Najma alimwangalia Roma aliekuwa na Begi lake mgongoni na kumfanya taswira ya miezi sita nyuma ijijenge katika kichwa chake , alikumbuka siku ambayo alimpokea Roma alikuwa amebeba begi hilo hilo utofauti wa leo ni kwamba Roma alikuwa kwenye mavazi mazuri kuliko kipindi kilichopita.
“Kaka anaroho mbaya ni kweli kamfukuza Roma kama alivyosema”
Najma alimwangalia Roma kwa uso uliojaa maswali mengi , huku akiwaza moja kwa moja kuwa Juma atakuwa amemfukuza Roma na sasa Roma alikuwa akiondoka kwenda kupanga kwingine.
“Najma naomba tuongee kabla sijaondoka”
“Juma naomba niongee na Najma , sitaki kuacha deni nyuma”Aliongea Roma na Juma alitikia kwa kutingisha kichwa huku akiwaacha.
“Jana ulikuwa wapi Roma , Nisamehe kaka yangu kachukua maamuzi ya kukufukuza”
“Nifate Najma nje tukaongee”aliongea Roma huku akitangulia na Najma alitangulia , ila Najma alishangaa pale alipomuona Roma akifungua mlango wa gari ya kifahari ambayo hakuwahi kuwaza mtu kama Roma anaweza kuinunua , ghafla yale mawazo aliokuwa nayo juu ya Roma kuwa mtu mkubwa aliekuwa akijifanyisha masikini yalianza kurudi upya , ila kwake hakuwa na shida , aliingia ndani ya gari kwa kusitasita.
“Hii gari umeitoa wapi Roma , ni nzuri mno nitakuja kununua yangu kama hii”Aliongea Najma na kumfanya Roma Atoe tabasamu lililojaa uchungu moyoni mwake kwani aliamini taarifa anayokwenda kumwambia mwanadada huyu itamwachia machungu mengi moyoni.
“Najma naomba unisikilize jambo ninalokuambia, na pia nitaomba unisamehe kama nitakukwaza na kukuumiza , ila sitaki kukuficha ukweli wote Najma”Aliongea Roma na kumfanya Mrembo huyu amwangalie.
“Usijali wewe niambie tu Roma nipo tayari kusikilia lolote ili mradi liwe jambo la ukweli”Roma alivuta pumzi na kukusanya ujasiri aliokuwa nao ndani yake .
“Jana nimefanikiwa kukutana na mwanamke niliepotezana nae kwa miaka mingi ambaye nilidhania amefariki na baada ya kuonana tumefunga ndoa rasmi na unavyoniona hapa mimi ni mume wa mtu , najua ni kiasi gani unanipenda Najma na ndio maana siku zote nilikuwa nikijizuia kutokuzikubali hisia zako….”Roma kabla hata hajamaliza mlango wa gari ulifunguliwa na Najma alitoka na kukimbilia ndani kwao hakutaka tena kusikiliza maneno ya Roma,
Roma alibaki akiwa hajui ni kipi afanye , lakini hakuwa na jinsi , ili mradi ashauweka wazi ukweli wote mbele ya Najma, basi aliona ni vyema kwa mwanadada huyo kumsahau kaika maisha yake.
****
Ni muda wa Asubuhi ndani ya jengo la Club B, katika chumba ambacho kilikuwa ni ofisi ya mwanadada mrembo maarufu ndani ya eneo hili la Chalambe Maji matitu , alionekana Rose akiwa amekaa kwenye kiti chake cha kuzunguka huku mbele yake kukiwa na tarakishi kubwa iliokuwa imewashwa , huku mwanadada huyu akionekana kusoma taarifa iliokuwa kwenye mfumo wa Softcopy.
Ofisi yake ilikuwa ni kubwa , iliokua imependezeshwa na samani za bei ya juu kuonesha kuwa mwanadada huyu hakuwa vibaya kwenye swala la kifedha na kwa namna alivyokuwa amevaa na namna ambavyo alikuwa kaitumia Tarakishi hio alionekana kuwa Profesheno.
Baada ya dakika kadhaa za kukaa hapo ndani , mlango wake uligongwa na akaingia kijana mmoja alievalia suti na miwani ya jua akiwa na kipara kilichokuwa kinang`aa , bwana huyu alionekana kuwa ni wale vijana waliokuwa wakifanya mazoezi.
“Niambie Zonga unataarifa gani?”
“Madam taarifa niliokuwa nayo ni kwamba Roma kapata mke”
“Unamaanisha nini?”
“Kwa taarifa nilizokuwa nazo sasa Roma kafunga ndoa jana na leo amekuja sehemu anayoishi na kuchukua mizigo yake na kuhamia kwa mke wake”Maneno ya Zonga yalikuwa kama kisu cha moto kilichokuwa kikipita katika moyo wa mwanadada huyu.
