vyuma vyuma na viti na matofali yalikusanywa na kuweka katika eneo moja na kutengeneza kifusi.
Ukiachana na Hamza , magwiji wengine ambao walienda kupumzika walilerejea pia.
Mzee Maxim , ambae ni raisi wa Baraza la maksi alimsogelea Raisi wa Adept Association na kisha waliongea kidogo kwa sauti ya chini. Kwa namna alivyokuwa akiongea mtu wa kawaida angesema Maxim ni kichaa kwa kuongea na koti na suruali hewani.
“Jamani naombeni utulivu wenu , kutokana na jukwaa letu kuharibika tutajenga la dharula sasa hivi na nimemuomba Mr Air kutusaidia katika jambo hili, naombeni tumshukuru kwa kumpigia makofi mengi”
Mara baada ya Maxim kuongea hivyo , watu walianza kupiga makofi mengi ya kumshangilia na hio yote ni kwamba Mr Air alikuwa ni mtu wa mambo ya chini chini sana , ni adimu sana kuonyesha uwezo wake , hivyo ni kama kujenga jukwaa la dharula ni nafasi ya kuona uwezo wake.
Hata Hamza mwenyewe na magwiji wengine , walijawa na shauku ya kutaka kuona ni kwa namna gani Mr Air anakwenda kujenga jukwaa ndani ya muda mchache.
Mr Air alisogea mpaka katikati ya eneo la wazi na bila ya kutoa sauti , chini ya macho zaidi ya watu elfu therathini , ghafla tu hali ya mkondo wa upepo ndani ya eneo hilo ilibadilika na kufumba na kufumbua ule upepo uligeuka kimbunga na kuanza kumuinua kutoka chini na kumpandisha juu hewani.
Comments