Reader Settings

SEHEMU YA 211.

Mwanamke aliekuwa mbele   yake , hakuwa mwingine bali ni  Rehema Mndeme , katibu muhtasi wa balozi  Rajabu.

Rehema mara baada ya kumuona  Hamza mbele yake , sura yake ilijawa na wasiwasi mwingi kiasi cha  kufubaa.

“Mr Hamza , kwa kwanini..”

“Kwanini  nimejua upo hapa , si ndio unataka kuuliza hivyo? kukujibu swali lako ni kwasababu kuna mtu  alikuwa akikufuatilia”

“Kunifuatilia! Nimefanya nini mpaka kuwe na mtu wa kunifuatilia?”

“Sister Ray , kwasababu mambo yamefikia hatua hii , kuna haja ya wewe kukimbia. Ukweli tokea siku niliokutana na wewe kwa mara ya kwanza nilihisi una tatizo , hivyo huna haja ya kuendelea kujificha”Aliongea Hamza na kumfanya Rehema  kuwa katika hali ya mshangao.

“Wewe..! Kwani uliona nini?”Aliuliza kwa shauku.

“Wewe sio sekretari wa  idara ya kawaida . Bali ni katibu muhtasi wa  kitengo cha  Malibu idara ya mambo ya nje ya nchi. Hata kama unafahamika kuwa Katibu   wa balozi  lazima utakuwa unajua sheria zote zinazoangazia idara nyeti kama ya Malibu. Itifaki ya kwanza katika idara zote za usalama wa taifa kwa wafanyakazi wake ni kutokuongea sana. Lakini  mara baada ya  kukutana na wewe  pale hotelini , uliongea mambo mengi sana kuhusu Mboma. Ingawa  ni kwasababu ya  Mboma kutokuniheshimu  na ulitaka kunifariji lakini tukirudi katika misingi ya kitaaluma  kama katibu wa  usalama wa taifa  ulichokifanya kilikuwa nje ya miiko ya  kisheria  kama mwanausalama. Kuongea kwako sana  ilikuwa  ni kwa ajili ya kupoza  hatia  yako  na lazima  utakuwa pia unafahamu  ujio wangu   hapa  kama  moja ya wawakilishi wa Malibu ni kwasabbu ya  Himidu kanipa kazi ya kutafuta msaliti , ndio maana ulivyokuwa ukiongea  ulikuwa ukitaka niwe na aina flani ya mawazo ambayo yanakuweka mbali na hatia . Lakini kwa bahati mbaya umekutana na  Hamza  na  ulichokifanya  kimekufichua”Aliongea Hamza akiwa na tabasamu.

Rehema mara baada ya kusikia maelezo ya Hamza alijikuta  akishangaa sana , hakutarajia werevu wake ndio umemfanya kuumbuka.

“Kama ukitoka  kwenda kumnunulia bosi wako Rajabu chakula , watu wengi  wataona ni sehemu ya kazi yako ya  kuagizwa ,  na sio  tu kununua chakula lakini pia muda mwingine unaagizwa na kutoa kopi baadhi ya mafaili na  hata kuyapangilia , hivyo  hata kama utoe  kopi zaidi ya mbili hakuna atakaekushitukia , hususani na mwonekano wako wa kipole”Aliongea Hamza huku akicheka.

Muda ule  Rehema alibadilika kabisa , alijawa na ukauzu na kuwa tofauti na mwanamke alieonekana mara  ya kwanza alipokutana na Hamza.

“Hamza sina uadui wowote na wewe , ninachotaka ni  kutumia hela na kuishi maisha ya furaha yasio  na upweke na kuachana na kazi ya kutumwa tumwa. Nimeteketeza ujana wangu wote  kwa ajili ya usalama wa taifa , sina mume, sina mtoto , sina kitu. Sidaiwi na nchi  bali mimi ndio naidai nchi . Watu  wa aina yangu huoni  kama tunasikitisha sana?. Kwanini usijifanye hujaniona na kuniacha nikaishi  kwa uhuru  kwa  sehemu ya maisha yangu yaliobakia?”

Rehema alionekana akiwa na mwonekano wa majonzi makubwa, ikionesha anaongea kutoka moyoni.

“Kama ulichofanya ni kuvujisha baadhi ya nyaraka pengine ningekuacha , lakini  Dada Rehema , ulichokifanya kimesababisha watu kupoteza  maisha  katika shambulizi lile la kigaidi”

Rehema mara baada ya kusikia hivyo , uso wake ulijikunja , huku akiwa amegandishwa katika eneo moja.