“Bosi..!”Aliita zonga mara baada ya kumuona bosi wake akitoa machozi, na Rose aliyafuta haraka haraka na kisha aliachia tabasamu la ujasiri.
“Endelea kufatilia ni mwanamke gani Roma kamuoa” Aliongea Rose na Zonga alitoka
“Huyu fala ana nyota bwana , yaani mrembo kama bosi anatoa machozi kwa ajili ya fala mbeba mizigo , huyu jamaa ana nini mimi sina” Alijiongelesha Zonga ndani ya moyo wake huku akitoka ne ya ofisi.
Rose alisimama na kusogelea dirisha na kuangalia baadhi ya watu waliokuwa kwenye pilikapilika za kutafuta maisha huku akionekana ni mwenye mawazo sana huku akijizuia kulia.
“Stori yetu haiwezi kuisha hivi Roma ,Siku ulionikoa kwenye mikono ya baba yangu ndio ulikuwa mwanzo wa stori yetu na haikuwa bahati mbaya hata kidogo , nimetumia pesa nyingi sana kukutafuta na mpaka kukupata , siwezi kukuachia kirahisi” Alijiongelesha Rose.
****
Roma hakujali sana , aliendesha gari lake mpaka Kigamboni na kupokelewa na Bi Wema kwani mke wake hakuwa amerudi kutoka kazini, baada ya kuweka lile begi , alitoka nje na kuzunguka upande wa Yard ya magari huku mkononi akiwa ameshikilia kile kiboksi alicho toka nacho Mbagala , aliangalia sehemu ya kificha kiboksi hiko , lakini hakupata na mara akapata wazo na kuondoka ndani ya eneo hilo na kuingia chumba cha mazezi , aliangalia sehemu rahisi ya kuhifadhi kiboksi hicho , na alifanikiwa kupaona na kisha alikiweka vizuri na kuziba na kisha alitoka nje.
Baada ya kurudi ndani kwenye chumba chake aliwasha tarakishi na kisha akaingia kwenye mtandao na kuangalia namna ya kupata kazi , bahati nzuri , aliona baadhi ya makampuni mbalimbali yaliokuwa yakitangaza ajira , alichagua kazi aliona inafaa na kisha aliandika CV yake na kuituma pamoja na vivuli vya vyeti ambavyo alivitoa kwenye akaunti ya Barua Pepe yake , aliomba kwenye kampuni tatu harakaharaka na kisha alijilaza kitandani , lakini hakukaa muda mrefu , aliitwa na Bi wema na kuambiwa chakula tayari ashuke wakale.
Roma baada ya kula chakula kitamu kilichokuwa kimeandaliwa na Bi Wema , alirudi chumbani kwake huku kwenye kichwa cheke akiwa na mpango wa kwenda kupiga misele mjini maana alikuwa na kiasi cha pesa kilichokuwa kikimruhusu kufanya hivyo.
Alijiandaa haraka haraka, kwa kuvalia tisheti yake iliomtoa vyema na Jeans pamoja na Raba kisha alichukua ufunguo wa gari na kumuaga Bi Wema na kisha alitoa gari nduki.
Masaa machache tu alikuja kuonekana akiwa maeneo ya Posta kwenye moja ya saluni ya kisasa maarufu ,aliegesha gari yake kwa ustadi mkubwa huku waliokuwa karibu na eneo hilo wakiliangalia gari lake kwa matamanio.
Roma hakujali sana , alitoka kwenye gari na kisha aliingia ndani ya saluni hii ya kiume kwa ajili ya kutengenezwa nywele zake kitendo ambacho kilifanyika kwa muda mfupi sana , baada ya kupendeza kwa staili aliokuwa anataka yeye , aliendesha gari yake kuelekea upande wa Ocean road.
Muda wa saa kumi na mbili ndio muda ambao Roma alikuwa anarudi na sasa alikuwa anaingiza gari yake ndani ya jumba lao la kifahari , lakini ile anaingia aliona gari ambayo kwa haraka haraka alijua sio gari ya Edna , aliamini kulikuwa na ugeni ila hakujua ni ugeni wa mtu gani , ila aliamini kwakuwa ashafika , basi majibu ya maswali yake yatajibiwa akiingia ndani.
Baada ya kuingia ndani ni kweli aliona mwanaume mmoja ambae baada ya kumwangalia sura yake ilikuwa inakuja hivi na kupotea , mwanaume huyu hakuwa peke yake bali na mke wake alikuwepo.
“My Wife Am back!”Aliongea Roma na kumfanya kijana aliekuwa amekaa kwenye sofa amwangalie huku akionyesha chuki ya waziwazi na Roma aliliona hilo na kwakua alikuwa sio mtu wa kujali sana alisogea upande wa kushoto alipokuwa mke wake na kumbusu shavuni , kitendo ambacho Edna hakuzuia na Roma aligundua jambo pia kwa mara ya pili.
“Babe huyu ni nani?”
