SEHEMU YA 210.
Mchawi wa wafu(Necromancer).
Muda ulionekana kusimama kwa muda , mara baada ya kusikia jibu lake . Regina macho yake yalioyaa maji yalimwangalia Hamza kama vile alikuwa amepotelea katika mawazo.
Hategemea kabisa jibu la Hamza lingekuwa la moja kwa moja na jepesi. jepesi kiasi kwamba alishindwa kuelewa ni nini hasa mwanaume huyo anajaribu kumaanisha.
Mara baada ya dakika moja yote, Hamza aliona mwanamke huyo hakushituka , hivyo aliishia kutoa tabasamu na kunyoosha mkono wake kumgusa Regina usoni.
“Silly wife, unaota nini mchana wote huu? Ingia kwenye gari”
Muda huo ni kama sasa Regina alishituka katika mawazo yake , na alipiga hatua moja kurudi nyuma huku akiongea kwa sauti hafifu;
“Wewe ni mjinga , nilikuwa nikikudanganya lakini bado tu unaniamini”
“Wewe ndio unaejua kama unaigiza au ni kweli , lakini kwangu mimi sijali kabisa kama wewe ni halisi au feki. Napenda unavyoonekana na napenda unachokifanya , kila kinachohusiana na wewe nakipenda . Na kingine kama utaendelea kuniigizia kwa maisha yako yote unadhani unachokifanya kitaendelea kuwa maigizo?”
Regina kusikia hivyo alijikuta akishangaa , aliishia kumwangalia mwanaume huyo mwenye uso wake mweupe ulivyokuwa katika hali ya utulivu na kuishia kuuliza kiwasiwasi.
“Unapanga kuishi na mimi maisha yako yote?”
“Ndio , nimekuoa maana yake nitaishi na wewe milele”Aliongea Hamza.
“Lakini nimekudanganya” Regina alishindwa kuelewa.
“Wife nadhani unashindwa kuelewa kitu kimoja , tokea mwanzo sikujali kama ulikuwa ukidanganya kuhusu Helena . Kama ulipanga kumchukua Helena kama mtu wako , hilo ni juu yako. Naona anafaa pia maana ana mafunzo ya hali ya juu , ni muaminifu na tabia nzuri na kingine ni mwanamke . Chaguo lako ni sahihi na hata sijaliwazia sana”Aliongea Hamza
“Lakini kwanini? Sasa hivi tu ulionekana ku…”
“Niache nimalize….”
“Nimefikiria kwa kina na kugundua wewe ni mfanyabiashara. Na kama mfanyabiashara kama ungekuwa mwepesi kiasi cha kuitwa mtu mwenye roho nzuri basi kampuni ya Dosam isingekuwa hai mpaka sasa h ivi . Ukweli wakati tunakutana sikukuona kama mwanamke mpole. Kwangu mimi ulionekana kama mwanamke ambae una mtazamo wako binafsi kwenye mambo mazuri na mabaya”
Regina kusikia hivyo alishindwa kuongea na kufanya mikono yake kugang’ania gauni lake kwa nguvu.
“Pia nilikuwa na wasiwasi unaweza kuwa mtu mwenye roho nzuri kupitiliza na siku moja kujiingiza katika matatizo . Lakini sasa hivi kuona mpango wako juu ya Helena , nimepatwa na amani , kwa kuona angalau mke wangu sio mjinga bali ana akili kuliko nilivyotegemea. Ila nisiwe mnafiki sijapenda namna ulivyoniigizia na kunifanya nione kila kitu ni kweli”
“Mwisho wa maneno yote bado unaonekana kunichukia kwa kile nilichyofanya…”Aliongea Regina akikunja sura.
Hamza alitabasamu na kisha alimsogelea Regina na kumkumbatia kiwepesi na kisha palepale alimgeuza na kwenda kumwegamiza kwenye gari.
“Wewe … unataka kufanya nini?”
Mikono yote ya Regina ilikuwa imajishikiza katika kifua cha Hamza kumzuia , alihisi hofu na aibu kwa wakati moja.
“Wife kwanini unashindwa kuelewa? Mimi sijali kile unachokifanya , kwasababu unachofanya ndio utashi wako. Kama unao uwezo wa kunidanganya basi huo ni uwezo wako maana mimi pia sio mwepesi kudanganyika kutokana na uwezo wangu wa akili . kitu pekee ninachotaka angalau kujua ni kuhusu hisia zako kwangu kama ni za kweli au lah , kwasababu hisia zangu kwako ni za dhati kabisa..”