“Kama ni hivyo .. kwahio  huna mpango wa kuniachia ?”Aliuliza na Hamza alitngisha kichwa.

“Sister Rehema , weka vitu vyako chini na nifuate”

“Haha..” Rehema alicheka kikauzu ,” Nikirudi na wewe  naenda kufa, siwezi kuondoka hapa na isitoshe sipo mwenyewe. Unachopaswa kufanya ni kunikamata na  kunichukua kwa nguvu”

“Unajigamba tu.  Haina haja hata ya  Bro kukumamata”Aliongea Rhoda na palepale alifyatuka aliposimama kumsogelea  Rehema  kwa nia ya kumzimisha  lakini sasa  sekunde ileile  mikondo miwili ya nishati ya rangi ya kijivu ilichomoza kama  radi kumsogelea  Black Fog.

“Rhoda!!”

Hamza  pia aliweza kuhisi msisimko wa  nguvu hio isio ya kawaida  na palepale kumpigia makelele Rhoda.

Black Fog alikuwa mwepesi mno  , kwani haraka sana  alitumia nishati ya mbingu za ardhi  na kujifyatua pembeni  na kukwepa  mishale ile ya mwanga.

Ule mwanga wa kinishati  ulienda moja kwa moja kutua katika benchi  la mbao na mara baada ya kugusana , benchi lile liligeuka unga unga kama vile limeliwa na mchwa  na kusambaratika.

“Uchawi wa kifo!!”

Hamza alimaka  baada ya fahamu zake kufanya kazi  mara baada ya  kugundua nishati hio, haraka sana alisogea mbele na kumkinga  Rhoda kwa mbele  huku akiangalia nyuma ya kanisa.

“Hii ni ajabu , kuna mtu  ndani ya hili kanisa mwenye uwezo wa kutumia  aina hii ya uchawi! Au tumeingia  ndani ya kanisa feki?” Hamza aliwaza.

Tokea dakika ambayo Hamza aliingia katika kanisa hilo hakuweza kuhisi nguvu yoyote isiokuwa ya kawaida  ambae amejificha , kutoweza  kuhisi uwepo wake ilimtisha.

Uchawi wa kifo  ni aina  pia ya mafunzo ya nishati  ambayo mtu hategemei  nishati ya kawaida kupandisha  uwezo wake , bali  mchawi anavuna  nishati kwa kukinga mvuke unaotolewa na maiti. Mvuke huo humtoka  mtu pale tu anapokata  roho na kuiachia  huru nafsi yake kutengana na mwili. Sasa  kadri  mtu anavyovuna nishati ya wafu kwa mtindo huo,  hufikia katika daraja la  kuwa na uwezo hata wa kuongea na wafu, na watu hao ndio sasa huitwa Necromancer.

Yote hayo Hamza aliyajua , hivyo kitenod cha kutokuhisi uwepo wake huyo necromancer, maana yake alikuwa na uwezo mkubwa kulingana na wa kwake  na  kuna uwezekano pengine mtu huyo alikuwa na uwezo wa juu zaidi kumzidi.

“Father!!” Aliita  Rehema kwa furaha.

Hamza aliweza kumuona mwanaume ambae alikuwa amevalia joho  la rangi  nyeusi  akitokea nyuma. Alikuwa ni mzungu mwenye nywele zilizobadilika rangi kutokana na umri. Alikuwa amevalia miwani yenye fremu za chuma  na uso wake ulikuwa mwembamba.

Hamza alizidi kuhisi hatari mara baada ya kumwangalia Padri huyo  na kugundua  hakuwa akitisha kabisa  na kulingana na uzoefu wake wa  kivita alijua kadri mtu anavyozidi kuwa wa  kawaida ndio  hatari zaidi.

“Ikitokea mapigano na huyu mzee , usije kukurupuka , sio mtu wa kawaida kabisa”Aliongea Hamza kwa  kumuonya Black Fog.

Black Fog  mara baada ya kusikia kauli hio , hisia zake zilikakamaa.Alijiuliza ni mtu gani wa kumfanya mtu kama Hamza kuwa  katika  hali ya tahadhari namna hio.

“I didn't expect you to be here, Lucifer,” Aliongea akimaanisha hakutegemea kumuona hapo Hamza.

“Unanijua?”

“Ndio  nakujua , ijapokuwa  hunifahamu , lakini nimekujua kwa muda mrefu mno”Aliongea padri yule  kwa sauti ya  kujiamini.