“Anaitwa Abubakari ni mwanaume ambaye nilikuwa nikikuambia”.
“Oooh ! unamaanisha yule mwanaume ambaye humpendi ndio huyu bwana”.
Maneno hayo yalimkera mno Abuu ila alijitahidi kujizuia mbele ya Edna.
“Braza vipi mimi ni Roma , ni mume wa Edna nimesikia habari nyingi juu ya kumsumbua mke wangu hivyo braza kaa mbali na mke wangu ama nitakufanya jambo baya”Aliongea Roma na kumfanya Abuu atabasamu kifedhuli.
“Wewe mbeba mizigo utanifanya nini labda.. usifikiri nimekaa kimya ukajua nakuogopa Edna ni wangu wewe ni wakuja tu na muda wowote utaondoka na kuurudia umasikini wak..”Ilikuwa ni kitendo cha haraka sana ambacho Roma alikifanya kwani kabla ya Abuu hajamaliza kuongea alikuwa hewani akining`inia kwenye mkono wa Roma,bwana huyu alikuwa akivuta pumzi kwa shida huku akijaribu kuongea neno lakini ni kama Roma hakujali na nia ya kumuua bwana huyu ilionekana waziwazi kwenye macho ya Roma.
“Roma Stoop..!!”Ilikuwa ni sauti ya kitetemeshi ya Edna iliomfanya Roma amtupe Abubakari chini kama furushi.
“Nikihesabu mpaka nne bado upo hapa ndani nakuaa .. moja,, mbili .. tatu..” Lakini kabla hajamaliza Abuu alisimama na kumwangalia Roma kwa macho makali na kisha alitoka huku akishika shingo yake, na hii ni baada ya kuona kuwa Roma hakuwa akitania kwani macho yake yalikuwa yamejaa hasira kali kiasi kwamba alionekana kuwa tayari kwa kuua muda wowote.
Upande wa Edna alishangazwa na uwezo wa nguvu aliokuwa nao Roma, namna ambavyo Roma alimning`iza hewani Abuu kilimuogopesha na kumuacha kwenye maswali.
“Mbona haupo makini Roma , unajitafutia matatizo , unajua nguvu iliokuwepo nyuma ya Abuu wewe?”
“Kwa hio kukiwa na nguvu kubwa nyuma yake nimuogope na akikanyaga mguu wake hapa tena namuua..”Aliongea Roma huku kiini cha macho yake kilichokuwa kimebadilika rangi kuwa kijani kilirudi na kuwa kama kawaida na kutokana na hasira alizokuwa nazo Roma hakutaka kubaki hapo sebuleni na kupandisha ngazi kwenda chumbani kwake na kufunga mlango kwa nguvu , huku akimuacha Edna aliekuwa akimwangalia kwa wasiwasi mkubwa.
Baada ya Roma kuingia kwenye chumba chake moja kwa moja alienda kuoga huku akituliza hasira zake, baada ya kujiona yupo sawa alisogelea Laptop yake na ile anaiwasha aliona ‘Notification’ kwenye barua pepe ikionesha kuna ujumbe , alifungua na kukuta kuna jumbe tatu.
“Mr Roma Ramoni we are happy to inform you that tomorrow we would like to do an interview with you regarding the job request you submitted to us , it will be our honor to see you tomorrow at xxx time”
“Ndugu Roma tunafuraha kukuambia kwamba tunapenda kufanya usaili na wewe kesho kulingana na ombi la kazi uliloliwasilisha kwetu , itakuwa heshima kwetu kama tutakuona kesho”.
Alifungua meseji ya pili na kisha akasoma.
“Hellow Mr Roma Ramoni we reviewed your job Request and your Credential’s that you submitted to us and confirmed they are Valid,We are replaying back to inform you to attend interview tomorrow morning at xxx time”
Karibia kampuni zote tatu zilikuwa zimerudhisha majibu ya kumtaka Roma kwenda kwenye interview siku ya kesho , alitabasamu na kuona kumbe kutafuta kazi ni rahisi hivyo, lakini licha ya majibu hayo alipanga kwenda kwenye kampuni moja tu na hivyo alitakiwa kuchagua kamouni moja ya kwenda kwa siku ya kesho.
“Vexto Group of Companies ndio moja ya kampuni ambayo Roma alidhamiria kwenda kufanya usaili kesho , kilichomvutia kuhusu hii kampuni kwanza ilikuwa ni kampuni kubwa sana ndani ya Afrika Mashariki na Kati yote ambayo ilikuwa inaendeshwa kwa thamani ya pesa kiasi cha Dola bilioni ishirini, Pili makao makuu ya kampuni hii yalikuwa makao makuu ya kampuni ya mavazi na mitindo ifahamikayo kwa jina la E- Styllus Wear , kampuni ambayo ilikuwa ikiaminika kwa kuwa na warembo wakali.
“Hii ndio kampuni nzuri , nitakutana na warembo wengi”
Comments