Regina kusikia hivyo alijikuta akishituka na kuacha kuleta ukinzani huku akimwangalia Hamza na macho yake yaliojaa maji.
Wawili hao walijikuta wakiangaliana na mara baada ya kuangaliana kwa kitambo kirefu. Hamza alishusha lipsi zake na kupokelewa na Regina na walijikuta wakidendeka kwa hisia kali.
Ingawa haikuwa mara yao ya kwanza kukiss , lakini picha waliotengeneza katika eneo hilo pembeni mwa hospitalini , ilikuwa ya aina yake . Baada ya mgogoro wao dakika chache zilizopita , Regina mara baada ya lipsi zake kukutanisha na za Hamza alihisi shoti za umeme zikisambaa mwili mzima.
Aliishia kutoa macho huku mwili wake laini ukitingishika zaidi ya mara mbili. Alitaka kutoa kilio mara baada ya kuhisi joto na hisia kali kutoka kwa mwanaume huyo, alijihisi ni kama anazamishwa majini na kuibuliwa.
Baada ya kushindana na hisia zake na zikamdhibiti kisawasawa , alijikuta akifumba macho yake yaliojaa machozi na kufanya yatengeneze mfereji wa maji. Alijikuta bila kuelewa amekwisha kupitisha mikono yake na kuizungusha katika mgongo wa mwanaume huyo huku akimvutia kwake kwa nguvu.
Hakuna aliekuwa akijua ni kwa muda gani walikuwa wamegandana , mara baada ya kuhisi pumzi zinataka kumwishia. Hamza hatimae alimwachia mrembo wake.
Hamza mara baada ya kumwangalia mwanamke huyo na kuona jinsi macho yake yalivyokuwa mekundu na kuonekana kama amekosewa sana, alijikuta akishindwa kujizuia na kuachia kicheko.
“Haha.. Wife mbona unalia?” Aliongea Hamza huku akinyoosha mkono wake na kumfuta Regina machozi kutoka kwenye mashavu yake.
Regina alijikuta akihema kwa nguvu na kisha kuinua kichwa chake na kumwangalia Hamza na kisha akiwa siriasi aliongea;
“Na mimi hisia zangu kwako ni za dhati , siwezi kudanganya kuhusu hisia zangu”
“Najua, kwa namna ulivyonikumbatia kwa nguvu inatosha. Kwangu mimi ili mradi uwe mkweli juu ya hisia zako , mambo mengine sitojali”Aliongea Hamza akiwa na tabasamu.
“Sikutaka kukudanganya kuhusu Helena, ni kama ulivyosema ni utashi wangu… nili..”Alionekana kukosa neno zuri la kuongea;
“Na mimi nilitaka kuwa na nguvu haraka iwezekanavyo ili kupunguza gepu lililopo kati yetu. Ndio maana nilitaka kumchukua Helena , isitoshe anao uwezo wa kuniambia kila kitu kuhusu ulimwengu wa Giza”Aliongea Regina kwa sauti hafifu.
“Kupunguza gepu! Kuna utofauti gani kwani na sasa?”
“Kuna haja hata ya kuuliza? Wewe ni Gwiji na una madaraka makubwa , mimi ni mfanyabiashara mdogo tu kutoka nchi masikini , naona wasiwasi nitakuangusha …Na mimi pia nataka kuwa na nguvu haraka iwezekanavyo. Hata kama siwezi kuvuna nishati za mbingu na ardhi. Ila kwasababu asili yangu ni kutoka kwa watu wa Bondeni familia ya urithi wa damu. Nataka kutumia fursa hii kukirudisha kitengo cha Binamu na teknolojia ya jicho la Anga katika himaya yangu , nikifanikiwa najua hautonichoka” Hamza kusikia hivyo alijikuta akishangaa na kukosa usemi juu ya namna Regina anavyoyachukulia mahusiano.