“Wewe ni nani? Maana kwa kile ninachofahamu katika ulimwengu huu hakuna mtu mwenye mwenye  mafunzo ya nishati za wafu na  kuongea nao zaidi  ya Mr Skeleton”

“Oh! Ndio unavyojua?” Aliongea yule father na kisha alimpotezea Hamza na kwenda moja kwa moja mpaka aliposimama  Rehema

“Rehema haupo makini , sababu ya  mambo kufikia hatua hii ni kwasababu ya  uzembe wako”

“Father tafadhari naomba uniondoe hapa , nipo tayari kukupatia nusu ya hela  zangu”Aliongea Rehema.

“Lady , money means nothing to me..”  Wakati akiongea hivyo  palepale  Rehema alionekana kuingiwa na mvuke  mweusi kupitia pua , masikio  na mdomo.

“Arghhhhh!!”

Rehema aliishia kutoa ukulele mkubwa , huku akidondoka chini  na kuanza kutetemeka kwa nguvu.  Ndani ya sekunde chache tu mwili wake wote ulitoa mvuke  na kukauka..

Hamza alikwisha kutarajia  suala kama hilo lingetokea  na aliishia kuhema  kwa nguvu   kwa masikitiko ndani ya moyo wake. Hata hivyo hakuwa na muda wa kujali kuhusu kifo cha Rehema.

“Lucifer , sikutarajia kama utakuja  na kuharibu mpango wangu, unachukiza  mno ..”Aliongea huku akimwangalia Hamza kwa namna ya kumchunguza na  kisha akaendelea.

“Ila kwasababu ya  kuhakikisha mpango  unaendelea kukamilika kama ilivyopangwa .  kwa leo  nitaondoka”

Hamza akili yake palepale  iliingiwa na hisia zisizo za kawaida  mara baada ya kusikia mtu huyo bado ana mpango  sehemu nyingina katika muda tofauti , alijiuliza au  anamaanisha muda wa  kufungua kiboksi.

Kwa mchawi mwenye nguvu namna hio kujitokeza ndani ya  mji wa Limour bila ya kushitukiwa . Ilikuwa ni adimu na  isio kawaida.

Hamza palepale hisia zake zilimwambia bwana huyo mpango wake haikuwa kwa  Rehema kabisa bali  ni kupitia Baraza la maksi.

“Rhoda rudi haraka  ukumbini  na umwambie  Rais Maxim kuna Necromancer anaepanga  kushambulia  Baraza”

Black Fog palepale alijua   hali ilivyo  hatari  na haraka sana aliitikia na  kugeuka kuondoka.

Mara baada ya kuona hivyo , yule padri  haraka sana aligeuzia mkono kuelekea upande wa  kutokea  na ghafla tu mlango ulijaa  kiwingu kilichokuwa kikitoa  msisimko uliokuwa ukipambana na nafsi.

Black Fog  uwezo wake wa nishati bado ulikuwa mdogo , hivyo palepale aligeukia madirisha , lakini ile anakaribia  dirisha ili kuruka , ghafla tu aliona kisu kilichotengekezwa kwa mfupa kikisogea kutoka nje kwa kurushwa.

“Clang!!”

Kioo cha dirisha kilipasuliwa na  kisu kilichoonekana kurushwa na mtu kutoka nje. Black Fog mara baada ya kuangaza macho yake  nje alijikuta mwili ukimsisimka mara baada ya kuona  maskeleton ya watu yakitembea kusogelea kanisa hilo , huku kila moja likiwa limeshikilia siraha, mbaya zaidi yalikuwa zaidi ya ishirini hivi huku yakiwa  yamezungukwa na kiwingu cha ajabu kama mvuke.

Hamza  mara baada ya kuona vile mara moja alianza kumshambulia yule  padri.

Eneo hilo lilikuwa na makaburi  na kwa jinsi  lilivyozingirwa na nguvu ya  ajabu , ilionyesha kabisa bwana huyo kuna uwezekano alikuwa ameficha maskeletoni hayo  kwa ajili ya kuyatumia kama  wanajeshi.

Na kwa mantiki hio Hamza aliona haitokuwa busara kupigana na  maskeleton  na   badala yake  ni vizuri kupambana na mwenye maskeletoni.

Hamza alikuwa na spidi mno   na ile anamkaribia yule  Padri alirusha ngumi nzito kumlenga  kichwani  na ilifanikiwa kumpata.

“Bang!”

Hamza alijikuta akishangaa  na hio  ni mara baada ya  mwanzo kufikiria  Padri huyo angekuwa na uwezo wa  kukwepa na kujilinda lakini  matokeo yake ngumi yake ilitua vizuri tu  katika paji la  uso wake na kumchangua.