“Wife sijawahi kuwaza nitakuja kukuchoka kwasababu ya ulivyo , kwanini unafikiria sana? Kama unataka kumiliki teknolojia ya jicho la Anga itakuwa ngumu sana , maana Huge sio mtu mwepesi , alitengeneza kitengo cha Binamu kwa ajili ya kujilinda kimadaraka kutoka kwa Babu na Bibi yako”
“Lazima nifanikishe , wewe unaweza usijali mimi nilivyo , ila kwa marafiki zako ni tofauti , wakiendelea kuniona wa kawaida watasema sistahili kuwa na wewe na kadri watakavyoonyesha hisia zao utajisikia vibaya na pengine baada ya muda utaniona sina maana”Aliongea Regina katika hali ya kuchukia.
Hamza aliona mwanamke huyo alikuwa akifikiria sana, alijiambia kwanini afikirie kuhusu watu wanavyomuongelea mke wake.
“Wife acha kufikiria mbali , ikitokea mtu akakuongelea vibaya na kusema hustahili kuwa na mimi atakula kibano”
“Mimi sitaki hivyo , sitaki muda wote niwe nakutegemea kwenye kunilinda. Nataka kuwa na nguvu haraka iwezekanavyo na kuajiri watu wengi.. Ukweli sikutaka kukudanganya, ilikuwa ni wasiwasi wangu utaniona ni mtu mwenye hila na mitego mingi kwasababu unapenda mwanamke mpole na mwenye utoto utoto, sikutaka kuharibu picha yangu iliojijenga ndani ya moyo wako..”
Aliongea Regina akiwa na aibu kiasi cha kuinamisha kichwa chini,upande wa Hamza baada ya kusikia maneno hayo alijikuta akishindwa kujizuia na kutoa kicheko kikubwa.
“Hahahaha… Haha.. Wife . haha.. kumbe una vituko namna hii. Kwahio ndio unavyojiona , kama mwanamke mpole na mwenye utoto? Haha.. dah!”
Hamza alicheka mpaka kufikia hatua alianza kushika tumbo lake.
“Wewe unacheka nini vyote hivyo?”
Regina hata yeye aliona maneno aliongea hayakuwa ya kawaida na kufanya sura yake kuiva kutokana na aibu nyingi huku akipiga piga miguu chini kwa hasira.
“Wewe usicheke tena nakuambia”
Hamza alicheka sana kiasi cha kufanya machozi kuanza kumtoka . Aliishia kuinua macho yake juu angani huku akivuta pumzi nyingi huku akiongea
“Mungu baba kwanini umenipa mwanamke mjinga kama mke wangu? Inakuwaje kukawa na mwanamke wa hivi dunia hii?”
“Umekuwa chizi! Mimi nina tatizo gani? Au nyie wanaume mnapenda wanawake wenye mambo ya kuficha ficha?”
“Sio kuhusu hilo . Kuwa mke hupaswi kujitahidi kujua kila kitu. Najua kila ulichofanya ulitaka kunivutia. Ila kilichonichekesha ni namna ulivyoongea kile kilichopo ndani ya moyo wako kwa usiriasi mkubwa. Niimehisi umeongea kijinga sana ..hahaha”
“Nimekudanganya hukupenda , nimekuambia ukweli unaniona mjinga. Mbona unakuwa mgumu hivyo kueleweka ? Mimi nina hasira , sitaki kuwongea na wewe tena , nenda mwenyewe kwenye mkutano” Regina alihisi kushikwa na aibu na kugeuka kutaka kuondoka.
Hamza palepale alimsogelea na kumkumbatia kwa nyuma huku akiongea kwa kumnong’oneza katika sikio lake.
“Mke wangu usiwe na hasira ni kwa jinsi ulivyokuwa cute ndio maana nilicheka na sio kwamba nakuchukia wala nini. Ukweli huna haja ya kunifanya nikufikirie vipi katika moyo wangu , wewe unaweza kufanya unavyotaka. Ni kama kipindi kile ulivyomtafuta Lamla ili kurudi nyumbani , nina uhakika hujategemea kupata kitu chochote kutoka kwako , si ndio?”
Regina mara baada ya kusikia hivyo , aligeuza kichwa chake na kumwangalia.
“Kuna vitu vingi unafanya sio kwamba unaigiza , kwa mfano namna unavyoonekana ukiwa unakula donati , ni kwasababu unazipenda kweli. Ninachomaanisha siwezi kuwa mnafiki kwako . Watu tunazaliwa na tabia nyingi sana , nyingine zimejificha na zinaibuka kadri tunavyongeza umri , pengine hata mimi nina tabia ambazo huzijui na mimi pia bado sizijui , lakini je kwasababu ya upande wangu mwingine inatufanya tuachane?”
Regina mara baada ya kusikia hivyo , alijikuta akipata ahueni baada ya kuona mwanaume huyo alikuwa akimwelewa vyema. Alijikuta furaha ikimjaa na moyo wake kuhisi utamu kama sukari.
“Muda wa kwenda kwenye mkutano ushafika , twende zetu”Aliongea Hamza na Regina alitingisha kichwa , lakini muda ule alihisi kitu hakipo sawa.
“Vipi nibadilishe nguo? Hizi nguo nimevaa tokea jana”
“Kwanini , mbona ziko sawa tu”
“Wewe ni maarufu , nikionekana kurudia rudia nguo kwa siku nzima si nitaonekana wa kawaida?”
“Wife uzuri wako haupo kwenye nguo unazovaa bali kwa urembo wako wa sura. Kama ukivaa vizuri kupitiliza si itawafanya vidume kukumezea mate , unataka kuniongezea maadui?”Aliongea na Regina kusikai hivyo alishangaa kidogo.
“Kweli?”
“Ndio , sipendi kabisa watu kumkodolea macho mke wangu”
“Oh, so you’re that petty … haya basi twende” Aliongea Regina ambae alikuwa katika mudi nzuri na kuingia kwenye gari.
Ingawa lisaa limoja la maongezi nje ya hospitali kutokuwa kawaida. Lakini ni mazungumzo ambayo yaliwafanya kuwa karibu zaidi na kuimarisha uhusiano wao.
Hamza aliweza kuona Regina kila alichofanya kilitokana na hisia zake na hiko ndio alichotaka kuona. Lakini suala lingine lilingiia akilini na hilo ni juu ya Regina kutaka kurudisha nguvu zake ndani ya Binamu na kumiliki teknolojia ya jicho la Anga. Mpango wake huo ulimfanya Hamza kuwa na wasiwasi mkubwa , lakini hakutaka kumzuia vilevile na alijiambia atajitahidi kwenda nae hatua kwa hatua.
Mara baada ya kufika nje ya ukumbi , Regina alipokelewa na washikaji zake na kisha yeye alichukua uelekeo wa VIP kama kawaida. Muda ambao aliingia katika chumba cha mapunziko aliweza kumuona Khalid akiongea na Huge.
“Sir Luciger , umekuja katika muda muafaka . Nipo hapa kuwajulisha kwamba hamtaondoka mapema kwasababu leo Kikao cha Magwiji kitafanyika pia”
“Kikao chetu ni leo? Kama ni hivyo kwanini tunaendelea kukaa kwenye jukwaa? Si leo ni mkusanyiko wa ajenda za kitaasisi na wawakilishi?”
Hamza aliona haikuwa na muhimu sana kwa wao kukaa jukwaani kwasababu ajenda za siku hio hazikuwa zikiwahusu. Ukweli kama isingekuwa suala la kitengo cha Malibu angemchukua Regina kwenda Shopping.
“Ukweli ni kwamba , kuna tatizo lingine ambalo linahitaji utatuzi katika baraza hili la maksi . Sir Luciger nadhani utakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu mwanasayansi maarufu duniani , Dokta Genesha ambae alipotea”Aliongea Khalid.
“Dokta Genesha! Mbona alishakufa na ni mimi niliemuona kwa macho yangu kabisa na sio hivyo tu nilimchoma na kumwaga majivu yake baharini”
“Nini! Dokta Genesha amekufa ?” Khalidi alionekana kushangaa na Hamza aligeuza sura yake na kumwangalia Mathias Huge.
“Vipi na wewe huniamini au? Nadhani utakuwa na taarifa juu ya hili kama sikosei?”Aliongea Hamza akimlenga Huge.
“My information is not free.”Aliongea akimaanisha taarifa zake sio za bure.
“F*ck , inachosha sana kudili na mtu kama wewe , kwanini unapenda sana hela kuliko mimi?”Aliongea Hamza huku akimpotezea na kumgeukia Khalid.
“Ni kama nilivyosema bwana Khalidi , Genesha amefariki , ni juu yako kama utaamini au lah , lakini kwanini umemtaja?”Aliuliza Hamza na kumfanya Khalid kushangaa kidogo kabla ya kujibu.