Hamza kuona vile  alihisi kuchanganyikiwa mara baada ya kugundua hali haikuwa shwari.

Ilikuwa ni  tofauti na alivyotegemea , kwani mara baada ya kushambulia kichwa kile na kupasuka , tofauti na damu  kumtoka , kulitokea moshi mweusi  wenye msisimko wa ajabu mno.

Hamza palepale alijihisi  kuwa mjinga , alipaswa kujua tokea mwanzo sababu ya kutokujua kwanini hakuweza kuhisi uwepo wa huyo Padri tokea mwanzo , sio  kwasabbau ya uwezo wake bali alikuwa ni skeletoni pia  akiongea  kwa niaba ya mtu mwingine na kwa mantiki hio aliamini lazima  Padri huyo  alikuwa ni  wa  hilo kanisa na alizikwa hapo.

Moja ya uwezo  wa wachawi  wa aina hio ni kwamba wanaweza kukutengenezea uhalisia wa mtu , kwa kumvalisha ngozi bandia , ila ki uhalisia sio ngozi ni  macho  yako mwenyewe  ndio yanayokudanganya na ndio kilichomtokea Hamza, Rhoda na Rehema.

Hamza alijikuta akiwaza palepale na kuona kumbe hata Rehema mtu ambae  alikuwa akiongea nae  alikuwa amekwisha kufa kitambo.

Hamza alijikuta  akijiuliza kama ni hivyo  huyo mchawi halisi yupo wapi, hakutaka kujiuliza mara mbilimbili na haraka sana alitoka nje ya kanisa kumsaidia Rhoda kushambulia maskeletoni mawili kwa mpigo.

Black Fog alikuwa ni mwanamke  na  pia   alikuwa akipambana vita vya aina mbili kwa wakati mmoja vya  kimwili na  nafsi , hivyo  ilizidi kuwa ngumu kwake kupambana na hayo maskeletoni.

“Bro tunafanyaje sasa?” Aliuliza Black Fog  kwa wasiwasi

“Nitaharibu kwanza haya majitu wewe  umpigie simu Asmuntis, mwambie Maxim kusitisha mara moja kikao”

Wakati Hamza akiongea  alikuwa akishambuliana na maskeletoni kwa kasi ya ajabn ila licha ya hivyo  wanajeshi hao wa  vifo hawakuwa wakichoka hata kidogo. Maana kila wakipigwa chini kudondoka walikuwa wakisimama tena na kuendelea kushambulia.

Kilichomsumbua zaidi Hamza ni kwamba  yalionekana yakiongezeka  kadri muda unavyosogea.

“Bro  hili eneo halina mtandano , nina uhakika  wameukata”Aliongea Black Fog alieshikilia simu akijaribu kupiga.

“Damn it .. hawa watu wanajaribu kufanya nini?”

Hamza palepale alijikuta akiwaza kwa sekunde na kisha  aling’ata meno yake na kuongea.

“Haina  haja ya kuendelea kushambuliana nayo ,  tutaruka kwenda kutoa taarifa”Aliongea Hamza.

“Tutaruka!?”

Black Fog alionekana kutokuelewa lakini muda ule Hamza alishambeba juu juu  na mara baada ya kushambulia  maskeletoni mawili  alipiga hatua mbili kwenda mbele na ile anapiga  ya  tatu kama mwanariadha aliruka hewani.

Hamza alikwenda kutua mita kumi mbele  mbali na  yale Maskeletoni na kumuweka chini  BlackFog . Lakini sasa  ile wanataka kuanza kukimbia  waliweza kuona kivuli cha mtu alievalia joho  la rangi nyeusi akiwa amesimama katikati ya barabara  kwa namna ya kuwazibia njia.

Ilikuwa ngumu kumuona , kwasababu   alikuwa amezingirwa na kiwingu  cheusi  usoni  huku mkononi akiwa ameshikilia kitu cha  maajabu kama fimbo ilioning’iniza mifupa mingi  ya kila aina kwanzia  ya ndege, binadamu   na wanyama.

Hamza mara baada ya kuangalia ile fimbo  ilivyokuwa ikitoa msisimko  wa nguvu ya uchawi ya kutosha  alijikuta  akikaza macho yake na kumwangalia kwa umakini na palepale moyo wake ulipiga kite. Haikuwa kwake tu  hata kwa Black Fog hivyo hivyo.

“Mr Skeleton!!!”

Hawakuamini , mtu ambae alikuwa  akiwashambulia alikuwa  ni mchawi wa  misitu ya Amazoni , Mr Skeleton moja ya magwiji kumi wa Baraza la  maksi.

Previoua Next