“Ni hivi , ukweli ni kwamba taasisi yetu imekuwa ikifanya kazi pamoja na Dokta Genesha.. Alikuwa ni mshauri wetu mkuu kwenye masuala ya kitafiti . Kabla ya kupotea aliweka Safe box kwenye umoja wetu na alitoa maekelezo ifunguliwe wakati wa Baraza la maksi”
“Ni kitu gani amehifadhi katika hicho kiboksi?”Aliuliza Hamza.
“Niwie radhi, siwezi kufahamu kutokana na nafasi yangu. Lakini moja ya sababu ya kualikwa kwa magwiiji wote kumi ni kwa ajili ya kuonyesha kilichopo ndani ya hio safe box. Kwasababu Dokta Genesha alikuwa akifanyia utafiti juu ya Ankh , teknolojia ya dawa ya kuzuia kifo , tuna kila sababu ya kuamini alichoacha kinahusiana na dawa hio”
“Na kama ndivyo , basi litakuwa suala linalohusisha utajiri mkubwa, kama tusingekuwa na wataalamu wengi ndani ya baraza letu basi tusingethubutu kufungua hiki kiboksi wala kukitaja kabisa”
Hamza aliishia kuguna ndani kwa ndani , kabla Dokta Genesha anafariki alimwabia kabisa hakuna dawa ya kuzuia kifo zaidi ya uwepo wa nadharia tu ambazo nyingine zilihusisha tafsiri ya kitabu ambayo alipaswa kuifanyia kazi , ukweli ni kwamba hata kama utafiti huo ungemalizika bila ya elementi maalumu isingeweza kufanikiwa .Lakini alijiuliza kwanini akaamua kuweka kiboksi muhimu katika Baraza la Maksi? Au kuna kitu kingine hakuwa akijua tofauti na Ankh alichokuwa akifanyia kazi?”
“Hatukutangaza mapema kwasabu ya kuhofia mtu mwenye nia mbaya anaweza kujaribu kuikwapua , lakini sasa hivi kwasababu ya uwepo wa Magwiji wote kumi tunayo kila sababu ya kutangaza ,tunakwenda kuifungua usiku wa leo”Aliongea Khalid.
Hamza alifikiria kwa muda , lakini hakuweza kudhania ni kitu gani ambacho Genesha ameweka katika hicho kisanduku cha usalama.
“Wewe si una jicho la Anga , unajua nini kipo ndani ya hicho kiboksi? Usiniambie unataka hela kunijibu swali langu?”Aliongea Hamza akimwangalia Huge.
“Siri za mbingu hazitoki bure”Aliongea
“Kama isingekuwa inachosha kupambana na mtu kama wewe ningeshakupiga na kukushikisha adabu”Aliongea Hamza huku akitingisha kichwa chake.
****
Ajenda ya kikao cha kwanza ilikuwa ni juu ya masuala makubwa yanayoendelea katika ulimwengu wa giza. Kulikuwa na mikinzano mingi inayotokana na wanufaika na kufanya watu kuanza kurushiana maneno.
Moja ya kitu kilichoibua mapingano ni juu ya Earth Axis , ambayo ipo chini ya mikono ya Watanzania , kila taasisi ilikuwa ikivutia upande wake kutaka kujumuishwa kwenye kujua siri za Earth Axis.
Lakini hata hivyo Balozi Rajabu na wenzake kama wawakilishi , walionekana kujiandaa vyema kwa hali hio.
Ukiachana na hayo kulikuwa na masuala mawili ambayo yalikuwa muhimu zaidi , kwanza Tanzania haikuwa ikijua Earth Axis ni nini na wala haikuwa na uhakika kama ni kitu kibaya kwa binadamu au kizuri hivyo halikuwa jukumu lao kugawa taarifa za Earth Axis.
Hamza mara baada ya kusikiliza watu wa kitengo cha Malibu wakiweka mezani hoja zao , aliishia kukubali na kujiambia ndio maana licha ya kutokuwa na uwezo wa mapigano lakini waliaminiwa mno kuja kuwakilisha taifa , walionekana kuwa vizuri mno katika kujenga hoja.
Wakati wa mapumziko mafupi ya vikao, Balozi Rajabu na wenzake walimsogelea Hamza aliekuwa na washikaji zake wa Inferno na kuwasalimiua kwa ukarimu. Alieonyesha uchangamfu zaidi alikuwa ni Mboma ambae mwanzo alionyesha kumdharau Hamza sana katika kikao chao cha kwanza.
Hamza upande wake alijua watu hao walitaka kuazima nguvu ya ushawishi wake huku ughaibuni ili kuwanyamazisha watu wasitoe vitisho kwa Tanzania.
Haikuwa hivyo tu Balozi Rajabu pia alionekana kuchangamkiana na Mathias Huge , akionyesha kumtega kwa maneno. Ukweli ni kwamba licha ya Binamu kuongozwa na Huge lakini teknolojia ya jicho la Anga ilikuwa ni miliki ya watu wa Bondeni ambao asili yao ni Afrika , hivyo ni sawa na kusema Huge ni mwafrika pia ambae asingeweza kuona Tanzania inaingia matatizoni, licha ya kwamba ana unafiki mwingi likija suala la kuuza taarifa. Hivyo uwepo wa Hamza , Nyakasura na Huge ilikuwa ni kama msingi wa kuilinda Earth Axis ili mataifa yenye nguvu yasijaribu kushurutisha kugawa siri zake kwa nguvu.
Hamza mara baada ya kuona watu hao wa Malibu walikuwa wakijiweza vyema katika vikao hivyo , hakuona haja ya kushiriki kwa kila kitu, alichopanga ni kutumiza nusu ya yale alioomba rafiki yake Himidu kuhusu kumjua msaliti ndani ya kitengo.
Alikuwa na watu wake aliowaweka kutoka Baffodil na walikuwa wakiwachunguza vigogo hao kwa umakini mkubwa.
Usiku wakati wa chakula , Hamza alichomoka kutoka nje ya ukumbi na kwenda kuingia kwenye gari moja hivi ya rangi nyeusi aina ya cadillac.
Mara baada ya kuingia aliweza kukutana na Black Fog ambae ndio aliekuwa dereva wa gari hio na liliondoshwa mara moja.
“Una uhakika ndio yeye?”Aliuliza Hamza.
“Tumethibitisha ni yeye kabisa unaemtilia shaka. Ile siku wakati mvua ikiwa inanyesha na alieiba Nyaraka. Yote ilikuwa ni mipango yake”
“Inasikitisha sana , kwanini asingekuwa mwaminifu tu”Aliongea Hamza huku akitingisha kichwa.
“Bro , nimekubali sana uwezo wako wa kusoma watu , kama ingekuwa mimi mtu ambae ningemtilia shaka ni Mboma”
“Mboma ni mtu anaependa maisha ya starehe tu na kuwa na uwezo mdogo wa kufikiria , lakini hana ujasiri wa kusaliti nchi”Aliongea Hamza
“Karibia ya watu wote wa kitengo cha Malibu wanaonekana kupenda starehe , tuliowafuatilia karibia wote walihudhuria Casino na wengine walilala na makahaba kasoro yeye tu”Aliongea Black Fog na kumfanya Hamza kutabasamu tu.
Mara baada ya Black Fog kuendesha gari kwa umbali kama wa dakika kumi au ishirini hivi walikuja kusimamisha gari upande wa magharibi mwa mji wa Limour katika makaburi.
Ni sehemu iliokuwa na mazingira mazuri sana , ukiachana na makaburi yaliokuwa kwenye bustani safi , lakini vilevile kulikuwa na kanisa kubwa la Cathedral.
Kulikuwa na magari kadhaa yalioegeshwa kando ya barabara mkabala na kanisa na yalionekana sio ya waumini , bali ni wafanyakazi wa eneo hilo.
Black Fog na Hamza waliingia ndani ya kanisa , mlango ulikuwa wazi licha ya kuwa usiku na ile wanazama ndani waliweza kumuona mwanamke alievalia nguo nyeusi na hat kubwa ya rangi nyeusi pia , akiwa anasali mbele ya sanamu la bikra maria . Pembeni yake alikuwa ameweka Briefcase. Alionekana ni kama ndio anamalizia kusali baada ya kuonyesha ishara ya msalaba huku akitamka maneno.
“Mungu , ili mradi nifike salama nchini America. Nitatumia muda wangu wote kukutukuza na kuliabudu jina lako..”
Mara baada ya kumaliza kuongea maneno hayo , palepale alishika ile briefcase na kusimama. Ile tu anataka kuondoka , alijikuta akiinua uso wake na kukutana na sura ya Hamza na Black Fog wakiwa katika eneo la kuingilia ndani ya kanisa .
“Ah! Hamza.. Mr Hamza!?”Alionekana kushituka mno.
Comments